Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Desemba kur. 26-30
  • Enyi Wakristo Wenye Umri Mkubwa​—⁠Mnathaminiwa Kutanikoni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Enyi Wakristo Wenye Umri Mkubwa​—⁠Mnathaminiwa Kutanikoni
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YEHOVA ANATARAJIA NINI KUTOKA KWAKO?
  • UNAWEZA KUWANUFAISHA SANA WENGINE
  • YEHOVA ANATHAMINI UTUMISHI WAKO UNAOFANYA KWA UAMINIFU
  • ENDELEA KUWA NA MAMBO MENGI YA KUFANYA KADIRI UWEZAVYO
  • Mzee Aliyepata Thawabu kwa Sababu ya Imani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Alitimiza Tamaa ya Moyo Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Yehova Anawatunza kwa Upendo Watumishi Wake Waliozeeka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Pata Shangwe kwa Kumpa Yehova Kilicho Bora Kulingana na Uwezo Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Desemba kur. 26-30
Mkusanyo wa picha: Ndugu na dada wenye umri mkubwa wakifurahia utumishi wao kwa Yehova. 1. Ndugu anatabasamu anapotazama mbele kwa uhakika. 2. Dada aliyeketi kwenye kiti cha magurudumu akimpa trakti mhudumu wa afya. 3. Dada akitoa maelezo mkutanoni. 4. Dada akiwa ameshikilia mkono wa ndugu kijana wanapohubiri pamoja. 5. Ndugu akitumia wakati pamoja na watoto wadogo wawili na mama yao katika Jumba la Ufalme.

Enyi Wakristo Wenye Umri Mkubwa—Mnathaminiwa Kutanikoni

“Ninapokumbuka zamani, ninashangazwa na mambo niliyoweza kutimiza. Sasa ninashindwa kufanya mengi kwa sababu ya umri kusonga.”—Connie, dada mwenye umri wa miaka 83.

Huenda wewe pia unashindwa kutimiza mambo mengi kwa sababu ya umri kusonga. Licha ya kwamba umemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka mingi, huenda ukawa na maoni yasiyofaa kujihusu kwa sababu huwezi kutimiza mambo mengi kwa sasa. Kwa mfano, huenda ukawa na mwelekeo wa kulinganisha mambo unayofanya sasa na mambo uliyofanya zamani. Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini ili kushinda mtazamo huo?

YEHOVA ANATARAJIA NINI KUTOKA KWAKO?

Jiulize hivi: ‘Yehova anatarajia nini kutoka kwangu?’ Unaweza kufarijika na maneno ya Kumbukumbu la Torati 6:​5, inayosema hivi: “Ni lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.”

Kulingana na mstari huo, Yehova anatarajia umtumikie kwa moyo, nafsi, na nguvu zako zote. Ukweli huo unaweza kukusaidia kuepuka kujilinganisha na wengine—au kulinganisha mambo unayoweza kutimiza sasa na mambo uliyoweza kutimiza zamani.

Fikiria jambo hili: Ulipokuwa kijana, ulikuwa ukimpa Yehova nini? Watu wengi wa Yehova watajibu kwamba walikuwa wakimpa kilicho bora. Kwa upande wako, ulimpa kilicho bora kulingana na hali zako za wakati huo. Kwa sasa unaweza kumpatia Yehova nini? Inaelekea unampatia kilicho bora kulingana na hali zako leo, mambo unayoweza kufanya kwa wakati huu. Ikiwa utakuwa na maoni hayo, utafikia mkataa kwamba unampatia Yehova kilicho bora kama ulivyokuwa unafanya zamani. Ulikuwa ukimpa kilicho bora wakati huo, na unampa kilicho bora sasa.

Mkusanyo wa picha: Dada akimtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka mingi. 1. Miaka mingi iliyopita, dada akiwa kijana anazungumza na mwanamke katika huduma ya nyumba kwa nyumba. 2. Sasa, umri wake ukiwa umesonga, dada huyo anahubiri kwa njia ya simu pamoja na dada kijana.

Unapompa Yehova kilicho bora licha ya umri kusonga, unafanya kama ulivyofanya ulipokuwa kijana

UNAWEZA KUWANUFAISHA SANA WENGINE

Fikiria jambo hili lingine: Badala ya kufikiria tu mambo ambayo huwezi kutimiza kwa sababu ya kusonga kwa umri, fikiria kuhusu fursa nyingi ulizo nazo za kuwasaidia wengine. Kwa kweli, ukiwa Mkristo mwenye umri mkubwa, kuna baadhi ya mambo unayoweza kufanya sasa ambayo hungeweza kufanya ulipokuwa kijana. Kwa mfano, unaweza kufanya mambo yafuatayo:

Shiriki uzoefu wako na wengine. Fikiria maneno haya yanayopatikana katika Biblia:

Mfalme Daudi: “Nilikuwa kijana lakini sasa nimezeeka, lakini sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa, wala watoto wake wakitafuta mkate.”—Zab. 37:25.

Yoshua: “Basi sasa nakaribia kufa, nanyi mnajua vizuri kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya ahadi zote nzuri ambazo Yehova Mungu wenu aliwaahidi. Zote zimetimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja aliloahidi.”—Yos. 23:14.

Huenda wewe pia umekuwa na maoni kama hayo. Mambo ambayo Daudi na Yoshua walisema yalikuwa mambo ambayo walijionea maishani. Kwa kuwa watumishi hao waaminifu wa Yehova walikuwa wakieleza mambo waliyojionea na kusikia kwa miaka mingi, mambo waliyosema yalikuwa na uzito.

Ikiwa umekuwa ukimtumikia Yehova kwa miaka mingi, wewe pia unaweza kuzungumzia thawabu ulizojionea maishani katika utumishi wako kwa Yehova. Je, unakumbuka wakati ulipoona Yehova akiwabariki watu wake kwa njia ya pekee? Basi, jisikie huru kuwaeleza wengine kuhusu pindi hiyo! Hilo linaweza kukutia moyo, kama ambavyo huenda tayari umejionea. Hivyo, wengine wanaposikia kuhusu mambo uliyojionea katika utumishi wako kwa Yehova, wanaweza kutiwa moyo sana.—Rom. 1:​11, 12.

Njia nyingine unayoweza kuwatia moyo wengine ni kwa kuhudhuria mikutano ya kutaniko uso kwa uso kadiri utakavyoweza. Katika mikutano, unaweza kuwanufaisha wengine na kujinufaisha pia. Dada Connie, aliyetajwa awali, anasema hivi: “Kuhudhuria mikutano hunisaidia nisivunjike moyo. Siwezi kushuka moyo ninapoonyeshwa upendo na ndugu na dada katika Jumba la Ufalme. Ninajitahidi kuwaonyesha wengine kwamba ninawashukuru kwa kuwapatia zawadi ndogondogo. Na ninahakikisha kwamba ninaendelea kushiriki katika utendaji wa kiroho pamoja na ndugu na dada zangu.”

YEHOVA ANATHAMINI UTUMISHI WAKO UNAOFANYA KWA UAMINIFU

Katika Maandiko, kuna mifano mingi ya watu ambao walipendwa na Yehova licha ya kushindwa kutimiza mengi kwa sababu ya hali zao. Mfikirie Simeoni, Mwisraeli mwenye umri mkubwa aliyekuwa hai Yesu alipozaliwa. Simeoni alipoenda hekaluni, huenda aliwaona wanaume vijana wakifanya kazi muhimu. Lakini namna gani kuhusu Simeoni mwenyewe? Kwa maoni ya kibinadamu, angeweza kufikiri kwamba kwa kuwa amezeeka, hakuwa na thamani yoyote machoni pa Yehova. Lakini Yehova alikuwa na maoni tofauti. Alimwona Simeoni kuwa mtu ‘mwadilifu na aliyemwogopa Mungu’ na alimbariki kwa kumpatia pendeleo la kumwona mtoto Yesu. Yehova hata alimtumia Simeoni kutoa unabii kuhusu Masihi wa wakati ujao! (Luka 2:​25-35) Ni wazi kwamba Yehova aliona zaidi ya mwili uliozeeka wa Simeoni, badala yake aliona mwanamume mwenye imani yenye nguvu, na ambaye “roho takatifu ilikuwa juu yake.”

Yosefu na Maria wakimwonyesha Simeoni kwa shangwe mtoto Yesu.

Yehova alimbariki Simeoni kwa kumpatia pendeleo la kumwona mtoto Yesu na alimtumia kutoa unabii kuhusu Masihi wa wakati ujao

Wewe pia unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anathamini utumishi wako unaofanya kwa uaminifu licha ya changamoto zozote unazokabili. Machoni pa Yehova, dhabihu “hukubalika zaidi kulingana na kile ambacho mtu anacho, si kulingana na kile ambacho mtu hana.”—2 Kor. 8:12.

Ukiwa na hilo akilini, kazia fikira mambo unayoweza kutimiza. Kwa mfano, unaweza kushiriki katika aina gani ya huduma—hata kwa vipindi vifupi vya wakati? Je, unaweza kuwatia moyo wengine kwa kuwapigia simu au kuwaandikia kadi? Matendo hayo madogo-madogo ya upendo yanaweza kuwa na matokeo makubwa kwa waabudu wenzako, hasa yanapofanywa na mtu aliyemtumikia Yehova kwa muda mrefu.

Baadhi ya watu wana matatizo ya afya. Fikiria jambo lililoonwa kutoka Afrika Mashariki katika sanduku lenye kichwa “Biblia Iliokoa Uhai Wake.”

Kumbuka kwamba rekodi yako ya imani na ushikamanifu itawatia moyo wengine. Wewe ni mfano ulio hai wa uvumilivu, na uwe na uhakika kwamba ‘Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuhudumu na kuendelea kuwahudumia watakatifu.’—Ebr. 6:10.

ENDELEA KUWA NA MAMBO MENGI YA KUFANYA KADIRI UWEZAVYO

Utafiti unaoonyesha kwamba wanaume na wanawake wengi wenye umri mkubwa ambao wanawasaidia wengine wana afya nzuri zaidi, uwezo mzuri zaidi wa kufikiri, na maisha marefu zaidi.

Bila shaka, kufanya yaliyo mema hakuondoi madhara ya kuzeeka. Ni Ufalme wa Mungu tu utakaofanya jambo hilo kwa kuondoa chanzo halisi cha kuzeeka na kufa—hali yetu ya dhambi.—Rom. 5:12.

Hata hivyo, utumishi unaomtolea Yehova—unaotia ndani kuwasaidia watu wengine wamjue—hudumisha tumaini letu likiwa imara na huenda hata ukawa na faida kiafya. Enyi Wakristo wenye umri mkubwa, muwe na uhakika kwamba Yehova anathamini mambo mnayotimiza katika utumishi wenu kwake, na kutaniko linathamini sana mfano wenu wa imani.

Dada mwenye umri mkubwa akishiriki katika mahubiri ya kigari. Anasoma andiko pamoja na mwanamke kijana ambaye machozi yanatiririka usoni.

Biblia Iliokoa Uhai Wake

Mwanamke kijana alikuwa akipita karibu na kigari chetu cha machapisho. Baada ya kumsalimu mwanamke huyo, dada mwenye umri mkubwa aliyekuwa kwenye kigari cha machapisho alimuuliza ikiwa angeweza kushiriki naye andiko lenye kutia moyo. Dada huyo alisoma andiko la Yeremia 29:​11, linalotaja kwamba Yehova ana mawazo ya amani wala si ya msiba kutuelekea. Dada yetu akamuuliza hivi: “Je, umetambua Mungu anataka uwe na wakati gani ujao?”

Mwanamke huyo kijana aliguswa moyo sana. Macho yake yakiwa yamejaa machozi, alijibu hivi: “Anataka niwe na wakati ujao wenye amani na tumaini. Asante sana kwa mstari huo. Ninaamini kwamba hili ni jibu la sala yangu. Hivi karibuni nimekuwa nikikabiliana na majaribu mengi, moja baada ya lingine. Hali ilikuwa mbaya sana hivi kwamba nilikuwa nikifikiria kujiua. Leo asubuhi, nilisali kwa Mungu na kumwomba anionyesha ishara ya kwamba bado ananijali, kisha wewe—mtu nisiyemfahamu kabisa—umenisimamisha na kusoma andiko linaloonyesha hasa mawazo ya Mungu kunielekea. Najua hilo limetukia kwa sababu Mungu anataka kunisaidia.”

Dada yetu alimwonyesha mwanamke huyo makala kadhaa kwenye jw.org ambazo zinaweza kumsaidia kutumia Biblia ili kukabiliana na mawazo ya kutaka kujiua. Kisha dada huyo alimweleza jinsi ambavyo funzo la Biblia linafanywa na alimwalika katika mikutano yetu. Juma lililofuata, mwanamke huyo alihudhuria mkutano wa mwisho juma na sasa ameanza kujifunza Biblia kwa kutumia broshua Furahia Maisha Milele!

Iwe wewe ni kijana au mwenye umri mkubwa, unaweza kushiriki katika utumishi wa kigari.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki