Je! Unavunjika Moyo?
KIZAZI hiki cha kisasa kinaweza kuitwa kizazi cha kuvunjika moyo. Zaidi na zaidi watu wanaonyesha kuvunjika kwao moyo kwa njia ya jeuri au kwa njia nyingine. Kwa mfano, kuna “Mke Aliyeshindwa,” anayeelezwa kama “Tukio la Ajabu la Karibuni,” na anayeelezwa katika gazeti la Life, March 17, 1972.
Gazeti hilo lilieleza juu ya mwanamke huyo, mwenye umri wa miaka 35, aliyehitimu chuoni, mke wa afisa wa serikali mwenye cheo cha kadiri na mama wa watoto watatu. Nyuma ya miaka kumi na minne ya maisha ya ndoa kwa ghafula aliiacha jamaa yake na kuanza maisha yake mwenyewe, akimchukua binti yake mwenye umri wa miaka kumi na kuwaacha watoto wa kiume wawili wachanga zaidi na baba yao. Sababu gani? Kwa kuwa alianza “kuona maisha kama yakizidi kuvunja moyo na kuchukiza.” Sasa anafundisha ili kupata riziki na ameungana na ‘chama’ cha wanawake.
Lakini inaweza kuulizwa juu ya mtu anayevunjika moyo, Ni kwa kadiri gani kosa ni lako mwenyewe? Je! linakuwa jambo lisiloweza kuzuiwa kwamba hali ambazo katika hizo unafanya kazi ni lazima ziwe za kuvunja moyo?
Kweli, kuna, hata kama vile Biblia inavyoonyesha, hali fulani tusizoweza kuzuia na zinazovunja moyo. Kwa sababu ya dhambi ya wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, sisi sote ‘tumetiishwa chini ya ubatili.’ Zaidi wapenda haki wote wanataka ‘kuwekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu.’—Rum. 8:20-22.
Neno la Mungu linatoa tumaini la kitulizo cha kuvunjika moyo huko, yaani, kwa njia ya ufalme wa Mungu, ambao Wakristo wote wanaombea: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani.” Mpaka wakati ambao ufalme huo utaleta mwisho wa kuvunjika moyo huko kunaweza kuvumiliwa kwa msaada wa Neno la Mungu, roho yake na watumishi wake.—Mt. 6:9, 10.
Sababu nyingine kwa nini wengine wanavunjika moyo ni kwamba wanajaribu kufanya mambo mengi kupita kadiri kwa wakati ule ule. Nyuki akiwa katika kichaka cha maua ya michungwa havunjiki moyo kwa sababu ya kuona maua mengi namna hiyo ambapo atapata asali. Hapana, anashughulika na ua moja nyuma ya jingine. Na hivyo kwa mambo yanayotakiwa kufanywa—chukua moja nyuma ya jingine.
Kweli, hapa tena tunapaswa kutumia hekima inayofaa na kujua kwamba ikiwa kuna mambo mengi yanayotakiwa kufanywa, mengine huenda yakakosa kuangaliwa, na kwa hiyo inatupasa tuyaweke mambo ya kwanza kwanza; anza na yaliyo ya maana zaidi na uepuke kushindwa na jaribu la kuanza yaliyo mepesi zaidi au yanayopendeza zaidi. Ndipo kama jambo fulani halifanywi, itakuwa si kitu sana.
Kwa kufanya hivi, lakini, usitoe wakati wako wote kwa jambo moja au mawili na kuyaacha mengine kabisa. Watu wenye bidii sana sana wanatakiwa waangalie jambo hili. Usishughulike na kazi moja mno hivyo kwamba unakuwa huna wakati wa kufanya mengine. Kama Yesu, Mwana wa Mungu, alivyoangalia, weka mambo ya kwanza kwanza lakini usiyaone mambo yaliyo madogo zaidi kama ovyo ovyo.
Ukija kuvunjika moyo kwa sababu ya kuwa na mambo mengi kupita kadiri ya kufanya, huenda ikawa kwamba unaweza kupata msaada wa wengine. Ikiwa chakula kikubwa kitatayarishwa, mama anaweza kuwauliza waliobaki wa jamaa kusaidia, hata kuwaruhusu wachanga kushiriki. Huenda ikachukua muda mrefu mara ya kwanza kumwonyesha mtoto namna ya kusaidia, lakini, hata hivyo, nyumaye katika nyakati fulani wakati utapatikana kwa mambo mengine. Na si hayo tu. Kuwazoeza watoto kuwa wenye usaidizi kutawasaidia kukomaa katika akili na maoni ya moyoni.
Vile vile mume huenda akavunjika moyo nyakati fulani kwa sababu ya kuwa na mambo mengi kupita kadiri ya kufanya. Lakini ikiwa ana nia ya kuvumilia anaweza kumsaidia mkewe kuwa wa msaada wa kweli; mkewe anaweza kujifunza kutumia motokaa ya jamaa kwa safari ndogo-ndogo, kutengeneza vitu vya nyumbani, na mambo kama hayo.
Vivyo hivyo ikiwa aliye na uangalizi, kama mnyapara au msimamizi, nyakati nyingine anavunjika moyo kwa sababu ya kuwa na kazi nyingi kupita kadiri, anaweza kutoa kazi fulani kwa wadogo wake. Kwa hiyo vile vile hapa mwendo wa hekima ni kwa mtu kuwa na nia ya kutoa wajibu kwa msaidizi na kwa hiyo kuepuka matokeo yanayochukiza ya kuvunjika moyo.
Kwa upande mwingine, kuna kuvunjika moyo kunakokuja wakati mambo zaidi yanatazamiwa kutoka kwa mtu kuliko awezayo kufanya au ya kadiri isiyopaswa atazamiwe kufanya. Uchunguzi unaonyesha kwamba namna hii ya kuvunjika moyo ni ya kawaida katika kazi na biashara. Halafu?
Kama vile mshairi anavyosema, ‘Wewe fanya tu yote uwezayo, kisha sifa au lawama ikujiayo, ina maana ile ile.’ Maadamu dhamiri yako haikuhukumu, jaribu kujipatanisha na maombi yasiyo ya busara ya wengine, wawe kazini au katika jamaa yako, kwa kutoyachukua maombi yenyewe kwa uzito mno, au kwa kuyafanya yapendeze, kwa ukunjufu kidogo. Huenda vile vile ikawa unaweza kufanya marekebisho mahali pengine katika maisha yako ili kutengeneza hali yenye kuvunja moyo ambayo unaweza kufanya machache juu yake. Kumbuka kanuni ya Biblia kwamba katika mchanganuo wa mwisho kila mmoja anasimama au kuanguka mbele za Mfanyi wake. Hivyo, “lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa [Yehova].”—Rum. 14:4; Kol. 3:23, 24.
Lo lote ufanyalo, usiache uvunjike moyo kwa kadiri ya kufoka kwa hasira. Kama vile mtaalamu wa mambo ya akili alivyoeleza: “Ikiwa usemi unaweza kukutia taabuni, njia bora ni kumaliza kuvunjika moyo kwako.” Ndiyo, “usikasirike, mwisho wake ni kutenda mabaya,” Biblia inaonya.—Zab. 37:8.
Na usiwe mtu wa kushindwa, mwoga. Mke aliyeshindwa aliyetajwa katika habari iliyotangulia alikubali ana kisirani kama alichokuwa nacho mbeleni, ila kwamba sasa ni kisirani chake. Lakini namna gani juu ya wale watoto wawili wachanga wa kiume alioacha? Namna gani atakapozeeka zaidi? Mumewe huenda akaoa tena, lakini ni nani ambaye angetaka kuoa mwanamke mwenye nia kama hiyo ya akili? Je! ‘wana wake wa kiume watakua na kumwita heri’? Je! mumewe atampa sifa ambayo Mfalme Lemueli alisema ingepewa mke anayefaa? Kwa kutoroka magumu yake ya jamaa anaweza kuingia katika magumu hata zaidi.—Mit. 31:10, 28.
Ndiyo, kuna njia bora za kushughulika na kuvunjika moyo kuliko kukimbilia kufanya jeuri au kuwa mtu wa kushindwa!