“Iweni na Akili” kwa Kuwa Taratibu Mpya Inakaribia
“Mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili.”—1 Pet. 4:7.
1. Ni ushuhuda gani unaoonekana unaoonyesha kwamba karibuni taratibu ya sasa ya ulimwengu itakwisha?
KUNA ushuhuda mwingi unaoonyesha kwamba taratibu mpya i karibu. Kwa upande mwingine, kwa habari ya taratibu ya sasa ya ulimwengu, sisi tunaishi katika wakati wa pekee. Kwa mara ya kwanza katika historia ya kibinadamu, taratibu zote ambazo wanadamu wamesimamisha ziko katika hali ya hatari. Ebu tazama kila mahali, zifikirie taratibu nyingi zo zote zinazoungana pamoja kuwa taratibu moja ya sasa, na utaona ishara za taabu kubwa. Taratibu za kisiasa, taratibu za kidini, taratibu za kijamii, taratibu za polisi, taratibu za elimu, taratibu za usafirishaji, taratibu za fedha—zote hizo ziko katika hatari isiyo na mwisho. Hata mambo ambayo ni ya msingi sana, kama hewa, maji na chakula, yanahatirishwa sana.
2. Kwa sababu gani wanadamu hawawezi kuifanya taratibu ya sasa iendelee milele?
2 Taratibu ya sasa ni kama nyumba ambayo misingi, nguzo na mihimili yake yote imevunjika na kuoza sana. Huenda wanadamu wakaongeza rangi mpya au mapambo yenye kupendeza sana na vyombo vipya vya nyumbani, lakini hakuna kitu kiwezacho kulipa jengo lililooza nguvu ambayo linaihitaji ili liendelee kwa muda mrefu. Bila kujali namna wanadamu wanavyojaribu kuondoa mafarakano ambayo yameimarika sana katika jamii ya wanadamu wakati inapotengenezwa sasa, hawawezi kuzuia matokeo yaliyotajwa katika maneno ya Yesu: “Nyumba ikijifarakanya yenyewe huanguka.”—Luka 11:17, NW.
3. Ni msingi gani ulio imara sana kwa kusadiki kwamba taratibu mpya i karibu?
3 Lakini ushuhuda ulio bora na wenye kusadikisha zaidi kwamba taratibu mpya i karibu unatokana na ahadi na unabii wa Neno la Mungu, Biblia. Unabii wake ulitabiri, si kuharibika kwa adili za sasa na kuiacha kweli na haki ambako kumeifikisha taratibu ya sasa kwenye hali yake yenye hatari ya dunia yote tu, bali unatuambia vile vile kusudi la Mungu lililotangazwa kuzifuta kabisa taratibu hizi zote za sasa katika “dhiki kubwa” ambayo haina mfano wake mbele ya kumalizika “kizazi hiki” na kuimarisha taratibu yake mwenyewe ambayo taratibu zake zina msingi wa haki, kumpenda Mungu na kumpenda jirani.—Mt. 24:21, 33, 34; Ufu. 7:14-17.
4, 5. Ahadi ya Biblia ya “mbingu mpya na dunia mpya” ina maana gani kwetu?
4 “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizi haki itakaa.” (2 Pet. 3:13, NW) “Ahadi” ambayo mtume Petro anataja hapa inapatikana katika Isaya 65:17 katika Maandiko ya Kiebrania. Kwa muda mrefu wanachuo wa Biblia wamekubali kwamba “mbingu” na “dunia” zinazosemwa hapa ni za mfano. Cyclopædia ya M’Clintock na Strong (Vol. IV, kur. 122-127), kwa mfano, inaeleza hivi: “Katika Isa. LXV [65], 17, mbingu mpya na dunia mpya zinamaanisha serikali mpya, ufalme mpya, watu wapya. . . . ”
5 Hii maana yake ni taratibu mpya. Wakati ufalme wa Mungu kupitia kwa Mwana wake utakapokwisha kuja juu ya adui zote za enzi ya Mungu, ndipo utakapotimiza mapenzi ya Mungu katika dunia yote, hata kama Sala ya Bwana inayojulikana sana inavyosihi. (Mt. 6:10) ‘Ufalme huo wa mbinguni’ ndivyo utakavyotoa “mbingu mpya” ili ziongoze na kuwatawala wanadamu. Na jamii mpya ya watu ya kidunia itakayookoka kuingia katika taratibu hiyo mpya haitasumbuliwa na taratibu zisizokamilika, zisizofaa na zenye pupa ambazo sasa zinafanyiza masumbufu na mapingamizi na hatari hizo. Ikiwa juu ya msingi na kujengwa juu ya haki, jamii hiyo itajifurahisha taratibu mpya zitakazoongozwa na serikali ya kimbinguni.
MAULIZO YENYE KUCHUNGUZA
6, 7. Maneno ya mtume katika 2 Petro 3:11, 12 yanatokezaje maulizo yenye kuchunguza kwetu leo?
6 Tukiwa na taraja hilo mbele yetu, tunaonaje? Je! mawazo yetu yanapatana na yale ya mtume aliyeongozwa na roho ya Mungu, aliyeandika hivi: “Kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa, mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza”?—2 Pet. 3:11, 12.
7 Kwa kuwa taratibu mpya hiyo i karibu sana, je! wewe huelekei kutua na kujiuliza mwenyewe hivi: ‘Kwa kweli, mimi ni mtu wa namna gani kwa habari ya “mwenendo mtakatifu na utauwa”? Je! kweli mimi ndiyo namna ya mtu ambaye Mungu anamtaka katika taratibu yake mpya? Je? kweli mimi mwenyewe nataka kuishi katika dunia ambamo “haki itakaa” na kuenea katika dunia yote?’ Haya ni maulizo yenye kuchunguza, lakini sasa ndio wakati wa maulizo hayo.
8, 9. Ni habari gani juu ya Taratibu Mpya ambayo wengine wangependa kujua, kwa sababu ya mageuzi makubwa yatakayoletwa nayo?
8 Walakini, huenda wengine wakaelekea kusema: ‘Kama tungejua zaidi juu ya ambavyo maisha yatakavyokuwa katika Taratibu Mpya, kama tungepata habari zaidi juu yake, labda tungeweza kuyajibu maulizo hayo kwa kufaa sana.’ Kweli, taraja la taratibu ambayo ni mpya kabisa linamfanya mtu atake kujua na kwa wepesi kutokeza maulizo akilini. Kwa mfano, wengine wanauliza hivi, ‘Katika taratibu hiyo mpya, ni nani atakayetoa utumishi wote ambao taratibu za kilimwengu za sasa zimekuwa zikiutoa? Ikiwa taratibu zote za sasa zinakoma katika “dhiki kubwa” inayokuja, watakaookoka watapelekeanaje habari kuzunguka dunia yote? Ikiwa taratibu za posta, simu na radio zinakwisha, kungewezaje kuwako umoja wa kuongoza shughuli, kama kwa baraza inayoongoza yenye kutumikia chini ya ufalme wa kimbinguni?’ Wengine wanauliza hivi: ‘Watu watajuaje mahali pa kuishi? Je! kila mtu atajichagulia mwenyewe mahali anapopenda na kukaa hapo tu na kuhamia katika nchi nyingine? Ikiwa sivyo, mahali pa kukaa patagawiwaje na ni nani atakayegawa?’
9 Bado wengine wanataka kujua juu ya njia za usafirishaji wakati huo, kama kutakuwako motokaa, ndege au njia nyinginezo kama hizo zenye nguvu za usafirishaji. Huenda wanawake wenye kuuliza wakataka sana kujua kama vitakuwako vifaa kama meko za stimu za kupikia, mashine za stimu za kufua nguo na vifaa vinavyofanana na hivyo. Na namna gani juu ya vitu kama mavazi? Wakati mavazi au viatu ambavyo mtu atakuwa akivaa wakati wa kuokoka vitakapochakaa, vipya vitatoka wapi? Au ikiwa mtu anataka kujenga, atapata wapi nyundo, misumari, msumeno na vifaa vingine vinavyotolewa sasa na taratibu hii ya sasa?
10, 11. Ni jibu gani la maulizo yao, na hili lina matokeo gani juu ya kujitayarisha kwetu kuishi katika Taratibu Mpya?
10 Maulizo kama haya ni mengi. Lakini kuna jibu jepesi na fupi kwa maulizo yote. Ni: Neno la Mungu, Biblia, halisemi na kwa hiyo sisi hatujui.
11 Lakini je! hii haituzuii kujitayarishia kuishi katika taratibu mpya ya Mungu? Hapana, kwa maana hatuna haja na haya ili tujitayarishe sana, kwa kuwa maulizo hayo yanashughulika na mambo ambayo si ya lazima hata kidogo kwa kujitayarisha kwetu. Basi, ni mambo gani yaliyo ya lazima sana kwetu kuyafikiria katika kujitayarisha kwetu wenyewe kuishi katika taratibu hiyo mpya inayokuja?
KUENDELEA KUWA NA AKILI
12. Kwa sababu gani tunaweza kusadiki kwamba shauri la mtume kuanzia na 1 Petro 4:7 linatufaa sisi wakati huu?
12 “Mwisho wa mambo yote umekaribia,” akaandika mtume Petro katika barua yake ya kwanza (4:7). Ijapokuwa taratibu ya mambo ya Kiyahudi iliyokuwako wakati huo ilikuwa karibu kumalizika miaka michache wakati barua hii ilipokwisha kuandikwa (kwa vile Warumi waliuharibu Yerusalemu na hekalu lake katika mwaka wa 70 C.E. na kuukomesha ukuhani wa Kiyahudi na matendo na dhabihu zake), maneno yaliyoongozwa na roho ya Mungu ya mtume yana matumizi makubwa na maana kwa wakati wetu, taratibu nzima ya ulimwengu inapotazamiwa kukoma. Mitajo mingi ya mtume katika barua hii juu ya wakati wa “ufunuo” wa Yesu Kristo inahakikisha hili.—1 Pet. 1:5, 7, 13; 2:12; 4:13.
13. Sisi kama Petro tunawezaje ‘kutazamia hata ije siku ile ya Yehova, na kuihimiza,’ na kwa sababu gani hii ni lazima leo?
13 Mtume alifuata shauri lake mwenyewe kuwa wenye ‘kutazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza,’ wakati wa Mungu wa kuikomesha taratibu ya sasa ya ulimwengu na kuleta taratibu yake mpya yenye haki. Kuna usalama katika ‘kuuhimiza’ wakati huo, si kuuona kama uko mbali, kama ukiruhusu wakati mwingi wa kujitia katika shughuli za kichoyo na bado kuweza kuirudia haki bila kuchelewa ili kuokoka uharibifu wa dunia yote. Sisi tu hai sasa; huenda tusiwe na njia ya kujua kama tutakuwa hai kesho au juma ijayo. Hivyo wakati wa kujitayarisha wenyewe kwa taratibu mpya ya Mungu ndiyo sasa.—Yak. 4:13-15.
14. Ni nini maana ya shauri “iweni na akili”?
14 Kwa kuwa sasa mwisho unakaribia kwa haraka, imetupasa tukazie fikira juu ya nini? “Basi, iweni na akili,” ndilo shauri la mwandikaji aliyeongozwa na roho ya Mungu, “mkeshe katika sala.” (1 Pet. 4:7) Mahali pa ‘kuwa na akili’ tafsiri nyingine zinasomwa “tulieni” (The New American Bible), “mwe wenye busara timamu” (New American Standard). Mtume Paulo alitumia neno lile lile la Kigiriki lililotumiwa na Petro wakati alipokuwa akisihi, “Tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali tuwe macho na kuzitunza akili zetu.” (1 The. 5:6, NW) Kwa wazi huu sio wakati wa kuwa bila akili, wa kufanya mchezo au wa kufanya uamuzi wa bila kufikiri. Ni wakati wa kufikiri na mwenendo wa makini.
15. (a) Tunawezaje kujaribu “akili” zetu juu ya matumaini yetu ya wakati ujao, kutia na maoni yetu ya maandiko kama Isaya 65:21? (b) Andiko hili limekwisha kupata utimizo gani?
15 Inatupasa tuonyeshe akili ile ile juu ya tumaini letu la uzima katika taratibu mpya ya Mungu. Ni kwa sababu gani tunalishindania? Ni jambo gani linalotuvutia kwenye tumaini hilo? Je! ni faida za kimwili? Labda andiko kama Isaya 65:21 linaweza kutokea katika akili: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake.” Juu ya hilo, je! tujione wenyewe tukiishi katika nyumba kubwa mno na kuvutwa na hili? Kwa kweli andiko linataja “nyumba” tu, sivyo? Na hivyo ndivyo karibu sote tunavyoishi leo. Kwa kweli unabii huu ulikuwa na utimizo wa kwanza juu ya kurudi kwa Israeli kutoka uhamishoni kwenda kwenye nchi ya Yuda iliyokuwa ukiwa, bila nyumba na mizabibu. Walipokwisha kufika, walijenga nyumba na wakapanda mizabibu. Katika wakati wetu kumekuwako utimizo wa kiroho wa unabii huo tangu mwaka wa 1919, kwa kuwa watu wa Mungu wanaotumikia katika njia ile ile kama mashahidi wa Yehova kama walivyokuwa Waisraeli (Isa. 43:10-12) walitoka katika uhamisho wa kiroho na wakaanza kuirudisha ‘nchi’ yao ya kiroho au shamba la utendaji na ibada, wakijenga makundi na kusitawisha rutuba ya kiroho.
SABABU KUBWA ZA KUTAMANI TARATIBU MPYA
16. Ni jambo gani linalosemwa hapa juu ya ombi la Biblia wakati inapotoa tumaini la taratibu mpya?
16 Bila shaka, kufuata “dhiki kubwa” kutakuwako kazi nyingi za kujenga nyumba. Na, bila kuwa na mizigo ya taratibu ya sasa na pupa yake ya biashara, waokokaji wa kidunia watakaokuwa wakiishi katika taratibu mpya ya Mungu bila shaka wataweza kujenga nyumba ambazo ni nzuri sana. Basi, ni jambo gani linalosemwa? Hili: Kwamba Neno la Mungu halielezi namna nyumba hizo zitakavyokuwa, ukubwa wake, udogo au uzuri wake. Katika kurasa zake zote Neno la Mungu linaacha hili bila kusema. Kwa sababu gani? Kwa sababu ombi lake si la mambo ya kimwili; linaweka mkazo mkubwa zaidi juu ya baraka nyingine kuwa ndiyo mambo ya maana ambayo inatupasa tuyafikirie sana. Ebu ifikirie, kwa mfano, hali yenye kupendeza inayotolewa kwetu katika Zaburi 85:10-13. Ikionyesha kibali na baraka za Mungu zinazoweza kutokea kwa nchi na watu wake, inasema hivi:
17, 18. (a) Zaburi 85:10-13 inaonyeshaje jambo hili? (b) Basi, ni mambo gani ya maisha ya Taratibu Mpya ambayo yamepaswa yatuongoze zaidi sana kuliko yote, na kwa sababu gani?
17 “Fadhili na kweli zimekutana, haki na amani zimebusiana. Kweli imechipuka katika nchi, haki imechungulia kutoka mbinguni. Naam, [Yehova] atatoa kilicho chema, na nchi yetu itatoa mazao yake. Haki itakwenda mbele zake, nayo itazifanya hatua zake kuwa njia.”
18 Angalia kwamba hali hii inapata uzuri wake hasa kutokana na baraka za kiroho, ikitaja kwa ufupi tu baraka za kimwili kutokana na “mazao” ya nchi. Baraka za kiroho ndizo zimepaswa zitufanye sisi tutamani sana taratibu mpya ya Mungu. Ni kwa sababu ya mambo haya kwamba imetupasa tuwe na nia ya kufanya kazi, nia ya kujitoa, ndiyo, na hata kufa ili tupate uzima katika taratibu mpya ya Mungu. Kwa maana haya ndiyo mambo ya kiroho ambayo taratibu ya sasa haijatupa sisi hata kidogo na haitatupa hata kidogo. Mahali pa “fadhili” taratibu ya sasa ina moyo mgumu, ni yenye pupa, ikimtumia mtu wakati anapotumikia kusudi lake kisha inamtupilia mbali kama asiyefaa kitu na wa kusahauliwa. Inajaa uongo, unafiki na udanganyifu, haijai “kweli.” Kwa hakika haki na amani ‘hazikubusiana’ katika taratibu ya sasa. Lakini katika taratibu mpya baraka hizi za kiroho zitaonekana duniani pote nazo zitaungana katika uzuri na upatano ili kuyafanya maisha yawe yenye kupendeza kweli kweli—kwa wale ambao mioyo yao ni ya haki. Taratibu ya kale inaweza kutoa nyumba kubwa, hata majumba yenye fahari, kwa watu, pamoja na chakula kizuri—katika nchi nyingine watu wengi wanavyo vitu hivi. Lakini haikuleta na haitaleta hata kidogo fadhili, kweli, amani na haki inayotofautisha taratibu mpya ya Mungu.
19. Ni maoni gani ambayo ni ya lazima kwa habari ya Taratibu Mpya, na twawezaje kuonyesha kwamba tunayo maoni hayo sasa?
19 Basi, kujitayarisha kuishi katika taratibu mpya inayokaribia kunataka tuzifikirie kwa kufaa baraka zilizoahidiwa na sikuzote kuweka ubora mkubwa zaidi juu ya baraka za kiroho. Tukifanya hivi, ndipo uharibifu wa Har–Magedoni utakapopita, mngurumo wake utakapotoweka, na dunia itakapoacha kutikisika chini ya mshindo wa ukali wa kimungu utakaoonyeshwa juu ya mataifa, tutatoka mahali po pote ambapo Yehova ameona yafaa kutuhifadhi nasi tutafurahia asubuhi ya siku mpya, kupambazuka kwa taratibu yake mpya. Tutakapotazama huku na huku, labda tutakayoona yatakuwa magofu matupu—lakini, ikiwa hivyo, itaonekana vizuri kwetu. Kwa sababu gani? Kwa sababu ndipo tunapoweza kusema kwa mioyo yetu yote, ‘Asante Mungu, mwisho taratibu ya kale pamoja na ubaya wake wote, ukatili na kumwasi Mungu, vimetoweka kabisa! Sasa haki itakaa katika dunia.’ Tunaweza kuonyesha kwamba hivi ndivyo tuonavyo hata sasa kwa kutokuyaacha mambo ya kimwili yasonge mambo ya kiroho katika maisha zetu au kuwa kishawishi kikubwa zaidi.
UTII WA MOYO WOTE
20. Ni jambo gani tunalojua sana juu ya Taratibu Mpya, na Ufunuo 20:11, 12 unafunua nini?
20 Katika kuwa “na akili,” itafaa tuyafikirie mambo fulani ambayo tunajua juu ya taratibu mpya inayokuja. Tunajua kwamba utii wa enzi ya Mungu, inayoonyeshwa kupitia kwa serikali yake ya Ufalme, utatakiwa. Katika Ufunuo 20:11, 12, tunapashwa habari kwamba wakati wa utawala wa Mwana wa Mungu wa miaka elfu ‘vitabu vitafunguliwa.’ Wale wote watakaokuwa wakiishi, kutia na wale watakaofufuka kutoka kwa wafu, watahukumiwa “sawasawa na matendo yao” kwamba yanapatana au hayapatani na “vitabu” hivyo. Vitabu, kama vinavyosimuliwa katika unabii wa Biblia, vinamaanisha ufunuo fulani wa mapenzi ya Mungu, Ufunuo ulioandikwa. Hivyo inaonekana kwamba wakati wa utawala wa Kristo Yesu wa miaka elfu utakuwako ufunuo zaidi wa mapenzi ya Mungu na kusudi na kwamba haya yataandikwa ili wote wapate kupashwa habari. Ndipo itakapokuwa juu ya kila mtu kuonyesha kufaa kwake kupata uzima wa milele kwa kupatanisha matendo yake na vitabu hivyo.
21, 22. (a) Kwa sababu gani huenda wengine wakaona kwamba, wakiisha kuokoka “dhiki kubwa,” kupata uzima wa milele kutakuwa kwepesi sana wakati huo? (b) Ni jambo gani la maana ambalo huenda likaachwa?
21 Kwa hiyo, kuokoka “dhiki kubwa” hakutoi uhakikisho wa kuokoka na kupata uzima wa milele. Walakini, huenda wengine wakaona kwamba, mara taratibu hii ya kale itakapotoweka na, kama kitabu cha Ufunuo kinavyotabiri, Shetani na mashetani wake watakapotupwa shimoni, hapo ndipo itakapokuwa vyepesi kutii na karibu hakutakuwa na haja ya kutii. Je! huku ndiyo kuwa “na akili,” na je! kunatutayarisha sisi kwa uzima katika Taratibu Mpya?
22 Kweli, kutoweka kwa taratibu ya kale pamoja na vishawishi vyake vyote na mikazo ya kuelekea kufanya maovu itakuwa faraja kubwa. Vile vile ndivyo utakavyokuwa uhuru wa vita ambavyo sasa lazima tuvipige juu ya “pepo wabaya” ambao bila kuonekana wanaitawala taratibu ya sasa. (Efe. 6:10-13) Hata hivyo je! hivyo ndivyo vyanzo viwili tu vikubwa vya upinzani wa haki ambavyo inatupasa kushindana navyo? Je! hakuna chanzo kingine kikubwa? Ndiyo; na bila kuwa kama vyanzo hivyo vya nje hiki ni cha ndani, ndani yetu sisi. Ni hali yetu yenye dhambi tuliyorithi, urithi tuliopokea sote kutoka kwa Adamu. Na “akili” zitatufanya tufahamu kwamba hii ndiyo nguvu ambayo labda ndiyo yenye hatari zaidi kuliko zote, yenye kuamua. Namna gani hivyo?
23. Mwanzo wa udhalimu unaonyeshaje uzito wa nguvu za nje na za ndani zinazopingana na kumtii kwetu Mungu?
23 Ebu fikiria mwanzo wa udhalimu, wa kuasi utawala wa kimungu. Kweli, katika Edeni, Hawa alipata uvutano wa nje, halafu naye, akautumia uvutano juu ya mume wake. Lakini namna gani yeye aliyeanzisha uasi? Ni uvutano gani wa nje uliotenda juu ya mwana huyo wa kiroho wa Mungu kumfanya awe mbaya? Kwa hakika Mungu hakumshawishi wala kumvuta afanye hivyo, wala mtu mwingineo. Hata hivyo mwana huyo wa kiroho akawa mwasi wa Baba yake wa kimbinguni. Chanzo cha uasi wake kilikuwa—si cha nje—bali cha ndani, kutokana na moyo wake mwenyewe. (Linganisha Yakobo 1:13-15.) Ndivyo na sisi, bila kujali nguvu mbaya za nje zilizoko, jambo lenye kuamua uaminifu li ndani yetu, kile tulicho nacho katika mioyo yetu. Bado hii itakuwa hivyo wakati wa kipindi cha miaka elfu wakati watu watakapohukumiwa “sawasawa na matendo yao.”
24. Ili wafanye mageuzi yanayohitajiwa katika utu na mazoea yao, wengine wanatumainia nini? Na tunataka tujue nini katika funzo linalofuata?
24 Walakini, huenda mtu akasema hivi: ‘Ndiyo, mimi nakubali kwamba ninayo mazoea fulani mabaya, tabia mbaya na njia mbaya ambazo sijazishinda bado. Lakini nina hakika kwamba mara tutakapookoka “dhiki kubwa” n’takuwa tofauti—kwa kweli, bado sitakuwa mkamilifu bali nitakuwa tofauti.’ Je! huku ndiyo kuwa “na akili”? Je! tufikiri kwamba ogofyo la “dhiki kubwa” na vita yake ya Har–Magedoni litafanya mageuzi fulani mazuri katika mioyo yetu? Ebu angalia habari inayofuata.