Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w26 Aprili kur. 8-13
  • Sikuzote “Mungu wa Ukweli” Anatimiza Kusudi Lake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sikuzote “Mungu wa Ukweli” Anatimiza Kusudi Lake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2026
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KWA NINI TUNAWEZA KUMTUMAINI MUNGU WA UKWELI?
  • MUNGU WA UKWELI ANATIMIZA KUSUDI LAKE
  • MUNGU WA UKWELI ANAWAKUSANYA WATU WOTE WANAOPENDA UKWELI
  • TARAJIA WAKATI UJAO UKIWA NA UHAKIKA
  • Tafuta Majibu ya Maswali Haya
    Programu ya Kusanyiko la Mzunguko la 2025-2026 Lililo na Mwakilishi wa Ofisi ya Tawi
  • Uwe Mwenye Kiasi Inapohusu Mambo Usiyoyajua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Tafuta Majibu ya Maswali Haya
    Programu ya Kusanyiko la Mzunguko la 2025-2026 Lililo na Mwangalizi wa Mzunguko
  • Mtumaini Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2026
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2026
w26 Aprili kur. 8-13

JUNI 8-14, 2026

WIMBO 8 Yehova Ni Kimbilio Letu

Sikuzote “Mungu wa Ukweli” Anatimiza Kusudi Lake

“Umenikomboa, Ee Yehova, Mungu wa ukweli.”—ZAB. 31:5.

JAMBO KUU

Kuimarisha uhakika wetu kwamba Yehova atatimiza ahadi zake zote na kwamba hivi karibuni Ufalme utakomesha uwongo wote.

1. Kwa nini tunaweza kumtumaini Yehova? (Zaburi 31:​2-5)

TUNAISHI katika ulimwengu unaotawaliwa na Shetani. Uwongo, udanganyifu, na usaliti ni mambo ya kawaida. Inaweza kuwa vigumu kujua mtu wa kumtumaini. Wafanyabiashara hawatendi kwa unyoofu. Matangazo ya biashara hayasemi ukweli kuhusu bidhaa zinazotangazwa. Na wengine wametambua kwamba hawawezi kuwategemea marafiki wao wa karibu watimize ahadi zao. Hata hivyo, inafariji sana kujua kwamba sikuzote tunaweza kumtumaini Yehova! Yeye ni “Mungu wa ukweli.” (Soma Zaburi 31:​2-5.) Kusema ukweli ni sehemu ya utu wake—hawezi kamwe kusema uwongo. Yehova anategemeka katika kila jambo analosema na kutenda.

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Katika makala hii, tutazungumzia kwanza, kwa nini tunaweza kumtumaini Yehova kwa moyo wetu wote. Kisha, tutachunguza jinsi ambavyo Mungu wa ukweli ataleta mwisho wa ulimwengu mwovu wa Ibilisi na kile ambacho Mungu anafanya sasa ili kutimiza kusudi Lake. Kufanya hivyo, kutatusaidia kuwa Mashahidi wa Yehova wenye ujasiri na wasio na woga.

KWA NINI TUNAWEZA KUMTUMAINI MUNGU WA UKWELI?

3. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kabisa katika Yehova?

3 Tunaweza kumtumaini Yehova kwa sababu yeye ndiye Muumba. Yeye ndiye Muumba wa mbingu na dunia na Chanzo cha uhai wote. (Mwa. 1:1; Zab. 36:9; Ufu. 4:11) Yeye pia ni Mtegemezaji wa uhai. Aliumba mifumo inayofanya iwezekane kuwe na uhai duniani. Sikuzote yeye ndiye anayedhibiti kikamili ulimwengu wote. Hivyo, kwa uhakika tunaweza kumkabidhi Muumba wetu mwenye hekima na nguvu zote maisha yetu na wakati wetu ujao.

4. Tunajuaje kwamba Yehova anatupenda?

4 Tunaweza kumtumaini Yehova kwa sababu anatupenda. Yehova aliwaumba wanadamu kwa sababu alitaka kufurahia zawadi nzuri ya uhai pamoja nao. Yehova alieleza kusudi lake aliposema hivi: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kulingana na sura yetu.” (Mwa. 1:26) Alitupatia uhuru wa kuchagua. Aliiumba dunia iwe makao maridadi kwa ajili yetu. (Zab. 115:16) Naye aliwabariki wazazi wetu wa kwanza kwa kuwapa mgawo wenye kusisimua wa kuibadili dunia kuwa paradiso. (Mwa. 1:28; 2:15) Aliwapatia chakula cha kutosha, mimea na wanyama mbalimbali, na mambo mengine mengi ili wafurahie maisha. Kwa kweli, matendo hayo yanathibitisha kwamba “upendo mshikamanifu wa Yehova ni wa milele na milele.”—Zab. 103:17.

5. (a) Yehova alitimizaje ahadi yake licha ya jitihada za Ibilisi za kuiangamiza familia ya wanadamu? (b) Ni baadhi ya ahadi gani ambazo Mungu ametimiza? (Tazama sanduku “Rekodi ya Mungu ya Kusema Ukweli.”)

5 Tunaweza kumtumaini Yehova kwa sababu sikuzote anatimiza ahadi zake. Yehova hakuiumba tu dunia “bila sababu, lakini aliiumba ili ikaliwe.” (Isa. 45:​18, 19) Adamu na Hawa walipoasi, walihukumiwa kifo. Hivyo, ilionekana ni kana kwamba kusudi la Mungu lisingetimia. Lakini Yehova ni Mtimizaji wa ahadi zote anazotoa. (Isa. 46:​10, 11) Kusudi lake la kuijaza dunia na wanaume na wanawake waadilifu halikuathiriwa. Hiyo ndiyo sababu Yehova aliwaruhusu Adamu na Hawa wapate watoto. Pia, alimtoa Mwana Wake mzaliwa pekee kuwa fidia ili kuwakomboa wazao wa Adamu na kuwapatia tumaini zuri la kuishi milele.—Yoh. 3:16.

Rekodi ya Mungu ya Kusema Ukweli

Fikiria baadhi ya ahadi ambazo Yehova ametimiza:

  • Alimwahidi Musa kwamba Waisraeli wangeishi katika nchi yao wenyewe inayotiririka maziwa na asali.—Kut. 3:​6-8; Kum. 27:3.

  • Aliahidi kwamba Masihi angekuja na kuwaweka huru wanadamu kutokana na laana ya dhambi na kifo.—Isa. 53:​11, 12.

  • Aliahidi kwamba kungekuwa na kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ambayo ingewasaidia watu wamjue kabla ya mwisho kuja.—Mt. 24:14.

Je, unaweza kufikiria pindi nyingine ambazo Yehova ametimiza ahadi zake?

MUNGU WA UKWELI ANATIMIZA KUSUDI LAKE

6. Yehova alitabiri nini baada ya uasi katika bustani ya Edeni?

6 Aliyewachochea Adamu na Hawa wamwasi Mungu ni “yule nyoka wa zamani, anayeitwa Ibilisi na Shetani.”a (Ufu. 12:9; Mwa. 3:​4, 5; Yoh. 8:44) Yehova alitoa hukumu dhidi yake kwamba hatimaye angeangamizwa. (Mwa. 3:15) Kabla ya hilo kutokea, wengi wangemfuata Shetani na kutenda kama yeye. Hata hivyo, baadhi ya watu wangekuwa washikamanifu kwa Yehova.

7. Ni nani wanaomfuata Ibilisi, na mwisho wao utakuwaje?

7 Wale wanaomfuata Shetani Ibilisi ni malaika na wanadamu walioasi. Kwa kuwa wanapinga, au kukataa kusudi la Mungu, wanakuwa sehemu ya uzao wa Shetani. Lakini kwa wakati uliowekwa na Mungu, Shetani na wale wote wanaomfuata wataangamizwa.—Dan. 2:44; Rom. 16:20.

8. Yesu alichukua hatua gani mwaka wa 1914? (Tazama pia picha.)

8 Ni uthibitisho gani unaotupatia uhakika kwamba kusudi la Mungu la kumwangamiza Shetani na wafuasi wake waovu litatimizwa? Mwaka wa 1914, Yesu alianzisha vita dhidi ya Shetani Ibilisi na roho wake waovu na kuwatupa chini duniani. (Ufu. 12:​7-9) Ingawa pambano lenyewe lilitukia mbinguni, kwa hakika wale walio duniani waliathiriwa na pambano hilo. Biblia inasema hivi: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufu. 12:12) Tangu mwaka wa 1914, Shetani ameikazia fikira dunia, na matokeo ni kwamba hali ulimwenguni zimekuwa mbaya zaidi na zaidi. Kwa kweli, “ole wa dunia”! Hata hivyo, hivi karibuni Yesu ‘atakamilisha ushindi wake,’ na Shetani na wafuasi wake wataondolewa. (Ufu. 6:2) Yesu atalitetea jina la Yehova mara moja kwa wakati wote. (Zab. 45:​4-6) Kila mtu atajua kwamba Yehova ni Mungu wa ukweli!—Eze. 38:23.

Mkusanyo wa picha: Mambo yaliyotukia duniani tangu mwaka wa 1914. 1. Shetani akiwa joka mwenye vichwa saba anatupwa chini duniani. 2. Wanajeshi wenye silaha wakisubiri huku wakiwa wamelala kwenye mtaro wakati wa vita. 3. Wingu linalofanana na uyoga lililotokezwa na bomu. 4. Mama asiye na mahali pa kuishi akiwa ameketi barabarani huku akimbeba mtoto wake anayelia. 5. Mwanajeshi akilenga bunduki yake. 6. Mwanamume akitembea katika mji ulioharibiwa. 7. Kiwanda kinachotoa hewa inayochafua mazingira. 8. Watu wakitembea jijini huku wamevaa barakoa. 9. Waandamanaji wakipambana na kikundi cha polisi.

World War I: U.S. National Archives photo; bomb: USAF photo; pandemic: blvdone/stock.adobe.com; riot: inhauscreative/E+ via Getty Images

Tangu mwaka wa 1914, hali ulimwenguni zimezidi kuwa mbaya (Tazama fungu la 8)


MUNGU WA UKWELI ANAWAKUSANYA WATU WOTE WANAOPENDA UKWELI

9. Yehova anawakusanya akina nani leo?

9 Wakati huohuo, Yehova anakusanya “pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” (Efe. 1:10) “Vitu vilivyo mbinguni” vinarejelea watiwa-mafuta ambao Yehova amewachagua watawale pamoja na Kristo mbinguni. “Vitu vilivyo duniani” vinarejelea wale watakaoishi milele katika Paradiso duniani. Waabudu hao wote wa Yehova wanashiriki kwa bidii katika kazi ya kufunua uwongo wa Shetani na kuwasaidia wenye mioyo minyoofu wajifunze ukweli kumhusu Yehova.

10. Yehova anawawekaje watu huru kutokana na udanganyifu wa dini za uwongo? (Ufunuo 14:​6, 7)

10 Kupitia kazi kubwa zaidi kuwahi kufanywa ulimwenguni ya kutoa ushahidi, Yehova anawakusanya wanaopenda ukweli. (Soma Ufunuo 14:​6, 7.) Ingawa Yehova anawatumia wanadamu kuwaambia wengine kuhusu habari njema, malaika wanahusika katika kuwakusanya watu wenye mioyo minyoofu kwenye kutaniko la Kikristo. Kazi hii ya kutoa ushahidi inafunua uwongo unaofundishwa na Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo, ambazo Ibilisi amezitumia kwa karne nyingi kusambaza uwongo kumhusu Yehova. (Ufu. 18:​2, 4) Hivi karibuni, dini zote za uwongo zitaangamizwa kabisa, na wale wote wanaompenda Mungu wa ukweli watampa utukufu anaostahili kabisa.—Ufu. 17:16.

11. Tunawezaje kuwatambua waabudu wa kweli wa Yehova?

11 Watu wanaopenda ukweli wanatoka katika jamii, tamaduni, hali mbalimbali za kiuchumi, na katika mataifa yote. (Ufu. 7:​9, 10) Waliposikia “habari njema,” waliutambua ukweli na kwa furaha wakajiunga na watu wa Yehova. (Marko 13:10) Kadiri muda unavyopita, imekuwa wazi zaidi na zaidi ni nani wanaomwabudu Mungu kwa njia inayokubalika na ni nani ambao hawafanyi hivyo. Nabii Malaki alitabiri hivi: “Mtaona tena tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu, kati ya yule anayemtumikia Mungu na yule asiyemtumikia.” (Mal. 3:18) Kupitia mwenendo na kazi yao ya kuhubiri, watumishi wa Yehova wameonyesha kwamba wanamwabudu Mungu wa ukweli.

12. Kazi ya kuhubiri inasaidiaje kutimiza kusudi la Yehova?

12 Kwa kuhubiri “habari njema ya Ufalme,” tunatii amri ya Yesu, na wakati uleule tunatimiza unabii. (Mt. 24:14; 28:​18-20) Na kwa sababu ya kazi hiyo, watu ulimwenguni pote wanakuwa wanafunzi wa Kristo wakiwa na tumaini la kumwabudu Mungu wa ukweli milele. Ni pendeleo lililoje kushiriki katika kutimiza kusudi la Yehova!

TARAJIA WAKATI UJAO UKIWA NA UHAKIKA

13. Shetani anawashambulia nani kihususa, na kwa nini?

13 Shetani Ibilisi ana hasira kali kwa sababu anajua kwamba “ana kipindi kifupi cha wakati” kabla ya ulimwengu wake kuharibiwa. (Ufu. 12:​12, 13) Anawashambulia kihususa wawakilishi wa Ufalme wa Mungu walio duniani, “wanaoshika amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufu. 12:17; 14:12) Shetani humshambulia pia mtu yeyote anayewaunga mkono wawakilishi hao na kazi wanayofanya.

14. Ni nini kitakachotukia Shetani atakapowashambulia watu wa Yehova? (Tazama pia picha.)

14 Baada ya kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa, wanaomuunga mkono Shetani watajaribu kuwaangamiza watu wote wa Yehova. Shambulizi hilo litaongoza kwenye vita vya Har–​Magedoni. (Ufu. 16:​13, 14, 16) Yesu na majeshi ya mbinguni watawaokoa waabudu wa Yehova na kuangamiza kabisa kila sehemu ya ulimwengu wa Ibilisi. (Ufu. 19:​19-21) Waongo, watu waovu, na wapanga njama za udanganyifu, wote hawatakuwapo tena. (Ufu. 21:8) Mungu wa ukweli na mwadilifu atakuwa ametetewa kikweli.

Yesu na jeshi lake la mbinguni wakiwa juu ya farasi weupe, wanawashambulia wanajeshi wenye silaha walio duniani. Yesu analenga upinde wake, na malaika wengine wameinua upanga wao.

Yesu na jeshi lake la mbinguni wakipanda kuelekea katika vita vya ­Har–​Magedoni ili kuwaangamiza maadui wa Mungu (Tazama fungu la 14)


15. Kwa nini tunaweza kutarajia wakati ujao tukiwa na uhakika? (Isaya 65:​16, 17) (Tazama pia picha.)

15 Leo, kuliko wakati mwingine wowote, watu ulimwenguni wamegawanyika. Lakini kwa msaada wa Yehova, watumishi wake wanaendelea kuwa na umoja. Kazi ya kuwakusanya watu tayari inaendelea. Hakuna kitu chochote kitakachomzuia Yehova kuwabariki watu wake na kazi wanayofanya. (Soma Isaya 65:​16, 17.) Tunautarajia wakati ujao tukiwa na uhakika. Maneno ya mtume Paulo kwenye Waroma 8:​38, 39 yanatuhakikishia hivi: “Wala kifo wala uzima wala malaika wala serikali wala mambo yaliyopo sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala uumbaji mwingine wowote havitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

Wazazi wakiwa wameketi kwa furaha pamoja na mwana na binti yao kwenye baraza wakitazama bonde maridadi. Karibu nao kuna kifaru anayekula majani.

Katika ulimwengu mpya, matatizo tunayokabili leo hayataingia tena akilini (Tazama fungu la 15)


16. Kwa nini unamtumaini Yehova kwa moyo wako wote?

16 Tuna kila sababu ya kumtumaini Yehova, Mungu wa ukweli. Yeye ni Muumba wetu. Na anatupenda sana. Umati mkubwa unaongezeka kwa kasi, kadiri watu kutoka katika mataifa yote wanavyokuja kumwabudu Yehova. (Isa. 60:22; Zek. 8:23) Tunajua kwamba sikuzote anatimiza kusudi lake na kwamba hivi karibuni atakomesha uwongo na udanganyifu wa Shetani. Tunasali hivi kama Daudi: “Na asifiwe Yehova Mungu, . . . ambaye peke yake hutenda mambo yanayostaajabisha. Jina lake tukufu na lisifiwe milele, na utukufu wake ujae duniani pote.”—Zab. 72:​18, 19.

UNGEJIBUJE?

  • Kwa nini tunaweza kumtumaini “Mungu wa ukweli”?

  • Yehova atakomeshaje ulimwengu wa Ibilisi, na anafanya nini ili kutimiza kusudi Lake?

  • Kwa nini tunaweza kutarajia wakati ujao tukiwa na uhakika?

WIMBO 2 Jina Lako Ni Yehova

a Malaika huyo wa zamani hatambulishwi kwa jina la kibinafsi. Anafafanuliwa tu kwa maneno kama “Ibilisi” [Mchongezi] na “Shetani” [Mpinzani].

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki