Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 9/1 kur. 389-393
  • Haki au Wajibu—Jambo Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Haki au Wajibu—Jambo Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAONI YA WAKRISTO
  • KUYACHANGANUA MAKUSUDI YETU
  • SI MTINDO, BALI KUJITENGA NA MAZOEA YA ULIMWENGU
  • “MAUMBILE YENYEWE” YANATUFUNDISHA SISI
  • Je, Mtindo Wako wa Mavazi Unamtukuza Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Watu Walio Huru—Lakini Watiifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Mataraja Kutoka Orofa ya 29
    Amkeni!—1998
  • Je, Mashahidi wa Yehova Huwashinikiza Watu Wabadili Dini?
    Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi Kuhusu Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 9/1 kur. 389-393

Haki au Wajibu​—Jambo Gani?

“Mwanangu, usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku, na miaka ya uzima, na amani.”​—Mit. 3:1, 2.

1-3. (a) Ni maoni gani ya watu wa ulimwengu leo juu ya haki? (b) Mtume Paulo anasema juu ya nani katika 2 Timotheo 3:1-5, na jambo gani litakalowapata wote walio na roho inayosemwa katika Waefeso 2:2?

ULIZO KUBWA katika akili za watu wa ulimwengu leo ni kuwekwa kwa haki zao. Wengi wanaona kwamba ni haki yao kufanya wapendalo bila kuwajali wengine. Kwa sababu hiyo, ulimwengu, zaidi ile sehemu inayoitwa ya “Kikristo,” imefikia hali ile iliyotabiriwa katika Biblia, kwamba watu wangekuwa ‘wenye kujisifu, wenye kiburi, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wakaidi.’​—2 Tim. 3:1-4.

2 Hii ndiyo roho ya ulimwengu. Ndiyo ya “roho ambayo sasa inatenda katika wana wa kutokutii.” (Efe. 2:2, NW) Sisi twajua kwamba inatuzunguka na inaweka mkazo juu ya kila mtu. Haitupasi tufikiri ya kwamba mtume Paulo, katika kusimulia hali mbaya zilizotajwa juu, alikuwa akiutaja ulimwengu wa watu wasiomwamini Mungu. Sivyo, yeye alisema kwamba watu hawa wasiotii wangekuwa “wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake.” (2 Tim. 3:5) Ni katika Kristendomu ndimo Biblia ilimosema hali hizi zingekuwamo, na ndivyo imekuwa. Watu wote walio na roho hii mbaya mwisho watakufa.

3 Basi, mtu ye yote akifuata namna hii mbaya yuko chini ya kutopendelewa na Mungu, kwamba yeye ni mtu wa kanisa au sivyo, au hata ikiwa amejitenga na taratibu za kidini za Kristendomu na amekuwa mmoja wa mashahidi wa Yehova. Wote walio na roho ya kujitegemea, ya kujisifu, ya ukaidi au hata wameambukizwa na roho hiyo kwa kadiri ndogo wamo katika hatari kubwa.

4, 5. Roho hii imetokeza nini upande wa wote, vijana na watu wazima?

4 Roho hii inaonekana katika habari tunazosoma, zaidi juu ya vijana leo. Ghasia shuleni na vyuo vikuu ni mfano. Wanashule wanazidi mno hata kuchukua bunduki na silaha nyingine zenye hatari katika shule. Wanaharibu mali ya shule wanakokwenda kupata elimu. Tunasoma juu ya ghasia zinazofanywa na vijana pasipo sababu hata kidogo. Wanakwenda mjini, wanavunja maduka na kupindua magari ya watu wasio na hatia wanaoendesha magari​—yote pasipo sababu.

5 Matendo haya ya uharibifu yanatokana na maoni ya kujiamulia, ya kujitegemea bila kutegemea sheria na kanuni zote. Ili kutetea matendo yao wanadai ati wanatumia “haki” zao. Watu hao wanataka waonyeshe ati hawana wajibu kwa ye yote. Hata kati ya watu wazima waliokomaa roho ya kujitegemea kwa uasi imeenea. Maelfu wanajidai haki ya mapato yaliyohakikishwa, lakini hawataki kufanya kazi. Wao wanataka mambo mazuri ya maisha, lakini hawataki kufanyiza cho chote. Kati ya wale waliokuwa wakitumikia watu wote, zamani, zawadi au “bakshishi” zilitolewa kwa utumishi uliofanywa kupita kadiri iliyotakiwa. Lakini sasa bakshishi hizo zinadaiwa, bila kujali ubora wa kazi inayofanywa.

6-8. Eleza tofauti iliyo katika maisha ya jamaa na katika shughuli nyingine ambazo zingeletwa na kuangalia wajibu pahali pa haki?

6 Hivyo, haki zinapodaiwa sana, wajibu haufikiriwi. Lakini ebu fikiri namna mambo yangekuwa ikiwa kila mtu angekuwa na maoni yale yale juu ya wajibu kama alivyo nayo juu ya haki. Hali ya leo ingekuwa vingine. Ndipo hapana mtu ambaye angeona yampasa asumbukie haki zake zote. Hii ingekuwa kwa sababu yeye na wengine wangekuwa wakiangalia wajibu wao.

7 Kwa kweli, kupigania haki kunatenganisha. Kutimiza wajibu kunaleta furaha na amani. Si vigumu kutazamia namna jamaa ingekuwa yenye umoja ikiwa kila mtu angefikiria wajibu wake, watoto wazazi wao, wazazi watoto wao. Kungekuwako kutumainiana na kufikiriana kuliko kutiliana mashaka na ugomvi.

8 Katika biashara, ikiwa wafanya kazi wangefahamu ya kwamba tajiri wao alikuwa na haki ya kuwatazamia kufanya kazi kwa uaminifu na ikiwa tajiri angefikiria hali njema ya wafanya kazi, akifahamu wajibu wake wa kulipa mshahara unaofaa, wote wangekuwa na hali nzuri. Nao wanunuzi wangekuwa wenye furaha, kwa sababu wangekuwa wakitumikiwa. Biashara ingekuwa bora na kazi salama zaidi. Lakini ulimwengu haukubali jambo hili kwa sababu ya choyo, mkazo juu ya ambacho kila mtu anaweza kupata, bila kuwafikiria wengine. Choyo hiki kinaenea sana katika watu wote na kimekuwa imara sana hata ulimwengu hauwezi kutengenezwa.

MAONI YA WAKRISTO

9. Ni maoni gani ya Wakristo juu ya kupigania haki?

9 Lakini Wakristo wanaonaje shauri la haki na wajibu? Wao wanayo haki waliyopewa na Mungu na vile vile wajibu wa kumwabudu Mungu na kutimiza amri zake, kutumia kanuni za Biblia katika maisha zao. (Mt. 4:10) Imewapasa wasimame imara kwa ajili ya haki hii. (Mt. 22:21) Si haki ya kipekee au iliyofanywa na wanadamu, bali ni haki ya kutoka kwa Mungu ndiyo wana wajibu wa kufanya mbele zake. (Mt. 28:18, 19) Wanapoendelea kuitumia haki hii, Mungu anawategemeza. Lakini Biblia haitii mkazo juu ya haki za kipekee. Inasema sana juu ya wajibu.​—Mhu. 12:13; Luka 17:10.

10-12. (a) Ni maoni gani ya Mkristo mbele za Mungu juu ya haki na wajibu? (b) Yamepaswa yawe maoni gani ya Mkristo juu ya kuzoea mambo fulani ya “kisasa”?

10 Ni maoni gani ya Wakristo wa kweli ambao wameuacha mwendo wa ulimwengu huu na wanaozoea imani katika dhabihu ya ukombozi ya Kristo? Biblia inawaambia hivi: “Ninyi si mali yenu wenyewe; maana mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu.” (1 Kor. 6:19, 20) Kwa hiyo, kuna sababu ndogo sana kwa watu hawa kusema juu ya haki za Mungu, kwa sababu wao ni mali yake kupitia kwa damu ya Mwana wake. Wao wanao wajibu. Wajibu ni: “Mtukuzeni Mungu.” Tunaweza kumtukuza Mungu kwa kuwa wenye amani, kwa kuwa wenye kuridhika, kwa kuwa wenye kusubiri hata ikiwa haki zetu zinaingiliwa na mtu mwingine. Tunamtukuza Mungu tunapotimiza wajibu wetu, si kudai kile tunachoona kuwa haki zetu, na kutofanyiza huzuni au kuudhika kwa wengine katika kudai “haki” hizo.​—Mit. 11:2.

11 Kwa hiyo, haiwapasi Wakristo wafikiri kwamba kwa sababu mazoea fulani yanaenea katika ulimwengu, wanaweza kusisitiza juu ya hayo kuwa ndiyo haki yao mbele ya kundi la Kikristo na kufikiri kwake kwa kukomaa. Kwa sababu gani Mkristo ajaribu kuleta roho ya ulimwengu, au mambo yanayoonyesha mfano wake, kama mitindo ya kupita kadiri ya mavazi, muziki wa kupita kadiri na yaitwayo mazoea ya kisasa, katika maisha yake ambapo yeye yu sehemu ya kundi? Kwa kweli, ni kwa sababu gani yeye ajaribu kuingiza mambo haya katika kundi la Mungu?

12 Huenda mtu akasema: ‘Huko ndiyo kuwa mtu wa kisasa. Sisi twataka tufanye yaliyo ya kisasa na kusonga pamoja na ulimwengu.’ Lakini fikiria juu yake​—roho ya ulimwengu huu inaharibika kwa haraka, inakuwa mbovu; na twaweza kutazamia mambo kuwa mabaya zaidi kadiri wakati usongavyo. Kila kizazi zamani kilifikiri kwamba ilikuwa “kuwa mtu wa kisasa” na kuwatangulia wengine, lakini jambo gani limevipata vizazi hivi na njia zao? Biblia inasema: “Kuna kizazi cha watu walio safi, machoni pao wenyewe; ambao hawakuoshwa uchafu wao.”​—Mit. 30:12.

13. Kuliko kuwa wenye kujitegemea, imetupasa tufanye nini sasa, na kwa sababu gani?

13 Je! tufanyize msukosuko katika kundi, au tuwe watu wenye kujitegemea na tujiondoe hata kidogo tusishirikiane sana na kundi sasa? Pahali pake, tunapoona ishara za “dhiki kubwa” zinaendelea kuongezeka zaidi, na hali ya ulimwengu huu kuwa mbaya zaidi, imetupasa tukaribie karibu zaidi na tengenezo la Kikristo, karibu zaidi na zaidi katika uchangamfu wa upendo. (Mit. 18:1) Imetupasa tuwe waangalifu zaidi juu ya maoni yetu na hali yetu na Mungu. Mtume Petro anasema juu ya uhitaji huu kwa nguvu sana anaposema hivi: “Na mwenye haki akiokoka kwa shida, yule asiyemcha Mungu na mwenye dhambi ataonekana wapi?”​—1 Pet. 4:18.

14. Kwa sababu gani ni jambo la bure kusisimka juu ya mtindo au namna fulani inayofuatwa na ulimwengu huu?

14 Tena, jambo ambalo huenda tukafikiria kuwa la maana sasa hivi huenda likawa si la maana kabisa katika taratibu mpya ya Mungu. Ndiyo, hata mwaka mmoja tangu sasa, jambo ambalo huenda tukapigania kama haki (mtindo fulani, mazoea fulani, namna fulani ya muziki) huenda likawa mtindo wa kale. Ndipo sisi wenyewe tusingelitaka. Basi kwa sababu gani sisi tutake kuliingiza katika kundi sasa? Mitindo na namna ya ulimwengu vinatoweka upesi na kusahauliwa. Lakini kundi la Mungu linaendelea milele. Biblia inasema hivi: “Mambo ya ulimwengu huu yanapita.” (1 Kor. 7:31) Sasa yanazidi kuwa mabaya, lakini mahali pake yatakaa mambo mengine. (1 Yohana 2:17) Yanaendelea kuwa ya mtindo wa kale kabisa. Basi itakuwaje na mitindo ya kisasa? nywele za matimutimu? mavazi yasiyo ya malidadi? Itakuwaje na mambo ambayo huenda sasa tunasisitiza kufanya kama haki yetu?

KUYACHANGANUA MAKUSUDI YETU

15. Kwa sababu gani ni jambo lenye faida kwetu kuliangalia shauri ambalo wenye madaraka katika kundi wanaweza kutoa?

15 Yehova awapenda wale wote wanaomfikia katika imani. Yeye anatamani utumishi na utii unaotokana na moyo. (Rum. 6:17) Kwa hiyo ni shabaha ya kundi la Kikristo kueleza namna mapenzi ya Yehova yalivyo, na kusaidia washiriki wote wa kundi wafahamu sababu gani​—kuwasaidia wote wamjue Yehova zaidi sana. Kwa hiyo, ni jambo lenye faida sana kwetu kuliangalia shauri ambalo wenye madaraka katika kundi wanatoa juu ya matatizo yanayotokea.​—Linganisha Kutoka 18:15, 16.

16-18. Mtu anawezaje kuyachanganua maoni yake mwenyewe na makusudi yake kukamatana na kufanya jambo fulani ambalo huenda likaonekana kuwa ni haki?

16 Ikiwa wewe unasumbuliwa na ulizo fulani linalotia haki zako, inafaa uchanganue namna fikira na makusudi yako yalivyo na namna yanavyopatana na njia ya kufikiri kwa Mungu. Ili tuonyeshe mfano, tutachagua shauri la mwanamume au kijana wa kiume mwenye nywele ndefu, zisizochanuliwa vizuri. Labda wewe unapenda mtindo huo na unataka nywele zako ziwe hivyo, na mmoja wa ndugu ameshauri kwamba ingefaa unyolewe nywele zako ili uonekane malidadi zaidi.

17 Ungeweza kuuliza hivi, ‘Je! mimi naupenda mtindo huo wa nywele kwa sababu nafikiri unanifanya nionekane vizuri zaidi, au ni kwa sababu ya watu ninaoshirikiana nao? Je! watu hawa ni washiriki katika kundi, au nje? Ikiwa wengine katika kundi wanao mtindo huo wa nywele, je! ni watu waliokomaa, je! ni wazee au watumishi wa huduma, wale ambao ni wenye bidii katika huduma ndio wanaofanya hivyo?’ Katika kufikiria hili, likumbuke shauri la mtume ‘kuwakumbuka wale waliokuwa wakiwaongoza, waliowaambia neno la Mungu; tena, kwa kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, iigeni imani yao.’​—Ebr. 13:7.

18 Halafu uulize hivi, ‘Mtindo wangu unaniweka upande wa jamii gani machoni pa watu wote? Je! mtu fulani ninayetembelea angeniweka upande wa kuwa mhudumu wa mashahidi wa Yehova?’ Kwa sababu gani ungejiona mmashamba ukiwa kati ya washiriki wa nje ikiwa hungekuwa na nywele ndefu? Je! waogopa watakayosema? Je! wajiona kwamba wanakutazamia wewe, kama mmoja wa mashahidi wa Yehova, kuvaa kama wao wanavyovaa? Au wewe wadhani kwamba kama mhudumu, ukivaa kama wao wanavyovaa ndipo wangekuheshimu zaidi?

19, 20. Ni mfano gani ambao ni hekima kuufuata ikiwa ndugu katika kundi wanashauri tugeuze mtindo au mazoea tunayofuata?

19 Ikiwa ndugu wenye madaraka katika kundi wanashauri kwamba ugeuze mtindo wako, au ikiwa wengine wanaona kwamba haumfai mhudumu, je! ungekuwa na nia ya kugeuza? Labda ungefikiri kwamba wanakosea, au labda ni watu wa mashamba, na ya kwamba hakuna haja ya kugeuza kwa sababu tu wengine katika kundi wanaudhika. Basi, je! ungeukubali mfano ambao Kristo mwenyewe aliweka?

20 Kwa habari ya Yesu, mtume Paulo alisema: “Kwa maana Kristo naye hakujipendeza mwenyewe; bali kama ilivyoandikwa, Malaumu yao waliokulaumu wewe yalinipata mimi.” (Rum. 15:3) Kristo hakudai haki zake. Ingalimfaa zaidi sana kuchukua mwendo ulio tofauti. Lakini, basi, yeye angalikuwa msaada gani kwetu?​—Mt. 26:53, 54; 2 Kor. 5:14, 15.

21. Mtume Paulo anaonyeshaje kwamba si jambo la Kikristo kwa mshiriki wa kundi kusisitiza juu ya mazoea fulani yanayowakwaza wengine?

21 Namna gani ikiwa mtu fulani angekuomba uache kula nyama kwa sababu wengine katika kundi wangekwazwa kwa sababu yake? Kitu gani? Kuacha haki ya msingi sana kama hii? Hata hivyo mtume Paulo aliufuata mfano wa Kristo alipoandika hivi: “Basi kama ni hivyo, na tufuate mambo ya amani na mambo yafaayo kwa kujengana. Kwa ajili ya chakula usiiharibu kazi ya Mungu. . . . Ni vyema kutokula nyama wala kunywa divai wala kutenda neno lo lote ambalo kwa hilo ndugu yako hukwazwa.” Ndipo Paulo anaposema kwa yeye ambaye dhamiri yake haikumsumbua kwa kula nyama bali ambaye angeshika mwiko kwa ajili ya hali njema ya kundi: “Ile imani uliyo nayo uwe nayo nafsini mwako mbele za Mungu.”​—Rum. 14:19-22; linganisha 1 Wakorintho 8:12, 13.

22. Toa sababu nyingine kwa nini imetupasa tugeuze mazoea au mtindo ambao ndugu wanaona unaleta mashaka juu ya habari njema za Ufalme.

22 Basi ni bora kuacha na kuwa na furaha ya kujua ndani yako mwenyewe kwamba unampendeza Mungu ijapokuwa huenda usikubaliane sana na maoni ya wengine, ijapokuwa unaona jambo unalofanya sasa linakubalika. Ingawaje, ukifuata mtindo fulani unaokupendeza wewe, ni nani wanaouona wakati wote? Nani wanaojua namna mtindo huo unavyoonekana kwako na wanaoweza kulinganisha sura yako na ile ya wengine? Wewe hujioni mwenyewe, sivyo? Ndivyo, ni wengine wanaokuona pande zote. Ndugu zako wakiona kwamba sura yako inatoa maoni mabaya kwa watu, au inasingizia au inaleta mashaka juu ya ujumbe unaochukua, sababu gani usigeuze, na kuwa mwenye furaha?

SI MTINDO, BALI KUJITENGA NA MAZOEA YA ULIMWENGU

23. Ilikuwa hali gani katika Israeli kwa mwanamume aliyependelea kunyoa pahali pa kuwa na ndevu?

23 Tunaweza kulitazama shauri la mtindo, au mavazi, kutokana na maoni mengine. Ikiwa wewe, kama mwanamume, ungeishi katika nyakati za Waisraeli, chini ya Torati, na hukupenda ndevu. Labda ungependa namna Wamisri walivyokuwa na sura, wenye kunyoa ndevu. Ungefanya nini? Je! ungetumia haki yako unyoe? Sivyo, kwa maana hungekuwa na haki hiyo. Ingekupasa uwe na ndevu, kwa sababu Torati iliwaamuru wanaume wote hivi: “Msinyoe denge pembe za vichwani, wala msiharibu pembe za ndevu zenu.”​—Law. 19:27; 21:5.

24. Ilikuwa sababu gani iliyotaka Waisraeli wawe na ndevu?

24 Je! Torati hii ilipewa kwa sababu ya mtindo? Hapana. Ilipewa ili kuwafanya Waisraeli wasiige mazoea ya mengine kati ya mataifa ya kipagani yaliyowazunguka. Walakini, iliwapasa Waisraeli wazitengeneze ndevu zao, wazifanye nadhifu na malidadi. Ndevu zisizotengenezwa vizuri au zilizonyolewa zilikuwa mfano wa huzuni na matanga kwa sababu ya msiba fulani. (2 Sam. 19:24-28; Isa. 7:20) Vile vile nywele zilikuwa zikikatwa mara kwa mara, isipokuwa mtu alikuwa Mnadhiri. Katika unabii wa Ezekieli makuhani wanaamriwa kuzipunguza nywele zao na wasiziache ziwe ndefu sana.​—Eze. 44:15, 20.

25, 26. Neno la Mungu linatupaje sisi maoni yake juu ya kufaa katika mitindo ya mavazi?

25 Tena, Mungu alijua ya kwamba mtindo wa mavazi unaweza kumweka mtu katika jamii mbaya alipoamuru kwamba “mwanamke asivae mavazi yampasayo mwanamume, wala mwanamume asivae mavazi ya mwanamke; kwa maana kila afanyaye mambo hayo ni machukizo kwa [Yehova], Mungu wako.” (Kum. 22:5) Kwa sababu gani? Kwa sababu kingekuwa kishawishi cha ufisadi.

26 Hivyo, ingawa kuna mitindo ya mavazi ya namna kama hivyo, kama suruali za wanawake na suruali za wanaume, hata hivyo kwa kawaida kuna tofauti kabisa ya mtindo au kitambaa. Lakini mtu anapovaa vazi hata karibu inakuwa vigumu kumtofautisha kama ni mwanamume au mwanamke, jambo hili ni baya machoni pa Yehova. Hali iyo hiyo na vazi lenye kubana sana au fupi sana hata linakuwa kishawishi cha ufisadi na linamweka mtu katika jamii ya wale ambao ni malaya. Basi, ikiwa unataka kusisitiza juu ya mtindo fulani wa nywele au mavazi, au mazoea fulani, jiulize mwenyewe hivi, ‘Je! mimi ninafanya hivyo ili niwaige watu wa ulimwengu?’

“MAUMBILE YENYEWE” YANATUFUNDISHA SISI

27, 28. (a) Mtume Paulo anatupaje sisi uongozi mzuri juu ya jambo linalofaa kwa Mkristo, kwa habari ya mtindo? (b) Wanachuo fulani wa Biblia wanasema nini juu ya neno “maumbile”?

27 Hakuna sheria zilizoandikwa katika Biblia, kama, kwa mfano, nywele za mmoja zimepaswa ziwe ndefu kadiri gani, au urefu wa vazi. Lakini mtume aliyeongozwa na roho ya Mungu anatoa uongozi mzuri wa kumwezesha Mkristo mnyofu, aliye wakf na kundi, kujua wakati mtindo au desturi inapofaa. Yeye anasema hivi: “Je! hayo maumbile yenyewe hayawafundishi ya kwamba mwanamume akiwa na nywele ndefu ni aibu kwake? Lakini mwanamke akiwa na nywele ndefu ni fahari kwake. Kwa sababu amepewa zile nywele ndefu ili ziwe badala ya mavazi.”​—1 Kor. 11:14, 15.

28 Kwa habari ya maneno haya ya mtume, mwanachuo wa Biblia Albert Barnes alisema hivi:

“Neno maumbile [asili] . . . kwa wazi linaonyesha hali ile ya adabu waliyo nayo wanadamu wote, na inayoonyeshwa katika desturi yo yote iliyopo au ya ulimwengu wote. . . . Ni kama ile inayotakiwa na hali ya asili ya kufaa kati ya wanadamu. . . . Kwa hiyo, neno hili hapa halimaanishi tabia ya wanaume na wanawake, . . . wala matumizi na desturi ya vivi hivi, . . . bali linamaanisha hali ya ndani ndani sana ya kinachofaa na kilicho chema.”

Na mwanachuo Mgiriki Dr. A. T. Robertson anasema hivi:

“Hapa linamaanisha hali ya asili ya adabu (k.m. Rum. 2:14) kuongeza kwa desturi ya vivi hivi, lakini ile iliyo juu ya tofauti yenye kusudi katika umbo la vitu.”

29. (a) Kwa sababu gani Mkristo hana haja na sheria za kumwambia jambo la kufanya na lisilo la kufanya? (b) Ikiwa, mara nyingine, mtu hajui, imempasa afanye nini?

29 Kwa hiyo si shauri la kwamba uwe ukiambiwa hasa jambo la kufanya na lisilo la kufanya, kama kwa sheria. Sisi tukiwa Wakristo na mioyo yetu inapenda chema, sisi tunajua kwa maumbile, hasa kwa dhamiri yetu iliyozoezwa, kwamba jambo fulani linaongeza au kupunguza utukufu wa habari njema tunazohubiri. Sisi twajua kama tunajenga au tunabomoa sifa au mfano wa kundi machoni pa wengine. Lakini, ye yote akiwa hajui, hapo imempasa ajiache mwenyewe aongozwe na dhamiri njema ya kundi la Kikristo. Na alikubali shauri jema na kutegemea uamuzi mzuri wa ndugu wenye madaraka.​—Mit. 12:15.

30. (a) Wale wote walio na vyeo vyenye madaraka katika kundi wako chini ya wajibu gani? (b) Ni kanuni gani yenye kuongoza itakayotufanya tuwe salama? (c) Kwa sababu gani tupendezwe sana na wajibu kuliko na haki?

30 Wakristo wa kweli wanapendana wao kwa wao, na wale walio na vyeo vyenye madaraka wako chini ya wajibu kufanya yaliyo ya faida tu kwa ndugu zao, kwamba ni katika mfano ambao wanaweka, au kwa shauri wanalotoa. Na matendo ya sisi sote yamepaswa sikuzote yaongozwe na kanuni hii: Je! mimi ‘ninayapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote’? Tukiutimiza wajibu wetu, kufanya kazi kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kwa wanadamu, Yehova atatuthawabisha sisi kwa baraka ambazo ni kubwa zaidi kuliko “haki” zo zote ambazo huenda tukajiwekea wenyewe, pamoja na miaka ya uzima na amani.​—Tito 2:10; Kol. 3:23, 24; Mit. 3:1, 2.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki