Je! Wenye Pupa Watatoweka
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1. Ni kwa njia gani tumepatwa na madhara ya pupa ya mwanadamu?
SISI sote tumepatwa na matokeo mabaya ya pupa ya mwanadamu kwa njia fulani. Pupa ndiyo imesababisha uharibifu wa vilima na milima, uharibifu wa maeneo makubwa ya nchi kwa kuchimbua ardhi, kuchafuliwa kwa vijito na takataka ya mjini, na kugeuzwa kwa miji kuwa sehemu zilizojaa moshi na kelele. Wanadamu vile vile wamewatumia wenzao kwa kazi na kujitajirisha wenyewe. Je! pupa kama hiyo itakwisha? Je! wenye pupa watatoweka?
2. Ni nani ameona pupa ya mwanadamu, na ni uhakika gani hili linatupa juu ya kuendelea kwake?
2 Ndiyo, kwa kuwa matendo ya pupa hayakupita bila kuonwa na Yeye ambaye anachukia pupa na aliye na uwezo wa kutosha kuimaliza. Yeye ndiye Mwenye Enzi Yote mkuu wa ulimwengu wote, Yehova Mungu. Mfano wa kihistoria wa matendo yake na Israeli wa kale unaonyesha kwamba watu wenye pupa hawatavumiliwa milele na kwamba watu wenye nia ya haki watabarikiwa.
MFANO KUTOKA KWA HISTORIA YA KALE
3. Nia ya wenyeji wenye pupa wa Yerusalemu na nchi ya Yuda ilikuwa nini juu ya “ndugu” zao waliokuwa katika uhamisho wa Kibabeli?
3 Katika karne ya saba B.C.E. wakazi wengi wa Yerusalemu na nchi ya Yuda walikuwa wenye pupa. Hawakupendezwa na Waisraeli waliokuwa wamenyimwa mali yao ya kurithi kwa sababu ya uhamisho wa Kiashuru mwaka wa 740 B.C.E. na uhamisho wa Kibabeli mwaka wa 617 B.C.E. Nia ya wenye pupa juu ya wahamishwa hao ilikuwa: “Jitengeni mbali na [Yehova], nchi hii tumepewa sisi, iwe milki yetu.” (Eze. 11:15) Kama ndugu za Waisraeli waliokuwa wakiishi kama wahamishwa katika Milki ya Kibabeli, wakazi wa Yerusalemu na nchi ya Yuda wangalipaswa kuonyesha roho ya mnunuzi ambaye angekomboa mali ya kurithiwa ili kwamba nduguye asiye na makazi arudishwe kwenye mali aliyopewa na Mungu. (Law. 25:13-38) Lakini wenye pupa hawa walipendezwa ndugu zao wakilazimishwa kuwa “mbali na [Yehova]” kadiri ilivyowezekana, yaani, mbali na nchi ya Israeli ambapo ilifahamika Yehova alikuwa. Walitaka nchi iwe yao.
4. Yehova angekuwa kimbilio kwa wahamishwa waliotubu namna gani?
4 Lakini, Yehova Mungu, aliliona jambo hili kwa njia nyingine. Alikuwa na nia ya kuwakubali wenye kutubu kati ya wahamishwa, akiwa “patakatifu kwao kwa muda mchache.” (Eze. 11:16) Kwa huo “muda mchache” wa uhamisho wao Yehova angekuwa patakatifu. Angekuwa mahali patakatifu ambapo wangeweza kupata salama na kuhifadhiwa kwa makusudi yake mema ya wakati ujao. Halafu, tena, Yehova angekuwa patakatifu kwa kadiri ndogo. Hii ni kwa sababu hangeweza kuwakinga wahamishwa na matokeo yote waliyostahili ya mwenendo wao mbaya wala hangeweza kuufupisha urefu wa uhamisho uliokuwa umesemwa mapema, uliokusudiwa kuendelea kwa miaka 70 nyuma ya kuanguka kwa Yerusalemu.
5. Ahadi ya Yehova ya kuwarudisha waliotubu ilianza kutimizwa lini?
5 Lakini, mwishowe, Yehova alikusudia kuwarudisha kutoka uhamishoni. Aliahidi: “Nitawakusanya ninyi toka kati ya kabila za watu, na kuwakutanisha toka nchi zile mlizotawanyika, nami nitawapeni nchi ya Israeli.” (Eze. 11:17) Ahadi hii ilianza kutimizwa wakati, mwaka wa 537 B.C.E., mabaki waliotubu wa Kiyahudi waliporudi kwao nyumbani.
6. Matokeo kwa wenyeji wenye pupa wa Yerusalemu na nchi ya Yuda yalikuwa nini?
6 Kwa upande mwingine, Yehova hakuwavumilia wakazi wenye pupa wa Yerusalemu na nchi ya Yuda milele. Alikuwa ameonya: “Bali wao ambao mioyo yao huenda kwa kuufuata moyo wa vitu vyao vichukizavyo, na machukizo yao, nitaileta njia yao iwajilie juu ya vichwa vyao.” (Eze. 11:21) Kwa hiyo, kwa kuwatumia Wababeli, Yehova aliwaletea Wayahudi hao wenye pupa matokeo ya njia yao ya kuchukiza. Mwaka wa 607 B.C.E. Yerusalemu uliharibiwa, wenye pupa ama wakitoweka ama wakilazimishwa kuiacha nchi na kupelekwa uhamishoni.
ONYO KWA LEO
7. Ni onyo gani imetupasa kupata kutokana na yaliyotukia kwa wenyeji wasio waaminifu wa Yerusalemu na nchi ya Yuda?
7 Lililotukia nyuma huko katika Yerusalemu na nchi ya Yuda karibu karne 26 zilizopita si historia tu isiyo na maana. Linahakikisha kwamba Yehova Mungu atahakikisha kwamba wanaozoea pupa wanapata adhabu yao wanayostahili. Hii inatia ndani na watu wenye pupa wanaoshirikiana na taratibu za kidini za Kristendomu. Inapaswa ikumbukwe kwamba wakazi wa Yerusalemu na nchi ya Yuda walidai kuwa watumishi wa Mungu. Lakini, dai hilo, halikuwakinga na hukumu kali ya Mungu.
8. Yehova Mungu anaonaje taratibu za kinafiki za kanisa za Kristendomu?
8 Kulingana na aonavyo Yehova Mungu, taratibu za uongo, za kinafiki za kidini zote ni sehemu ya tengenezo kubwa sana la kimalaya linalotajwa katika Maandiko Matakatifu kama “Babeli ule mkuu.” Tengenezo hilo la kimalaya linatia ndani na taratibu za kinafiki za kanisa za Kristendomu, ambazo, kama sehemu nyingine ya “Babeli ule mkuu,” ‘zimeishi kwa anasa chafu.’ (Ufu. 18:7, NW) Je! si kweli kwamba makanisa ya Kristendomu mara kwa mara yamejaribu kupata kibali cha walio tajiri na wakuu? Je! hili halikufanya maskini waonewe hali viongozi wa kidini wakipewa maisha ya starehe, ndiyo, hata ya anasa? Je! majumba mengi ya kidini na taji za wakuu wa kidini havikupambwa na vito vya bei, dhahabu na fedha? Je! mwingi wa utajiri huu haukuwekwa katika makasha ya taratibu za makanisa kwa hasara ya maskini?
9. Jambo gani litatokea kwa “Babeli ule mkuu”?
9 Kwa sababu ya pupa hiyo ya kichoyo, “Babeli ule mkuu” utaangamizwa. Unabii wa Biblia unaonyesha kwamba Ufunuo 18:21 utatimizwa katika kizazi hiki: “Malaika mmoja mwenye nguvu akainua jiwe, kama jiwe kubwa la kusagia, akalitupa katika bahari, akisema, Kama hivi, kwa nguvu nyingi, utatupwa Babeli, mji ule mkuu, wala hautaonekana tena kabisa.”
10. Sababu gani uharibifu wa “Babeli ule mkuu” hautamaanisha mwisho wa dini ya kweli?
10 Hukumu hii haimaanishi mwisho kwa dini ya kweli na wale wanaoizoea. Sababu gani sivyo? Kwa kuwa Yehova Mungu anawaelekea kwa kupendezwa wale walioacha mazoea ya kuchukiza ya “Babeli ule mkuu” kwa kutubu. Watu kama hao wanaona kwamba matendo ya Mungu kwao yanalingana na maono ya wahamishwa waliotubu wa Kiyahudi waliorudi Yerusalemu na nchi ya Yuda mwaka wa 537 B.C.E.
11, 12. Tangu masika ya mwaka wa 1919 C.E., ni unabii gani umetimizwa kwa habari ya mabaki waliotiwa mafuta wa mashahidi wa Kikristo wa Yehova?
11 Ushuhuda wa kisasa wa kihistoria unaonyesha kwamba wakati wa vita ya ulimwengu ya miaka ya 1914-1918 mabaki waliojiweka wakf, watiwa mafuta waliobatizwa wa mashahidi wa Kikristo wa Yehova waliletwa katika utumwa wa Kibabeli. Lakini, katika masika ya mwaka wa 1919 C.E., walipata ukombozi. Tangu wakati huo wameona kwa upande wao wenyewe utimizo wa Ezekieli 11:18-20:
12 “Nao watafika huko, nao wataondolea mbali vitu vyake vyote vichukizavyo, na machukizo yake yote. Nami nitawapa moyo mmoja, nami nitatia roho mpya ndani yao; nami nitauondoa moyo wa kijiwe katika miili yao, nami nitawapa moyo wa nyama; ili waende katika amri zangu, na kuyashika maagizo yangu, na kuyatenda; nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao.”
13. Eleza namna Ezekieli 11:18-20 limetimizwa nyakati za kisasa.
13 Ndiyo, Waisraeli watiwa mafuta wa kiroho walirudia “nchi” ya mfano ya Israeli wa kiroho. Waliacha nyuma vitu vya kuchukiza vya Kristendomu na sehemu nyingine yote ya “Babeli ule mkuu.” Yehova amewapa “moyo wa nyama,” si mgumu kama jiwe bali unaowafanya wazishike amri zake kwa sababu ya upendo kwake. Vile vile aliweka “roho mpya,” yaani, roho takatifu yake, ndani yao. Hivyo matunda yake—upendo, furaha, amani, uvumilivu, wema, fadhili, imani, upole na kujiweza—yanaonekana waziwazi katika maisha zao. Wamekuwa watu wa Yehova kweli kweli na Yeye amekuwa Mungu wao.
14. Ni nani mbali na mabaki waliotiwa mafuta wanaofurahia kibali cha Yehova, na wanatazamia nini?
14 Lakini, si Waisraeli wa kiroho peke yao wanaoona baraka za Mungu. Nyuma katika karne ya sita B.C.E. si Waisraeli wa asili peke yao waliorudi kutoka uhamishoni wa Kibabeli. Kati ya waliorudi walikuwako watu wasio Waisraeli kama watumishi wa hekalu Wanethini. (Ezra 2:58) Vivyo hivyo, tangu mwaka wa 1935 C.E. “mkutano mkubwa” unaoongezeka sikuzote wa watu wenye mfano wa kondoo wameacha “Babeli ule mkuu” na sasa wanafurahia kibali cha Yehova pamoja na mabaki waliorudishwa katika “nchi” ya mfano ya Israeli wa kiroho. Kwa sababu wamekwisha fuata ibada safi isiyotiwa unajisi ya Yehova, wao, pamoja na mabaki watiwa mafuta, wataachiliwa wakati Kristendomu mwenye pupa na sehemu nyingine yote ya “Babeli ule mkuu” wanapoharibiwa.
ONYO LINATAKIWA
15. Sababu gani ni jambo la haraka kwamba watu wajulishwe linalomngoja Kristendomu na sehemu nyingine yote ya “Babeli ule mkuu”?
15 Uharibifu wa Kristendomu na sehemu nyingine yote ya “Babeli ule mkuu” utatukia bila shaka sawasawa na uharibifu ulioipata Yerusalemu wa kale mwaka wa 607 B.C.E. Namna lilivyo jambo la haraka basi kutangaza onyo juu ya mabaya yanayokuja! Tangazo la onyo kama hilo lingekuwa kuiga alivyofanya Ezekieli. Nyuma ya Yehova kumfunulia katika njozi kwamba wenye pupa wa Yerusalemu na nchi ya Yuda wangeona kulipiza kisasi kwa kimungu, Ezekieli anaripoti:
16, 17. Ezekieli alifanya nini na ujumbe uliofunuliwa kwake katika njozi?
16 “Roho hiyo ikaniinua, ikanichukua katika maono, kwa nguvu za roho ya Mungu, hata Ukaldayo, kwa watu wale wa uhamisho. Basi maono niliyoyaona yakaniacha. Ndipo nikawaambia watu wa uhamisho habari ya mambo yote aliyonionyesha [Yehova].”—Eze. 11:24, 25.
17 Alipotoka chini ya uwezo wa kumwonyesha njozi wa roho takatifu ya Mungu Ezekieli alijua kwamba alikuwa katika nyumba ya kuhamishwa kwake na wazee wa Yuda walikuwa wameketi mbele yake. Mara alianza kuwaambia wanaume hawa aliyokuwa ameona na kuamuriwa kusema. Hakusema kwao tu, bali vile vile alitoka nyumbani kuwaambia na wengine. Hili ni jambo lililowapasa wahamishwa wote.
18. Tutafanya nini ikiwa tunafahamu wazoeaji wote wa pupa karibuni wataharibiwa?
18 Ikiwa sisi leo tunafahamu kwamba karibuni hivi Yehova Mungu atamaliza pupa yote na vile vile wenye pupa wenyewe, tutamwiga Ezekieli na kuwaambia wengine juu yake. Hii itawapa nafasi ya kugeuza njia zao na kujiweka mahali wanapoweza kupata ulinzi wa Mungu na baraka. Kwa kuongeza, tutajitahidi kupatikana katika hali itakayomaanisha usalama kwetu “dhiki kubwa” inapoleta mwisho wa taratibu yote hii ya mambo yenye pupa, kutia ndani na Kristendomu.
—Kutoka Kitabu “The Nations Shall Know that I Am Jehovah’’—How?