Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Novemba kur. 16-21
  • Mfikirie Yesu​​—⁠Kuhani Wetu Mkuu Anayetusikitikia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mfikirie Yesu​​—⁠Kuhani Wetu Mkuu Anayetusikitikia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MWANA MPENDWA WA MUNGU AJA DUNIANI
  • YESU AWAONYESHA WATU HISIA-MWENZI
  • JINSI TUNAVYOWEZA KUMWIGA KUHANI WETU MKUU LEO
  • KUHANI WETU MKUU ANAWEZA KUKUSAIDIA
  • Fidia Inatufundisha Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Mambo Tunayojifunza Kutokana na Siku 40 za Mwisho za Yesu Akiwa Duniani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Uwe Mwenye Kiasi Inapohusu Mambo Usiyoyajua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Yehova “Huwaponya Waliovunjika Moyo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Novemba kur. 16-21

MAKALA YA 46

WIMBO 17 “ Nataka”

Mfikirie Yesu—Kuhani Wetu Mkuu Anayetusikitikia

“ Hatuna kuhani mkuu ambaye hawezi kuusikitikia udhaifu wetu.”—EBR. 4:15.

JAMBO KUU

Jinsi sifa ya Yesu ya kutusikitikia na kutuhurumia inavyomfanya astahili kuwa Kuhani Mkuu na jinsi tunavyonufaika leo na huduma zake akiwa kuhani.

1-2. (a) Kwa nini Yehova alimtuma Mwana wake duniani? (b) Tutachunguza nini katika makala hii? (Waebrania 5:​7-9)

MIAKA 2,000 hivi iliyopita, Yehova Mungu alimtuma Mwana wake mpendwa aje duniani. Kwa nini? Sababu moja ni ili kuwakomboa wanadamu kutokana na laana ya dhambi na kifo na kuondoa madhara yaliyosababishwa na Shetani. (Yoh. 3:16; 1 Yoh. 3:8) Yehova alijua pia kwamba maisha ya Yesu duniani akiwa mwanadamu yangemtayarisha zaidi kuwa Kuhani Mkuu ambaye angetusikitikia, angetuonyesha hisia-mwenzi, na huruma. Yesu alianza kutumikia akiwa Kuhani Mkuu baada ya kubatizwa mwaka wa 29 W.K.a

2 Katika makala hii, tutachunguza jinsi maisha ya Yesu akiwa duniani yalivyomsaidia astahili zaidi kuwa Kuhani Mkuu anayetusikitikia. Tunapoongeza uelewaji wetu kuhusu jinsi Yesu ‘alivyofanywa kuwa mkamilifu’ kwa ajili ya jukumu hilo, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwetu kumkaribia Yehova, hata ikiwa tumevunjika moyo kwa sababu ya dhambi au udhaifu wetu.—Soma Waebrania 5:​7-9.

MWANA MPENDWA WA MUNGU AJA DUNIANI

3-4. Yesu alipitia mabadiliko gani makubwa alipokuja duniani?

3 Wengi wetu tumewahi kupitia mabadiliko maishani, kama vile kuhama kutoka katika nyumba tunayoipenda na kuwaacha watu wa familia na marafiki. Mabadiliko hayo yanaweza kutokeza changamoto. Lakini hakuna mwanadamu aliyepitia mabadiliko mengi kama ambayo Yesu alipitia. Alipokuwa mbinguni, alikuwa Mwana wa kwanza wa kiroho wa Yehova na wa muhimu zaidi. Alipendwa na Yehova na sikuzote alikuwa na shangwe kwa sababu alitumikia kwenye ‘mkono wa kuume’ wa Mungu. (Zab. 16:11; Met. 8:30) Hata hivyo, Wafilipi 2:7 inasema kwamba kwa hiari “alijiondolea hali yake,” na kukubali kuacha cheo chake cha juu mbinguni ili aishi miongoni mwa wanadamu wasio wakamilifu duniani.

4 Pia, fikiria hali zilizohusika Yesu alipozaliwa, na katika maisha yake ya mapema alipokuwa duniani. Yesu alizaliwa katika familia maskini, kama inavyoonyeshwa na dhabihu ambayo wazazi wake walitoa alipozaliwa. (Law. 12:8; Luka 2:24) Aliposikia kuhusu kuzaliwa kwa Yesu, mfalme mwovu Herode alijaribu kumuua. Ili kumkimbia Herode, familia hiyo ilikimbilia Misri kwa kipindi fulani. (Mt. 2:​13, 15) Hilo lilikuwa badiliko kubwa sana kwa Yesu ikilinganishwa na maisha yake kabla ya kuwa mwanadamu!

5. Yesu alijionea nini duniani, na mambo hayo yalimtayarishaje kwa ajili ya jukumu lake akiwa Kuhani Mkuu? (Tazama pia picha.)

5 Yesu alipokuwa duniani, aliona watu wengi wakiteseka. Bila shaka, alikabili hisia zinazotokana na kuwapoteza watu anaowapenda katika kifo, inaelekea kutia ndani Yosefu, baba yake wa kambo. Wakati wa huduma yake, Yesu alikutana na watu wenye ukoma, vipofu, waliopooza, na wazazi waliofiwa, naye aliwahurumia. (Mt. 9:​2, 6; 15:30; 20:34; Marko 1:​40, 41; Luka 7:13) Ni kweli kwamba alipokuwa katika cheo chake cha juu mbinguni, Yesu alikuwa amewaona wanadamu wakiteseka. Lakini sasa, akiwa mwanadamu duniani, alijionea maumivu ya wanadamu kwa njia mpya. (Isa. 53:4) Maisha ya Yesu duniani yalimsaidia kuelewa hisia, changamoto, na maumivu ya wanadamu. Yeye mwenyewe alipata hisia ambazo wanadamu hupata, kutia ndani maumivu makali, uchovu, na huzuni.

Yesu amezungukwa na kikundi cha watu wanaomsihi awaponye magonjwa yao. Kwa huruma ananyoosha mikono yake na kushika mikono ya mwanamume mwenye umri mkubwa aliye mgonjwa.

Yesu alikuwa na huruma kuelekea watu waliomzunguka na alijali sana kuhusu mateso waliyopitia (Tazama fungu la 5)


YESU AWAONYESHA WATU HISIA-MWENZI

6. Lugha ya picha aliyotumia Isaya inatufundisha nini kuhusu huruma aliyoonyesha Yesu? (Isaya 42:3)

6 Katika huduma yake yote, Yesu aliwaonyesha hisia-mwenzi watu walio dhaifu na waliodharauliwa. Kwa kufanya hivyo, alitimiza unabii. Katika Maandiko ya Kiebrania, pindi fulani watu wenye ufanisi na nguvu wanafananishwa na bustani yenye rutuba au miti mikubwa mirefu. (Zab. 92:12; Isa. 61:3; Yer. 31:12) Lakini maskini na waliokandamizwa wanalinganishwa na tete lililovunjika na utambi unaofifia wa taa, vitu ambavyo kwa wengi havina thamani. (Soma Isaya 42:3; Mt. 12:20) Akiongozwa na roho, nabii Isaya alitumia lugha hiyo ya picha kutabiri kuhusu upendo na huruma ambayo Yesu angewaonyesha watu wa kawaida ambao walioonwa kuwa hawana thamani.

7-8. Yesu alitimizaje unabii wa Isaya?

7 Mwandikaji wa Injili, Mathayo, alionyesha kwamba Yesu alitimiza maneno haya ya Isaya: “Hataponda tete lililovunjika, wala hatazima utambi unaofifia.” Baadhi ya miujiza ya Yesu iliwanufaisha wale waliokandamizwa ambao ni lazima walijihisi kama tete lililovunjika au wale ambao walikosa tumaini na kuhisi kama utambi unaofifia ambao unakaribia kuzimwa. Kwa mfano, kulikuwa na mwanamume mmoja ambaye alikuwa amejaa ukoma. Ni lazima alihisi kwamba hana tumaini la kuponywa na kufurahia ushirika pamoja na watu wa familia na marafiki. (Luka 5:​12, 13) Pia, kulikuwa na mwanamume aliyekuwa kiziwi na mwenye tatizo la kuzungumza. Wazia jinsi alivyohisi alipowaona wengine wakizungumza kwa uchangamfu lakini hakuweza kuwaelewa. (Marko 7:​32, 33) Hata hivyo, kuna mengi zaidi.

8 Katika siku za Yesu, Wayahudi wengi waliamini kwamba wale waliokuwa wanateseka walikuwa wakiadhibiwa kwa sababu ya dhambi zao wenyewe au dhambi za wazazi wao. (Yoh. 9:2) Kwa sababu ya mafundisho hayo ya uwongo, watu walioteseka walifanywa wahisi kwamba hawana thamani. Akitimiza unabii wa Isaya, Yesu aliwaponya kimwili watu hao walioteseka na kurudisha tena tumaini lao katika Mungu. Jambo hilo linatupatia uhakika gani?

9. Andiko la Waebrania 4:​15, 16 linaonyeshaje kwamba Kuhani wetu Mkuu aliye mbinguni anawasikitikia kikweli wanadamu wasio wakamilifu?

9 Soma Waebrania 4:​15, 16. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote Yesu atatusikitikia. Hilo linamaanisha nini? Mtu anayewasikitikia wengine ni yule anayeguswa moyo na mateso na hisia za mtu mwingine. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kusikitikia” linamaanisha kuhisi kama mtu mwingine anavyohisi. Katika Waebrania 10:​34, Paulo alitumia neno hilohilo la Kigiriki kuonyesha kwamba tuna hisia-mwenzi kuelekea wale walio gerezani. Masimulizi ya miujiza aliyofanya Yesu yanaonyesha jinsi ambavyo Yesu alihangaishwa sana alipoona wengine wanateseka. Hakuwaponya watu ili kutimiza tu wajibu. Aliwajali kikweli na alitaka kuwasaidia. Kwa mfano, alipomponya mtu mwenye ukoma, angeweza kufanya muujiza huo akiwa mbali, badala yake alichochewa kumgusa mwanamume huyo—na huenda Yesu alikuwa mtu wa kwanza kumgusa mwanamume huyo baada ya miaka mingi! Yesu alionyesha ufikirio alipomtoa na kumpeleka mwanamume kiziwi mbali na eneo lenye kelele za umati, kisha akamponya faraghani. Na Farisayo alipomdharau mwanamke aliyetubu ambaye alikuwa ameosha miguu ya Yesu kwa machozi yake na kuifuta kwa nywele zake, Yesu alimtetea kwa bidii. (Mt. 8:3; Marko 7:33; Luka 7:44) Yesu hakuwapuuza watu walioteseka kwa sababu ya magonjwa au wale waliotenda dhambi nzito. Badala yake, aliwakaribisha na kwa huruma aliwahakikishia watu hao kwamba wanapendwa. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu anatusikitikia kwa njia hiyohiyo.

JINSI TUNAVYOWEZA KUMWIGA KUHANI WETU MKUU LEO

10. Tunaweza kutumia maandalizi gani ya kiroho leo ili kuwasaidia viziwi na vipofu? (Tazama pia picha.)

10 Tukiwa wafuasi waaminifu wa Yesu, tunajitahidi kumwiga inapohusu kuonyesha upendo, hisia-mwenzi, na huruma. (1 Pet. 2:21; 3:8) Ingawa hatuwezi kuwaponya viziwi au vipofu, bila shaka tunaweza kuwasaidia watu hao kiroho. Kwa mfano, machapisho yanayotegemea Biblia yanapatikana katika lugha za ishara zaidi ya 100. Na ili kuwanufaisha vipofu, machapisho katika maandishi ya vipofu yanapatikana katika lugha zaidi ya 60 na maelezo ya video huandaliwa katika lugha zaidi ya 100. Maandalizi hayo huwasaidia viziwi na vipofu kumkaribia Yehova na Mwana wake.

Mkusanyo wa picha: 1. Ndugu na dada wakiimba wimbo wa Ufalme kwa lugha ya ishara katika mkutano wa kutaniko la lugha ya ishara. 2. Dada aliye kipofu akisoma Biblia iliyo katika maandishi ya vipofu.

Machapisho yetu yanayotegemea Biblia yanapatikana katika lugha zaidi ya 1,000

Kushoto: Zaidi ya lugha 100 za ishara

Kulia: Zaidi ya lugha 60 katika maandishi ya vipofu

(Tazama fungu la 10)


11. Tengenezo la Yehova linaigaje hangaiko la Yesu kuelekea watu kutoka malezi mbalimbali? (Matendo 2:​5-7, 33) (Tazama pia picha.)

11 Tengenezo la Yehova linajitahidi kuwasaidia watu kutoka malezi mbalimbali. Kumbuka kwamba baada ya kufufuliwa, Yesu alimimina roho takatifu juu ya wanafunzi wake ili wote waliokusanyika kwa ajili ya sherehe ya Pentekoste waweze kusikia habari njema, kila mmoja “katika lugha yake mwenyewe.” (Soma Matendo 2:​5-7, 33.) Kwa kufuata mwongozo wake, tengenezo hutoa machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha zaidi ya 1,000, na baadhi ya lugha hizo huzungumzwa na watu wachache. Kwa mfano, baadhi ya lugha za wenyeji wa asili wa Amerika zinazungumzwa na watu wachache wanaoishi Amerika Kaskazini na Kusini. Hata hivyo, machapisho yametayarishwa katika lugha zaidi ya 160 za wenyeji wa asili wa Amerika ili kuhakikisha kwamba watu wengi iwezekanavyo wanaweza kupata habari njema. Machapisho yetu yanapatikana pia katika lugha zaidi ya 20 za Kiromani. Maelfu ya watu wanaozungumza lugha hizo wamekubali kweli.

Mkusanyo wa picha: 1. Dada aliye mwenyeji wa asili wa Amerika anatabasamu huku akiwa amekumbatia Biblia iliyo katika lugha yake. 2. Dada Mromani na binti yake wakifurahia programu ya kitheokrasi.

Kushoto: Zaidi ya lugha 160 za wenyeji wa asili wa Amerika

Kulia: Zaidi ya lugha 20 za Kiromani

(Tazama fungu la 11)


12. Tengenezo la Yehova linatoa msaada gani mwingine hususa?

12 Mbali na kusimamia jitihada hizo za kueneza habari njema, tengenezo la Yehova linatoa misaada kwa ajili ya wale walioathiriwa na majanga ya asili. Hivyo, maelfu ya wajitoleaji huwa tayari kuwasaidia ndugu na dada zao wenye uhitaji. Tengenezo pia linasaidia kuandaa sehemu za ibada ambapo watu wanaweza kukusanyika pamoja ili kujifunza zaidi kuhusu upendo wa Mungu kuwaelekea.

KUHANI WETU MKUU ANAWEZA KUKUSAIDIA

13. Taja baadhi ya njia ambazo Yesu anatumia ili kutusaidia.

13 Akiwa mchungaji wetu mwema, Yesu anahakikisha kwamba kila mmoja wetu anapata mahitaji yake ya kiroho. (Yoh. 10:14; Efe. 4:7) Nyakati fulani, hali maishani zinaweza kutufanya tuhisi kama utambi unaofifia au tete lililovunjika. Huenda tukavunjika moyo sana kwa sababu ya tatizo kubwa la afya, kosa tulilofanya, au kwa sababu ya kutokuwa na uhusiano mzuri na mwabudu mwenzetu. Na tunaweza kukazia fikira maumivu tunayopata sasa, badala ya tumaini letu la wakati ujao. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yesu anaona mambo unayopitia na anaelewa mawazo yako ya ndani kabisa. Huruma ya Yesu humchochea kutenda kwa niaba yako. Kwa mfano, anaweza kutumia roho takatifu kukupatia nguvu unapokuwa dhaifu. (Yoh. 16:7; Tito 3:6) Kwa kuongezea, Yesu anaweza kutumia ‘wanaume walio zawadi’ na waabudu wenzako ili kukutia moyo, kukutegemeza, na kukusaidia.—Efe. 4:8.

14. Tunaweza kufanya nini tunapovunjika moyo?

14 Ikiwa umevunjika moyo, tafakari kuhusu jukumu la Yesu akiwa Kuhani wetu Mkuu. Kumbuka kwamba Yehova alimtuma duniani ili atoe uhai wake kama fidia na pia kumsaidia aelewe vizuri matatizo wanayokabili wanadamu wasio wakamilifu. Tunapovunjika moyo kwa sababu ya dhambi au udhaifu tulio nao, Yesu yuko tayari kutusaidia kwa “wakati unaofaa.”—Ebr. 4:​15, 16, maelezo ya chini.

15. Toa mfano unaoonyesha jinsi ambavyo mtu aliyepotea mbali na kundi la Yehova anaweza kusaidiwa kurudi katika kutaniko.

15 Yesu pia anawaongoza watu wake katika jitihada zao za kuwatafuta na kuwasaidia wale waliopotea mbali na kundi la Yehova. (Mt. 18:​12, 13) Fikiria kisa cha Stefano.b Baada ya kuondolewa kutanikoni kwa miaka 12, aliamua kuhudhuria mkutano. Anasema hivi: “Haikuwa rahisi kwangu, lakini nilitaka tena kuwa sehemu ya familia ya Yehova yenye upendo. Wazee waliozungumza nami walinifanya nihisi nimekaribishwa. Pindi fulani, nilihisi kwamba sifai, na nilitaka kukata tamaa. Lakini akina ndugu walinikumbusha kwamba Yehova na Yesu walitaka nisikate tamaa. Niliporudishwa, kutaniko zima lilinikaribisha mimi na familia yangu kwa uchangamfu. Hatimaye, mke wangu alikubali funzo la Biblia, na leo tunamtumikia Yehova tukiwa familia.” Ni lazima Kuhani wetu Mkuu mwenye upendo anafurahi sana anapowaona wale wanaotubu wakipata msaada wanaohitaji na kurudi kutanikoni!

16. Kwa nini unashukuru sana kwamba tuna Kuhani Mkuu anayetusikitikia?

16 Wakati wa maisha yake duniani, Yesu aliwasaidia watu wengi kwa wakati unaofaa. Leo, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba atatupatia msaada wakati wowote tunapouhitaji. Na katika ulimwengu mpya unaokuja hivi karibuni, atawasaidia wanadamu wote watiifu wawekwe huru kikamili kutokana na madhara ya dhambi na kutokuwa wakamilifu. Tunamshukuru sana Yehova, Mungu wetu, ambaye kwa upendo wake mkubwa na rehema nyingi, alimweka rasmi Mwana wake awe Kuhani wetu Mkuu anayetusikitikia!

UNGEJIBUJE?

  • Maisha ya Yesu duniani yalimtayarishaje kutumikia akiwa Kuhani wetu Mkuu?

  • Yesu alitimizaje Isaya 42:3?

  • Kuhani wetu Mkuu anatusaidiaje leo?

WIMBO 13 Kristo, Kielelezo Chetu

a Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ambavyo jukumu la Yesu akiwa kuhani mkuu lilivyochukua nafasi ya kuhani mkuu wa Kiyahudi, tazama makala “Thamini Pendeleo Lako la Kuabudu Katika Hekalu la Kiroho la Yehova” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 2023, uku. 26, fu. 7-9.

b Jina limebadilishwa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki