APRILI 20-26, 2026
WIMBO 49 Kufurahisha Moyo wa Yehova
Endelea Kujitahidi Kufikia Ubatizo
“Sasa ndio wakati unaokubalika hasa.”—2 KOR. 6:2.
JAMBO KUU
Sasa ndio wakati wa kujenga urafiki wa karibu na Yehova na kubatizwa.
1. (a) Ni baadhi ya manufaa gani tunayopata kwa kubatizwa? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?
JE, UMEJIWEKA wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu wako kwa kubatizwa katika maji? Ikiwa ndivyo, umetoa ombi kwa Mungu ili kupata dhamiri njema. (1 Pet. 3:21) Kwa kufanya hivyo, umewawekea mfano mzuri sana vijana na wapya wanaoshirikiana na kutaniko lenu. Kwa kweli, umefanya uamuzi mzuri sana! Namna gani ikiwa bado hujabatizwa? Bila shaka, unampenda Yehova na unataka kufanya mapenzi yake. Unajua kwamba ubatizo ni hatua muhimu ili dhambi zako zisamehewe na upate kibali cha Yehova. (Mdo. 2:38-40) Lakini huenda bado ukasita kubatizwa. Ni nini kinachoweza kukusaidia? Katika makala hii, tutachunguza (1) kwa nini baadhi ya watu husita kubatizwa, (2) kwa nini ni jambo la hekima kuweka akilini mwisho wa mfumo huu wa mambo, na (3) jinsi utakavyonufaika kwa kujitahidi kufikia ubatizo bila kukawia.
KWA NINI WENGINE HUSITA KUBATIZWA?
2. Kwa nini baadhi ya watu husita kubatizwa?
2 Baadhi ya watu husita kubatizwa kwa sababu ya woga. Kwa mfano, ingawa wanataka kumtumikia Yehova, wanaogopa kwamba hawataweza kumpendeza kamwe. Ikiwa unahisi hivyo, pitia tena mistari ya Biblia inayoweza kukusadikisha kwamba Yehova hatarajii uwe mkamilifu na anafurahi unapofanya yote uwezayo ili kumwabudu. (Zab. 103:13, 14; Kol. 3:23) Ikiwa unaogopa upinzani, mwombe Yehova akupatie uhakika kama wa mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Yehova yuko upande wangu; sitaogopa. Mwanadamu atanifanya nini?”—Zab. 118:6.
3. Ni jambo gani lingine ambalo huenda likawazuia baadhi ya watu kubatizwa? (Tazama pia picha.)
3 Baadhi ya watu wanaompenda Yehova wanasita kubatizwa kwa sababu wanafikiri kwamba hawana ujuzi wa kutosha. Lakini kihalisi unahitaji ujuzi mwingi kadiri gani? Fikiria mfano huu wa Kimaandiko. Baada ya tetemeko la ardhi kutikisa gereza ambalo mtume Paulo na Sila walikuwa wamefungwa, walimhubiria mlinzi wa jela na watu wa nyumba yake. Inaelekea mwanamume huyo na familia yake walitambua kwamba muujiza ulikuwa umetokea. Kwa kuongezea, usiku huo walijifunza mambo mengi muhimu. Matokeo ni kwamba walichochewa nao “wakabatizwa bila kukawia.” (Mdo. 16:25-33) Ikiwa unamjua Yehova, unampenda kwa moyo wako wote, umepata ujuzi wa msingi wa mafundisho ya Biblia, umetubu dhambi zako, na umeazimia kuishi kulingana na viwango vyake, uko tayari kubatizwa.—Marko 12:30.
Paulo na Sila walimhubiria mlinzi wa jela na familia yake, nao “wakabatizwa bila kukawia.” (Tazama fungu la 3)
4. Baadhi ya watu wanakazia fikira jambo gani linalosababisha wasite kubatizwa? (Tazama pia picha.)
4 Baadhi ya watu wanaotaka kumfurahisha Mungu hukazia fikira gharama inayohusika ili kufanya hivyo. Bila shaka, ni jambo la hekima kuhesabu gharama inapohusu uamuzi wowote tunaofanya. (Luka 14:27-30) Hata hivyo, baadhi ya watu huwa na wasiwasi kuhusu mambo watakayohitaji kudhabihu ili kumtumikia Mungu. Alipokuwa mtoto, Candace alijifunza mambo ambayo mtu anapaswa kufanya ili kumpendeza Yehova, lakini hakutumia mambo hayo. Alipoalikwa kujifunza Biblia akiwa mtu mzima, alikuwa na wasiwasi kuhusu mambo atakayohitaji kudhabihu. Anasema hivi: “Nilijua mambo niliyopaswa kufanya kwa ajili ya Yehova, lakini nilisita kufanya hivyo kwa sababu nilifurahia mambo niliyokuwa nikifanya ulimwenguni. Nilijua kwamba isingekuwa rahisi kuacha mambo hayo.” Wengine wana wasiwasi kuwa hawataweza kufikia kiwango cha juu cha mwenendo kwa ajili ya wale wanaobatizwa. Wana wasiwasi kwamba baada ya kubatizwa, watatenda dhambi nzito na kuondolewa kutanikoni. Ikiwa unahangaishwa na mambo hayo unaweza kufanya nini?
Baadhi ya watu wanaotaka kumfurahisha Mungu wana wasiwasi kuhusu mambo watakayohitaji kudhabihu ili kumtumikia Mungu (Tazama fungu la 4)
5. Tunapaswa kukazia fikira nini tunapofikiria kuhusu kubatizwa? (Mathayo 13:44-46)
5 Tunapotaka kununua kitu, hatufikirii tu gharama yake, bali pia thamani ya kitu hicho. Ikiwa thamani ya kitu hicho ni kubwa kuliko gharama yake, inaelekea tutakinunua bila kusita. Vivyo hivyo, tunapofikiria kuhusu kubatizwa, hatupaswi kukazia tu fikira gharama zitakazohusika ili kufanya mabadiliko ya lazima, bali tukazie fikira thamani kubwa ya kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova. Yesu alitumia mifano miwili kufundisha jambo hilo. (Soma Mathayo 13:44-46.) Katika kila mfano, kwa furaha mtu huyo aliuza mali zake zote ili aweze kununua kitu chenye thamani alichokipata. Wewe pia umepata kitu chenye thamani kubwa—kweli kuhusu Ufalme. Kama unajiuliza ikiwa jitihada za kuishi kulingana na kweli ni za bure, fikiria kwa makini mifano ya Yesu. Unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninasadiki kabisa kwamba kweli niliyopata ni yenye thamani kubwa? Je, ninathamini uhusiano wangu na Yehova, tumaini alilonipa, na undugu wetu wenye upendo?’ Ikitegemea majibu yako, unaweza kukazia fikira kujenga uthamini wako kuelekea kweli au kutambua mambo yanayokuzuia kutenda kulingana na mambo unayojua.
6. Tunawezaje kusitawisha hali nzuri ya moyo?
6 Katika mfano wake wa mpandaji, Yesu alifafanua hali za moyo zinazoweza kumzuia mtu kufanya maendeleo ya kiroho. Hata hivyo, Yesu alisema pia kwamba baadhi ya watu “wenye moyo mzuri na mwema” wangesikia na kukubali ujumbe wa Ufalme. (Luka 8:5-15) Ikiwa una wasiwasi kwamba moyo wako umegawanyika, usikate tamaa. Kwa msaada wa Mungu, unaweza ‘kujipatia moyo mpya,’ ambao utakubali mwongozo wake. Mwombe Yehova katika sala akusaidie kulainisha moyo wako ili kweli za Ufalme zisitawi.—Eze. 18:31; 36:26.
7-8. Kwa nini baadhi ya vijana wanashindwa kufanya maendeleo ili kufikia ubatizo? (Tazama pia picha.)
7 Baadhi ya vijana wanaompenda Yehova wanashindwa kufanya maendeleo na kubatizwa kwa sababu ya kuathiriwa na wengine. Kwa mfano, huenda baadhi ya washauri shuleni wakawashauri wanafunzi wawe na mtazamo wa kukubali maoni ya wengine inapohusu viwango vya maadili, hata vile ambavyo vinapingana na viwango vya Mungu. Lakini ushauri kama huo unaweza kusababisha madhara makubwa. (Zab. 1:1, 2; Met. 7:1-5) Unaweza kuepuka hatari hiyo kwa kufuata mfano wa mtunga zaburi aliyemwambia Yehova hivi: “Nina ufahamu mwingi kuliko walimu wangu wote, kwa sababu ninavitafakari vikumbusho vyako.”—Zab. 119:99.
8 Ripoti zinaonyesha kwamba baadhi ya wazazi Mashahidi wanawazuia watoto wao kubatizwa. Wazazi hao wanakazia fikira kupita kiasi watoto wao kupata elimu na kazi nzuri, au ni kwamba tu wazazi wanashindwa kuwasaidia watoto wao wajiwekee miradi ya kiroho. Namna gani ikiwa unahisi kwamba wazazi wako wanahitaji kukusaidia zaidi ili ufikie lengo lako la kubatizwa? Kwa nini usizungumzie jambo hilo pamoja nao? Uwe na hakika kwamba umri wako haupaswi kukuzuia kujenga urafiki wa karibu na Yehova.—Met. 20:11.
Kwa nini usizungumzie suala la ubatizo pamoja na wazazi wako? (Tazama fungu la 8)
9. Kwa nini huenda baadhi ya watu wakasita kubatizwa?
9 Huenda baadhi ya watu wanaostahili kubatizwa wakasita kuchukua hatua hiyo kwa sababu ya kushinikizwa na marafiki wao, huenda hata wakamsubiri mtu fulani hususa achukue hatua hiyo pia. Kwa mfano, huenda wakatamani wabatizwe siku moja na rafiki au mpendwa wao. Bila shaka, unaweza kubatizwa pamoja na watu unaowapenda. Hata hivyo, je, kweli jambo hilo linapaswa kukufanya usite kubatizwa sasa? Kumbuka kwamba kujiweka wakfu kwa Mungu ni ahadi unayotoa wewe binafsi. Ubatizo wako haupaswi kutegemea maamuzi ya mtu mwingine.—Rom. 14:12.
KWA NINI UENDELEE KUWEKA KARIBU AKILINI MWISHO WA MFUMO HUU WA MAMBO?
10. Kwa nini huenda baadhi ya watu wakasita kufanya maendeleo ya kiroho?
10 Mbali na sababu zilizotajwa katika mafungu yaliyotangulia, huenda baadhi ya watu wakasita kufanya maendeleo ya kiroho kwa sababu wanahisi kwamba bado kuna wakati mwingi kabla ya mwisho kufika. Lakini je, njia hiyo ya kufikiri inafaa? Yesu aliwaonya hivi wanafunzi wake: “Endeleeni kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja saa msiyotazamia.”—Luka 12:40.
11. Kulingana na Zaburi 119:60, tunahisije kuhusu amri za Yehova kadiri tunavyomjua zaidi?
11 Ni lazima wakfu wetu kwa Yehova uchochewe na upendo. Kadiri tunavyomjua zaidi Mungu wetu mwenye upendo, ndivyo tunavyozidi kuchochewa kupenda amri zake na kuzifuata mara tu tunapozijua. (Soma Zaburi 119:60.) Mwanafunzi Yakobo alionyesha sababu nyingine muhimu ya kutii amri za Yehova bila kukawia: Hakuna yeyote kati yetu anayejua kesho itakuwaje. Huenda hata tusiwe na siku moja zaidi ya “kufanya yaliyo sawa,” hivyo tunapaswa kutenda sasa kulingana na mambo tunayojua.—Yak. 4:13-17.
12. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Yesu wa shamba la mizabibu?
12 Namna gani kuhusu mfano wa Yesu wa shamba la mizabibu? Je, hakufundisha kwamba baadhi wa wafanyakazi wangefanya kazi kwa saa moja na bado wapokee mshahara sawa na wale waliofanya kazi siku nzima? Alifundisha hivyo. Hata hivyo, ona sababu ya kuchelewa ambayo wale waliofanya kazi kwa saa moja walitoa. Walisema hivi: “Kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri.” Si kwamba wafanyakazi hao hawakujitahidi kutafuta kazi siku nzima—ni kwamba tu hawakupata ajira. Mara tu walipopewa ajira, walianza kufanya kazi. (Mt. 20:1-16) Leo, Yesu ametualika tuwe wanafunzi wake na tufanye kazi ya Ufalme. Tunapaswa kukubali mwaliko wake mara tu tunapoupata.
13. Tunajifunza nini kutoka kwa mke wa Loti?
13 Wale wanaokawia kuchukua hatua ili kufanya maendeleo ya kiroho huenda wakagundua kwamba ni vigumu sana kufanya mabadiliko dakika za mwisho ili kumfurahisha Mungu. Yesu alijua jambo hilo na aliwaonya hivi wanafunzi wake: “Mkumbukeni mke wa Loti.” (Luka 17:31-35) Mke wa Loti alijua vizuri kwamba Mungu angetekeleza hukumu yake juu ya majiji ya Sodoma na Gomora bila kukawia; hata hivyo, inaonekana kwamba bado hakuwa tayari kuacha nyuma mali alizokuwa nazo. (Mwa. 19:23-26) Kisa chake kinatukumbusha pia kwamba mlango wa wokovu hautaendelea kuwa wazi daima. Wakati aliouweka Mungu utakapofika, mlango huo utafungwa milele.—Luka 13:24, 25.
14. Unabii mbalimbali kuhusu mwisho unapaswa kukuchocheaje?
14 Kadiri siku zinavyopita, matukio ulimwenguni yanatimiza unabii wa Biblia kuhusu mwisho wa mfumo huu. Hata ikiwa bado hujaathiriwa na baadhi ya matukio hayo, kuona mambo yanayotukia katika sehemu moja baada ya nyingine kunapaswa kukuchochea kuongeza hisi yako ya uharaka na kufanya maendeleo ili kufikia ubatizo. Fikiria mfano huu katika karne ya kwanza. Mtume Petro aliwahimiza Wakristo ‘wakeshe,’ au ‘wawe chonjo,’ kwa sababu “mwisho wa mambo yote [ulikuwa] umekaribia.” (1 Pet. 4:7; maelezo ya chini.) “Mwisho” huo inaelekea ulikuwa wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi. Wale ambao Petro aliwaandikia walikuwa wakiishi mbali na jiji la Yerusalemu, hivyo hawangeathiriwa moja kwa moja na uharibifu wa jiji hilo. (1 Pet. 1:1) Hata hivyo, mara walipoona utimizo wa unabii huo, uhakika wao katika ahadi nyingine za Yehova uliimarishwa. Vivyo hivyo, unapoona unabii mbalimbali kuhusu mwisho ulio karibu ukitimizwa, utachochewa kuendelea kukesha kwa kujitahidi kufikia lengo lako la kubatizwa.
15. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu siku ya Yehova inayokuja? (2 Petro 3:10-13)
15 Katika barua yake ya pili iliyoongozwa na roho, Petro alitaja maoni tunayopaswa kuwa nayo kuhusu siku ya Yehova ya hukumu inayokuja. Kwa Wakristo wa karne ya kwanza, siku hiyo ingekuja baada ya miaka mingi; hata hivyo, Petro aliwaambia ‘waweke karibu akilini,’ au ‘watamani sana,’ siku hiyo. (Soma 2 Petro 3:10-13; maelezo ya chini.) Tunaweza kuweka karibu akilini siku hiyo kwa kuwa tayari na kutamani ifike. Tunaonyesha tamaa yetu kwa kufanya “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” Fikiria jinsi ambavyo Yehova atafurahi atakapoona ukifanya “vitendo vya ujitoaji-kimungu”! Bila shaka, atafurahi sana atakapoona ukijiweka wakfu kwake na kubatizwa.
MANUFAA YA KUCHUKUA HATUA SASA
16. Ni wakati gani ulio bora kabisa wa kufanya maendeleo ili kufikia ubatizo? (2 Wakorintho 6:1, 2) (Tazama pia picha.)
16 Wakati bora kabisa wa kufanya maendeleo ili kufikia ubatizo ni sasa hivi. (Soma 2 Wakorintho 6:1, 2.) Yule towashi Mwethiopia ambaye alikutana na Filipo, alitambua uhitaji wa kuchukua hatua bila kukawia. Mara alipoelewa kuhusu habari njema na kupata nafasi ya kubatizwa, hakuanza kufikiri hivi: ‘Ningependa kwanza kujifunza mengi zaidi kuhusu habari njema. Kutakuwa na sehemu nyingine yenye maji mbele ya safari.’ Badala yake, alimuuliza Filipo, “Ni nini kinachonizuia kubatizwa?” (Mdo. 8:26, 27, 35-39) Huo ni mfano mzuri sana! Baada ya towashi kubatizwa, “aliendelea na safari yake akishangilia.”
Jifunze somo hili muhimu kutoka kwa towashi Mwethiopia: Wakati bora kabisa wa kufanya maendeleo ili kufikia ubatizo ni sasa hivi (Tazama fungu la 16)a
17. Tunaweza kuwa na uhakika gani?
17 Ikiwa unasita kubatizwa, uwe na uhakika kwamba Yehova yuko tayari kukuongoza ili uwe na uhusiano mzuri pamoja naye. (Rom. 2:4) Anaweza kukusaidia kushinda woga, mahangaiko, au uvutano wowote ambao huenda unakuzuia kufanya maendeleo. Utakapopata dhamiri njema mbele za Mungu kupitia ubatizo wako, inaelekea utagundua kwamba “mambo ya nyuma” si ya muhimu tena kwako. (Flp. 3:8, 13) Kisha, unaweza kutazamia “mambo yaliyo mbele,” yaani, kutimizwa kwa ahadi za Yehova kwa ajili ya wale waliojiweka wakfu kwake na kubatizwa.—Mdo. 3:19.
WIMBO 38 Atakupa Nguvu
a MAELEZO YA PICHA: Kama tu ambavyo towashi Mwethiopia alimwambia Filipo kwamba anataka kubatizwa, mwanafunzi wa Biblia anawafikia wazee ili kuwaeleza kuhusu tamaa yake ya kutaka kubatizwa.