Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Novemba kur. 22-27
  • “Wewe Ni Mtu Mwenye Thamani Sana”!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Wewe Ni Mtu Mwenye Thamani Sana”!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINSI YESU ALIVYOWASAIDIA WATU WATAMBUE THAMANI YAO
  • JINSI YA KUJIONA KAMA YEHOVA ANAVYOTUONA
  • “Nimemwona Bwana! ”
    Tembea na Mungu kwa Ujasiri
  • Yehova “Huwaponya Waliovunjika Moyo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Yehova Anakuonyesha Upendo Mwororo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Mambo Tunayojifunza Kutokana na Siku 40 za Mwisho za Yesu Akiwa Duniani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Novemba kur. 22-27

MAKALA YA 47

WIMBO 38 Atakupa Nguvu

“ Wewe Ni Mtu Mwenye Thamani Sana”!

“ Wewe ni mtu mwenye thamani sana.”—DAN. 9:23.

JAMBO KUU

Kuwasaidia wale wanaohisi kwamba hawana thamani waelewe thamani yao ya kweli machoni pa Yehova.

1-2. Tunawezaje kuanza kukubali kwamba tuna thamani machoni pa Yehova?

MIONGONI mwa watumishi wenye thamani wa Yehova, kuna baadhi yao ambao wanahisi kwamba hawana thamani. Labda mtu fulani aliwatendea kana kwamba hawana thamani yoyote. Je, umekabili hali kama hiyo? Ikiwa ndivyo, unawezaje kuanza kukubali kwamba wewe ni mwenye thamani machoni pa Yehova?

2 Jambo moja linaloweza kukusaidia ni kuchunguza masimulizi ya Biblia yanayofunua jinsi ambavyo Yehova anataka watu watendewe. Yesu, Mwana wake, aliwatendea watu kwa staha na heshima. Kwa kufanya hivyo, alionyesha kwamba yeye na Baba yake wanawathamini sana watu wanyenyekevu wanaohisi kwamba hawana thamani. (Yoh. 5:19; Ebr. 1:3) Katika makala hii, tutachunguza: (1) jinsi Yesu alivyowasaidia watu watambue thamani yao na (2) jinsi tunavyoweza kujihakikishia wenyewe kwamba kwa kweli sisi ni wenye thamani machoni pa Mungu.—Hag. 2:7.

JINSI YESU ALIVYOWASAIDIA WATU WATAMBUE THAMANI YAO

3. Yesu aliwatendeaje Wagalilaya waliotafuta msaada kutoka kwake?

3 Katika safari yake ya tatu ya kuhubiri kwenye eneo la Galilaya, watu kutoka maeneo mbalimbali walimfuata Yesu, wakamsikiliza na kuponywa magonjwa yao. Yesu alisema kwamba “walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:36; tazama habari za utafiti, nwtsty.) Viongozi wao wa kidini waliwadharau watu hao, na hata waliwaita “watu waliolaaniwa.” (Yoh. 7:​47-49; habari za utafiti, nwtsty) Lakini Yesu aliwaonyesha heshima kwa kutumia wakati kuwafundisha na kuwaponya magonjwa yao. (Mt. 9:35) Zaidi ya hayo, ili kuwasaidia watu wengi zaidi, aliwazoeza mitume wake katika kazi ya kuhubiri na kuwapatia mamlaka ya kuponya magonjwa.—Mt. 10:​5-8.

4. Tunajifunza nini kupitia jinsi ambavyo Yesu aliwatendea wasikilizaji wake wanyenyekevu?

4 Kwa kuwatendea wasikilizaji wake kwa heshima na ufikirio, Yesu alionyesha kwamba yeye na Baba yake wanawaona watu ambao mara nyingi wanadharauliwa katika jamii, kuwa wenye thamani. Ikiwa unamtumikia Yehova lakini una shaka kuhusu thamani yako, fikiria kuhusu jinsi ambavyo Yesu aliwatendea watu wanyenyekevu waliotaka kujifunza kutoka kwake. Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia kuona jinsi ambavyo wewe ni mwenye thamani sana machoni pa Yehova.

5. Fafanua hali alizokabili mwanamke Mgalilaya aliyekutana na Yesu.

5 Yesu alifundisha umati wa watu, na pia alimsaidia mtu mmoja-mmoja. Kwa mfano, alipokuwa akihubiri katika eneo la Galilaya, Yesu alikutana na mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu kwa miaka 12. (Marko 5:25) Kwa kuwa ugonjwa wake ulimfanya asiwe safi kisherehe, mtu yeyote ambaye angemgusa asingekuwa safi. Ni lazima jambo hilo lilimzuia kushirikiana na watu kwa uhuru. Zaidi ya hilo, hangeweza kushirikiana na wengine katika maadhimisho na sherehe nyingine zilizohusisha ibada za hadharani. (Law. 15:​19, 25) Bila shaka, mwanamke huyo aliteseka kimwili na kihisia pia.—Marko 5:26.

6. Mwanamke mwenye mtiririko wa damu aliponywa jinsi gani?

6 Mwanamke huyo aliyeteseka sana alitaka Yesu amponye. Lakini hakumfuata moja kwa moja. Kwa nini? Huenda aliaibika kwa sababu ya hali yake. Au huenda aliogopa kwamba Yesu angemkataa kwa sababu aliingia katikati ya umati wakati hakuwa safi kisherehe. Hivyo, aliligusa tu vazi la nje la Yesu, akiwa na uhakika kwamba tendo hilo pekee lingemfanya aponywe. (Marko 5:​27, 28) Imani yake ilithawabishwa—na aliponywa. Kisha Yesu akauliza ni nani aliyemgusa, na mwanamke huyo akakiri kwamba yeye ndiye aliyemgusa. Yesu alimtendeaje?

7. Yesu alimtendeaje mwanamke ambaye alikuwa akiteseka sana? (Marko 5:34)

7 Yesu alimtendea mwanamke huyo kwa fadhili na heshima. Alitambua kwamba alikuwa “akitetemeka kwa hofu.” (Marko 5:33) Akizingatia hisia zake, alizungumza naye kwa fadhili na kumtia moyo. Hata alimwita “binti yangu”—maneno ya upendo ambayo hayakuonyesha tu kwamba anamheshimu, bali pia yalionyesha fadhili na wororo. (Soma Marko 5:34.) Ni sehemu hii tu katika Biblia ambapo Yesu anamwita mwanamke “binti.” Inaelekea alitumia neno hilo lenye fadhili katika hali hiyo kwa sababu aliona kwamba mwanamke huyo alikuwa na hofu sana. Wazia jinsi mwanamke huyo alivyofurahi! Ikiwa Yesu hangezungumza naye kwa fadhili na kumtia moyo, huenda angeondoka akiwa ameponywa kimwili lakini akiwa amelemewa na hisia za hatia. Badala yake, Yesu alimsaidia atambue kwamba yeye ni binti mwenye thamani wa Baba wa mbinguni mwenye upendo.

8. Dada kutoka nchini Brazili alikabili changamoto gani?

8 Leo pia, baadhi ya watumishi wa Mungu wanakabiliana na matatizo ya afya yanayowaathiri kihisia. Maria,a painia wa kawaida nchini Brazili, alizaliwa na ulemavu wa kutokuwa na miguu yote miwili na mkono wa kushoto. Anaeleza hivi: “Sikuzote nilinyanyaswa shuleni kwa sababu ya ulemavu wangu. Niliitwa majina ya utani yenye kuumiza. Hata nilibaguliwa na watu wa familia yetu.”

9. Maria alisaidiwa jinsi gani ajione kuwa mwenye thamani kwa Yehova?

9 Maria alipataje msaada? Alipokuwa Shahidi wa Yehova, Wakristo wenzake walimfariji na kumsaidia ajione kama Yehova anavyomwona. Anasema hivi: “Nafasi haitoshi katika kitabu changu ya kuandika kuhusu kila mtu aliyenisaidia! Ninamshukuru sana Yehova kwa moyo wangu wote kwa kunipatia familia maridadi ya kiroho.” Ndugu na dada wa kiroho wa Maria walimsaidia atambue kwamba yeye ni mwenye thamani machoni pa Mungu.

10. Maria Magdalene alikabili matatizo gani? (Tazama pia picha.)

10 Fikiria jinsi Yesu alivyomsaidia mtu mwingine—Maria Magdalene. Alikuwa na roho waovu saba! (Luka 8:2) Inaelekea alitenda kwa njia za ajabu kwa sababu ya uvutano wa roho waovu, na matokeo ni kwamba watu wengine walimwepuka. Wakati huo mbaya maishani mwake, ni lazima alihisi ametengwa, hayuko salama, na bila msaada wowote. Yesu aliwatoa roho hao waovu saba waliomsumbua, na Maria Magdalene akawa mwanafunzi wake mwenye bidii. Yesu alimsaidia Maria Magdalene kwa njia gani nyingine kuelewa jinsi alivyo mwenye thamani sana kwa Mungu?

Mkusanyo wa picha: 1. Yesu akimtazama Maria Magdalene ambaye amepiga magoti ardhini kwenye kijia chenye giza. 2. Maria Magdalene akiandamana kwa shangwe pamoja na Yesu na wanafunzi wengine.

Yesu alimhakikishiaje Maria Magdalene kwamba yeye ni mwenye thamani kwa Yehova? (Tazama fungu la 10-11)


11. Yesu alimwonyeshaje Maria Magdalene kwamba alikuwa mwenye thamani kwa Mungu? (Tazama pia picha.)

11 Yesu alimwalika Maria Magdalene aambatane naye katika safari zake alipokuwa akihubiri.b Matokeo ni kwamba aliendelea kunufaika alipomsikia Yesu akiwafundisha wengine. Pia, siku ileile alipofufuliwa, Yesu alimtokea Maria Magdalene. Alikuwa kati ya wanafunzi wa kwanza aliozungumza nao siku hiyo. Yesu hata alimpatia mgawo wa kuwaeleza mitume wake kwamba amefufuliwa. Huo ni uthibitisho mzuri kwamba kwa kweli Maria Magdalene alikuwa mwenye thamani machoni pa Yehova!—Yoh. 20:​11-18.

12. Eleza kwa nini malezi ya Lidia yalimfanya ajione kuwa hana thamani.

12 Kama ambavyo huenda ilikuwa kwa Maria Magdalene, wengi leo wanapambana na hisia za kujiona hawana thamani. Lidia, dada kutoka nchini Hispania, anasema kwamba kabla ya kuzaliwa, mama yake alikuwa akifikiria kutoa mimba yake. Hata alipokuwa mtoto, Lidia anakumbuka kwamba mama yake hakumjali na alimtukana. Anasema hivi: “Lengo langu maishani lilikuwa kukubaliwa na kupendwa na watu wengine. Niliogopa kwamba sitawahi kustahili upendo huo kwa sababu mama yangu alikuwa amefanya niamini kwamba nilikuwa mtu mbaya.”

13. Ni nini kilichomsaidia Lidia ajione kuwa mwenye thamani kwa Yehova?

13 Baada ya Lidia kujifunza kweli, sala na funzo la kibinafsi pamoja na maneno na matendo yenye fadhili kutoka kwa Wakristo wenzake, yalimsaidia kuelewa kwamba yeye ni mwenye thamani machoni pa Yehova. Anasema hivi: “Mara nyingi mume wangu ananiambia jinsi anavyonipenda sana. Tena na tena, ananikumbusha kuhusu sifa zangu nzuri. Marafiki wangu wengine wapendwa wanafanya vivyo hivyo.” Je, unaweza kumfikiria mtu anayehitaji msaada wa kukubali kwamba yeye ni mwenye thamani machoni pa Yehova?

JINSI YA KUJIONA KAMA YEHOVA ANAVYOTUONA

14. Andiko la 1 Samweli 16:7 linatusaidiaje kutambua maoni ya Yehova kuhusu watu? (Tazama pia sanduku “Kwa Nini Yehova Anawathamini Watu Wake?”)

14 Kumbuka kwamba Yehova hakuoni kama ulimwengu unavyokuona. (Soma 1 Samweli 16:7.) Hapimi thamani yako kwa kutegemea mwonekano wako, hali yako ya kiuchumi, au elimu yako. (Isa. 55:​8, 9) Badala ya kupima thamani yako kwa kutegemea viwango vya ulimwengu, pima thamani yako kwa kutegemea viwango vya Yehova. Unaweza kusoma masimulizi ya Biblia yanayoonyesha kwamba Yehova aliwaona watu ambao walitilia shaka thamani yao kuwa wenye thamani, kwa mfano Eliya, Naomi, na Hana. Unaweza pia kuandika mambo uliyojionea maishani yanayothibitisha kwamba Yehova anakuona kuwa mwenye thamani na anakupenda kikweli. Kwa kuongezea, unaweza kusoma habari zinazopatikana katika machapisho yetu zinazozungumzia jinsi ya kuwa na maoni yanayofaa kujihusu.c

Kwa Nini Yehova Anawathamini Watu Wake?

Yehova aliwaumba wanadamu kwa njia tofauti kabisa na wanyama. Alituumba tukiwa na uwezo wa kusitawisha uhusiano pamoja naye na kuwa rafiki zake. (Mwa. 1:27; Zab. 8:5; 25:14; Isa. 41:8) Jambo hilo pekee linatosha kutupatia sababu ya kuwa na mtazamo mzuri kujihusu. Hata hivyo, tunapata sababu kubwa hata zaidi ya kuwa na mtazamo mzuri kujihusu tunapojitahidi kumkaribia zaidi Yehova, kujiweka wakfu kwake, na kumtii. Tunapofanya hivyo, tunakuwa wenye thamani kwelikweli kwa Mungu na Muumba wetu.—Isa. 49:15.

15. Kwa nini Yehova alimwona Danieli kuwa “mtu mwenye thamani sana”? (Danieli 9:23)

15 Tambua kwamba uaminifu wako unakufanya uwe mwenye thamani machoni pa Yehova. Pindi moja, huenda mwishoni mwa miaka yake ya 90, nabii Danieli alihisi ‘amechoka kwelikweli’ na kuvunjika moyo. (Dan. 9:​20, 21) Yehova alimtiaje moyo? Mungu alimtuma malaika Gabrieli ili amkumbushe Danieli kwamba alikuwa “mtu mwenye thamani sana” na sala zake zilikuwa zimesikilizwa. (Soma Danieli 9:23.) Ni mambo gani yaliyomfanya Danieli awe mwenye thamani sana kwa Mungu? Alipenda uadilifu na alikuwa mwaminifu. (Eze. 14:14) Yehova alihifadhi simulizi hilo katika Neno lake ili kutufariji. (Rom. 15:4) Yehova anasikiliza pia sala zako na anakuthamini kwa sababu unapenda yaliyo sawa na unamtumikia kwa uaminifu.—Mika 6:​8, maelezo ya chini; Ebr. 6:10.

16. Ni nini kinachoweza kukusaidia kumwona Yehova kuwa Baba mwenye upendo?

16 Mwone Yehova kuwa Baba anayekupenda. Yehova anataka kukusaidia, wala si kutafuta makosa yako. (Zab. 130:3; Mt. 7:11; Luka 12:​6, 7) Kutafakari kuhusu hilo kumewasaidia watu wengi wenye hisia za kujiona kwamba hawafai. Kwa mfano, mfikirie Eliana, dada kutoka nchini Hispania ambaye alihisi hapendwi na hafai baada ya kutukanwa na kuambiwa maneno yenye kuumiza kwa miaka mingi na mume wake. Anasema hivi: “Kila mara ninapohisi kwamba sipendwi, ninajaribu kumwazia Yehova akinibeba katika mikono yake na kunionyesha upendo na kunilinda.” (Zab. 28:9) Lauren, dada kutoka nchini Afrika Kusini, anajikumbusha hivi: “Ikiwa Yehova kwa fadhili amenivuta kwake kwa kamba za upendo, ameniweka karibu naye miaka hii yote, na hata amenitumia kuwafundisha wengine, basi kwa kweli ananiona kuwa mtu mwenye thamani na anayehitajika.”—Hos. 11:4.

17. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuwa na uhakika kwamba una kibali cha Yehova? (Zaburi 5:12) (Tazama pia picha.)

17 Uwe na uhakika kwamba una kibali cha Yehova. (Soma Zaburi 5:12.) Daudi alilinganisha kibali cha Yehova na “ngao kubwa” inayowalinda watu waadilifu. Kujua kwamba una kibali na msaada wa Yehova kunaweza kukulinda dhidi ya kulemewa na hisia za kujiona kwamba hufai. Unawezaje kujua kwamba una kibali cha Yehova? Kama tulivyoona, Yehova anakupatia uhakikisho huo kupitia Neno lake. Kwa kuongezea, anatumia wazee, marafiki wa karibu, na watu wengine kukukumbusha kwamba wewe ni mwenye thamani machoni pake. Unapaswa kuhisije unapotiwa moyo kwa njia hiyo?

Dada akitabasamu anapotoka katika Jumba la Ufalme akielekea katika huduma ya shambani pamoja na dada mwingine ambaye amemkumbatia.

Kujua kwamba tuna kibali cha Yehova kunaweza kutusaidia kuepuka hisia za kujiona kwamba hatufai (Tazama fungu la 17)


18. Kwa nini unapaswa kukubali maneno ya pongezi?

18 Usikatae pongezi za unyoofu kutoka kwa wale wanaokujua na kukupenda. Kumbuka kwamba huenda Yehova anawatumia kukusaidia ukubali kwamba una kibali chake. Eliana, aliyetajwa awali, anasema hivi: “Hatua kwa hatua, nimeanza kujifunza kukubali moyoni mwangu maneno ya fadhili ambayo wengine wananiambia. Si rahisi, lakini ninajua kwamba hilo ndilo jambo ambalo Yehova anataka nifanye.” Eliana amenufaika kutokana na jitihada zenye upendo za wazee. Sasa anatumikia akiwa painia na mjitoleaji wa Betheli anayefanyia kazi nyumbani.

19. Kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba wewe ni mwenye thamani machoni pa Mungu?

19 Kwa fadhili, Yesu anatukumbusha kwamba sisi ni wenye thamani sana kwa Baba yetu wa mbinguni. (Luka 12:24) Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anatuona kuwa wenye thamani. Tusisahau hilo kamwe! Na acheni tufanye yote tuwezayo kuwasaidia wengine waona jinsi walivyo wenye thamani sana machoni pa Mungu!

UNGEJIBUJE?

  • Yesu aliwasaidiaje watu watambue kwamba wana thamani machoni pa Mungu?

  • Yesu alimsaidiaje mwanamke aliyekuwa akiteseka kwa sababu ya mtiririko wa damu?

  • Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kujiona kama Yehova anavyotuona?

WIMBO 139 Wazia Wakati Vitu Vyote Vitakuwa Vipya

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Maria Magdalene alikuwa mmoja kati ya wanawake waliosafiri na Yesu. Kwa kutumia mali zao wenyewe, wanawake hao walimtunza Yesu na mitume wake.—Mt. 27:​55, 56; Luka 8:​1-3.

c Kwa mfano, tazama sura ya 24 katika kitabu Mkaribie Yehova na pia soma maandiko na masimulizi ya Biblia yaliyopendekezwa chini ya kichwa “Shaka” katika kitabu Maandiko kwa Ajili ya Maisha ya Mkristo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki