Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w26 Aprili kur. 2-7
  • Yehova Amenizoeza Tangu Nilipokuwa Kijana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Amenizoeza Tangu Nilipokuwa Kijana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2026
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NAENDELEA KUZOEZWA
  • UPAINIA WANIPATIA SHANGWE
  • NAELEKEA SENEGAL
  • TUNAFANYA UPAINIA HUKO NEW BRUNSWICK NA QUEBEC
  • TUNAWAKUMBUKA WALE WALIOFANYA KAZI KWA BIDII SANA
  • MAMBO NILIYOJIFUNZA KUTOKA KWA NDUGU WAAMINIFU
  • TUNAHAMIA MAREKANI
  • Kujifunza Kutokana na Mifano Mizuri Kuliniletea Baraka Nyingi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • Sisi Tuligeukia Chanzo cha Uadilifu wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Upendezi wa Kibinafsi Huleta Baraka Maishani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Kuwazoeza Wahudumu wa Ufalme
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2026
w26 Aprili kur. 2-7
Ndugu David Splane akifanya kazi kwenye meza yake.

SIMULIZI LA MAISHA

Yehova Amenizoeza Tangu Nilipokuwa Kijana

LIMESIMULIWA NA DAVID SPLANE

NILITAZAMA kwa mshangao karatasi ambayo nilikuwa nimetoka tu kupewa na ndugu. Karatasi hiyo ilikuwa imeandikwa, “David Splane, Aprili 8, 1953: ‘Kutangaza Mwisho wa Dunia.’” Nikamuuliza hivi: “Hii ni nini?” Ndugu akajibu, “Huu ni mgawo wako wa kutoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.”a Nikamjibu hivi: “Lakini mimi sijajiandikisha!”

Lakini kabla sijaendelea, acheni nianze mwanzo. Nilizaliwa katika jiji la Calgary, Kanada, wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Mwishoni mwa miaka ya 1940, painia kijana anayeitwa Donald Fraser, alipiga hodi mlangoni kwetu na Mama akakubali kujifunza Biblia. Aliipenda sana kweli, lakini matatizo makubwa ya afya yalimzuia kuwa na utendaji mwingi kutanikoni. Hata hivyo, alifanya maendeleo na kubatizwa mwaka wa 1950. Inasikitisha kwamba haikupita miaka miwili naye akafa. Baba yangu hakuwa mwamini wakati huo, lakini aliwaruhusu Mashahidi wasimamie mazishi ya mama yangu.

Siku chache baada ya mazishi, dada mwenye umri mkubwa anayeitwa Alice, ambaye alikuwa mtiwa-mafuta, alinialika nihudhurie mkutano wa kutaniko. Alinifahamu kwa sababu nilikuwa nikihudhuria mikutano ya mwisho juma pamoja na mama yangu, afya yake ilipomruhusu kuhudhuria. Nilimwomba baba yangu ikiwa ninaweza kwenda. Alikubali na akaamua kwenda pamoja nami “mara moja” tu ili amshukuru ndugu ambaye alikuwa ametoa hotuba ya mazishi ya mama yangu. Usiku huo, kulikuwa na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Mkutano huo wa kwanza kwa baba yangu kuhudhuria ulimfaa kabisa. Alikuwa amejifunza masomo ya jinsi ya kuzungumza mbele za watu na alipendezwa na mambo aliyosikia katika mkutano huo. Baba yangu aliamua kwamba atahudhuria mkutano huo kila juma. Baada ya muda akaanza kuhudhuria mikutano mingine.

Siku hizo, mtumishi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi angeanza mkutano kwa kusoma majina ya akina ndugu walioandikishwa, na kila mmoja wao angejibu “Nipo.” Usiku mmoja tukiwa mkutanoni, niliomba jina langu lisomwe katika mkutano unaofuata. Ndugu alinipongeza lakini hakuniuliza ikiwa nilielewa mambo yanayohusika.

Sikujua kwamba nilikuwa nikijitolea kutoa hotuba katika shule—nilitaka tu jina langu lisomwe! Juma lililofuata, jina langu liliitwa na kwa furaha nilijibu, “Nipo.” Baada ya mkutano, akina ndugu na dada walinipongeza. Majuma kadhaa baadaye, nilipewa mgawo wa kutoa hotuba niliyotaja mwanzoni mwa makala hii.

Nilikuwa na wasiwasi! Wakati huo, wanafunzi walitazamiwa kutayarisha hotuba yenye urefu wa dakika sita hadi nane. Hakukuwa na mgawo wa kusoma tu Biblia. Baba yangu alinisaidia kutayarisha hotuba hiyo na kunifanyisha mazoezi mara 20 kabla ya kuitoa. Baada ya hotuba, ndugu alinipatia shauri lililonifaa sana. Kwa miaka mingi, Yehova amenizoeza kupitia baba yangu, ndugu na dada wenye uwezo mzuri, na tengenezo Lake.

NAENDELEA KUZOEZWA

Alice, dada niliyemtaja awali, alinizoeza nilipoanza kuhubiri. Katika siku hizo, tulitiwa moyo kusoma pamoja na mwenye nyumba maandiko matatu, kisha kumpatia kitabu. Zamu yangu ya kuzungumza mlangoni ilipofika, Alice angejitambulisha, angeanzisha mazungumzo, kisha angeniomba nisome andiko la kwanza. Halafu, ningeendeleza mazungumzo, ningesoma andiko la pili na la tatu na kutoa chapisho. Baadaye, nilijifunza jinsi ya kuanzisha mazungumzo. Baba yangu alipobatizwa mwishoni mwa mwaka wa 1954, aliendelea kunizoeza kuhubiri. Akiwa mzazi aliye peke yake, alifanya yote aliyoweza ili kunilea katika kweli. Alichukua kwa uzito sana utendaji wa kitheokrasi. Sikuzote nilijua mambo ambayo tungefanya katika usiku tuliokuwa na mkutano, na Jumamosi na Jumapili asubuhi.

Shuleni nilikuwa mwanafunzi wa kawaida; hata hivyo baadhi ya mazoezi niliyopata kwa miaka 12 shuleni yameninufaisha maishani. Kwa mfano, nilijifunza jinsi ya kujumlisha safu ndefu za takwimu. Nilipata pia mazoezi mazuri ya sarufi katika lugha ya Kiingereza. Mafunzo niliyopata ya lugha ya Kiingereza na uandishi, yamenisaidia sana katika mgawo wangu wa sasa kwenye Idara ya Uandikaji.

Mara nyingi watu huniuliza kwa nini ninapenda muziki. Wazazi wangu walipenda muziki. Kwa muda fulani nilipokuwa na umri wa miaka saba, nilijifunza kupiga piano, lakini mwalimu wangu hakufurahishwa na uwezo wangu. Alipendekeza kwa baba yangu niache kujifunza. Ninaelewa kwa nini alisema hivyo—wakati huo sikupenda sana masomo hayo.

Miezi michache baadaye, baba yangu alinitafutia mwalimu mwingine. Wakati huu, nilijifunza kucheza piano na kuimba, na nilifanya vizuri. Nilipokuwa mvulana niliimba sauti ya soprano, nilikuwa na sauti nzuri na nilishinda kwenye baadhi ya mashindano. Lengo langu la kujifunza muziki lilikuwa kupata shahada ambayo ingeniruhusu kufundisha muziki ili niweze kujitegemeza katika utumishi wa wakati wote. Hata hivyo, kadiri nilivyoendelea na masomo yangu, nilitambua kwamba ningehitaji kutumia muda mwingi kujitayarisha kwa ajili ya mitihani kwa kusoma kuhusu upatano wa sauti, historia ya muziki, na utunzi. Hivyo, nilisitisha masomo yangu na kuanza upainia wa kawaida. Huo ulikuwa mwaka wa 1963.

UPAINIA WANIPATIA SHANGWE

Baada ya kufanya upainia kwa mwaka mmoja, nilipata mgawo wa upainia wa pekee katika mji wa Kapuskasing, Ontario. Mwandamani wangu katika utumishi wa upainia, Daniel Skinner, alikuwa na umri ulio mara mbili ya umri wangu. Alinifundisha mambo mengi kuhusu utendaji wa kutaniko. Nilipokuwa na umri wa miaka 20, niliwekwa rasmi kutumikia katika Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, hivyo nilihitaji kujifunza mambo mengi. Nimefurahi sana kwamba kwa mara nyingine tengenezo linasisitiza umuhimu wa kuwazoeza ndugu vijana. Ikiwa watatumia kwa bidii mazoezi hayo, wanaweza kutumiwa na Yehova hata wakiwa na umri mdogo sana!

Maisha jijini Kapuskasing yalikuwa na changamoto zake. Wakati wa majira ya baridi, kulikuwa na hali ya hewa ya kiwango cha nyuzi 44 selsiasi chini ya sifuri, au nyakati nyingine “joto lingeongezeka kidogo” hadi nyuzi 33 selsiasi chini ya sifuri. Mimi na Dan tulitembea kila mahali kwa miguu. Hata hivyo, mojawapo kati ya shangwe nilizopata katika mgawo huo ni kukutana na dada anayeitwa Linda Cole, ambaye baadaye alikuja kuwa Linda Splane.

Linda alikuwa mhubiri mwenye bidii aliyekuwa na ziara nyingi nzuri za kurudia. Alikuwa mkarimu, mwenye urafiki, na mchangamfu. Goldie, mama yake, alikuwa dada mwaminifu. Mwanzoni, Allen, baba yake, aliipinga kweli. Licha ya upinzani wa Allen, Goldie alikuwa na kawaida ya kuja katika Jumba la Ufalme pamoja na Linda na ndugu zake, John na Gordon, na aliwazoeza katika utumishi wa shambani. Katika pindi moja au nyingine, Goldie, Linda, John, na Gordon walitumikia wakiwa mapainia. Miaka mingi baadaye, Allen alikubali kweli na kuwa na mengi ya kufanya kutanikoni.

Mwaka wa 1965, nilialikwa kwa mwezi mmoja kuhudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme kwenye Betheli ya Kanada ili kupata mazoezi zaidi. Nilipokuwa shuleni, nilipewa fomu ya mwaliko wa Shule ya Gileadi. Sikuwahi kamwe kufikiria kufanya kazi ya umishonari―nilihisi kwamba sistahili―hata hivyo nilijaza fomu hiyo. Nilialikwa kwenye darasa la 42. Tukiwa Gileadi, walimu wetu walikuwa na kawaida ya kutupatia ripoti ya maendeleo yetu. Ripoti yangu ya kwanza niliyopokea ilinitia moyo kwamba nikiwa shuleni nijifunze kila kitu ninachoweza kuhusu tengenezo. Nilikuwa na umri wa miaka 21 tu, hivyo shauri hilo lilinifaa sana.

Kati ya masomo tuliyojifunza Gileadi ni kuhusu jinsi ya kushughulika na vyombo vya habari: vituo vya redio, televisheni, na magazeti. Nilifurahia sana kujifunza jambo hilo. Sikutambua wakati huo jinsi ambavyo masomo hayo yangenisaidia wakati ujao, kama ambavyo nitawaeleza.

NAELEKEA SENEGAL

Siku chache baada ya kuhitimu, mimi na Michael Höhle, mwandamani wangu katika mgawo wa umishonari, tulianza safari kuelekea kwenye mgawo wetu mpya nchini Senegal, barani Afrika. Wakati huo, kulikuwa na wahubiri 100 hivi nchini.

Baada ya kuwa katika mgawo wangu kwa miezi kadhaa, nilialikwa kufanya kazi katika ofisi ya tawi siku moja kwa juma. “Ofisi hiyo ya tawi” ilikuwa chumba kimoja katika nyumba ya wamishonari. Licha ya ofisi hiyo kuwa ndogo, Emmanuel Paterakis, mtumishi wa ofisi ya tawi, aliendelea kunikumbusha kwamba ofisi hiyo ya tawi ilikuwa inawakilisha tengenezo la Yehova katika nchi hiyo. Pindi moja, Ndugu Paterakis aliamua kwamba tunapaswa kuandika barua ya kuwatia moyo wamishonari wote. Siku hizo, hakukuwa na njia rahisi au ya bei nafuu ya kutokeza nakala za barua, hivyo kila nakala iliandikwa kwa kutumia taipureta. Ilikuwa kazi ngumu sana, hasa kwa sababu makosa hayakuruhusiwa—kamwe!

Nilipokuwa nikijitayarisha jioni hiyo kurudi katika nyumba yetu ya wamishonari, Ndugu Paterakis alinipatia bahasha. Kisha akasema: “David, tengenezo limekuandikia barua.” Baadaye, nilipofungua bahasha hiyo, nilikuta mojawapo ya barua nilizochapa! Kisa hicho kilinifundisha kuliheshimu tengenezo bila kujali ikiwa ofisi ya tawi ni kubwa au ndogo.

Ndugu Splane na kikundi cha ndugu na dada wenye shangwe wakitabasamu wanapopigwa picha.

Pamoja na wamishonari wenzangu nchini Senegal, 1967

Nilipata marafiki wengi katika kutaniko na mara nyingi siku ya Jumamosi jioni, nilitumia wakati pamoja na familia hizo. Nilifurahia sana pindi hizo! Bado ninawasiliana nao. Na nimeweza kutumia ujuzi wangu wa lugha ya Kifaransa ninapotembelea ofisi za tawi ulimwenguni.

Mwaka wa 1968, mimi na Linda tulichumbiana. Kwa miezi kadhaa, nilijaribu kutafuta kazi ya muda ili mimi na Linda tuweze kufanya upainia pamoja nchini Senegal, lakini waajiri nchini humo walitarajiwa kuajiri wenyeji badala ya wageni. Mwishowe, niliporudi nchini Kanada, tulifunga ndoa na kupata mgawo wa upainia wa pekee katika jiji dogo la Edmundston, New Brunswick, lililo mpakani na jimbo la Quebec.

David na Linda Splane wakitabasamu huku wakiwa wamesimama kwenye eneo lenye maua mengi.

Siku tuliyofunga ndoa, 1969

TUNAFANYA UPAINIA HUKO NEW BRUNSWICK NA QUEBEC

Katika mji huo, hakukuwa na wahubiri na kulikuwa na wanafunzi wachache wa Biblia. Dini ya Kikatoliki iliongoza karibu kila sehemu ya maisha ya watu. Karibu kila nyumba ilikuwa na tangazo lililosema Mashahidi wa Yehova Hawaruhusiwi. Wakati huo, wazo la kuheshimu tangazo hilo halikukaziwa kama ilivyo sasa, hivyo tulihubiri kila nyumba iwe kuna tangazo hilo au la. Kila juma, shirika fulani la Wakatoliki lilitoa tangazo hili katika gazeti: “Twendeni tukawatafute na kuwaondoa Mashahidi wa Yehova.” Kulikuwa na Mashahidi wanne wa Yehova katika mji huo—Victor na Velda Norberg na mimi na Linda—hivyo tulijua kabisa kwamba walimaanisha sisi!

Siwezi kusahau kamwe ziara ya kwanza ya mwangalizi wa mzunguko. Baada ya kuwa pamoja nasi kwa juma moja, alisema hivi: “Huenda jambo pekee mnaloweza kutarajia kutimiza mkiwa hapa ni kubadili maoni ya watu kuhusu Mashahidi.” Kuanzia siku hiyo na kuendelea, hilo likawa lengo letu, na tulifanikiwa! Pole kwa pole, watu walianza kuona tofauti kati ya Mashahidi wa Yehova waliokuwa wanyenyekevu na makasisi Wakatoliki wenye kiburi. Leo, kuna kutaniko dogo katika jiji hilo.

Baada ya kutumikia kwa mwaka mmoja katika eneo hilo la mbali, tulipewa mgawo wa kutumikia katika kutaniko kubwa lililo Quebec City. Tulishirikiana vizuri kwa miezi sita na ndugu na dada wakarimu katika kutaniko hilo kabla ya kuanza kazi ya kuzungukia makutaniko.

Kwa miaka 14 iliyofuata, tulitumikia katika mizunguko iliyo kwenye jimbo la Quebec. Zilikuwa pindi zenye kusisimua sana! Kazi huko Quebec ilikuwa ikisonga kwa kasi, na lilikuwa jambo la kawaida kuona familia kadhaa katika kutaniko lilelile zikifanya maendeleo na kubatizwa!

TUNAWAKUMBUKA WALE WALIOFANYA KAZI KWA BIDII SANA

Ni rahisi kuwapenda ndugu na dada Wakanada wenye asili ya Kifaransa. Wao huzungumza mambo waziwazi, ni wenye shangwe, na shauku. Hata hivyo, haikuwa rahisi sikuzote kwao kuikubali kweli, na familia zao zingeweza kuwapinga vikali. Baadhi ya vijana wadogo waliambiwa hivi na wazazi wao wasio waamini, “Acha kujifunza na Mashahidi wa Yehova au uondoke nyumbani!” Hata hivyo, wameendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova licha ya upinzani. Ni lazima Yehova anajivunia sana vijana hao!

Ningependa pia kutaja kikundi cha pekee cha mapainia wa kawaida na mapainia wa pekee waliotumikia huko miaka hiyo. Wengi wao walitoka katika maeneo mengine nchini Kanada. Zaidi ya kujifunza lugha ya Kifaransa, walihitaji kujifunza kuhusu tamaduni na njia ya kufikiri ya wenyeji, ambayo kwa sehemu kubwa iliathiriwa na dini ya Kikatoliki.

Mara nyingi, mapainia wa pekee walipewa mgawo wa kutumikia katika maeneo ya mbali ambapo hakukuwa na wahubiri. Kwa sababu ya ubaguzi katika maeneo hayo, haikuwa rahisi kupata mahali pa kuishi na ilikuwa vigumu hata zaidi kupata kazi ya muda. Hata wenzi wapya wa ndoa waliishi na wengine katika vikundi vya watu wanne, sita, au wanane ili waweze kuchangia pamoja gharama za kodi. Wasingeweza kumudu gharama ikiwa wangeishi wenyewe. Mapainia hao walikuwa wafanyakazi wenye bidii. Walipoanza kujifunza Biblia na mtu, walifanya yote wawezayo ili kumsaidia. Kwa kuwa sasa eneo la Quebec lina wahubiri wa kutosha, mapainia hao wengi wameenda kutumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa.

Tulipokuwa katika kazi ya kuzungukia makutaniko, Jumamosi asubuhi tulikuwa na kawaida ya kuhubiri pamoja na matineja. Hilo lilitusaidia kujua kutoka kwao changamoto wanazokabili. Baadhi ya matineja tuliohubiri nao, sasa wanatumikia katika nchi za kigeni wakiwa wamishonari au katika migawo mingine.

Katika siku hizo, baadhi ya makutaniko hayakuweza kuturudishia gharama za usafiri, hivyo pindi fulani tuliishiwa na pesa kufikia mwisho wa mwezi. Katika pindi hizo, tulihitaji kumtegemea kabisa Yehova, kwa kuwa yeye tu ndiye aliyeelewa hali zetu. Sikuzote alitutegemeza. Kwa njia moja au nyingine, sikuzote tuliweza kusafiri kutoka kutaniko moja kwenda lingine.

MAMBO NILIYOJIFUNZA KUTOKA KWA NDUGU WAAMINIFU

Nilitaja awali kuhusu jinsi nilivyonufaika na masomo katika Shule ya Gileadi ya jinsi ya kushughulika na vyombo vya habari. Wakati huo katika jiji la Quebec, tulikuwa na fursa nyingi za kutoa ushahidi mzuri katika redio, televisheni, na magazeti. Mara nyingi nilipewa mgawo wa kufanya kazi na Léonce Crépeault, mwangalizi mwenzangu wa mzunguko aliyefahamu vizuri jinsi ya kushughulika na vyombo vya habari. Tulipokutana na mkurugenzi fulani wa muhimu katika shirika la habari, badala ya kujaribu kujionyesha kwamba anajua mambo mengi, angesema hivi: “Bwana, mimi na mwenzangu ni wahudumu tu wa kidini. Hatujui mengi kuhusu jinsi ya kuzungumza katika televisheni na redio. Hata hivyo, tumepewa kazi ya kuwaeleza watu kuhusu kusanyiko kubwa ambalo Mashahidi wa Yehova watafanya. Tutathamini sana msaada wowote utakaotupatia.” Njia hiyo ya kuzungumza kwa unyenyekevu ilifungua milango mingi ambayo huenda isingefunguliwa.

Baadaye, ofisi ya tawi ilinipatia mgawo wa kufanya kazi pamoja na Ndugu Glen How, mmoja kati ya wanasheria wetu, katika kesi ngumu ambazo zingeweza kuzungumziwa sana katika vyombo vya habari. Nilinufaika kutokana na mazoezi niliyopata katika Shule ya Gileadi na uzoefu niliopata kwa kufanya kazi na Léonce. Lilikuwa pendeleo kubwa kufanya kazi na Ndugu How. Hakuogopa hata kidogo aliposhughulika na mfumo wa kisheria, lakini zaidi ya yote, alikuwa mtu wa Mungu. Alimpenda sana Yehova.

Katika mwaka wa 1985, tulipewa mgawo katika mzunguko ulio karibu na nyumba ya baba yangu, magharibi mwa Kanada, jambo lililotuwezesha kumpatia msaada aliohitaji. Baada ya miezi mitatu alikufa. Tuliendelea na kazi ya kuzungukia makutaniko magharibi mwa Kanada hadi mwaka wa 1989 tuliposhangazwa na mwaliko wa kujiunga na familia ya Betheli ya Marekani. Hilo lilimaanisha kuacha kazi ya kuzungukia makutaniko baada ya kuifanya kwa karibu miaka 19. Katika miaka hiyo yote, tuliishi katika mamia ya nyumba na kushiriki chakula na ndugu na dada wakarimu. Tunawashukuru sana wote waliotukaribisha katika nyumba zao na kushiriki vyakula vyao pamoja nasi!

TUNAHAMIA MAREKANI

Tulipowasili Brooklyn, nilipewa mgawo katika Idara ya Utumishi. Sikuzote ninathamini mazoezi niliyopata huko. Mojawapo ya mambo niliyojifunza ni kuhakikisha kila jambo na kutokisia jambo lolote. Kisha mwaka wa 1998, nilipewa mgawo katika Idara ya Uandikaji, ambapo bado ninajifunza uandishi. Kwa miaka kadhaa, nilipata pendeleo la kumsaidia Ndugu John Barr, ambaye alikuwa mratibu wa Halmashauri ya Uandikaji. Sikuzote nitakumbuka kwa uthamini mazoezi niliyopata na wakati niliotumia pamoja naye. Alikuwa na utu mzuri wa Kikristo.

David na Linda Splane wakipiga picha pamoja na John na Mildred Barr.

Pamoja na John na Mildred Barr

Ninafurahia sana kufanya kazi bega kwa bega na ndugu na dada wanyenyekevu wanaotumikia katika Idara ya Uandikaji. Sikuzote wanamwomba Yehova awasaidie katika mgawo wao na wanatambua kikamili kwamba jambo lolote zuri wanalotimiza ni kwa sababu ya roho ya Yehova, na si kwa sababu ya uwezo wowote wa asili ambao huenda wanao.

Ndugu Splane akiongoza kikundi cha waimbaji cha Watchtower chenye ndugu na dada 20 huku dada akipiga piano.

Nikiongoza kikundi cha waimbaji cha Watchtower kwenye mkutano wa kila mwaka wa 2009

Ndugu Splane akimpatia dada mmoja Biblia kwa shangwe.

Nikigawa Biblia katika kusanyiko la kimataifa la 2014 jijini Seoul, Korea

Na limekuwa pendeleo kwa mimi na Linda kuwatembelea waabudu wenzetu waaminifu katika nchi 110. Tumejionea moja kwa moja upendo kutoka kwa wamishonari, washiriki wa Halmashauri za Tawi, na watumishi wengine wa wakati wote. Ilikuwa baraka kubwa kujionea bidii na uthabiti wa wahubiri, ambao wametanguliza Ufalme licha ya vita, hali ngumu za kiuchumi, na mateso. Bila shaka Yehova anawapenda sana!

Kwa miaka hiyo yote, Linda amekuwa msaada mkubwa kwangu ninapojitahidi kutimiza migawo yangu. Anawapenda watu na sikuzote anatafuta njia za kuwasaidia wengine. Pia, ana ustadi wa kuanzisha mazungumzo yasiyo rasmi. Amekuwa na matokeo mazuri ya kuwasaidia watu waikubali kweli, kutia ndani kuwasaidia wahubiri ambao waliacha kutenda. Kwa kweli, Linda ni zawadi kutoka kwa Yehova! Kadiri umri unavyosonga, tunathamini sana utegemezo tunaopata kutoka kwa ndugu na dada vijana wanaotusaidia katika safari zetu na inapohusu mahitaji mengine.—Marko 10:​29, 30.

Ninapokumbuka miaka hiyo 80 iliyopita, ninashukuru sana. Ninakubaliana na maneno ya mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Ee Mungu, umenifundisha tangu nilipokuwa kijana, na mpaka sasa ninaendelea kutangaza kazi zako zinazostaajabisha.” (Zab. 71:17) Nimeazimia kuendelea kufanya hivyo kwa maisha yangu yote.

a Leo, mazoezi hayo ni sehemu ya mkutano wetu wa katikati ya juma.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki