Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 10/15 kur. 475-478
  • Kungoja Sana Katika Tumaini Karibu Kumalizike

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kungoja Sana Katika Tumaini Karibu Kumalizike
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KWA KUGEUKIA KATIKA TUMAINI LA KWELI
  • Utawala wa Kimungu—Tumaini la Pekee la Wanadamu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Utawala wa Kimungu—Je! Sisi Tunauunga Mkono au Tunaupinga?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Utawala wa Kimungu— Juu ya Wanadamu Mwanzoni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Tumaini Katika Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 10/15 kur. 475-478

Kungoja Sana Katika Tumaini Karibu Kumalizike

1. Kulingana na Waebrania 10:12, 13, Yesu aliendelea kungoja kuumeni kwa Mungu mpaka lini, na Zaburi 110:1, 2 inaonyesha nini kitakachotukia tukijiunga na adui zake?

HATA nyuma ya kufufuliwa kwa wafu siku ya tatu, Yesu aliendelea kuungoja wakati wa Mungu wa kusimamishwa kwa ufalme wa kimbinguni juu ya wanadamu wote. Kwa habari ya hili iliandikwa kwa Wakristo Waebrania katika karne ya kwanza C.E. hivi: “Lakini huyu, alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu; tangu hapo akangojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake.” (Ebr. 10:12, 13) Huu ni mtajo wa Zaburi 110:1, 2, tunaposoma hivi: “Neno la [Yehova] kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako. [Yehova] atainyosha toka Sayuni fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako.” Kwa kuitii amri hii Yesu Kristo atakuwa na tegemezo la Utawala wa Kimungu na adui wote duniani watafanywa kuwa chini ya miguu yake, wote wakitiishwa kabisa na kuharibiwa. (Zab. 110:5, 6) Kwa hiyo sote leo twajua cha kutazamia tukijiunga na adui zake, ambao ni adui za utawala wa kimungu.

2. (a) Katika wakati uliobaki bado, utawala wa kibinadamu, ndiyo, Ibilisi mwenyewe, ana nini cha kutoa kwa wanadamu? (b) Tangu kutupwa kwa Shetani nje ya mbingu, imewalazimu wanadamu wajue maana ya makelele gani mbinguni?

2 Katika wakati unaobaki kwa adui hawa, je! wao wana nini cha kuwapa wanadamu? Si kitu cho chote bora kuliko ambacho tayari wamekwisha toa kwetu. Je! yeye asiyeonekana mwenye mamlaka isiyoonekana juu ya adui hawa, yaani, Shetani Ibilisi, ana nini cha kuwapa wanadamu kupitia kwa ‘falme za ulimwengu’? Hakuna ila kupondwa kwao pamoja na Shetani mwenyewe chini ya miguu ya Kristo. Kwa utimizo wa kitabu cha Ufunuo, sura ya kumi na mbili, Shetani Ibilisi na malaika zake za kishetani tayari wamekwisha tupwa nje ya mbingu takatifu kwenye ujirani wa dunia yetu. Wanadamu wote wameona matokeo ya kuzuiwa huku kwa Nyoka Mkubwa Shetani na mashetani zake katika dunia yetu, tangu vita ya kwanza ya ulimwengu ya miaka ya 1914-1918. Kwa zaidi ya karne moja na nusu tangu wakati huo wanadamu wamepata kujua kwa huzuni nyingi maana ya makelele yaliyosikiwa mbinguni wakati wa kutupwa kwa Shetani na mashetani zake: “Shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”​—Ufu. 12:12.

3, 4. (a) Je! utawala wa kibinadamu umeweza kuiondoa hiyo “ole” duniani na baharini? (b) Ni kwa kadiri gani “ghadhabu nyingi” ya Shetani kwa utawala wa kimungu itakavyoendelea, na Yesu alielezaje kitakachomaanishwa na hili kwa wanadamu?

3 Utawala wa kibinadamu, hata ukiwa na vifaa vyote vya kisasa vya kisayansi na elimu zaidi, umeshindwa kuiondoa “ole” hii ya kiibilisi duniani na baharini. “Ghadhabu nyingi” ya Shetani Ibilisi kwa Utawala wa Kimungu itavielekeza vyama vya kisiasa vya utawala wa kibinadamu kwenye kuharibiwa kabisa. Ikiwa yeye mwenyewe hawezi kutawala juu ya dunia, basi anajitahidi ili cho chote cha vyama hivi vya utawala wa kibinadamu kisije kikasalimika. Katika jaribio la kujiua, sasa anauongoza utawala wote wa kisiasa wa kibinadamu kwenye uharibifu chini ya miguu ya Uzao Ulioahidiwa wa Mungu, Yesu Kristo. Hii itamaanisha wakati wa taabu ambayo mfano wake wakaaji wa dunia hawajapata kuuona. Yesu Kristo, alipokuwa akiutabiri “mwisho wa taratibu ya mambo,” alieleza hili, akisema:

4 “Ndipo itakapokuwako dhiki kubwa ambayo haijawahi kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, la, wala haitatukia tena. Kwa kweli, kama siku hizo hazikufupizwa, hakuna mwili ambao ungeokoka; lakini kwa ajili ya wateule siku hizo zitafupizwa.”​—Mt. 24:3, 21, 22, NW; Marko 13:19, 20.

5. (a) Mazingiwa ya kuogofya na uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka wa 70 C.E. vilikuwa mfano wa nini? (b) Dhiki itakayouangamiza ulimwengu itakujaje kweli kweli, na ni ulizo gani juu yake linalotokea?

5 Maogofyo ya mazingiwa na uharibifu wa mji wa Yerusalemu ulioharibiwa na Warumi mwaka wa 70 C.E. yalikuwa mfano tu wa kuogofya kwa dhiki inayokaribia ya dunia nzima ambayo kwayo Kristendomu na sehemu nyingine yote ya taratibu hii ya mambo ya kibinadamu itaharibiwa kabisa. Kama vile gharika iliyotabiriwa ya dunia nzima ilivyokuja siku za mhubiri mwenye haki Nuhu, na kama vile uharibifu uliotabiriwa wa Yerusalemu wa kale ulivyokuja kweli katika siku za manabii wa Yehova na za mitume wa Yesu Kristo, ndivyo na dhiki hii iliyotabiriwa itakayouangamiza ulimwengu itakavyokuja kweli​—katika kizazi chetu wenyewe. Kwa karibu miaka mia moja sasa mashahidi wa Yehova wa Kikristo wamekuwa wakiwaonya wanadamu wote juu ya msiba huu mkuu wa ulimwengu. Si kuhakikisha mambo ambayo wao wamekuwa wakihubiri ni ya kweli, bali, kuhakikisha neno la unabii la Yehova ambalo wamekuwa wakilihubiri ni la kweli. Hakuna ye yote kati ya wanadamu anayeweza kuiepuka; wanadamu wote wataingia katika dhiki hiyo kubwa kuliko zote. Ulizo ni, Ni nani kati ya wanadamu atakayeiokoka?

6. Ni njia gani ya kuokokea “dhiki kubwa” itakayoshindwa, na kwa hiyo tumaini la pekee la wanadamu wote liko wapi?

6 Hapana ye yote duniani atakayeweza kuokoka kwa nguvu zake mwenyewe wala kwa kinga zo zote za kibinadamu anazoweza kujitafutia. Kristendomu hatakuwa kimbilio wala wokovu kwa sababu ya kulipanga tu jina la Kristo na misalaba juu ya minara yake ya makanisa. Umoja wa Mataifa, unaoendelea kuitwa “tumaini la mwisho” la wanadamu, utashindwa kuwa hivyo. Matengenezo ya udugu wa nchi na ya mapatano ya mataifa ya kisiasa yatashindwa kuwachukua salama ama watawala wa kibinadamu ama wanadamu wanaotawaliwa katika “dhiki kubwa” isiyoweza kulinganishwa. Hakuna shauri lo lote la kibinadamu linaloweza kutumainiwa. Unabii wa Maandiko Matakatifu unaonya mapema juu ya hali hii ya kukatisha tamaa ya wanadamu wote. Kwa sababu ya hali hii ya kukatisha matumaini kabisa iliyoko mbele ya taratibu yote ya kibinadamu ya mambo, inakuwa wazi kwa kila mtu mwenye busara kwamba lazima tumaini la pekee kwa wanadamu wote liwe nje ya makao ya kibinadamu. Wokovu wa wanadamu haujapata na hautapata kutoka kwa wanadamu wenyewe, kana kwamba wanadamu wanaweza kujiokoa wenyewe. Kwa hiyo fundisho la kifilosofia la Kikomunisti la mambo ya kimwili, yaani, kwamba hakuna kinachoishi isipokuwa kinachoonekana, halielekezi po pote!

KWA KUGEUKIA KATIKA TUMAINI LA KWELI

7. (a) Tumaini letu linapaswa liwe katika makao gani, na ni nani asiyetiwa humo kama tumaini hilo? (b) Mtawala wa Kimungu anawaambia “wafungwa wa tumaini” warudie nini?

7 Ili tumaini letu litimizwe kwa furaha, inalipasa litegemee jambo la kiroho. Hapana, si “mungu wa taratibu hii ya mambo” aliye wa kiroho, Nyoka Mkubwa Shetani Ibilisi, mwovu anayeleta “ole” iliyopo kwa wanadamu. (2 Kor. 4:4, NW) Yeye ndiye kile kinachoitwa na mtume wa Kikristo Paulo “roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi,” wote ambao ‘wameifuata kawaida ya ulimwengu huu.’ (Efe. 2:2) Hapana, inatupasa sisi tunaotaka sana tumaini la kweli tuyaondoe macho yetu kwenye huyo “mkuu wa ulimwengu.” (Yohana 12:31) Inatupasa tuyaondoe macho yetu yenye shauku kwenye taratibu yake ya mambo inayofisha na kuleta ole. Inatupasa tutazame nini kilicho cha kiroho na kilicho juu zaidi kuliko mwanadamu na Ibilisi? Ni kitu gani cha pekee tunachoweza kugeukia kwa matumaini? Kwa maelfu ya miaka maneno ya Mtawala wa Kimungu yanasema: “Irudieni ngome, enyi wafungwa wa tumaini.”​—Zek. 9:12.

8. (a) Maneno hayo ya Zekaria 9:12 yalisemwa kwa nani kwanza, na “ngome” ilikuwa nini huko nyuma? (b) Iliwapasa “wafungwa wa tumaini” hao warudi kutoka wapi, na njia ya kwenye uhuru ilifunguliwaje?

8 Maneno hayo yenye kusisimua yaliyotolewa kupitia kwa nabii Zekaria karibu miaka elfu mbili na mia tano iliyopita yalisemwa kwa waliotamani kwa unyofu wa moyo kuwa watu waliokubaliwa wa Roho Kubwa, ambaye juu yake Yesu alisema: “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” (Yohana 4:24) “Ngome” ambayo “wafungwa wa tumaini” walipaswa ‘warudie’ ilikuwa ni ufalme wa Kimasihi wa Mungu, ambao huko nyuma ulifananishwa na mji wa Yerusalemu, ambapo mfalme wa jamaa ya kifalme ya Daudi wa Bethlehemu alikuwa akiketi juu ya kiti cha enzi kilichoitwa ‘kiti cha enzi cha Yehova.’ (1 Nya. (Sik.) 29:23) Iliwapasa “wafungwa wa tumaini” ‘waurudie’ mfano huu wa utawala wa kimungu, kwa kutoka katika uhamisho wao wa muda mrefu katika Babeli mpagani, mahali ambapo dini ya uongo ilitengenezwa kwa kumpinga Yehova Mungu siku za Nimrodi mwindaji mbaya. (Mwa. 10:8-10; 11:1-9) Katika wakati wa nabii Zekaria Babeli huyu alikuwa ameketi juu ya kiti cha utawala wa ulimwengu, kama mamlaka ya tatu ya ulimwengu ya historia ya Biblia. Katika mwaka wa 539 B.C.E. Mwenyezi Mungu aliuondoa mshiko wa Babeli, kwa “wafungwa” wake na kuifanya njia ya uhuru wazi!

9. (a) Kwa sababu gani hiyo si sehemu tu ya historia iliyokufa? (b) Ni akina nani “wafungwa wa tumaini” leo, na wanahitaji nini?

9 Lo! hiyo ni sehemu ya historia ya kusisimua katika wakati wenye giza uliopita! Lakini siyo historia iliyokufa. Ni historia ya unabii inayoishi kwa ajili ya leo na kwa ajili ya kupata mfano wake leo, katika kizazi chetu. Ndiyo sababu iliandikwa na kuhifadhiwa kati ya unabii wa Zekaria, mmojawapo wa manabii wa mwisho wa Yehova mbele ya Yesu Kristo. Kwa hiyo, basi, je! sisi leo twaweza kutiwa katika kundi la “wafungwa wa tumaini”? Ndiyo, tukiliona na kulikubali tumaini ambalo “Mungu wa tumaini” anatupatia sisi. Kitabu cha mwisho cha Maandiko Matakatifu yake, Ufunuo, kilielekeza kwenye kuwako kwa Babeli Mkuu, si Babeli wa kale, katika siku zetu. Babeli huyu mwenye nguvu zaidi anafananisha milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, ambayo ina ujamaa wa kidini na serikali za kisiasa za taratibu hii ya mambo, hata na Urusi Mkomunisti. Watu wote wa ulimwengu, wawe ni wazoeaji wa mamia ya dini au wanaoshikilia vyama vya kilimwengu vya kisiasa, ni “wafungwa” wa Babeli Mkuu na washiriki wake wa kisiasa. Imewapasa “wafungwa” hawa wawekwe huru, kwa wokovu wao!

10. (a) Kwa sababu gani ni jambo la haraka sana kwamba uhuru huu utukie? (b) Ni nini “ngome” leo ambayo “wafungwa” inawapasa wairudie, na Yehova ametuma nini kutoka huko tangu mwaka wa 1914 C.E.?

10 Hili limepaswa litukie haraka sana. Kwa sababu gani? Kwa kuwa Babeli Mkuu na hawara zake zote za kisiasa wamehukumiwa uharibifu wa mapema! Watu wanawezaje kuwekwa huru kutoka gereza lao la kiroho, ambapo hapana jingine la kutazamia ila uharibifu katika “dhiki kubwa” inayokuja? Kuna njia moja tu inayoelekeza kwenye kuwekwa huru, na hiyo ni kwa kuigeukia “ngome” ambayo Yehova Mungu amewasimamishia “wafungwa wa tumaini” wote. “Ngome” hiyo ndio ufalme wa Mungu wa Kimasihi, uliofananishwa kale katika mji wenye ngome wa Yerusalemu. Ufalme wa Kimasihi wa kidunia katika Yerusalemu ya Mashariki ya Kati ulikwisha zamani. Umerudishwa wakati wetu, si huko katika Yerusalemu wa kidunia, bali katika mbingu, ambapo Mzao mwenye fahari wa Mfalme Daudi ameketi, yaani, Yesu Kristo. Kiti chake cha enzi si kinachoonekana na kinachoweza kutoweka katika Yerusalemu wa kidunia, bali ni ‘kiti cha enzi cha Yehova’ kweli kweli, kwa kuwa yeye ameketi katika ‘mkono wa kuume’ wa Yehova Mungu katika mbingu. (Zab. 110:1, 2; Matendo 2:34-36; 7:55, 56; 1 Pet. 3:22; Ufu. 3:21) Kutoka huko tangu mwisho wa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914 Yehova ameituma ‘fimbo ya nguvu za Kristo.’

11. (a) Kwa hiyo, basi, tumaini la pekee la wanadamu wote ni nini? (b) Tangu mwaka wa 1918 C.E. mashahidi wa Yehova wa Kikristo ‘wamerudi’ wapi na kutoka wapi, na wanawaambiaje “wafungwa” wengine wote waigeukie “ngome” hiyo?

11 Ni chini ya miguu ya Kristo huyu na wafuasi wake waaminifu kwamba Yehova “atamseta Shetani” karibuni. (Rum. 16:20) Ufalme wa Mkombozi huyu wa Kimasihi ndiye mjumbe aliyeagizwa wa Utawala wa Kimungu wa Aliye Juu Zaidi na Mwenyezi Mungu, Yehova. Ndilo tumaini la pekee la wanadamu wote. Ndiyo ngome iliyowekwa kwa kimungu ya kugeukia kwa uhuru na uzima katika furaha isiyokoma. Tangu mwisho wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu katika mwaka wa 1918 mashahidi wa Yehova wa Kikristo wametoka katika kifungo chao cha kiroho katika Babeli Mkuu na ‘wakairudia ngome,’ kwenye ufalme wa Kimasihi wa Mungu uliosimamishwa katika Yerusalemu wa kimbinguni. Ijapokuwa hali zenye hatari za ulimwengu zinazozidi kuwa mbaya, sasa wanafurahia uhuru wao wa kiroho wa ajabu na wanafurahi katika tumaini lao la ajabu kwa wakati ujao ulio karibu. Kwa huruma nyingi kwa wanadamu wote wanapiga kelele kwa haraka kwa “wafungwa” wote kila mahali ‘wairudie ngome,’ wakiitimiza amri ya unabii ya Kristo: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakuja.”​—Mt. 24:14, NW.

​—Kutoka The Watchtower, Oct. 15, 1972.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki