MAKALA YA 45
WIMBO 111 Sababu za Kuwa na Shangwe
Dumisha Shangwe Yako Unapowatunza Wapendwa Wako
“ Wale wanaopanda mbegu kwa machozi watavuna kwa kelele za shangwe.”—ZAB. 126:5.
JAMBO KUU
Jinsi wale wanaowatunza wapendwa wao wanavyoweza kushughulikia changamoto za kipekee wanazokabili na kudumisha shangwe yao.
1-2. Yehova anahisije kuhusu wale wanaowatunza wapendwa wao? (Methali 19:17) (Tazama pia picha.)
NDUGU kutoka nchini Korea anayeitwa Jin-yeol anasema hivi: “Mimi na mke wangu tumefunga ndoa kwa miaka zaidi ya 32. Kwa miaka mitano iliyopita, nimekuwa nikimtunza. Ana ugonjwa wa kutetemeka (Parkinson’s disease) unaofanya iwe vigumu kwake kutembea. Ninampenda na ninamthamini mke wangu, na ninafurahia kumtunza. Kila usiku, analala katika kitanda maalumu kwa ajili ya wagonjwa kilicho nyumbani kwetu. Mimi hulala kando yake, nasi hushikana mikono tunapolala.”
2 Je, wewe unamtunza mpendwa wako, kama vile mzazi, mwenzi, mtoto, au rafiki? Ikiwa ndivyo, inaelekea unathamini pendeleo la pekee la kumsaidia mpendwa wako kwa njia hiyo ya kibinafsi. Na unapomtunza mpendwa wako, unaonyesha kwamba unampenda Yehova. (1 Tim. 5:4, 8; Yak. 1:27) Hata hivyo, unakabili changamoto ambazo mara nyingi wengine hawazitambui. Pindi nyingine, huenda hata ukahisi kwamba ni wewe tu unayeteseka. Huenda ukatabasamu unapokuwa na watu, lakini unapokuwa peke yako unalia. (Zab. 6:6) Ingawa huenda wengine wasitambue changamoto zako, sikuzote Yehova anazitambua. (Linganisha Kutoka 3:7.) Anathamini machozi na kujidhabihu kwako. (Zab. 56:8; 126:5) Anatambua kila kitu unachofanya ili kumsaidia mpendwa wako. Yehova anaona ni kana kwamba unamkopesha na anaahidi kukulipa.—Soma Methali 19:17.
Je, una mpendwa wako ambaye unamtunza? (Tazama fungu la 2)
3. Ni changamoto gani ambazo huenda Abrahamu na Sara walipata walipokuwa wakimtunza Tera?
3 Biblia ina masimulizi mengi ya wanaume na wanawake waliowatunza wapendwa wao. Fikiria mfano wa Abrahamu na Sara. Walipoondoka jiji la Uru, Tera, baba yao, alikuwa na umri wa miaka 200 hivi. Hata hivyo, aliondoka pamoja nao. Walisafiri umbali wa kilomita 960 hivi mpaka Harani. (Mwa. 11:31, 32) Bila shaka, Abrahamu na Sara walimpenda Tera, lakini fikiria jinsi ambavyo huenda walikabili changamoto walipokuwa wakimtunza, hasa walipokuwa safarini. Inaelekea walisafiri kwa kutumia ngamia au punda, jambo ambalo huenda lilikuwa gumu sana kwa Tera aliyekuwa amezeeka. Inawezekana kwamba pindi fulani, Abrahamu na Sara walihisi wamechoka sana. Vyovyote vile, Yehova kwa kweli aliwapatia nguvu walizohitaji. Kama tu ambavyo Yehova aliwategemeza Abrahamu na Sara, atakutegemeza na kukuimarisha wewe pia.—Zab. 55:22.
4. Tutazungumzia nini katika makala hii?
4 Shangwe inaweza kukusaidia kuvumilia ukiwa mtunzaji. (Met. 15:13) Mtu mwenye shangwe anaweza kuendelea kuwa na furaha licha ya hali zake. (Yak. 1:2, 3) Unawezaje kusitawisha shangwe hiyo? Njia moja ni kwa kumtegemea Yehova kupitia sala na kumwomba akusaidie udumishe mtazamo mzuri. Katika makala hii, tutazungumzia mambo mengine ambayo mtunzaji anaweza kufanya ili kudumisha shangwe yake. Tutazungumzia pia jinsi wengine wanavyoweza kuwasaidia. Kwanza, acheni tuzungumzie kwa nini watunzaji wanahitaji kudumisha shangwe yao na ni changamoto gani zinazoweza kusababisha wapoteze shangwe yao.
JINSI AMBAVYO KUWATUNZA WENGINE KUNAWEZA KUATHIRI SHANGWE YAKO
5. Kwa nini watunzaji wanahitaji kudumisha shangwe yao?
5 Ikiwa watunzaji watapoteza shangwe yao, wanaweza kuchoka kwa urahisi. (Met. 24:10) Na wanapokuwa wamechoka, huenda wakakosa kuonyesha fadhili kwa njia inayofaa. Ni changamoto gani zinazoweza kusababisha watunzaji wapoteze shangwe yao?
6. Kwa nini baadhi ya watunzaji huchoka sana?
6 Watunzaji wanaweza kuchoka sana. Dada anayeitwa Leah anasema hivi: “Kuwa mtunzaji ni jambo linalokulemea sana kihisia hata ikiwa mambo yote ni sawa. Mara nyingi mwishoni mwa siku, mimi huhisi nikiwa nimechoka sana. Nyakati nyingine mimi hukosa hata nguvu za kujibu ujumbe wa simu.” Wengine wanaona kuwa vigumu kulala au kupumzika vya kutosha, jambo ambalo wanahitaji. Dada anayeitwa Inés anasema hivi: “Ni vigumu kwangu kulala vya kutosha. Mara nyingi mimi huamka usiku kila baada ya saa mbili ili kumtunza mama mkwe wangu. Na kwa miaka kadhaa sasa, mimi na mume wangu hatujaweza kwenda likizo.” Baadhi ya watunzaji wanashindwa kutumia wakati pamoja na rafiki zao na hata wanakataa migawo ya kitheokrasi kwa sababu wapendwa wao wanahitaji kutunzwa saa zote. Matokeo ni kwamba huenda wakahisi upweke na kwamba hawawezi kufanya mambo mengi ambayo wangependa kufanya.
7. Kwa nini baadhi ya watunzaji wanapambana na hisia za hatia au huzuni?
7 Watunzaji wanaweza kupambana na hisia kali za hatia au huzuni. Dada anayeitwa Jessica anasema hivi: “Mara nyingi mimi huhisi kwamba ninapaswa kufanya mengi zaidi ili kumsaidia baba yangu. Nami huhisi hatia ninapopumzika.” Baadhi ya watunzaji huhisi hatia kwa sababu pindi fulani wanakasirika kwa sababu ya hali yao. Wengine wana wasiwasi kwa sababu wanahisi hawatimizi mengi ili kumsaidia mpendwa wao. Na wengine wanahisi hatia kwa sababu walipokasirika, walimwambia mtu wanayemtunza jambo lenye kuumiza. (Yak. 3:2) Wengine wanahuzunika wanapomwona mpendwa wao aliyekuwa mchangamfu na mwenye afya nzuri akizidi kuwa mgonjwa. Dada anayeitwa Barbara, anasema hivi: “Changamoto kubwa zaidi kwangu ni kuona afya ya mpendwa wangu ikizidi kudhoofika kila siku.”
8. Baadhi ya watunzaji wamehisije watu wengine walipowashukuru kwa msaada wao?
8 Baadhi ya watunzaji wanahisi kwamba hawathaminiwi. Kwa nini? Kwa sababu hawapewi shukrani au pongezi kwa ukawaida kwa kazi yao ngumu na kujidhabihu kwao. Maneno machache yenye shukrani yanaweza kutia moyo. (1 The. 5:18) Dada anayeitwa Melissa, anasema hivi: “Pindi fulani, nimelia kwa sababu ya kuchoka na kuvunjika moyo. Lakini mimi hufurahi sana wale ninaowatunza wanaponiambia ‘Asante kwa yote unayonifanyia’! Maneno hayo hunichochea niamke siku inayofuata nikiwa tayari na nikiwa na hamu ya kuwatunza tena.” Ndugu anayeitwa Ahmadu anaeleza jinsi anavyotiwa moyo na maneno ya shukrani. Yeye na mke wake wanamtunza mpwa wao mdogo wanayeishi naye anayeugua ugonjwa wa kifafa. Anasema hivi: “Ingawa haelewi kikamili jinsi tunavyojidhabihu sana ili kumtunza, moyo wangu huwa na shangwe anapotoa shukrani au anapoandika kwenye karatasi, ‘Ninawapenda.’”
JINSI YA KUDUMISHA SHANGWE
9. Mtunzaji anawezaje kuonyesha sifa ya kiasi?
9 Uwe na kiasi. (Met. 11:2) Sote tuna mipaka inapohusu muda na nguvu za kufanya mambo tunayotaka. Hivyo, utahitaji kujiwekea mipaka ya mambo utakayoweza kutimiza na usiyoweza kutimiza. Na pindi fulani, utahitaji kukataa mambo ambayo watu wangependa ufanye. Na hilo ni sawa! Unaonyesha sifa ya kiasi. Ikiwa wengine watajitolea kukusaidia, washukuru na kubali msaada wao. Ndugu anayeitwa Jay anasema hivi: “Hatuwezi kutimiza mambo mengi kuliko uwezo wetu. Kuelewa na kutovuka mipaka yako kutakusaidia kudumisha shangwe yako.”
10. Kwa nini ni muhimu kwa watunzaji kuwa na utambuzi? (Methali 19:11)
10 Uwe mwenye utambuzi. (Soma Methali 19:11.) Unapokuwa na utambuzi, kuna uwezekano mkubwa kwamba utaendelea kuwa mtulivu unapokasirishwa. Mtu mwenye utambuzi hujitahidi kuelewa kwa nini mtu anatenda kwa njia fulani. Inaeleweka kwamba baadhi ya magonjwa ya kudumu yanaweza kusababisha mtu atende kwa njia isiyo ya kawaida. (Mhu. 7:7) Kwa mfano, mtu ambaye kwa kawaida ni mwenye fadhili na anayewajali wengine, anaweza kuwa mbishi au mgomvi. Au anaweza kuwa mwenye kudai mambo mengi, mchambuzi, au si rahisi kumfurahisha. Ikiwa unamtunza mtu mwenye tatizo kubwa la afya, huenda ikafaa ikiwa utajifunza kuhusu ugonjwa wake. Kadiri unavyozidi kujua kuhusu ugonjwa wake, ndivyo ambavyo huenda ukatambua kwamba tabia yake inatokana na ugonjwa wake, wala si utu wake.—Met. 14:29.
11. Ni mambo gani muhimu ambayo mtunzaji anahitaji kutenga wakati kila siku ili kuyatimiza? (Zaburi 132:4, 5)
11 Tenga wakati wa kuimarisha urafiki wako pamoja na Yehova. Pindi fulani, utahitaji kuweka kando utendaji fulani ili ushughulikie mambo ya “muhimu zaidi.” (Flp. 1:10) Mojawapo ya mambo muhimu zaidi ni kuimarisha uhusiano wako pamoja na Yehova. Mfalme Daudi alitanguliza ibada yake kwa Yehova. (Soma Zaburi 132:4, 5.) Vivyo hivyo, ni jambo la muhimu kwako kutenga wakati kila siku ili kusoma Biblia na kusali. Dada anayeitwa Elizaa anasema hivi: “Ninaweza kudumisha shangwe yangu kwa kusali na kutafakari zaburi zenye kufariji. Sala imenisaidia sana. Mimi husali kwa Yehova mara nyingi kwa siku ili anisaidie kuwa mtulivu.”
12. Kwa nini watunzaji wanahitaji kutenga wakati ili kutunza afya zao?
12 Tumia wakati ili kutunza afya yako ya kimwili. Watu wenye shughuli nyingi—kama vile watunzaji—wanaweza kuona kuwa changamoto kula vyakula vyenye lishe bora kwa sababu hawana muda wa kutosha wa kununua vyakula vyenye lishe bora na kupika vyakula hivyo. Vyakula vyenye lishe na ratiba nzuri ya kufanya mazoezi ni muhimu ili uwe na afya nzuri ya kimwili na kiakili. Hivyo, jaribu kutumia vizuri wakati wako kwa kula vyakula vyenye lishe na kufanya mazoezi kwa ukawaida. (Efe. 5:15, 16) Kwa kuongezea, jitahidi kulala vya kutosha. (Mhu. 4:6) Watafiti wanasema kwamba kulala usingizi kunaweza kusaidia ubongo ujirekebishe. Makala moja inayozungumzia mambo ya afya ilisema kwamba mtu akilala vya kutosha, hatahisi mkazo kupita kiasi na atakuwa na uwezo wa kuendelea kuwa mtulivu anapokuwa chini ya hali ngumu. Utahitaji pia kutenga wakati kwa ajili ya kufanya mambo unayofurahia. (Mhu. 8:15) Mtunzaji mmoja alitaja jambo linalomsaidia kudumisha shangwe yake. Anasema hivi: “Hali ya hewa inapokuwa nzuri, mimi hujitahidi kutoka nje na kufurahia mwangaza wa jua. Mimi hupanga kutumia siku moja kila mwezi pamoja na rafiki yangu ili kufurahia mambo tunayopenda.”
13. Kwa nini kucheka ni jambo linalofaa? (Methali 17:22)
13 Uwe mwenye ucheshi. (Soma Methali 17:22; Mhu. 3:1, 4) Kucheka ni jambo linalofaa afya yako ya kimwili na kiakili. Unapomtunza mtu, si mara zote mambo huenda kama unavyotaka. Lakini ikiwa utacheka kuhusu hali hizo, huenda ikawa rahisi kwako kuzivumilia. Na mnapocheka pamoja na yule unayemtunza, huenda kufanya hivyo kukaimarisha uhusiano wenu.
14. Kuzungumza na rafiki unayemwamini kunawezaje kukusaidia?
14 Zungumza na rafiki unayemwamini. Licha ya jitihada zako nzuri, bado pindi fulani utahisi umelemewa. Katika pindi hizo, huenda ikafaa kuzungumzia hisia zako pamoja na rafiki mzuri ambaye hatakuhukumu au kufanya uhisi vibaya. (Met. 17:17) Huenda usikivu wake na maneno yake yenye kufariji ndiyo mambo unayohitaji ili kudumisha shangwe yako.—Met. 12:25.
15. Kukazia fikira tumaini lako kunawezaje kukuletea shangwe?
15 Wazia maisha yenu mkiwa pamoja katika Paradiso. Jaribu kukumbuka kwamba jukumu lako ukiwa mtunzaji ni la muda tu, na si kazi ambayo awali Yehova alikusudia wanadamu waifanye. (2 Kor. 4:16-18) “Uzima ulio wa kweli” bado haujafika. (1 Tim. 6:19) Inaelekea utapata shangwe nyingi ukizungumza na mpendwa wako kuhusu mambo mtakayofanya pamoja katika Paradiso. (Isa. 33:24; 65:21) Dada anayeitwa Heather, anasema hivi: “Mara nyingi mimi huwaambia wale ninaowatunza kwamba hivi karibuni tutashona pamoja, tutakimbia pamoja, na tutaendesha baiskeli pamoja. Tutaoka mikate na kuwapikia chakula wapendwa wetu watakaofufuliwa. Pamoja, tunamshukuru Yehova kwa tumaini letu.”
JINSI WENGINE WANAVYOWEZA KUKUSAIDIA
16. Tunawezaje kuwasaidia watunzaji katika kutaniko letu? (Tazama pia picha.)
16 Wasaidie watunzaji ili wapate muda wa kupumzika. Sisi sote kutanikoni tunaweza kujitolea kuwasaidia wale wanaotunzwa. Tunapofanya hivyo, tunawapa watunzaji muda wa kupumzika na kushughulikia mambo yao ya kibinafsi. (Gal. 6:2) Baadhi ya wahubiri wametenga muda kila juma kwa ajili ya kufanya hivyo. Dada mmoja anayeitwa Natalya, ambaye anamtunza mume wake asiyeweza kutembea, anasema hivi: “Ndugu mmoja kutanikoni hufika mara moja au mbili kwa juma ili kutumia wakati pamoja na mume wangu. Wanahubiri pamoja, wanazungumza pamoja, na hata hutazama sinema pamoja. Pindi hizo ni zenye thamani sana kwa mume wangu, na hunipatia wakati wa kushughulikia mahitaji yangu ya kibinafsi kama vile kwenda kutembea.” Pindi fulani, huenda hata ukajitolea kukaa na mtu anayetunzwa usiku mzima ili yule anayemtunza aweze kulala vizuri.
Unawezaje kuwasaidia watunzaji katika kutaniko lenu? (Tazama fungu la 16)b
17. Tunawezaje kuwasaidia watunzaji wakati wa mikutano ya kutaniko?
17 Wasaidie watunzaji wakati wa mikutano ya kutaniko. Huenda watunzaji wasinufaike kikamili na mikutano ya kutaniko, makusanyiko ya mzunguko, na makusanyiko ya eneo kwa sababu ya kuwa na shughuli nyingi ili kumtunza mpendwa wao. Ndugu na dada kutanikoni wanaweza kujitolea kusaidia kwa kuketi na wanaotunzwa wakati wa kipindi chote cha mkutano au kwa sehemu. Ikiwa yule anayetunzwa hawezi kutoka nyumbani, unaweza kujitolea kwenda nyumbani kwake na kujiunga na mkutano kwa njia ya mtandao ili mtunzaji aweze kuhudhuria mkutano ana kwa ana.
18. Tunaweza kuwafanyia mambo gani mengine watunzaji?
18 Wapongeze watunzaji na sali kwa ajili yao. Wazee wanapaswa kuwafanyia ziara za uchungaji watunzaji kwa ukawaida. (Met. 27:23) Haidhuru hali zetu zikoje, sote kutanikoni tunaweza kuwapongeza kwa ukawaida watunzaji. Tunaweza pia kumwomba Yehova aendelee kuwaimarisha na kuwasaidia wadumishe shangwe yao.—2 Kor. 1:11.
19. Tunatazamia nini wakati ujao?
19 Hivi karibuni, Yehova atafuta machozi ya uchungu kutoka katika nyuso zote. Ugonjwa na kifo hakitakuwapo tena. (Ufu. 21:3, 4) “Kilema ataruka kama paa.” (Isa. 35:5, 6) Matokeo yenye kuhuzunisha yanayoletwa na uzee na uchungu unaotokana na kumtunza mpendwa ambaye ni mgonjwa, yatakuwa kati ya “mambo ya zamani [ambayo] hayataingia tena akilini.” (Isa. 65:17) Hata sasa tunapongojea kutimizwa kwa tumaini letu zuri sana, Yehova hatatuacha. Ikiwa tutaendelea kumtegemea ili atuimarishe, atatusaidia ‘kuvumilia kikamili kwa subira na shangwe.’—Kol. 1:11.
WIMBO 155 Shangwe Yetu ya Milele
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b MAELEZO YA PICHA: Dada wawili vijana wakimtembelea dada mwenye umri mkubwa ili yule anayemtunza awe na wakati wa kwenda kutembea.