MAKALA YA 51
WIMBO 132 Sasa Tumekuwa Mwili Mmoja
Jinsi ya Kupanga Harusi Itakayomletea Yehova Heshima
“Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.”—1 KOR. 14:40.
JAMBO KUU
Jinsi wachumba Wakristo wanavyoweza kumletea Yehova heshima katika siku yao ya harusi.
1-2. Yehova ana maoni gani kuhusu harusi?
JE, UNA mchumba? Ikiwa ndivyo, hongera! Inaelekea una mengi ya kufanya katika maandalizi ya harusi yenu. Yehova anapendezwa na ndoa yako. Anataka ufurahie siku yenu ya harusia na muwe na wakati ujao wenye furaha pamoja.—Met. 5:18; Wim. 3:11.
2 Yehova anastahili kuonyeshwa heshima katika siku yenu ya harusi. Kwa nini tunasema hivyo? Na unawezaje kufanya hivyo? Ingawa kimsingi makala hii inawahusu wale wanaofanya maandalizi ya harusi yao, kanuni zitakazozungumziwa zinaweza kutusaidia sisi sote kumwonyesha Yehova heshima tunapohudhuria harusi au ikiwa tunapoombwa kutoa maoni kuhusu mipango inayofanywa.
KWA NINI HARUSI YAKO INAPASWA KUMLETEA YEHOVA HESHIMA?
3. Wachumba Wakristo wanaopanga harusi yao, wanapaswa kuzingatia nini, na kwa nini?
3 Wale wanaopanga harusi ya Kikristo wanapaswa kufanya hivyo kulingana na kanuni za Yehova zilizo katika Neno lake. Kwa nini? Kwa sababu Yehova ndiye Mwanzilishi wa ndoa. Alipanga harusi ya kwanza kabisa—ambayo iliwaunganisha Adamu na Hawa katika kifungo cha ndoa. (Mwa. 1:28; 2:24) Hivyo, maoni ya Mungu yanapaswa kuzingatiwa sana na wale wanaopanga harusi.
4. Wachumba Wakristo wana sababu gani ya kumwonyesha Yehova heshima katika siku yao ya harusi?
4 Una sababu muhimu ya kuzingatia maoni ya Yehova kuhusu siku yenu ya harusi: Yeye ni Baba yako wa mbinguni na Rafiki yako wa karibu zaidi. (Ebr. 12:9) Bila shaka, ungependa aendelee kuwa Rafiki yako wa karibu. Usingependa jambo lolote litokee siku hiyo au siku nyingine yoyote ambalo litamuumiza Rafiki yako. (Zab. 25:14) Unapofikiria mambo yote ambayo Yehova amefanya na ambayo atakufanyia, je, hukubali kwamba anastahili kuheshimiwa katika siku yako ya harusi?—Zab. 116:12.
JINSI UNAVYOWEZA KUMHESHIMU YEHOVA KATIKA SIKU YENU YA HARUSI
5. Biblia inawezaje kuwasaidia wachumba kupanga harusi yao?
5 Biblia haina orodha ya sheria za jinsi ambavyo hotuba ya ndoa au sherehe ya harusi inapaswa kufanywa. Hivyo, wachumba wanaweza kupanga harusi yao kulingana na hali zao, utamaduni, na mapendezi yao. Waabudu wa kweli wanaheshimu pia sheria zilizowekwa na Kaisari. (Mt. 22:21) Hata hivyo, harusi iliyopangwa kulingana na kanuni za Biblia itamheshimu Yehova na kumfurahisha. Basi, ni kanuni gani unazopaswa kuzingatia?
6. Kwa nini ni muhimu kwa wachumba kutimiza matakwa ya kisheria kabla ya kufunga ndoa?
6 Tii matakwa ya kisheria. (Rom. 13:1, 2) Katika nchi nyingi, ni lazima wachumba watimize matakwa fulani ya kisheria kabla ya kufunga ndoa. Wachumba hao wanapaswa kujua matakwa ya kisheria ya eneo wanaloishi. Ikiwa unahitaji msaada ili kupata taarifa kuhusu matakwa hayo, jihisi huru kuwauliza wazee wa kutaniko.b
7. Ni mazingira gani mazuri yanayofaa katika siku ya harusi?
7 Tengeneza mazingira mazuri yenye kuheshimika. (1 Kor. 10:31, 32) Jitahidi kutengeneza mazingira mazuri yanayoonyesha sifa za tunda la roho ya Mungu, badala ya roho ya ulimwengu. (Gal. 5:19-26) Kulingana na kanuni ya Kimaandiko ya ukichwa, bwana harusi anapaswa kuhakikisha kwamba sherehe ya harusi ni tukio la furaha na linaloheshimika. Anawezaje kufanya hivyo? Hotuba inayotegemea Biblia inapotolewa kwa upendo, wororo, na heshima, inaongeza uthamini wetu kwa mpango wa Mungu wa ndoa. Wahudhuriaji wote wanaweza kunufaika kwa sababu hotuba itawasaidia kukazia akilini uzito wa tukio hilo. Hivyo, Wakristo wengi huamua kuwa na hotuba ya ndoa katika Jumba la Ufalme, inapowezekana. Ikiwa ungependa kutumia Jumba la Ufalme, unapaswa kuandika barua ya ombi kwa baraza la wazee mapema vya kutosha.
8. Ni nini kinachoweza kukusaidia kudumisha mazingira yenye heshima katika sherehe yako ya harusi? (Waroma 13:13)
8 Soma Waroma 13:13. Ikiwa utaamua kuwa na sherehe ya harusi, unawezaje kuhakikisha kwamba hakutakuwa na mazingira yanayoonyesha roho ya ulimwengu? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “karamu zenye vurugu” linarejelea mikusanyiko iliyohusisha kunywa kupita kiasi na kucheza muziki hadi usiku sana. (Tazama habari za utafiti za Waroma 13:13 kuhusu “wild parties,” nwtsty.) Ikiwa utaamua kuwe na kileo kwenye sherehe, chukua tahadhari kwa kuhakikisha kwamba hakuna mtu atakayekunywa kupita kiasi.c Ikiwa kutakuwa na muziki, hakikisha kiwango cha sauti kitawaruhusu wageni wako kufurahia mazungumzo. Pitia kwa makini aina ya muziki na maneno ya muziki ili mtu yeyote asikwazike.
9. Wenzi wa ndoa wanapaswa kukumbuka nini kuhusu mambo yatakayosemwa au burudani zitakazokuwepo wakati wa sherehe yao ya harusi?
9 Je, kwenye sherehe ya harusi watu watasimama na kuzungumza, utaonyesha picha, video, au kutakuwa na aina nyingine za burudani? Mara nyingi mambo hayo yanaweza kupendezesha siku yenu ya pekee. Hata hivyo, hakikisha kwamba mambo yanayofanywa ni yenye kujenga. (Flp. 4:8) Jiulize hivi: ‘Je, jambo hili litaonyesha kwamba ninawaheshimu wengine? Je, litadumisha heshima ya mpango wa ndoa?’ Na jambo muhimu zaidi, jiulize: ‘Je, litamheshimu Yehova?’ Ingawa kwa kiasi fulani huenda utani ukafaa, epuka utani wowote usiofaa, kama vile utani unaorejelea habari zinazohusu ngono. (Efe. 5:3) Hakikisha kwamba watu wa familia na marafiki watakaozungumza maneno machache wanaelewa maamuzi yako na watayaheshimu.
10. Kwa nini wachumba wanapaswa kuwa na sifa ya kiasi wanapopanga harusi yao? (1 Yohana 2:15-17)
10 Uwe mwenye kiasi. (Soma 1 Yohana 2:15-17.) Yehova anathamini waabudu wake wanapojitahidi kumheshimu yeye, badala ya kujielekezea fikira wenyewe. Hivyo, Wakristo wenye kiasi wataepuka kutumia pesa nyingi kupita kiasi na “kujionyesha.” Utanufaikaje kwa kufanya harusi yenye kiasi? Huenda ukapata matokeo kama aliyopata ndugu kutoka Norway, anayeitwa Mike. Anasema hivi: “Tuliepuka madeni na tukaweza kuendelea na utumishi wa upainia. Harusi yetu ilikuwa yenye kiasi, ilikuwa maridadi na itakumbukwa vizuri.” Tabitha, dada kutoka India, anasema hivi: “Tuliepuka mahangaiko mengi. Kwa sababu tulikuwa na harusi yenye kiasi, hatukuwa na maamuzi mengi ya kufanya, hivyo ilikuwa rahisi zaidi kukubaliana.”
Haidhuru mahali tunapoishi, harusi ya Kikristo inaweza kuwa yenye kiasi, maridadi, na itakayokumbukwa vizuri (Tazama fungu la 10-11)
11. Bwana na bibi harusi wanawezaje kuonyesha wana kiasi kupitia mavazi na mapambo yao? (Tazama pia picha.)
11 Je, tayari mmechagua nguo mtakazovaa siku hiyo? Bila shaka mngependa kupendeza. Hata katika nyakati za Biblia, bwana na bibi harusi walifikiria kwa uangalifu kuhusu mavazi yao. (Isa. 61:10) Ni kweli kwamba huenda mavazi utakayovaa katika harusi yako kwa njia fulani yakawa tofauti na unayovaa katika matukio mengine, hata hivyo, mavazi ya harusi bado yanapaswa kuwa yenye kiasi. (1 Tim. 2:9) Usiruhusu mavazi—au kitu kingine chochote cha kimwili—kuwa jambo la muhimu zaidi katika harusi yako.—1 Pet. 3:3, 4.
12. Kwa nini wachumba wanapaswa kukataa desturi zozote za harusi katika eneo lao ambazo si za Kimaandiko?
12 Kataa desturi zisizopatana na Maandiko. (Ufu. 18:4) Mfumo wa Shetani umechafua desturi za harusi kwa mazoea ya kipagani, uwasiliani roho, na ushirikina. Yehova anatuonya waziwazi tuepuke kabisa mambo hayo machafu. (2 Kor. 6:14-17) Ikiwa unatilia shaka baadhi ya tamaduni au desturi katika eneo unaloishi, fikiria vyanzo vyao na kanuni zozote za Biblia zinazohusika kabla ya kuamua mambo utakayofanya katika siku yako ya harusi.
13. Wachumba wanawezaje kuiga maoni ya Yehova kuhusu zawadi?
13 Je, ni jambo la kawaida mahali unapoishi kwa wageni kuwapatia wenzi wa ndoa zawadi? Hali ya kiuchumi ya baadhi ya wageni huenda ikaamua aina ya zawadi watakayotoa. Bila shaka, Wakristo wanatiwa moyo kutoa na wanafurahia kufanya hivyo. (Met. 11:25; Mdo. 20:35) Hata hivyo, tusingependa wageni wetu wahisi kwamba ni lazima watoe zawadi; wala tusingependa wahisi kwamba zawadi ya gharama ndogo haitathaminiwa. Tunamwiga Yehova kwa kujitahidi kuwa na maoni kama yake kuhusu zawadi kwa kuwaruhusu wengine watoe kulingana na uwezo wao na kutoka moyoni.—2 Kor. 9:7.
JINSI YA KUEPUKA CHANGAMOTO NA KUZISHINDA
14. Baadhi ya wachumba wanakabili changamoto gani?
14 Unaweza kukabili changamoto unapojitahidi kupanga harusi itakayomletea Yehova heshima. Kwa mfano, huenda ikawa vigumu kwako kupanga harusi yenye kiasi. Charlie, anayeishi katika Visiwa vya Solomon, anasema hivi: “Ilikuwa vigumu sana kuamua tutamwalika nani kwenye sherehe ya harusi. Tuna marafiki wengi, na katika utamaduni wetu, kila mtu anatarajia kualikwa!” Tabitha, aliyetajwa awali, anasema hivi: “Katika eneo ninaloishi, ni jambo la kawaida kuwa na watu wengi katika sherehe ya harusi. Ilichukua muda mrefu kwa wazazi wangu kukubali uamuzi wetu wa kuwaalika watu 100 tu hivi.” Sarah, kutoka India, anasema hivi: “Baadhi ya watu wanakazia fikira sana mwonekano wao katika jamii. Binamu zangu walifanya harusi za kifahari, hivyo mimi pia nilitamani kufanya harusi ya kifahari hata zaidi.” Ni nini kinachoweza kukusaidia kushinda changamoto hizo na nyingine?
15. Kwa nini sala ni sehemu muhimu katika mipango ya harusi?
15 Sali kuhusu mipango yenu ya harusi. Unaweza kumweleza Yehova katika sala kuhusu jambo unalokabili au kuhusu hisia zako. (Flp. 4:6, 7 na habari za utafiti “in everything” nwtsty) Unaweza kumwomba Yehova akusaidie kufanya maamuzi mazuri, kuwa mtulivu unapokuwa na mahangaiko, na kuonyesha ujasiri inapohitajika. (1 Pet. 5:7) Utazidi kumtumaini Yehova unapoona akijibu sala zako. Tabitha, aliyetajwa awali, anasema hivi: “Mimi na mchumba wangu tulikuwa na wasiwasi kuhusu kutoelewana sisi wenyewe na familia zetu. Hivyo, tulianza na sala kila mara tulipokuwa tukizungumzia mipango ya harusi. Kwa kweli, tulihisi msaada wa Yehova na tulifurahia hali ya amani kati yetu na wanafamilia.”
16-17. Mawasiliano mazuri yanawezaje kukusaidia unapopanga harusi?
16 Zungumzieni mambo kwa njia ya wazi na kwa busara. (Met. 15:22) Mkiwa wachumba, mtahitaji kufanya maamuzi mengi kuhusu harusi yenu. Hilo linatia ndani kuchagua tarehe, kupanga bajeti, orodha ya wageni mtakaowaalika, na mambo mengine mengi. Kabla ya kufanya maamuzi, pitieni pamoja mambo mbalimbali mnayoweza kuchagua na zungumzieni pamoja kanuni za Biblia zinazohusika na ushauri wowote mtakaopata kutoka kwa Wakristo wakomavu wenye uzoefu. Unapoeleza mapendezi yako ya kibinafsi, uwe mwenye fadhili, usawaziko, na mwenye kunyumbulika. Ikiwa watu wa familia wa karibu—kama vile wazazi wako—wana maombi yenye usawaziko, jitahidi kukubaliana nao. Tukio hilo ni la pekee kwao pia. Ikiwa hutaweza kukubali mapendekezo yao, waeleze kwa busara sababu zako. (Kol. 4:6) Waeleze wazi watu wako wa familia kwamba lengo lako ni kuwa na pindi ya furaha itakayomletea Yehova heshima.
17 Kuwaeleza wazazi wako kuhusu maamuzi yako kunaweza kuwa vigumu hasa ikiwa si Mashahidi, lakini unaweza kufaulu. Ndugu kutoka India, anayeitwa Santhosh, anasema hivi: “Familia zetu zilitaka tutie ndani desturi kadhaa za Kihindu katika harusi yetu. Ilinichukua mimi na mchumba wangu muda mrefu kuwafafanulia uamuzi wetu. Tulifanya mabadiliko katika maeneo tuliyohisi kwamba tunaweza kufanya hivyo bila kumkosea Yehova. Kwa mfano, tulibadili chakula kitakacholiwa katika sherehe na kuweka chakula ambacho wangefurahia, na tuliamua hakungekuwa na kuimba au kucheza dansi, kwa sababu hawakuwa wamezoea mambo hayo.”
18. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuhakikisha kwamba siku yako ya harusi itaenda vizuri? (1 Wakorintho 14:40) (Tazama pia picha.)
18 Pangeni mambo kwa umakini. Mnapopanga mambo vizuri, huenda mkapunguza mkazo mwingi katika siku yenu ya harusi. (Soma 1 Wakorintho 14:40.) Wayne, kutoka Taiwan, anasema hivi: “Siku chache kabla ya harusi yetu tulifanya mkutano mdogo na wale waliojitolea kutusaidia. Tulizungumzia mipango yetu na kufanya mazoezi ya baadhi ya mambo tutakayofanya katika harusi ili kuhakikisha kwamba mambo yataenda vizuri.” Waonyeshe heshima wageni wako, kwa kujitahidi kufanya mambo kwa wakati.
Mipango mizuri kabla ya harusi inaweza kuhakikisha kwamba mambo yataenda vizuri (Tazama fungu la 18)
19. Unawezaje kuhakikisha kwamba harusi yako itakuwa yenye kuheshimika?
19 Tunaweza kuepuka matatizo mengi kwa kufikiria mambo kimbele. (Met. 22:3) Kwa mfano, ikiwa unaishi katika eneo ambalo ni kawaida kwa wageni wasioalikwa kufika katika sherehe ya harusi, fikiria jambo unaloweza kufanya ili kuzuia hali hiyo. Hakikisha kwamba watu wa ukoo ambao si Mashahidi wanajua mambo wanayoweza kutarajia, na wafafanulie maoni yako kuhusu desturi fulani zinazofanywa katika harusi. Unaweza kuwaonyesha makala inayopatikana kwenye jw.org yenye kichwa, “Ni Nini Hutendeka Katika Harusi za Mashahidi wa Yehova?” Ili kukusaidia kudhibiti mambo yatakayoendelea katika sherehe yako ya harusi, panga kuwe na ndugu mkomavu atakayetumikia kama “msimamizi wa karamu.” (Yoh. 2:8) Ikiwa utamweleza waziwazi mipango yako ya harusi, anaweza kukusaidia kuhakikisha kwamba harusi yenu itakuwa yenye kuheshimika na mambo yote yataenda kama yalivyopangwa.
20. Wachumba wanapaswa kukumbuka nini kuhusu harusi yao?
20 Huenda ukahisi umelemewa unapofikiria kila kitu kinachohusika katika kupanga harusi yako. Hata hivyo, kumbuka kwamba sherehe yako ya harusi ni jambo la siku moja. Ni siku ya kwanza ya maisha yenu mazuri pamoja mkiwa watumishi wa Yehova. Jitahidi kadiri unavyoweza kuhakikisha kwamba harusi yako ni ya kiasi na yenye kuheshimika. Mtumaini Yehova. Kupitia mwongozo wake, utaweza kupanga harusi ambayo utakapoikumbuka itakupatia kumbukumbu nzuri na zenye furaha, bila majuto yoyote.—Zab. 37:3, 4.
WIMBO 107 Mungu—Kielelezo cha Upendo
a UFAFANUZI WA MANENO: Katika tamaduni nyingi, harusi inatia ndani hotuba ya ndoa ambapo wachumba wanaweka nadhiri mbele za Mungu. Sherehe inaweza kufuata baadaye. Katika tamaduni zisizo na hotuba au sherehe rasmi ya harusi, bado wenzi wanaweza kunufaika kwa kufikiria kanuni za Biblia kwa ajili ya siku yao ya ndoa.
b Ili kupata habari zaidi kuhusu maoni ambayo Mkristo anapaswa kuwa nayo kuhusu matakwa ya kisheria kwa ajili ya ndoa, tazama makala “Arusi Zenye Kuheshimika Machoni pa Mungu na Wanadamu” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 2006.
c Tazama kwenye jw.org video Je, Niandae Kileo?