Watoto Ni “Urithi Kutoka kwa Yehova”
NI JAMBO gani linalokuja akilini unaposikia neno “urithi”? Huenda ukafikiria pesa, ardhi au nyumba, au kitu chenye thamani ambacho kimerithishwa katika familia yenu kwa miaka mingi. Haidhuru ni urithi wa aina gani, urithi ni kitu chenye thamani sana na bila shaka ungependa kuutunza vizuri.
Biblia inasema kwamba watoto ni “urithi kutoka kwa Yehova.” (Zab. 127:3) Bila shaka, wazazi Wakristo wanawaona watoto wao kuwa zawadi zenye thamani kutoka kwa Baba yao wa mbinguni na wanataka kufanya yote wawezayo ili kuwalinda na kuwatunza vizuri kimwili, kihisia, na kiroho.
Hata hivyo, inasikitisha kwamba baadhi ya wazazi leo, hawaoni watoto wao kuwa zawadi kutoka kwa Mungu. (Isa. 49:15; 2 Tim. 3:1-3) Huenda wengine wakatamani kutoka moyoni kuwatunza watoto wao, lakini ikawa vigumu kwao kufanya hivyo kwa sababu ya changamoto mbalimbali. Ni baadhi ya changamoto gani zinazofanya iwe vigumu kwa wazazi kuwatunza watoto wao? Yehova anataka wazazi wafanye nini? Na wazazi Wakristo wanawezaje kufaulu kuwalea watoto wao vizuri?
CHANGAMOTO
Kushinikizwa na watu wa familia na jamii. Katika baadhi ya maeneo duniani, wazazi wenye watoto wengi wanaheshimiwa zaidi katika jamii. Hivyo, wenzi wa ndoa wanaweza kushinikizwa na watu wa familia au majirani kupata watoto wengi—huenda watoto wengi kuliko wanaoweza kuwatunza kibinafsi.
Wasiwasi kuhusu wakati ujao. Katika nchi ambazo kuna vifo vingi vya watoto wachanga kwa sababu ya utapiamlo, magonjwa, na uhaba wa vituo vya afya, baadhi ya wenzi wa ndoa hupata watoto wengi ili kuhakikisha kwamba angalau baadhi yao wanakua na kufikia utu uzima. Huenda wenzi wengine wa ndoa wakaamua kuwa na watoto wengi ili kuhakikisha kwamba watatunzwa watakapozeeka. Hali hiyo hutokea hasa katika nchi ambazo serikali haitoi msaada kwa wale waliozeeka.
Kupanga uzazi. Katika maeneo mengine, si rahisi kwa baadhi ya wenzi wa ndoa kupata dawa au njia za kuzuia mimba. Watu wengine wanaogopa kupata madhara yanayotokana na dawa za kuzuia mimba zisizo na ubora ambazo zinapatikana katika eneo lao. Ilhali wengine hawana uwezo wa kulipia gharama za juu za dawa za kuzuia mimba.a
YEHOVA ANATAKA WAZAZI WAFANYE NINI?
Tumia wakati pamoja na kila mtoto wako
Waandalie watoto wako mahitaji yao. Yehova amewakabidhi wazazi jukumu la kuwaandalia watoto wao wadogo mahitaji yao. Anatarajia wazazi wawe tayari kufanya kazi kwa bidii ili kumwandalia kila mtoto chakula, mavazi, na malazi. Yehova pia anataka wazazi wawafundishe watoto wao. Hivyo, wazazi Wakristo hawatawapeleka watoto wao katika shule za bweni. Badala yake, wanahakikisha kwamba watoto wanaishi nyumbani wanapoendelea kukua ili waweze kupokea elimu inayofaa na kupewa uangalifu wa kibinafsi, jambo linalowafanya wahisi salama na kwamba wanapendwa. Hata hivyo, Yehova ana usawaziko; hatarajii wazazi wawe matajiri. Isitoshe, Yehova alichagua wazazi waliofanya kazi kwa bidii, lakini waliokuwa maskini kimwili ili wamlee Mwana wake mpendwa.—Mt. 13:55, 56; Luka 2:24.
Kanuni ya Biblia: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji watu wake mwenyewe, hasa watu wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.”—1 Tim. 5:8.
Yehova anaelewa kwamba huenda wazazi wakahitaji msaada hususa kadiri umri wao unavyozidi kusonga. Kwa kweli, njia moja ambayo watoto wanaweza kuwaheshimu wazazi wao ni kwa kupanga jinsi watakavyowatunza watakapozeeka. (Kut. 20:12; 1 Tim. 5:4) Hata hivyo, Yehova anafurahi wazazi wanapofikiria hasa kuhusu jinsi watakavyowatunza watoto wao, badala ya jinsi ambavyo watoto wao watawatunza.—2 Kor. 12:14.
Waandalie mahitaji yao ya kiroho. Wazazi Wakristo pia wana jukumu la kuwazoeza watoto wao kumpenda na kumwabudu Yehova. Anaona mazoezi ya kiroho ambayo wazazi wanawapatia watoto wao kuwa sehemu muhimu ya malezi ya watoto.—Kum. 6:6, 7.
Kanuni ya Biblia: “Endeleeni kuwalea [watoto wenu] katika nidhamu na maagizo ya Yehova.”—Efe. 6:4.
YEHOVA ANATAKA UFANIKIWE
Zungumzieni mapema idadi ya watoto mtakaoamua kuwa nao
Fanya mipango mapema. Ikiwa unafikiria kupata watoto, chunguza kwa makini hali zako. Kwa mfano, je, utakuwa na uwezo wa kuwapatia chakula, mavazi, na elimu watoto wengi? Ikiwa hutaweza, zungumza na mwenzi wako kuhusu ikiwa mnaweza kuamua kutokuwa na watoto wengi ili mweze kuwaandalia kulingana na matakwa ya Yehova, mahitaji watoto wote mtakaoamua kuwa nao. Bila shaka, Yehova anaelewa kwamba si kila kitu maishani kinaweza kupangwa mapema. (Mhu. 9:11) Lakini atabariki jitihada zenu za kutoka moyoni ili mfanikiwe mkiwa wazazi.
Kanuni za Biblia: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio, lakini wote walio na haraka kwa hakika watakuwa maskini.”—Met. 21:5.
“Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?”—Luka 14:28.
Mtangulize Yehova katika familia yako. Tanguliza ibada ya Yehova katika familia yako. Ikiwa tayari una watoto, azimia kumfundisha kila mmoja wao ampende Yehova. Wasaidie kusikiliza na kujifunza katika mikutano ya kutaniko. Dumisha ratiba ya kila juma ya Ibada ya Familia. Wazoeze watoto wako katika huduma. Usiwakabidhi watoto wako wakubwa au watu wa ukoo jukumu lako ukiwa mzazi. Kuwalea watoto ili wampende Yehova kunahitaji wakati na jitihada, lakini kuna baraka nyingi.
Kanuni ya Biblia: “Sina shangwe kubwa kuliko hii: kwamba nisikie watoto wangu wanaendelea kutembea katika kweli.”—3 Yoh. 4.b
Mtumaini Yehova. Iwe unafikiria kuanzisha familia au tayari una watoto, uwe na hakika kwamba viwango vya Yehova ni muhimu zaidi kuliko tamaduni au desturi za eneo lenu.
Kutunza mahitaji ya kiroho ya watoto kunahitaji wakati na jitihada
Ikiwa utaamua kutokuwa na watoto wengi, uwe na uhakika kwamba bado Yehova atakupatia mahitaji yako hata utakapozeeka. Epuka kushinikizwa kufikiri kwamba watoto ni kama “pensheni yako.” Hupaswi kamwe kuogopa kwamba utaachwa bila msaada. Yehova ameahidi kukutunza, na sikuzote yeye hutimiza ahadi zake.—Yos. 23:14.
Kanuni za Biblia: “Mtumaini Yehova kwa moyo wako wote, wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Katika njia zako zote mtambue yeye, naye atavinyoosha vijia vyako.”—Met. 3:5, 6.
“Nilikuwa kijana lakini sasa nimezeeka, lakini sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa, wala watoto wake wakitafuta mkate.”—Zab. 37:25.
“Basi, endeleeni kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—Mt. 6:33.
Watoto ni zawadi zenye thamani ambazo Yehova amewakabidhi wazazi. Ni lazima Yehova anafurahi sana wenzi wa ndoa Wakristo wanapowatunza watoto kulingana na matakwa yake! Kwa upendo wanawaandalia watoto wao mahitaji ya kimwili, kihisia, na kiroho; wanapanga idadi ya watoto watakaokuwa nao; na kwa uaminifu wanafuata viwango vya Mungu badala ya tamaduni au desturi za eneo lao. Kwa kufanya hivyo, wenzi wa ndoa Wakristo wanaonyesha kwamba watoto wao ni zawadi wanayothamini sana—“urithi kutoka kwa Yehova.”
a Wenzi wa ndoa wataamua idadi ya watoto watakaokuwa nao, wataanzisha familia wakati gani, na ikiwa watatumia mbinu ya kupanga uzazi ambayo haihusishi utoaji wa mimba. Hakuna mtu anayepaswa kuwahukumu kwa maamuzi ya kibinafsi watakayofanya. (Rom. 14:4, 10-13) Kwa kuongezea, wenzi wa ndoa Wakristo wanakumbuka shauri lililo katika andiko la 1 Wakorintho 7:3-5.
b Ingawa watoto wanaotajwa katika mstari huo wa Biblia wanarejelea wanafunzi Wakristo, mzazi anaweza kuelewa kwa urahisi hisia anazoeleza Yohana.