Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Mataifa yatatoa lini tangazo la “amani na usalama”?
Kama tulivyozungumzia katika makala ya “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” iliyochapishwa katika toleo la karibuni la Mnara wa Mlinzi,a hivi karibuni Yehova atatia ndani ya mioyo ya “zile pembe kumi” (serikali zote za kisiasa) “wazo lake,” yaani, kwamba wampe nguvu na mamlaka yao “mnyama wa mwituni mwenye rangi nyekundu”—Umoja wa Mataifa. Mnyama huyo anaitwa pia “sanamu ya mnyama wa mwituni.” (Ufu. 13:14, 15; 17:3, 16, 17) Kisha “zile pembe kumi” na mnyama wa mwituni aliyetoka kupewa mamlaka wataondoa dini za uwongo ulimwenguni pote. Je, mataifa yatatoa tangazo la “amani na usalama”b kabla au baada ya kuharibiwa kwa dini za uwongo?—1 The. 5:3.
Kwa ufupi, hatujui kwa uhakika wakati ambapo tangazo hilo la “amani na usalama” litatolewa. Ikiwa tungejua habari zote zinazohusika, hatungehitaji kuwa chonjo na kukaa macho. Hata hivyo, Yesu aliwashauri tena na tena wafuasi wake ‘waendelee kukesha.’ (Mt. 24:42; 25:13; 26:41) Acheni sasa tuchunguze zaidi unabii ulioongozwa na roho ambao mtume Paulo aliandika katika barua yake kwa Wathesalonike.
Paulo aliandika hivi: “Wakati watakapokuwa wakisema, ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafla utakapowapata mara moja.” (1 The. 5:2, 3) Mara nyingi machapisho yetu yamefafanua hivi maneno hayo ya Paulo: Tangazo la “amani na usalama” litatolewa kabla tu ya kuanza kwa dhiki kuu, ambayo itaanza kwa kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa—milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo. Tangazo hilo la wakati ujao limefafanuliwa kuwa ishara ya mwisho ya kwamba dhiki kuu inakaribia kuanza.
Hata hivyo, baada ya kuchunguza kwa makini zaidi, inaonekana kwamba huenda kuna ufafanuzi mwingine tunaoweza kuufikiria. Huenda tangazo la “amani na usalama” litatolewa baada ya kuharibiwa kwa dini za uwongo. Kwa nini tunasema hivyo? Fikiria maswali yafuatayo.
Dini za uwongo zimehusikaje katika vita vya mataifa? Biblia inafafanua hivi: “Ndani yake [“yule kahaba mkubwa,” Babiloni Mkubwa] ilipatikana damu ya . . . wale wote ambao wameuawa duniani.” (Ufu. 17:1, 5; 18:24) Katika historia yote ya wanadamu, yule kahaba mkubwa ameendeleza vita vya mataifa na mara nyingi kuchochea vitendo vya ugaidi. Hivyo, amekuwa kichocheo cha vita na mashambulizi, na si amani na usalama. Swali hili linazuka: Je, mataifa yatatangaza “amani na usalama” baada tu ya kumwondoa Babiloni Mkubwa? Hilo linawezekana, lakini hatuwezi kuwa na uhakika.
Ni nini kitakachofuata baada ya tangazo la “amani na usalama”? Paulo anasema hivi: “Ndipo uharibifu wa ghafla utakapowapata mara moja.” (1 The. 5:3) Ikiwa mataifa yangetoa tangazo la “amani na usalama” kabla ya kuharibiwa kwa dini za uwongo, basi kipindi fulani cha wakati kingepita kabla ya wao kuharibiwa. Lakini kwa kuwa Paulo anasema kwamba ‘uharibifu wa ghafla utawapata mara moja,’ inawezekana kwamba mataifa yatatoa tangazo la “amani na usalama” baada ya kuharibu dini za uwongo.
Watu wa Yehova watatendaje mambo hayo yaliyotabiriwa yatakapotukia? Paulo anasema hivi: “Akina ndugu, [ninyi] hamko gizani, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ghafla kama vile ingewafikia wezi.” (1 The. 5:4) Fikiria jambo hili: Ikiwa tangazo la “amani na usalama” linatolewa baada ya kuharibiwa kwa dini za uwongo, basi watu wa Yehova watajua kwamba kuharibiwa kwa mataifa kumekaribia sana. Hata hivyo, kwa upande wa mataifa, kuharibiwa kwao kutawafikia kama mwizi—ghafla, bila onyo lolote.
Hivyo basi, tunaweza kutarajia nini? Hivi karibuni, “zile pembe kumi” na mnyama wa mwituni atakayepewa mamlaka kubwa wataharibu dini za uwongo. Huo utakuwa mwanzo wa dhiki kuu. Tunajua pia kwamba itakapofika pindi fulani, mataifa yatatoa tangazo la “amani na usalama.” Hilo litatukia lini? Tumezungumzia mambo mawili yanayowezekana. Jambo la kwanza linalowezekana: Tangazo hilo litatolewa kabla ya kuharibiwa kwa dini za uwongo. Jambo la pili linalowezekana: Tangazo hilo litatolewa baada ya serikali za kisiasa kuharibu kabisa dini za uwongo. Tutahitaji kusubiri ili tuone kitakachotukia. Mara nyingi unabii wa Biblia hueleweka kikamili wakati unapotimizwa au baada ya kutimizwa.—Linganisha Yohana 12:16.
Kwa sasa, jambo muhimu zaidi ni msimamo wetu mbele za Mungu, si wakati ambapo tangazo hilo la “amani na usalama” litatolewa. Ni lazima “tukae macho na kutunza akili zetu,” ili tuweze kujitayarisha kikamili haidhuru mambo hayo yatatukia jinsi gani.—1 The. 5:6.
a Tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 2025.
b Maneno ambayo mtume Paulo anatumia yanatokeza uwezekano wa kwamba kutakuwa na mfululizo wa matangazo, na si tangazo moja tu.