Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Desemba kur. 14-19
  • Iga Unyenyekevu wa Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Iga Unyenyekevu wa Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YEHOVA NI MWENYE KUFIKIKA
  • YEHOVA NI MWENYE USAWAZIKO
  • YEHOVA NI MWENYE SUBIRA
  • YEHOVA ANAWAHESHIMU WATU WA HALI YA CHINI
  • Mwige Yehova na Yesu Katika Njia Yako ya Kufikiri
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Uwe Mwenye Kiasi Inapohusu Mambo Usiyoyajua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Pata Furaha Kubwa Inayotokana na Kutoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Sitawisha Unyenyekevu wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Desemba kur. 14-19

MAKALA YA 50

WIMBO 48 Kutembea na Yehova Kila Siku

Iga Unyenyekevu wa Yehova

“Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.”—EFE. 5:1.

JAMBO KUU

Kujifunza njia nne hususa za kuiga unyenyekevu wa Yehova.

1. Kwa nini unyenyekevu wa Yehova ni wa pekee?

UNAPOWACHUNGUZA watu wenye mamlaka leo, je, wanaonyesha sifa ya unyenyekevu? Huenda ukajibu la. Hata hivyo, Yehova ambaye ni mweza-yote, ni mnyenyekevu. (Zab. 113:​5-8) Yehova anaonyesha sifa ya unyenyekevu katika kila jambo analofanya; hana kiburi hata kidogo. Tutanufaika kwa kuchunguza sifa nne za utu maridadi wa Yehova na kutambua jinsi anavyoonyesha sifa ya unyenyekevu katika kila moja ya sifa hizo. Pia, tutachunguza jinsi Yesu alivyoiga unyenyekevu wa Baba yake. Kwa kuchunguza sifa hizo, tutasaidiwa kumkaribia Yehova na kuiga unyenyekevu wake kwa kiwango kikubwa zaidi.

YEHOVA NI MWENYE KUFIKIKA

2. Andiko la Zaburi 62:8 linafunua nini kumhusu Yehova? (Tazama pia picha.)

2 Mara nyingi watu wenye kiburi si wenye kufikika. Kiburi chao kinasababisha watende kwa njia ambazo zinawafanya wengine wasite kuwafikia au wawaepuke kabisa. Yehova yuko tofauti kabisa! Kwa sababu Baba yetu wa mbinguni ni mnyenyekevu, anatualika tumfikie na tumwambie mambo yanayotulemea moyoni na akilini. (Soma Zaburi 62:8.) Kama tu ambavyo baba anayejali alivyo tayari kusikiliza mahangaiko ya watoto wake, Yehova anafurahia na anasikiliza sala za waabudu wake. Kwa kweli, alihakikisha kwamba sala hizo nyingi zimeandikwa katika Biblia. Hilo linaonyesha jinsi alivyo mwenye kufikika. (Yos. 10:​12-14; 1 Sam. 1:​10-18) Lakini namna gani ikiwa kwa sababu fulani nyakati nyingine tunahisi kwamba hatustahili kumfikia Yehova?

Baba akimsikiliza kwa subira mwana wake anayemweleza jinsi alivyovunja chungu cha maua bila kukusudia alipokuwa akicheza na ndege yake.

Akimwiga Yehova, baba anamsikiliza kwa unyenyekevu mwana wake aliyevunja chungu cha maua alipokuwa akicheza (Tazama fungu la 2)


3. Kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anataka umfikie kwa ukawaida katika sala?

3 Tunaweza kumfikia Yehova katika sala hata tunapohisi kwamba hatustahili upendo wake. Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Katika mfano wa Yesu wa mwana mpotevu, alimfananisha Yehova na baba mwenye upendo mwororo ambaye mtoto wake aliyetubu alihisi kwamba hastahili kukubaliwa kurudi tena katika familia. Baba huyo alitendaje mtoto wake aliporudi nyumbani? Yesu alisema kwamba mara tu baba huyo alipomwona mwana wake, “akakimbia, akamkumbatia na kumbusu kwa wororo.” (Luka 15:​17-20) Yehova ni kama baba huyo. Mara tu anaposikia sala za watu ambao mioyo yao imevunjwa na kupondwa kwa sababu ya kulemewa na hatia au wasiwasi, kwa kuwa Yeye ni mnyenyekevu, anawasikiliza kwa makini. (Omb. 3:​19, 20) Yehova anawaonyesha huruma, na ni kana kwamba anawakimbilia, ili kuwafariji na kuwahakikishia rehema na upendo wake. (Isa. 57:15) Leo, Yehova “anatukimbiliaje”? Mara nyingi anafanya hivyo kupitia wazee wa kutaniko, watu wa familia walio Mashahidi, na waabudu wenzetu wengine. (Yak. 5:​14, 15) Yehova anatuandalia msaada huo kwa sababu anataka tumkaribie.

4. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa mwenye kufikika?

4 Yesu anamwiga Baba yake. Kama Baba yake, Yesu pia ni mnyenyekevu. Kwa sababu hiyo, alipokuwa duniani, watu walijihisi huru kumfikia. Hawakuogopa kumuuliza maswali. (Marko 4:​10, 11) Hivyo, alipowaomba watoe maoni yao kuhusu jambo fulani, walimweleza jinsi walivyohisi kikweli. (Mt. 16:​13-16) Na walipofanya makosa, hawakuogopa na kutetemeka; walijua kwamba Yesu ni mwenye fadhili, rehema, na subira. (Mt. 17:​24-27) Kwa sababu Yesu alimwiga Baba yake vizuri sana, wafuasi wa Yesu waliweza kumjua Yehova vizuri zaidi. (Yoh. 14:9) Walijifunza kwamba Yehova alikuwa tofauti sana na viongozi wa dini wa siku zao ambao walikuwa wakali, wenye kiburi, na wasiofikika. Badala yake, alikuwa mnyenyekevu na mwenye kufikika.

5. Sifa ya unyenyekevu inawezaje kutusaidia kuwa wenye kufikika zaidi?

5 Tunawezaje kumwiga Yehova? Tukisitawisha sifa ya unyenyekevu, tutakuwa wenye kufikika zaidi. Sifa ya unyenyekevu itatuzuia kuwa wenye wivu, kiburi, na wasiosamehe—sifa ambazo zinawafanya watu wasitake kutukaribia. Lakini unyenyekevu utatusaidia kuwa wenye fadhili, subira, na wenye kusamehe—sifa ambazo zitawafanya watu watukaribie. (Kol. 3:​12-14) Ni lazima wazee hasa wajitahidi kuwa wenye kufikika. Bila shaka, ili wawe wenye kufikika, wanahitaji kuwa pamoja na akina ndugu na dada. Hilo linamaanisha kwamba watajitahidi kuhudhuria mikutano uso kwa uso, badala ya kuhudhuria kupitia video mtandaoni bila sababu za msingi. Na kadiri hali zao zinavyoruhusu, wanajitahidi kuhubiri pamoja na ndugu na dada katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Ndugu na dada wanapowafahamu vizuri zaidi wazee, watajihisi huru zaidi kuzungumza nao wakati wowote wanapohitaji msaada.

YEHOVA NI MWENYE USAWAZIKO

6-7. Toa mifano inayoonyesha jinsi Yehova anavyokubali maombi ya watumishi wake.

6 Watu wengi wenye kiburi hawaonyeshi usawaziko wanaposhughulika na wengine. Lakini kwa sababu Yehova ni mnyenyekevu, anaonyesha usawaziko na ni mwenye kukubali sababu—ingawa yeye ni mkuu zaidi ya kila mtu na kwa kila njia. Fikiria jinsi alivyoshughulika na Miriamu, dada ya Musa. Miriamu, pamoja na Haruni, walinung’unika dhidi ya Musa, ambaye alikuwa mwakilishi wa Yehova. Hivyo, kimsingi Miriamu hakumwonyesha heshima Yehova. Matokeo ni kwamba Yehova alimkasirikia sana Miriamu na kumpiga kwa ukoma. Lakini Haruni alipomsihi Musa amsaidie Miriamu, na Musa alipomsihi Yehova amponye dada yake, Mungu alitendaje? Mungu hakushikilia kwa kiburi hukumu yake dhidi ya Miriamu. Kwa sababu Yehova ni mnyenyekevu, alikubali sababu na kumponya Miriamu.—Hes. 12:​1-15.

7 Yehova alionyesha pia unyenyekevu aliposhughulika na Mfalme Hezekia. Kupitia nabii wake, Yehova alimwambia mfalme kwamba angekufa. Hezekia alilia na kumsihi Yehova amponye. Na kwa rehema Yehova alimjibu, na akamwongezea mfalme huyo miaka 15 ya kuishi. (2 Fal. 20:​1, 5, 6) Naam, kwa kuwa Yehova ni mnyenyekevu anaonyesha huruma na anakubali sababu.

8. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba Yesu ni mwenye usawaziko? (Marko 3:​1-6)

8 Yesu anamwiga Baba yake. Alipokuwa duniani, Yesu hakukosa kuwatendea watu mema ilipohitajika kufanya hivyo. Kwa mfano, aliwaponya watu katika siku ya Sabato licha ya kupingwa na wapinzani wake waliokuwa na mioyo migumu. (Soma Marko 3:​1-6.) Yesu anaendelea kuonyesha usawaziko akiwa kichwa cha kutaniko la Kikristo. Kwa mfano, mtu kutanikoni anapotenda dhambi nzito, anamwonyesha subira, akimpatia nafasi ya kutosha ili abadili mwenendo wake.—Ufu. 2:​2-5.

9. Tunawezaje kusitawisha na kuonyesha usawaziko? (Tazama pia picha.)

9 Tunawezaje kumwiga Yehova? Kwa unyenyekevu, tunapaswa kujitahidi kusitawisha njia ya Yehova ya kufikiri na kutenda kwa usawaziko. (Yak. 3:17) Kwa mfano, ingawa wazazi wenye usawaziko hawawaendekezi watoto wao, hawatarajii wafanye mengi kuliko wanavyoweza kufanya. Hilo linaonyeshwa vizuri na Yakobo, kama tunavyosoma kwenye simulizi linalopatikana katika Mwanzo 33:​12-14. Wazazi walio wanyenyekevu na wenye usawaziko wanapaswa pia kujitahidi kuepuka kuwalinganisha watoto wao isivyo haki. Ni lazima pia wazee Wakristo wawe wenye usawaziko. Njia moja wanayoweza kufanya hivyo ni kwa kukubali maamuzi ya wengi katika baraza la wazee, ikiwa kufanya hivyo hakuvunji kanuni yoyote ya Biblia. (1 Tim. 3:​2, 3) Na sote tunaweza kujitahidi kuelewa maoni ya wengine, hata ikiwa tunaona mambo kwa njia tofauti. (Rom. 14:1) Naam, kila mtu kutanikoni anapaswa kujitahidi kuacha ‘usawaziko wake ujulikane kwa watu wote.’—Flp. 4:5.

Mkusanyo wa picha: Baba akihubiri kwa shangwe pamoja na watoto wake wadogo katika huduma ya nyumba kwa nyumba. 1. Anatabasamu mwana wake anapompa mwanamume fulani broshua “Furahia Maisha Milele! ” 2. Baadaye, anatabasamu binti yake anapompa mwanamke fulani kadi ya mawasiliano.

Baba anaonyesha usawaziko kuhusu mambo anayotarajia kutoka kwa watoto wake katika huduma (Tazama fungu la 9)


YEHOVA NI MWENYE SUBIRA

10. Ni katika njia gani Yehova ameonyesha subira?

10 Huenda umetambua kwamba watu wenye kiburi hawapendi wengine wanapowafanya wasubiri. Kiburi kinawafanya wakose subira. Yehova ni tofauti sana, yeye ndiye mwenye subira zaidi kuliko mtu mwingine yeyote! Kwa mfano, katika siku za Noa, Yehova alisema kwamba angesubiri miaka 120 kabla ya kuwaharibu waovu. (Mwa. 6:3) Noa alikuwa na muda wa kulea watoto wake na kujenga safina akisaidiwa na familia yake. Baadaye, malaika aliyemwakilisha Yehova alimsikiliza kwa subira Abrahamu alipomuuliza maswali kuhusu kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora. Huenda mtu mwenye kiburi angejibu hivi, ‘Unathubutu kuniuliza hivyo!’ Lakini kwa kumwiga Yehova, malaika huyo alimwonyesha Abrahamu subira.—Mwa. 18:​20-33.

11. Kama inavyotajwa katika andiko la 2 Petro 3:​9, kwa nini Yehova anaonyesha subira leo?

11 Kwa unyenyekevu Yehova anatuonyesha pia subira leo. Anasubiri hadi wakati aliouweka ufike ili alete mwisho. Kwa nini anaonyesha subira? “Kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (Soma 2 Petro 3:9.) Je, subira anayoonyesha Yehova ni ya bure? Hapana! Mamilioni ya watu wenye mioyo minyoofu wamemkaribia. Na tunatumaini kwamba watu wengi hata zaidi watafanya hivyo. Hata hivyo, subira ya Yehova ina mipaka. Yehova anawapenda watu, lakini hawaendekezi. Hataruhusu uovu uendelee milele.—Hab. 2:3.

12. Yesu anaigaje subira ya Yehova?

12 Yesu anamwiga Baba yake. Kwa maelfu ya miaka, Yesu ameiga subira ya Yehova. Yesu alimwona Shetani akimchongea Yehova na wanadamu waaminifu. (Mwa. 3:​4, 5; Ayu. 1:11; Ufu. 12:10) Yesu amejionea wanadamu wakiteseka sana. Bila shaka, anatamani sana ‘kuvunja kazi za Ibilisi’! (1 Yoh. 3:8) Ni jambo gani linalomsaidia Yesu kungojea kwa subira kibali cha Yehova ili aweze kuharibu kabisa kazi za Ibilisi? Jambo moja ni kwamba unyenyekevu wa Yesu unamchochea amwachie yule anayestahili—Yehova—aamue wakati unaofaa wa kuleta mwisho.—Mdo. 1:7.

13. Ni kwa njia gani na kwa nini Yesu aliwaonyesha subira mitume wake?

13 Alipokuwa duniani, Yesu aliwaonyesha pia mitume wake subira. Kwa mfano, mitume walipobishana tena na tena kuhusu aliyekuwa mkuu zaidi kati yao, Yesu hakukata tamaa. Badala yake, aliendelea kuwa na subira. (Luka 9:46; 22:​24-27) Alitumaini kwamba baada ya muda wangefanya mabadiliko yaliyohitajika. Je, umerudia tena na tena kosa lilelile? Ikiwa ndivyo, je, huthamini kuwa na Mfalme anayekutawala aliye mnyenyekevu na mwenye subira?

14. Tunawezaje kusitawisha sifa ya subira?

14 Tunawezaje kumwiga Yehova? Tunapositawisha “akili ya Kristo,” tunakuwa katika hali bora zaidi itakayotuwezesha kufikiri na kutenda kama Yehova. (1 Kor. 2:16) Tunawezaje kuelewa vizuri zaidi akili ya Kristo? Hakuna njia ya mkato. Lazima tusome vitabu vya Injili. Kisha, tunahitaji kutumia wakati kutafakari jinsi masimulizi tuliyosoma yanavyoonyesha njia ya kufikiri ya Yesu kuhusu mambo mbalimbali. Na bila shaka, ni lazima tumwombe Yehova atusaidie kuiga unyenyekevu na subira ya Yesu. Kadiri tunavyositawisha akili ya Kristo, ndivyo tutakavyomwiga Mungu zaidi kwa kuwaonyesha subira zaidi waabudu wenzetu na sisi wenyewe.—Mt. 18:​26-30, 35.

YEHOVA ANAWAHESHIMU WATU WA HALI YA CHINI

15. Yehova ametimizaje maneno yanayopatikana katika Zaburi 138:6?

15 Soma Zaburi 138:6. Ni pendeleo kubwa sana kwa watu wanyenyekevu kutambuliwa na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwenguni pote! Fikiria mifano michache ya watu wa hali ya chini ambao Yehova amewaonyesha heshima. Baadhi yao huenda tusiwakumbuke kwa urahisi, lakini wametajwa katika Biblia. Yehova alimwongoza Musa aandike kuhusu mlezi aliyeitwa Debora, ambaye aliishi katika nyakati za wazee wa ukoo. Alitumikia kwa uaminifu katika nyumba ya Isaka na ya Yakobo kwa jumla ya miaka 125 hivi! Ingawa hatujui mengi kuhusu mwanamke huyo mshikamanifu, Yehova alihakikisha kwamba Musa aliandika jambo linaloonyesha jinsi alivyopendwa. (Mwa. 24:59; 35:​8, maelezo ya chini) Karne nyingi baadaye, Yehova alimchagua Daudi, kijana mchungaji, na kumfanya awe mfalme wa taifa la Israeli. (2 Sam. 22:​1, 36) Muda mfupi baada ya Yesu kuzaliwa, Mungu aliwatuma malaika kwa wachungaji wanyenyekevu na kuwapa pendeleo la kuwa wa kwanza kujua kwamba katika mji jirani wa Bethlehemu, Masihi wa wakati ujao alikuwa amezaliwa. (Luka 2:​8-11) Na Yosefu na Maria walipompeleka Yesu hekaluni, Yehova aliwapa Simeoni na Ana waliokuwa na umri mkubwa pendeleo la kumwona Mwana Wake. (Luka 2:​25-30, 36-38) Naam, “ingawa Yehova yuko juu, yeye huwaona wanyenyekevu”!

16. Yesu aliigaje njia ambayo Baba yake anawatendea wanadamu?

16 Yesu anamwiga Baba yake. Kama tu Baba yake, Yesu anawaonyesha heshima watu wanyenyekevu. Aliwafundisha “watu wasio na elimu na wa kawaida tu” kweli kuhusu Ufalme wa Mungu. (Mdo. 4:13; Mt. 11:25) Pia, Yesu aliwaponya wagonjwa na kuwatendea kwa njia ambayo haikuwarudishia tu afya yao, lakini pia iliwafanya wahisi wameheshimiwa. (Luka 5:13) Katika usiku wa mwisho kabla ya kifo chake, Yesu aliwaosha miguu mitume wake, kazi ambayo ilifanywa na watumishi. (Yoh. 13:5) Na kabla ya kwenda mbinguni, aliwaheshimu wafuasi wake wote wanyenyekevu, kutia ndani sisi leo, kwa kuwapa kazi muhimu zaidi ambayo wanadamu wamewahi kufanya—kuwasaidia wengine kupata uzima wa milele.—Mt. 28:​19, 20.

17. Tunawezaje kuwaonyesha wengine heshima? (Tazama pia picha.)

17 Tunawezaje kumwiga Yehova? Tunawaonyesha heshima watu tunapowahubiria habari njema wote wanaosikiliza, licha ya malezi yao, rangi yao, au kiwango chao cha elimu. Na tunawaheshimu ndugu na dada zetu tunapowaona kuwa bora kuliko sisi, licha ya vipawa au mapendeleo ambayo huenda tunayo. (Flp. 2:3) Yehova anafurahi tunapoonyesha unyenyekevu na ‘kuwa wa kwanza’ katika kuonyeshana heshima katika njia hizo na nyingine.—Rom. 12:10; Sef. 3:12.

Akina dada wawili wakimfundisha Biblia mwanamke aliyefungwa gerezani.

Tunaiga unyenyekevu wa Yehova tunapowahubiria habari njema watu wa namna zote (Tazama fungu la 17)a


18. Kwa nini unataka kuiga unyenyekevu wa Yehova?

18 Kadiri tunavyojitahidi kuiga unyenyekevu wa Baba yetu wa mbinguni anayetupenda, tutakuwa wenye kufikika zaidi, wenye usawaziko zaidi, na wenye subira zaidi. Na tutawaonyesha wengine heshima, kama Yehova anavyofanya. Acheni jitihada zetu za kumkaribia Mungu wetu mwenye sifa ya unyenyekevu, zifanye kila mmoja wetu awe mwenye thamani hata zaidi machoni pake!—Isa. 43:4.

SIFA YA UNYENYEKEVU INAWEZAJE KUKUSAIDIA KUWA . . .

  • mwenye kufikika?

  • mwenye usawaziko?

  • mwenye subira?

WIMBO 159 Mpe Yehova Utukufu

a MAELEZO YA PICHA: Kwa unyenyekevu, akina dada wanamwiga Yehova wanapowafundisha wafungwa gerezani.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki