JUNI 15-21, 2026
WIMBO 122 Iweni Imara, Thabiti!
Dumisha Mtazamo Unaofaa Kuelekea Majaribu
“Hata nikipatwa na taabu na shida, nitaendelea kuzipenda sana amri zako.”—ZAB. 119:143.
JAMBO KUU
Kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea majaribu kunaweza kutusaidia kukabiliana nayo kwa mafanikio.
1-2. Tunahitaji kufanya nini ili tukabiliane na majaribu yetu kwa mafanikio? (Tazama pia picha.)
JE, KWA sasa unakabiliana na ukosefu wa haki, upinzani katika familia, au mateso kwa sababu ya imani yako? Je, una matatizo ya afya au unakabiliana na athari zinazotokana na kusonga kwa umri? Au je, unakabiliana na msiba, huenda kutokana na kumpoteza mpendwa wako katika kifo? Kama ilivyo kwa kondoo wengi sana wenye thamani wa Yehova, huenda maisha yako ‘yamejaa taabu na huzuni.’—Zab. 90:10.
2 Ili tukabiliane na majaribu kwa mafanikio, ni lazima tuwe na mtazamo unaofaa kuyaelekea. Hilo linatia ndani nini? Tunaweza kutumia mfano ufuatao: Matatizo unayokabili maishani ni kama hali za hatari unazoweza kukutana nazo unapoendesha gari. Ikitegemea hatari, huenda ukaongoza gari upande wa kushoto au kulia, ukapunguza mwendo, au ukasimama kwa muda fulani. Hata hivyo, ili kuchukua hatua inayofaa, ni lazima uone vizuri hatari iliyopo. Huwezi kuona hatari hiyo ikiwa madirisha yako yamefunikwa na barafu au matope. Vivyo hivyo, ili kukabiliana na majaribu kwa mafanikio, tunahitaji kuyaona majaribu kama Yehova anavyoyaona. Katika makala hii, tutajifunza (1) mtazamo unaofaa kuelekea majaribu, (2) jinsi mtazamo usiofaa kuelekea hali yetu unavyoweza kutudhuru, na (3) baadhi ya hatua tunazoweza kuchukua ili kudumisha mtazamo unaofaa tunapokabili jaribu.
Ni lazima tuwe na mtazamo unaofaa kuelekea majaribu yetu ili tuweze kukabiliana nayo kwa mafanikio (Tazama fungu la 2)
MTAZAMO UNAOFAA KUELEKEA MAJARIBU
3. Ni lazima tukubali nini kuhusu mfumo huu mwovu?
3 Hatuwezi kuepuka majaribu katika mfumo huu mwovu. Maadamu sisi si wakamilifu na Shetani anatawala ulimwengu, majaribu yatatuathiri. Kwa kuongezea, kadiri mfumo huu unavyokaribia mwisho wake, tutakabili matatizo hata zaidi, iwe ni majanga ya asili au yanayosababishwa na wanadamu, au matatizo kutoka kwa watu wanaotenda maovu. (Mt. 24:8; 2 Tim. 3:13) Ikiwa Yehova angerekebisha matatizo yote hayo sasa, ingeonekana kana kwamba anamsaidia Shetani kutawala ulimwengu huu. Katika mfumo huu, hatuwezi kuepuka kuathiriwa na “msiba.”—Mhu. 9:12.
4. Wakristo wanakabili matatizo gani mengine?
4 Wakristo wanakabili matatizo zaidi. Mara nyingi, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba wangeteswa kwa sababu ya imani yao. (Mt. 24:9; Yoh. 16:2) Kujua hilo kunatusaidia tusiruhusu imani yetu itikiswe na majaribu kama hayo. (1 The. 3:3, 4) Tunapovumilia majaribu kwa sababu tuna imani yenye nguvu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba bado tuko katika njia inayoongoza kwenye uzima wa milele. Kwa kuongezea, tunaonyesha upande tunaounga mkono katika lile suala kuu kati ya Yehova na Shetani. Ikiwa sehemu ya shambulio lake kuelekea jina la Mungu, Shetani alidai kwamba wanadamu wanamtumikia Mungu wakichochewa tu na ubinafsi. Ili kuthibitisha dai hilo, anawashambulia vikali watu wa Yehova. (Ayu. 1:9-11) Tunapovumilia kwa sababu tunampenda Yehova, tunaufanya moyo wake ushangilie.—Met. 27:11.
5. Tunaweza kujifunza nini kutokana na Mhubiri 7:13, 14? (Tazama pia picha.)
5 Yehova anaruhusu majaribu. Kamwe Yehova hatendi kwa uovu au kutujaribu kwa mambo maovu. (Yak. 1:13) Hata hivyo, Mfalme Sulemani aliandika kwamba “siku ya taabu” ni “kazi ya Mungu wa kweli.” (Soma Mhubiri 7:13, 14.) Kama ilivyo mara nyingi, hapa Biblia inamrejelea Yehova kuwa anafanya jambo fulani, wakati ni kwamba anaruhusu tu litukie. Sulemani alitoa ushauri mzuri ambao unaweza kutusaidia kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu majaribu yetu. Kwanza, tunahitaji kuwa na matarajio yaliyo halisi kuhusu maisha yetu yasiyo makamilifu katika ulimwengu wa Shetani—tutakuwa na siku nzuri na mbaya. Tunapokuwa na siku iliyo njema, tunaweza kuonyesha uthamini wetu kwa wema wa Mungu na kuona siku hiyo kuwa zawadi kutoka kwake. Pili, Sulemani anatukumbusha kwamba ‘hatuwezi kuwa na uhakika kuhusu jambo lolote litakalotupata,’ kwamba siku itakuwa njema au ya taabu. Matatizo yasiyotazamiwa huwapata waadilifu na wasio waadilifu pia.
Tunahitaji kuwa na matarajio yaliyo halisi kwa kutambua kwamba tutakuwa na siku nzuri na mbaya katika ulimwengu huu wa Shetani (Tazama fungu la 5)
6. Kwa nini huenda Yehova akaruhusu tukabili majaribu? (Waebrania 12:7, 11)
6 Ikiwa tuna mtazamo unaofaa kuelekea majaribu yetu, tutaona kwamba Yehova anatufundisha tumtegemee yeye badala ya kujitegemea wenyewe. Yehova hashindwi kamwe kuyaona majaribu yetu au kujali kuhusu kuteseka kwetu. Hata anaporuhusu tuingie katika “bonde lenye kivuli kizito,” anaendelea kutuongoza, kutuhakikishia upendo wake, na kutupatia nguvu tunazohitaji ili kuvumilia. (Zab. 23:4) Majaribu yanaweza kutusaidia kutambua udhaifu wetu mbalimbali, na kwa msaada wa Mungu, hutusaidia kuboresha utu wetu. (Soma Waebrania 12:7, 11.) Kwa mfano, Ayubu alihitaji kuboresha sifa yake ya unyenyekevu. Yehova hakusababisha majaribu ya Ayubu, badala yake aliyaruhusu na kuyatumia kumsaidia Ayubu ajifunze masomo muhimu. (Ayu. 42:1-6) Hata iwe tutakabili jambo gani, tunajua kwamba jambo lolote ambalo Yehova ataruhusu halitatupatia madhara ya kudumu. Tunapovumilia kwa uaminifu majaribu yetu, tunatoka tukiwa “tumeshinda kabisa.”—Rom. 8:35-39.
7. Kwa nini unaweza kuwa na furaha unapoteswa kwa sababu ya imani yako?
7 Tunaweza kuwa na furaha tunapoteswa. Ikiwa unateswa kwa sababu ya imani yako, usifikiri kwamba umepoteza baraka za Yehova. Badala yake, upinzani huo unaonyesha kwamba una kibali chake. (Mt. 5:10-12) Ukiwa na mtazamo unaofaa, unaweza kupata shangwe na kuendelea kujiheshimu unapoteswa kwa sababu ya kuwa Mkristo, kama ilivyokuwa kwa mitume. (Mdo. 5:40-42) Kwa kuongezea, unaweza kuwasaidia watu ambao si Mashahidi wajifunze kweli na “wamtukuze Mungu.” (1 Pet. 2:12) Kama Yosefu, unaweza kupata mafanikio wakati wa majaribu—si tu yanapoisha.—Mwa. 39:3, 23.
8. Ni jambo gani lingine linalotuchochea kuvumilia majaribu yetu?
8 Majaribu yetu yataisha. Kisa cha Ayubu kinatukumbusha kwamba matatizo yetu yataisha. Isitoshe, “Yehova alibariki sehemu ya mwisho ya maisha ya Ayubu kuliko ya kwanza.” (Ayu. 42:12) Vivyo hivyo, Yehova anaahidi kubariki “sehemu ya mwisho” ya maisha yako, sehemu itakayodumu milele, kuliko mwanzo mfupi ambao umejaa matatizo. Hicho ni kichocheo kikubwa sana kwa kila mmoja wetu cha kuvumilia hadi mwisho!—Mt. 24:13.
JINSI MTAZAMO USIOFAA UNAVYOWEZA KUTUDHURU
9. Mtazamo usiofaa kuelekea majaribu yetu unawezaje kutudhuru?
9 Licha ya majaribu tunayokabili, tunahitaji kuwa na mtazamo unaofaa kuyaelekea ili kuepuka kujiongezea matatizo. Kwa mfano, huenda tukahisi kwamba Yehova ndiye anayesababisha jaribu letu. Kwa kipindi fulani, Ayubu alihisi kuwa Yehova ndiye aliyesababisha matatizo yake, na mtazamo huo usiofaa ulimfanya ajaribu “kujithibitisha mwenyewe kuwa mwadilifu badala ya Mungu.” (Ayu. 32:2) Vivyo hivyo, mwanzoni Naomi alimlaumu Yehova kwa sababu ya misiba aliyokabili. (Rut. 1:13, 20, 21) Ikiwa Ayubu na Naomi wangeendelea kuwa na mtazamo huo usiofaa, wangeharibu uhusiano wao na Yehova. (Met. 19:3) Hata hivyo, Yehova aliwasaidia kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu matatizo yao na akawabariki kwa ushikamanifu wao.
10. Tunapokuwa chini ya jaribu, huenda tukaanza kujiuliza nini?
10 Hata ikiwa tuna uhakika kwamba Yehova hasababishi majaribu yetu, huenda tukaanza kujiuliza ikiwa bado anatujali. Mtazamo huo usiofaa unaweza kufanya nguvu zetu ziwe chache. (Met. 24:10) Mfalme Daudi na nabii Habakuki walikabili majaribu na pindi fulani walijiuliza ikiwa Yehova alikuwa akisikiliza kilio chao cha msaada. (Zab. 10:1; Hab. 1:2) Hata hivyo, hawakuacha kusali. Yehova aliwahakikishia wanaume hao waaminifu kwamba atawategemeza, naye atakutegemeza wewe pia.—Zab. 10:17.
11. Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa hatutakuwa na mtazamo unaofaa kuelekea majaribu?
11 Tusipokuwa na mtazamo unaofaa kuelekea majaribu, huenda tukashangazwa tunapoyapata na kuhisi kwamba mambo hayo hayapaswi kutupata. (1 Pet. 4:12) Ilikuwa vigumu kwa wanafunzi wa Yesu kuelewa kwamba Yesu angekabili mateso makali. (Luka 18:33, 34) Licha ya Yesu kuwaeleza waziwazi mambo ambayo yangempata, mtume Petro alifikiri kwamba Mungu hangeruhusu Yesu ateseke kwa njia hiyo. Yesu alijua kwamba mtazamo huo ungeweza kumzuia kufanya mapenzi ya Yehova, hivyo alimkemea Petro. (Marko 8:31-33) Na hata baada ya kifo cha Yesu, ilichukua muda kwa wanafunzi wake kuelewa matukio hayo. Licha ya hilo, Yesu hakukata tamaa kuwaelekea. Alipozungumza nao baada ya kufufuliwa, aliwasaidia wawe na mtazamo unaofaa kuhusu kuteseka kwake kwa ‘kuwafungulia Maandiko waziwazi.’ (Luka 24:25-27, 32, 44-48) Kutafakari kuhusu mambo ambayo Yesu alikuwa akiwafundisha kungewasaidia wajitayarishe kwa ajili ya upinzani ambao wangekabili karibuni wakiwa wafuasi wake. Kuchunguza kweli za Kimaandiko kunaweza pia kutusaidia kujitayarisha kwa ajili ya majaribu.
12. Mtazamo usiofaa kuhusu hali yetu unaweza kutufanya tuhisije?
12 Mtazamo usiofaa kuhusu hali yetu unaweza kutufanya tuhisi kwamba tuna hali mbaya kuliko ilivyo kihalisi. Yesu alionyesha jinsi ambavyo hilo linaweza kutukia katika mfano wake wa wafanyakazi kwenye shamba la mizabibu. Baadhi ya wafanyakazi walilalamika kuhusu mshahara ambao walifikiri haukuwa wa haki, lakini bwana wao alimwambia mmoja wao hivi: “Mwenzangu, sijakukosea.” (Mt. 20:10-13) Malalamiko ya wafanyakazi hao yalitokana na matarajio yao yasiyo sahihi na si ukosefu wa haki. Leo, baadhi ya Mashahidi wamehitaji kupambana na hisia kama hizo—kwa mfano, walipokosa pendeleo fulani la utumishi au walipohitaji kuliacha. Tunaweza kufanya mambo gani hususa ili kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu hali ngumu tunayokabili?
HATUA TUNAZOWEZA KUCHUKUA TUNAPOKABILI JARIBU
13. Ni nini ambacho huenda kikatokea tunapokabili majaribu?
13 Huenda unajua kweli zinazopatikana kwenye Maandiko kuhusu kuteseka. Huenda hata umewaeleza wengine kweli hizo ili kuwasaidia wakabiliane na majaribu. Hata hivyo, unapokabili kibinafsi jaribu, huenda ikawa vigumu kwako kudumisha mtazamo unaofaa. Kwa mfano, huenda ukahisi kwamba Yehova anakuadhibu au kwamba hasikilizi sala zako. Unaweza kuchukua hatua gani ili kudumisha mtazamo unaofaa?
14. Unaweza kusali kuhusu nini unapoteseka? (Wafilipi 4:13)
14 Mwombe Yehova akusaidie. Mweleze Yehova kuhusu kuteseka kwako na jinsi kunavyokuathiri. Unaweza kusali kwa Yehova kihususa kuhusu jinsi ambavyo unataka akusaidie. Unaweza kumwomba akupatie roho yake takatifu ili upate nguvu na hekima unayohitaji ili kuvumilia. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova anaweza kujibu sala yako kwa njia usiyotarajia. (Efe. 3:20) Pia, huenda akawaongoza malaika au ndugu na dada zako wakusaidie. (Zab. 34:7) Hivyo, kubali msaada wowote ambao Yehova atakupatia. Anatupatia roho yake kwa ukarimu, nayo inaweza kutupatia nguvu ya kukabiliana na changamoto yoyote.—Soma Wafilipi 4:13.
15. Ni nini kitakachokusaidia kuvumilia jaribu? (Tazama pia picha.)
15 Dumisha ratiba nzuri ya mambo ya kiroho. Fanya yote unayoweza hata ikiwa huwezi kudumisha ratiba yako ya awali. Unahitaji kujaza hata zaidi mawazo ya Mungu akilini mwako wakati wa “taabu na shida.” (Zab. 119:143) Endelea kusoma Biblia kwa ukawaida, jifunze na kutafakari kuihusu. Shiriki katika huduma kadiri utakavyoweza, na uhudhurie na kushiriki katika mikutano. Endelea kuwasiliana na ndugu na dada zako. Epuka mwelekeo wowote wa kujitenga na wengine.—Met. 18:1.
Jitahidi kadiri uwezavyo kudumisha ratiba nzuri ya mambo ya kiroho (Tazama fungu la 15)
16. Ni mambo gani unayoweza kutilia shaka unapokabili jaribu, na unawezaje kushughulikia shaka hizo? (2 Wakorintho 10:4, 5)
16 Shughulikia shaka ulizo nazo. Unapokabili jaribu, huenda ukahitaji kupindua mawazo yaliyo kama “ngome zenye nguvu,” kutia ndani shaka ulizo nazo kujihusu na kumhusu Yehova. (Soma 2 Wakorintho 10:4, 5.) Unaweza kushughulikia shaka hizo kwa kutumia “ujuzi wa Mungu,” unaopatikana katika Biblia na machapisho yanayoandaliwa na tengenezo lake. Kwa mfano, je, unatilia shaka ikiwa bado una kibali cha Yehova? Jifunze kuhusu mambo aliyopitia mtume Paulo. Alikabili majaribu makali wakati wa huduma yake; hata hivyo, mambo hayo yaliimarisha hata zaidi uhakika wake kwamba yeye ni mhudumu wa Kristo aliyekubalika. (2 Kor. 11:23-27) Je, unatilia shaka ikiwa kwa kweli Yehova amekusamehe kwa sababu ya makosa uliyotenda zamani? Ikiwa ndivyo, andika orodha ya maandiko yanayoonyesha kwamba Yehova anasamehe dhambi. (Isa. 43:25) Kisha soma mistari hiyo na kuitafakari. (Zab. 119:97) Je, tukio fulani baya limekufanya utilie shaka ahadi ya Mungu ya kuwalinda watumishi wake waaminifu? Fanya utafiti kuhusu kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka na jinsi anavyotulinda kiroho haidhuru jambo litakalotupata. (Zab. 91:9-12) Pia, soma masimulizi ya ndugu na dada waliokabiliana na tukio baya kwa mafanikio.a
17. Tunapaswa kufanya nini tunapokabili jaribu?
17 Je, kwa sasa unafurahia siku iliyo njema, isiyo na magumu? Basi, mshukuru Yehova na kutumia wakati huo vizuri kwa kutafakari kuhusu wema wake. (Mhu. 7:14) Lakini unapokabili jaribu, dumisha mtazamo unaofaa kuelekea jaribu hilo na imarisha uhakika wako katika Yehova. Unapofanya hivyo, Yehova ‘ataifanya pia njia ya kutokea ili uweze kulivumilia.’ (1 Kor. 10:13) Hata hivyo, namna gani kuhusu ndugu na dada zetu wapendwa? Tunawezaje kuwasaidia wanapokabili majaribu? Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.
WIMBO 150 Mtafute Mungu Upate Ukombozi
a Kwa mfano, simulizi la maisha lenye kichwa, “Familia Yenye Furaha Yatikiswa na Kuwa Imara Tena” linalopatikana kwenye jw.org linasimulia jinsi Ndugu David Maza na familia yake walivyokabiliana na kifo chenye kuhuzunisha cha mwana wake.