Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 12/15 kur. 560-565
  • Je! Wewe Uko Tayari Kwa Uzima Katika Taratibu Mpya ya Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Uko Tayari Kwa Uzima Katika Taratibu Mpya ya Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAGEUZI YA UTU SI YA MWUJIZA WA KIMUNGU
  • KUKESHA KATIKA SALA
  • KUHESHIMU UKICHWA WA KITHEOKRASI
  • WENYE KUHESHIMU INGAWA MAKOSA
  • “Iweni na Akili” kwa Kuwa Taratibu Mpya Inakaribia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Kuishi kwa Kutumaini Uzima Katika Taratibu Mpya ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Taratibu Mpya Inayokuja Inayotegemezwa na Roho Takatifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Namna Ufalme wa Mungu Unavyoweza Kukufaidi Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 12/15 kur. 560-565

Je! Wewe Uko Tayari Kwa Uzima Katika Taratibu Mpya ya Mungu?

1-3. (a) Ni tukio gani lenye kuogofya walilopata Waisraeli katika Bahari ya Shamu? (b) Je! liliwageuza Waisraeli? Twajuaje?

EBU ufikirie wakati wa kutoka kwa Israeli wa kale katika Misri. Walipozifikia pwani za magharibi za Bahari ya Shamu, Waisraeli walijiona wako mtegoni wakati majeshi ya Farao yaliwafuatia nyuma. Walianza kunung’unika wakisema: ‘Kwa sababu gani Musa huyu akatuleta huku jangwani tupate kuuawa pamoja na wake na watoto wetu?’ Walionyesha kukosa imani katika uongozi wa Mungu. Hata hivyo Yehova alimwagiza Musa ainyoshe fimbo yake juu ya bahari, kisha Mungu akaifanya bahari ipasuke, ikifanya njia mpaka kwenye pwani za mashariki. Bila shaka walikuwako watu kama milioni tatu, kama kielezavyo kitabu Aid to Bible Understanding (ukurasa 546):

“Kwa kuwa Israeli alivuka bahari usiku mmoja, isingeweza kudhaniwa kwamba maji yalipasuka yakafanyiza njia nyembamba. Mahali pake, bila shaka ilikuwa maili moja (1.6 kilomita), au maili fulani, katika upana. Ijapokuwa kilikuwa katika mwandamano wa karibukaribu, kikundi hicho, pamoja na magari waliyokuwa nayo, mizigo na ng’ombe zao, hata kikaribiane sana, kingechukua eneo la maili za miraba kama tatu (7.7 kilomita za miraba). . . . Ingechukua saa nyingi kwa kikosi hicho kuingia katika bonde la bahari na kulivuka.”

2 Bila shaka lilikuwa tukio la ajabu kuivuka bahari kwenda ng’ambo nyingine na, wakiisha kuwa huko, kugeuka na kuyaona maji yakirudi tena kwa nguvu na kuyazamisha majeshi ya Farao kama mapanya walio mtegoni! Ni jambo lenye kuogofya, lenye kusisimua sana! Lakini je! liliwageuza Waisraeli? Je! walikuwa watu tofauti katika pwani za mashariki ya Bahari ya Shamu na walivyokuwa katika pwani za magharibi?

3 Ebu soma habari na utaona kwamba wakati mwezi haujamalizika manung’uniko yao yalikuwa yametokea tena​—sasa kulikuwa hakuna maji ya kutosha. Katika manung’uniko haya ya mwisho hawakumnung’unikia Mungu mbinguni. Hapana, walimnung’unikia mjumbe wa kibinadamu aonekanaye ambaye alikuwa akitumia. Kukosa kwao imani kuliendelea.​—Kut. 15:22-24; 16:1, 2.

4-6. (a) Ni jambo gani linaloamua kama miujiza au matukio fulani yenye kuogofya yana matokeo ya daima juu ya mmoja au hayana? (b) Luka 17:11-19 anaonyeshaje hili?

4 Kwamba mwujiza wa Mungu una matokeo ya muda tu ama kweli unamgeuza mtu inategemea juu ya kama moyo wa mtu unavutwa ama hauvutwi. Hivi ndivyo ilivyokuwa juu ya miujiza ambayo manabii wa Mungu na Mwana wake mwenyewe waliifanya. Ni nani ambaye hajapata kusikia juu ya ukoma, ugonjwa wa kuogofya unaoshika sehemu mbalimbali za mwili​—vidole vya mikono na vidole vya miguu, masikio, pua, midomo? Hivi vinaoza polepole. Namna gani ikiwa ni wewe ungepatwa na ugonjwa huu na ukaona mwili na uso wako polepole unaumbuka hivyo? Lakini, basi, namna gani ikiwa mtu fulani angekuponya, ikiwa angeuponya mwili na uso wako hata yaliyokupata yangekuwa kama jambo la kuogofya ambalo sasa limepita? Wewe ungeonaje? Ungesema nini?

5 Katika Luka 17:11-19, tunasoma juu ya kukutana kwa Yesu na wenye ukoma kumi, wakati alipokuwa akitoka kwenye kijiji kimoja kwenda kwa kijiji kingine. Kama Torati ilivyoamuru, watu hawa walisimama mbali, nao walipaza sauti wakisema, “Ee Yesu, Bwana mkubwa, uturehemu!” Aliwarehemu, akiwaagiza waende wakapige ripoti kwa makuhani, kulingana na Torati. Walipokuwa wakienda wote kumi walipona. Halafu walifanya nini?

6 Mtu mmoja tu ndiye aliyerudi kwa Yesu kutoa shukrani, naye alikuwa Msamaria. Na wengine kenda? Bila shaka waliendelea na safari yao huku wakifurahi. Walikuwa wamepokea walichotaka. Nacho kilikuwa kitu gani? Afya.

7. Je! kutamani sana afya kunaonyesha kwamba tunajitayarisha kuishi katika taratibu mpya ya Mungu?

7 Ni nani ambaye sisi tunafanana naye hapa? Ni jambo la asili kwetu kutarajia afya itakayoletwa na taratibu mpya ya Mungu. (Ufu. 21:3, 4) Lakini, basi, ni watu wangapi unaowajua ambao hawangependa kuwa na afya kamilifu, kuondolewa maumivu, au ambaye hangependa kutunza au kupata tena nguvu za ujana? Kwa wazi, wingi wa watu walio duniani leo wangependa. Basi kutamani afya tu kungewezaje kuwa jambo lenye kututofautisha kama watu walio tayari kwa uzima katika taratibu mpya ya Mungu? Lazima liweko jambo fulani zaidi kuliko hilo. Lazima liweko kusudi zuri la kutamani afya kamilifu ambayo taratibu mpya ya Mungu inatoa.

8. (a) Mwenye ukoma mmoja aliyemrudia Yesu alionyeshaje maoni yanayofaa? (b) Tunaposoma ahadi za Biblia za baraka za Taratibu Mpya, imetupasa sikuzote tujitahidi kufanya nini?

8 Ni lazima tuwe kama mtu aliyegeuka akarudi kwa Yesu, bila shaka akijiona kana kwamba moyo wake ulikuwa karibu kupasuka katika kifua chake na labda uso wake ukitiririka machozi. Yeye alitofautianaje na wengine? Tofauti ilikuwa kwamba fadhili za Mungu kupitia kwa Kristo Yesu ziliufikia moyo wake. Katika kupona kwake aliona ushuhuda wa ambavyo Mungu Yehova alivyo mwema sana, naye alijaa tamaa ya kumsifu yeye. Alikuwa mwenye moyo mzuri; aliona faida ya kiroho. Wakati tunapofikiria kila moja ya baraka zinazotolewa na Taratibu Mpya imetupasa sisi vile vile tuone lazima ya kufikiria yale ambayo baraka hizo zinatuambia juu ya Mungu wetu. Ndipo zitakapoongeza ndani yetu kumshukuru yeye na kusitawisha tamaa yenye nguvu​—si ya afya kamilifu na uzima wa milele tu​—bali ya kuwa na baraka hizi ili tuweze kumtumikia Muumba wetu mkuu na kuweza kuwaonyesha jirani zetu upendo vile vile.

MAGEUZI YA UTU SI YA MWUJIZA WA KIMUNGU

9. (a) Kwa sababu gani hata ufufuo wa wafu peke yake hautawageuzia watu kwenye haki? (b) Mathayo 21:31, 32 anaonyeshaje sababu watu wa Tiro, Sidoni na Sodoma huenda wakafanya maendeleo bora katika taratibu mpya ya Mungu kuliko watu wa miji ambayo Yesu alikemea?

9 Hata ufufuo peke yake kutoka kwa wafu hautawageuza watu. Twajua haya kwa sababu ya maneno ambayo Yesu aliwaambia watu wa miji fulani ya Israeli: “Itakuwa rahisi Tiro na Sidoni [na nchi ya Sodoma] kustahimili adhabu zao siku ya hukumu kuliko ninyi.” (Mt. 11:20-24) Kwa sababu gani? Kwa sababu watu hawa waliokuwa katika Tiro, Sidoni na Sodoma ya kale walikuwa hawajafaidika na mahubiri, mafundisho na kufanywa kwa miujiza ambayo Wayahudi hawa wa karne ya kwanza walikuwa wakiipokea kupitia kwa Mwana wa Mungu. Hivyo, Yesu alikuwa akisema ya kwamba wakati wakaaji wa miji hiyo kama Kapernaumu, Korazini na Bethsaida wangerudi katika ufufuo wakati wa utawala wake wa miaka elfu wangerudi wakiwa na utu ule ule wenye kiburi na mshupavu waliokuwa wakiuonyesha wakati huo. Wajapokuwa si wenye haki, watu wa Tiro, Sidoni na Sodoma hawakuwa wameonyesha tabia hizo na hivyo wangekuwa bora katika kupokea kweli na maagizo katika kanuni za haki za Mungu.​—Linganisha Mathayo 21:31, 32.

10. “Akili” zitatuambia nini juu ya jambo lililo kubwa kwa kupata uzima wa milele katika Taratibu Mpya?

10 Basi, tukiwa “na akili” hatutategemea tukio fulani lenye nguvu, hata liwe kubwa kama “dhiki kubwa” iliyoko mbele, lifanye mageuzi fulani ya mwujiza ndani yetu ambayo yatatuhakikishia matokeo mema katika taratibu mpya ya Mungu. Na mwisho, tutafahamu kwamba kama tukipata uzima wa milele ama tusipate haitategemea kushirikiana tu na watu fulani au tengenezo fulani. Kwa kumaliza itategemea namna sisi tulivyo kama watu, namna sifa zetu wenyewe zilivyo.

11, 12. (a) Onyesha namna udhaifu wa kiroho ikiwa hauondolewi sasa, ungeweza kuzuia maendeleo ya ukamilifu ya watakaookoka kuingia katika taratibu mpya ya Mungu. (b) Mtu akishindwa kufuata yaliyomo katika “vitabu” vitakavyofunguliwa wakati huo, ni nani atakayelaumiwa?

11 Basi, katika uzito wote na katika kuwa na akili zetu zote, inatupasa tuwe wanyofu katika kujichunguza wenyewe, bila kuona mazoea au maoni mabaya yanayoonyesha udhaifu mkubwa wa kiroho kuwa ni madogo au kuyaachilia. Kwa mfano, huenda mwanamume akawa mwenye ‘macho ya nje.’ Huenda asiwe mwasherati au mzinzi kweli, lakini anapendezwa mno na wanawake; macho yake yanakuwa kwa huyu na huyu. Ikiwa mtu huyo anaokoka kwa mwujiza “dhiki kubwa,” huenda macho yake yakawa sawasawa kwa muda. Lakini ikiwa hajauondoa moyo wake katika maelekeo yenye tamaa, huenda upesi akaanza kutokeza macho tena, ndiyo, hata ingawa yeye yuko katika Taratibu Mpya. Jambo lile lile linaweza kutukia kwa mtu anayezoelea mno vileo. Ajapokuwa si mlevi, ikiwa anapendezwa katika kunywa kupita kiasi na anashindwa kujizuia, huenda mwisho ikamletea matatizo kama mwokokaji katika Taratibu Mpya. Kutokuwako kwa viwanda vya kutengenezea vileo kusingezuia hili, kama vile hakukumzuia Nuhu asilewe pindi moja kufuata gharika ya dunia yote.​—Mwa. 9:20, 21.

12 Hivyo ndivyo na mazoea au tabia nyingine zenye hatari. Maelekeo ya kutaka makuu kwa choyo, majivuno, husuda, porojo, uvivu, au kukosa kunyenyekea ukichwa​—kuna mambo mengi ambayo yangeweza kufanyiza magumu kwetu ikiwa hatujifunzi namna ya kuyashinda. Yangeweza kuzuia maendeleo yetu ya kukamilika wakati wa kipindi cha miaka elfu ambacho katika hicho Kristo Yesu na warithi wake washirika wa kimbinguni watatumikia kama makuhani wa kuponya raia za kidunia za Ufalme. (Gal. 5:19-21; Ufu. 5:10; 22:1, 2) Ikiwa ye yote wa sisi anashindwa kustahili uzima kwa sababu ya kushindwa kufuata yale yaliyomo katika “vitabu” vya wakati huo, hakuna mtu tutakayelaumu​—si ulimwengu mwovu wa kisasa, wala Shetani na mashetani wake​—bali sisi wenyewe.

KUKESHA KATIKA SALA

13. ‘Kukesha katika sala’ kunatia nini?

13 Akiisha kutia moyo kuwa “na akili” kwa vile “mwisho wa mambo yote” unakaribia, tunaweza kuona kwa vyepesi sababu gani mtume Petro alisihi, “mkeshe katika sala.” (1 Pet. 4:7) Ijapokuwa kwa hakika sala zinafaa katika nyakati za kawaida, kama katika nyakati za chakula, wakati wa kuamka au kulala, je! huku ndiyo ‘kukesha katika sala’? Pahali pake, tunataka tuwe ‘tukiutafuta uso wa Yehova’ siku nzima, tukisali si kwa sauti au kwa midomo yetu tu bali kwa mioyo yetu. (Zab. 27:8, 9) Tunataka tuwe wepesi wa kuona uhitaji wetu wa msaada wake na kumwendea tukimwomba uongozi na nguvu wakati wo wote tunapoona udhaifu wo wote wa imani yetu au maelekeo yo yote ya kuziacha kanuni za haki za Yehova.

14, 15. (a) Ni ujamaa gani unaotaka kukesha zaidi ili tuuendeleze katika hali nzuri? (b) Ni sala ya namna gani inayoonyesha kujitayarisha kwa maisha katika Taratibu Mpya?

14 Je! sisi tu macho katika kushughulika kwetu na wengine, je! tunakuwa waangalifu tusije tukakwaza, ili tuepuke hatari au kuona kwamba shughuli zetu za biashara zinafanikiwa? Namna imetupasa tukeshe na kuwa macho zaidi ili tuendeleze ujamaa mwema na Yehova Mungu na kujifaidi wenyewe na msaada na uongozi wake kamili! Uhitaji wetu wa kusali ni wa haraka sasa. Hautakoma ati kwa sababu tunaingia katika taratibu mpya inayokuja.

15 Wakati tunaposema na Mungu tunaweza kuonyesha kwamba sisi sio wenye kinaya au wenye kufuata namna ile ile bali, pahali pake, kwamba tunamfungulia mioyo yetu, tukimwambia magumu yetu, jitihada zetu za kufanya maendeleo na labda tukikata tamaa, kutafuta msaada na fadhili zake zisizostahili, kumwomba atuonyeshe huruma. Kuwa wenye kukesha na wepesi wa kuona uhitaji wa kusali sasa bila shaka kutatusaidia tujitayarishe kwa uzima wakati huo. Sala za moyo wote ni ushuhuda wa kuwa na imani nyingi.

KUHESHIMU UKICHWA WA KITHEOKRASI

16, 17. (a) Twajuaje kwamba kanuni ya ukichwa itatumika katika taratibu mpya ya Mungu katikati ya waokokaji wa kidunia? (b) Jambo hili linatokeza maulizo gani juu ya kujitayarisha kwetu kupata uzima wakati huo?

16 Imani kama hiyo itatusaidia sana tufanikiwe katika taratibu mpya ya Mungu. Kati ya mambo tunayojua juu ya maisha wakati huo ni kwamba ukichwa utakuwa ukitumika. Kama Mfalme Daudi alivyokiri: “Ufalme ni wako, Ee [Yehova], nawe umetukuzwa, u mkuu juu ya vitu vyote.” (1 Nya. (Sik.) 29:11) Katika kuendesha kwa haki enzi yake, Yehova amefanya ukichwa kuwa mojawapo ya kanuni za msingi za mpango wa kimungu. Kwamba ni ukichwa unaotumiwa na kila mtu, kama ule wa Mfalme Yesu Kristo ama wa kila kichwa cha jamaa, ama ukichwa unaotumiwa kupitia kwa baraza ya watu waliopewa daraka la kuongoza au kuamua na kuhukumu chini ya Mfalme wa Mungu aliyewekwa, je! sisi tutauheshimu ukichwa huo katika Taratibu Mpya? Je! tunauheshimu sasa?

17 Wakati wa utawala wa miaka elfu Kristo Yesu ataitimiza sana sehemu yake kama “kiongozi na jemadari” wa raia zake wote. (Isa. 55:4) Serikali yake itachukua mahali pa ile ya “Kaisari” nayo itakuwa serikali itendayo ambayo uongozi wake wa mambo ya kidunia utaonekana katika njia nyingi. Je! tutaziitikia amri za Mfalme kwa nia? Maendeleo ya kukamilika na hata ya uzima yatategemea hili.

18. Ni hali gani za kulinganisha zilizotokea katika nyanda za Shinari na katika Yerusalemu uliorudishwa zinazoonyesha matokeo ya ukichwa juu ya hali za maisha ya watu?

18 Kufuata gharika ya dunia yote ya siku za Nuhu, Yehova Mungu aliwaagiza waliookoka waenee na kuijaza dunia. Wakati wengi, wakikusanyika katika nyika za Shinari, walipoamua vingine na wakaazimu kusongamana katika mji mkuu, Yehova alitimiza mapenzi yake ya enzi, akiwachafulia lugha yao na katika njia hiyo “akawatawanya kutoka huko waende usoni pa nchi yote.” (Mwa. 9:1; 11:1-9) Kwa upande mwingine, karne nyingi zilizofuata wakati wahamishwa wa Kiyahudi walipoujenga Yerusalemu, maandishi ya Nehemia yanaonyesha kwamba mji haukujaa watu, na hivyo kura zilipigwa na kwa wazi kichwa kimoja cha jamaa kutoka katika kila kumi kilichaguliwa kihamie katika mji pamoja na jamaa yake. Inaonekana bado wengine walijitolea kufanya hivyo nao walibarikiwa na watu kwa kufanya hivi. Labda si wote waliochaguliwa waliopenda sana shauri hilo la kuhamia katika Yerusalemu. Lakini itikio lao lilionyesha imani na kupendezwa sana kuona “mji mtakatifu” ukiweza kutenda kwa kufaa.​—Neh. 7:4; 11:1, 2.

19, 20. (a) Hili linatokeza ulizo gani kwetu wakati tunapofikiria kuishi katika taratibu mpya ya Mungu? (b) Tunawezaje kujionyesha wenyewe kuwa tuko tayari sasa kwa habari ya mambo hayo ya maisha ya Taratibu Mpya?

19 Basi, namna gani ikiwa katika taratibu mpya ya Mungu ungeagizwa kuhamia katika eneo jingine, labda hata mahali ambapo ni mbali, na kupafanya kuwa nyumbani kwako? Je! ungeitikia? Namna gani ikiwa ungeombwa kuhamia katika eneo lenye watu wengi zaidi, jamii ya watu ambapo kazi fulani ya pekee ya serikali ya Ufalme ingekuwa ikifanywa ambayo ingetaka ushirika wa wengi? Au namna gani ikiwa wewe ungetolewa nafasi ya kujitolea kufanya hivyo? Ungefanya nini? Je! ungeacha mambo yanayokupendeza mwenyewe yakuongoze, na je! ungeona kwamba furaha yako inazuiliwa mahali fulani au kufanya uchaguzi wako mwenyewe?

20 Kwa kadiri fulani, tunaweza kuonyesha nia yetu nzuri sasa kwa kuitikia nafasi au mashauri ambayo ni ya namna moja. Je! tunaitikia kwa nia, hata katika mambo madogo kama vile kuombwa kujazia viti fulani katika mahali pa kukutania au katika kusanyiko? Je! tunakataa kuhubiri katika maeneo fulani wakati tunapofanya kazi ya kuhubiri? Wakati hali na madaraka ya kipekee yanaporuhusu, je! tunajitolea kutumikia mahali ambapo uhitaji ni mkubwa zaidi ijapokuwa hii inamaanisha kuhama kabisa na labda kuacha mambo fulani mazuri na yale ambayo tunapenda? Ni kwa kadiri gani tunaonyesha imani na kupendezwa sana na kuendeleza faida za “Yerusalemu mpya,” serikali ya Ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo Yesu?

WENYE KUHESHIMU INGAWA MAKOSA

21. Kutumia kwa Mungu wajumbe wa kibinadamu kunatakaje imani ya kweli kwetu?

21 Pamoja na haya inatupasa tuwe na imani katika uwezo wa Yehova Mungu na Mwana wake wa kuwatumia wajumbe wa kibinadamu katika kutawala. Labda mtu angeitikia kwa nia na kwa bidii sana maagizo au migawo iliyosemwa na malaika au kupelekwa kwa sauti yenye nguvu na hata yenye ngurumo kutoka mbinguni. Lakini namna gani ikiwa mgawo unatokana na wajumbe wa kibinadamu wa serikali ya kimbinguni? Hii inataka imani zaidi, sivyo?

22, 23. (a) Ni kwa kadiri gani makosa ya kibinadamu yanavuta utumishi wa wajumbe hawa wa kidunia, na huenda yakatuvutaje sisi? (b) Je! makosa katika kuhukumu yatatoweka mara hiyo ikiisha kupita “dhiki kubwa”? (c) Jambo hili linatokeza maulizo gani?

22 Leo, baraza za wazee zinatenda kazi katika makundi ya mahali na baraza inayoongoza ya wazee inatumikia makundi duniani pote. Sasa wale waliomo katika baraza hizo wote ni wanaume wenye makosa; lakini kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu wanaweza kutumikia vizuri mapenzi na makusudi Yake. Je! tunaona vigumu kuwaheshimu watu hao au kushirikiana nao kwa sababu tunajua kwamba ni wenye makosa? Basi, namna gani kipindi cha kwanza cha Taratibu Mpya?

23 Ijapokuwa toka mwanzo wake taratibu mpya ya Mungu italeta furaha kubwa, walakini, makosa hayatakwisha kwa siku moja ya kwanza, juma moja, mwezi mmoja, mwaka mmoja au hata miaka kumi ya kwanza kufuata “dhiki kubwa” na kufungwa kwa Shetani shimoni. Ikiwa ingekuwa hivyo, ni kwa sababu gani miaka elfu ya kurudishwa kabisa kwa ukamilifu na kuwapatanisha kabisa wanadamu na Mungu inawekwa? Namna gani, basi, ikiwa kosa fulani upande wa watu waliopewa madaraka kama wajumbe wa serikali ya Ufalme lingemvuta vibaya mmoja wa sisi, labda kutokeza tendo au mpango fulani ambao sisi tunaona hauko kama upaswavyo kuwa, likifanyiza chuki au kutoridhika kwingi? Je! tutakosa kuvumilia na kukasirika ikiwa mambo hayatengenezwi mara hiyo? Je! tutashawishwa tujichukulie wenyewe mamlaka ili tujaribu kuyatengeneza yale ambayo tunaona lazima yatengenezwe? Je! sasa tunaonaje hali zinazofanana na hii wakati tunapojitayarisha kuishi katika taratibu mpya ya Mungu?

24, 25. (a) Ni kwa sababu gani Uza alifia mikononi mwa Mungu? (b) Yaelekea alikuwa na kusudi gani, na lilionyesha maoni gani?

24 Tunao mfano wa kutuongoza katika kujitahidi kwa Daudi kulipeleka sanduku la agano Yerusalemu. Pahali pa kulipeleka sanduku kwa miti mabegani mwa Wakohathi na Walawi (kulingana na Torati), liliwekwa katika gari. Walipofika mahali fulani wale ng’ombe waliokuwa wakilivuta gari “walikunguwaa,” na mtu mmoja aitwaye Uza alinyosha mkono akalikamata sanduku. Jambo gani lilitukia? Yehova Mungu “akampiga huko kwa kosa lake; hata akafa pale pale penye sanduku la Mungu.” (2 Sam. 6:1-7) Lilikuwa kosa gani?

25 Sheria ya Mungu ilikataza kabisa mtu ye yote asiliguse sanduku takatifu asije akafa, isipokuwa wajumbe wa kikuhani peke yao walioruhusiwa. Sheria hiyo ilijulikana na watu wote, na bila shaka Uza (ajapokuwa si kuhani) alikuwa Mlawi, aliijua sana amri ya Mungu iliyosemwa kuliko wengine. Yeye alichagua kuivunja amri hiyo, labda akidhani kwamba hali ziliruhusu kufanya hivyo. Labda aliona kwamba ikiwa yeye asingelitegemeza sanduku bila shaka lingeanguka. Ikiwa ni hivyo, hakuwa na imani ya kwamba Mungu ana uwezo wa kuyaangalia mambo katika njia ambayo hakuna mmoja wa watumishi wake anayehitaji kuasi amri zake zilizosemwa. Kwa upande mwingine, labda alifikiri kwamba alipata nafasi ya kujifanya mwenyewe ‘shujaa,’ ili apate kujulikana sana kama ‘Uza, mwanamume aliyelizuia sanduku takatifu lisianguke.’ Katika njia mojawapo ya hizo alionyesha kutokuheshimu.

26. Tunapata onyo gani kutokana na hili litakalolinda maisha yetu katika Taratibu Mpya?

26 Matendo na njia zisizo za Maandiko, kiburi na unyakuaji havihesabiwi kuwa haki hata kidogo. Kwa vile yatakuwako mambo mengi sana ya kufurahisha katika taratibu mpya ya Mungu, si lazima hali zo zote za kwanza zitakazoonyesha makosa ya kibinadamu zitufanye tukasirike au kusema au kutenda bila kufikiri. Inatupasa ‘tuwe na akili katika mambo yote,’ tukikumbuka kwamba kanuni inayosema, “heri mwisho wa neno kuliko mwanzo wake,” itatumika hata katika utawala wa miaka elfu wa Mwana wa Mungu, na heri “mvumilivu rohoni kuliko mwenye roho ya kiburi . . . maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu.”​—2 Tim. 4:5; Mhu. 7:8, 9.

27, 28. Wakati mambo fulani yanaonekana kuwa yanahitaji kutengenezwa, ni mwendo gani unaofaa kufuata ili tupate kibali na baraka ya Mungu?

27 Ikiwa hatuna ruhusa ya kutenda katika jambo fulani, tunaweza kuwapasha habari wale walio na ruhusa. Pahali pa kujichukulia wenyewe mamlaka bila kuvumilia, tunaweza kuonyesha wakati huo kwamba tuna imani na uongozi wa Mungu wa mambo, tukiwa hakika kwamba katika wakati wake yeye atatokeza mema matupu. Kama Zaburi 4:4 inavyoshauri: “Mwe na hofu wala msitende dhambi, tafakarini vitandani mwenu na kutulia.”​—Linganisha Zaburi 63:6-8.

28 Kwa hiyo, tunaweza kujitayarisha kwa taratibu ya Mungu sasa kwa kuonyesha heshima kwa mipango ambayo Mwana wake anafanya katika kundi la Kikristo, tukiwa na uhakika wa kwamba Yehova Mungu na Kristo Yesu wanajua sana mambo yanayohitaji kutengenezwa.

[Picha katika ukurasa wa 561]

Je! kutamani afya kunamaanisha kwamba mtu yu tayari kuishi katika taratibu mpya ya Mungu? Wenye ukoma kumi walitaka waponywe na Yesu, lakini mmoja tu ndiye aliyekuwa na moyo uliomwongoza amtukuze Mungu. Moyo wako ukoje?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki