Watu Walio Huru—Lakini Watiifu
“Mwe kama watu walio huru, lakini mkiushika uhuru wenu, si kama kisetiri cha ubaya, bali kama watumwa wa Mungu. Waheshimuni watu wa aina zote, mwupende ushirika mzima wa ndugu, mwogopeni Mungu.”—1 Pet. 2:16, 17, NW.
1. Ni uhuru gani ambao mtume Paulo alionyesha kwamba yeye na wanafunzi wenzake walikuwa nao?
“KRISTO alituandika huru; kwa hiyo simameni, wala msinaswe tena chini ya kongwa la utumwa.” Hivyo ndivyo alivyoandika mtume Paulo akiisha kusimulia juu ya uhuru wa wana Mungu, ambao vile vile walikuwa wana wa tengenezo Lake la kimbinguni lililo huru, “Yerusalemu wa juu,” “mama” yao. Tengenezo hili ambalo ni “mama,” lenye uhuru wa ujamaa mkamilifu na Mungu, lilifananishwa kama ‘mke’ wa Yehova Mungu. Basi, akiwa hivyo, uhuru wake ulikuwa wa kadiri. Yeye alitii ukichwa wa Mume wake mkuu wa kimbinguni. Na kama wana, Paulo na wafuasi wenzake wa Kristo vile vile walikuwa na uhuru wa kadiri, kwa maana walimtii “Baba” na “mama” yao wa kimbinguni. Kama watoto, iliwapasa watii ‘mafundisho ya baba yao na sheria ya mama yao.’—Gal. 5:1; 4:26; Mit. 1:8.
2. Kwa sababu gani watu wa Mungu wako huru, hata hivyo kwa sababu gani uhuru wao si kamili?
2 Watu wa Mungu wako huru leo kwa sababu wao ‘wanaijua kweli, nayo hiyo kweli imewaweka huru.’ (Yohana 8:32) Walakini, uhuru walio nao ni wa mema, si wa mabaya. Wanaweza kujizoeza sana matunda ya roho, kwa maana “juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.” (Gal. 5:23) Haya ndiyo matunda yanayohitajiwa ili kupata furaha kamili; kufanya ubaya kunaleta tena utumwa wa dhambi na mauti. Ili waendelee kujizoeza yaliyo mema na yenye faida, inawapasa wamtii Yeye aliyewaweka huru, Yesu Kristo.
UTII UNAOLETA MEMA
3. Ni mpango gani, wenye kutaka utii, ambao Mungu ameweka katika kundi la Kikristo?
3 Tena, Mungu amefanya mpango duniani ambao amewafanya watu wake wautii. Hili ni tengenezo la kundi. Ndani yake amewaweka watu fulani walichunge na kuliongoza “kundi” lake. Wanaume wanawekwa katika vyeo ili wasaidie kundi litimize kazi ambayo limepewa, yaani, kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme. Tena, wanaume hawa wanatafuta hali njema ya kila mmoja wa washiriki wa kundi, ili kuwasaidia wazitumie kanuni za Biblia katika maisha zao. Vile vile inampasa Mkristo awatii wanaume hawa, mtume akiamuru hivi: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya roho zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.”—Ebr. 13:17.
4. Mungu amewaweka Wakristo chini ya sheria gani nyingine za utii, na je! hizi ni kizuizi kwa huduma ya Kikristo?
4 Zaidi, Wakristo wanaamriwa ‘waitii mamlaka iliyo kuu,’ watawala wa kiserikali katika ulimwengu huu. Inawapasa wazitii sheria zisizopingana na sheria za Mungu. (Rum. 13:1; linganisha Matendo 4:19; 5:29.) Inawapasa watumwa wa Kikristo wawatii mabwana zao, kanuni hii inawapasa wafanya kazi wanaoajiriwa leo, ambao imewapasa “wauonyeshe uaminifu mwema wote.” (Tito 2:9, 10) Inawapasa watoto wawatii wazazi wao. (Efe. 6:1-3) Amri hizi zote haziwazuii Wakristo kufanya mema na kuitimiza huduma yao ya Kikristo, bali, kwa kuzitii sheria hizi wanamtukuza Mungu na kuendesha faida za Ufalme.
5. Ni katika njia gani Wakristo wanawatii ndugu zao wote?
5 Sasa, kuongeza kwa mamlaka hizi za namna mbalimbali ambazo inampasa Mkristo azitii, utii unaomletea mema na uhuru na furaha yake kubwa zaidi, mtume anaendelea hata zaidi, akitia moyo hivi: “Katika kuonyesha kuheshimiana ongozeni.” (Rum. 12:10, NW) Basi, Wakristo wote wanawatii ndugu zao wote, kwa maana inawapasa watumikie faida za ndugu zao kwanza kuliko zao wenyewe.—Marko 10:44; 1 Pet. 5:5.
UTII ALAMA YENYE KUTOFAUTISHA
6. Ni jambo gani ambalo kwa kutokeza linaonyesha tofauti kati ya Mkristo wa kweli na mlimwengu leo?
6 Hili linamweka Mkristo katika cheo gani akilinganishwa na wale wote walio na maoni ya ulimwengu? Mwendo wake ni wa utii, hali mwendo wao ni wa kutokutii. Hili ndilo jambo kubwa linalotofautisha. Lo! namna imetupasa tulione shauri la utii kwa uzito!
7. Huenda tukashawishwaje kujiunga na walimwengu, lakini imetupasa tukumbuke nini?
7 Walakini, huenda mara nyingine tukashawishwa kufanya vingine. Karibu na sisi tunaona kuasi kila namna ya mamlaka. Tunausikia usemi wa namna hiyo. Tunaona mambo yasiyo ya haki, na huenda tukaanza kujiona kwamba watu hawa wasiotii wanahesabiwa haki. Huenda tukaanza kujiunga nao na huenda hata kuanza kufikiri kama tunaziona sababu za kufanya vita katika kundi la Kikristo. Huenda ikawa kwamba vijana na wengine katika ulimwengu wanaona wanazo sababu za kuasi hali zilizomo katika ulimwengu. Kweli, yako mambo yasiyo ya haki. Waache walimwengu wafanye wapendavyo. Lakini wala vijana walio kati yetu wala wo wote wa watu wa Mungu haiwapasi wawe wakipigana vita vya ulimwengu. Na kwa hakika hawana sababu ya kuasi au hata kuwa wasiotii mpango wa Mungu.
8. Ungesemaje juu ya kutokutii maneno ya Musa, kwa sababu ya yaliyotokea katika Mlima Sinai?
8 Ebu ifikirie hali ya watu wa Mungu sasa, kama inavyosimuliwa katika Maandiko. Paulo analinganisha hali ya Israeli chini ya Musa na ile ya kundi la Kikristo, akisema: “Maana hamkufikilia mlima uwezao kuguswa, uliowaka moto, wala wingu jeusi, na giza, na tufani, na mlio wa baragumu na sauti ya maneno; ambayo wale walioisikia walisihi wasiambiwe neno lo lote lingine; maana hawakuweza kustahimili neno lile lililoamriwa, Hata mnyama akiuguza huo mlima atapigwa kwa mawe. Na hayo yaliyoonekana jinsi yalivyokuwa ya kutisha, hata Musa akasema, Nimeshikwa na hofu na kutetemeka.” (Ebr. 12:18-21) Hata hivyo, wengine walifikiri kwamba walikuwa na haki ya kuonyesha kutokumtii Musa. Je! wewe ungaliungana na wanaume na wanawake hao kama ungalikuwapo penye wonyesho huo wenye kuogofya katika Mlima Sinai?
9, 10. Kwa sababu gani ni jambo zito zaidi sana kwa Mkristo kuwa asiyetii?
9 Paulo anaendelea kusimulia matukio yenye kuogofya zaidi: “Bali ninyi mmeufikilia mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni, na majeshi ya malaika elfu nyingi, mkutano mkuu na kanisa la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni, na Mungu mwamuzi wa watu wote, na roho za watu wenye haki waliokamilika, na Yesu mjumbe wa agano jipya, na damu ya kunyunyizwa, inenayo mema kuliko ile ya Habili.”—Ebr. 12:22-24.
10 Ndipo Paulo anapoonya hivi: “Angalieni msimkatae yeye anenaye. Maana ikiwa hawakuokoka wale waliomkataa yeye aliyewaonya juu ya nchi, zaidi sana hatutaokoka sisi tukijiepusha na yeye atuonyaye kutoka mbinguni.” “Na tuwe na neema, ambayo kwa hiyo tumtolee Mungu ibada ya kumpendeza, pamoja na unyenyekevu na kicho.”—Ebr. 12:25, 28.
WEWE UNALIPOKEAJE SHAURI?
11, 12. Ni katika njia gani huenda tukaonyesha kutojali au dharau kwa shauri tunalopewa na ndugu mwenye madaraka, lakini kwa sababu gani tungekuwa tukizipinga faida zetu bora kwa kufanya hivyo?
11 Je! twasadiki kwamba hivi ndivyo ilivyo, kwamba Wakristo wako katika hali hiyo yenye kuogofya sana? Basi imetupasa tusikilize kwa maoni gani onyo la kiroho tunalopokea kila siku? Na imetupasa tuoneje ikitukia hali ambayo katika hiyo mtu fulani mwenye mamlaka, ndugu, anatoa shauri? Je! tulione kama matusi, tukisema, ‘Ana haki gani kusema kwangu namna hii?’ au, ‘Mimi nina haki ya kufanya (au kutofanya); yeye hana mamlaka ya kunishauri mimi’?
12 Kwa sababu gapi maoni hayo yangekuwa yenye makosa? Na kwa sababu gani lingekuwa kosa vile vile kusingizia kusikiliza tu kwa sababu tunajua inatupasa tumheshimu anayesema kwetu, na hata kukubali kwa mdomo tu, lakini kumbe kweli hatupokei shauri? Kwa sababu, ijapokuwa kuna mambo fulani ambayo kundi haliwezi kutoa amri, ni mambo ambayo ni kwa faida ya kundi zima, kutia na wewe, kwa maana hali yako njema inafungamana na kundi, ikiwa wataka miaka ya uzima na amani iongezwe kwako.
13. Mtu anayedharau shauri linalopewa anasema nini kweli, na ni shauri gani la Biblia ambalo imetupasa tulifikirie kwa uzito?
13 Kwa hakika, mtu angekuwa akifanya nini ikiwa angeonyesha maoni hayo yaliyotajwa juu? Kwa kweli, yeye angekuwa akisema kwamba Mungu haliongozi kundi lake, kwamba Yeye hatufundishi sisi njia ya kweli katika tengenezo lake. Ni kuonyesha kukosa imani. Je! kweli wo wote kati ya sisi wanataka kusema hivyo? Imempasa afikirie kwa uzito maneno ya mtume katika Waebrania 3:16-19; 4:11-13; 12:1.
SI UHURU WOTE ULIO HAKI
14. (a) Ni kanuni gani itakayotuwezesha kujua mambo ambayo huenda tukawa huru kwa kimwili kuyafanya, lakini tusiwe na haki ya kuyafanya? (b) Ikiwa tunakataa kufuata shauri linalotoka kwa kundi juu ya mashirika, tutapata nini?
14 Na tuifikirie hali ambayo katika hiyo kundi haliwezi kutuamuru sisi tufanye au tusifanye jambo fulani. Kuna mambo ambayo tuna uhuru wa kuyafanya, katika namna ambayo hapana mtu ambaye anaelekea kutuzuia. Tunao uhuru wa kimwili, kwa mfano, kushirikiana na ye yote tunayetaka, lakini sisi hatuna haki kama Wakristo kushirikiana na ulimwengu. Mashirika mabaya si yenye faida kwa mtu au kwa ndugu zake katika kundi, wala hayajengi. Kwa kweli, kundi haliwezi kumwadhibu mtu kwa kuhalifu kanuni ya kwamba “mashirika mabaya yanaharibu mazoea mema,” lakini yeye atavuna matokeo yenye hatari, kwa maana Mungu anaweza na atazifikiliza sheria zake zote. “Mungu hadhihakiwi.”—1 Kor. 15:33, NW; Gal. 6:7.
15. Tukifuata mitindo isiyo ya kadiri, tunashirikiana na nani?
15 Ikiwa tunataka tufuate au tuige mitindo ya ulimwengu isiyo ya kadiri na njia zake za kufanyia mambo, tunaweza kufanya, lakini je! inajenga? Tunashirikiana na nani? Zaidi na ulimwengu wenye kufurahisha. Huenda ikaonekana kwetu kwamba wamo katika watu wengi na ya kwamba sauti yao inawakilisha watu wengi kwa sababu ndio tunaowaona katika televisheni na katika sinema. Lakini ni nani aliye kati ya wale wa kwanza katika kueneza uchafu? Tena, ni ulimwengu wenye kufurahisha. Jukwaani na kiwamboni wanaonyesha uchi, ngono, mambo ya uhanithi, na wanajaribu kuzifanya picha kuwa zenye kuchukiza zaidi na zaidi, zenye kuogofya na zenye kutapisha zaidi. Sinema moja ilitangaza kwamba kila mtazamaji angepewa mfuko wa kutapikia ikiwa angechafuka moyo wakati wa kuonyesha sinema.
16. Mtu akianza kuiga makutano ya kilimwengu, ni ulizo gani ambalo huenda likaulizwa juu yake?
16 Sasa, ikiwa mtu ye yote anaanza kuiga makutano ya watu wenye kuonyesha mambo hayo katika sinema na televisheni, au wale wanaopenda mambo ambayo wanaonyesha, yeye atafika wapi? Je! atavua mavazi yake wanapofanya hivyo? Je! atafanya kama walivyokaribishwa watazamaji wafanye katika jumba la sinema la New York, yaani, waende jukwaani washiriki mchezo? Wachache ndio watakaotaka kufanya hivyo. Lakini mtu akipotoka akiufuata mfano ambao watu hawa wanaweka, atafika mpaka wapi? Na Mkristo anayeingiza alama ndogo ya maoni yao katika maisha yake anayachafua. Kwa hiyo yeye hana haki ya kuingiza mambo hayo katika kundi, bali, yeye ana WAJIBU wa kuyaondoa.
17. Mtu anawezaje kujua kama mazoea fulani ni mazuri au si mazuri?
17 Mtume anatuambia jambo linaloamua kwamba imetupasa tufuate mazoea fulani ama tusiyafuate. Yeye anasema hivi: “Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake.” Kila mtu anaweza kuchanganua matendo yake. Ikiwa kweli haya yanawasaidia wengine kwa kiroho, anafanya vyema.—1 Kor. 10:24.
KULISAIDIA KUNDI KATIKA VITA VYAKE
18. Ni ulizo gani ambalo ni zito sana wakati huu, na sisi tunakamatanaje na ulizo hilo?
18 Katika wakati huu, ambapo kila sehemu na kila desturi ya taratibu hii ya ulimwengu ya mambo inapochafuliwa, kuharibiwa na kuwa mbovu, swali la maana ni, Je! kundi la Mungu vile vile litaambukizwa na kuchafuliwa polepole? Je! litabaki kuwa safi kama tengenezo peke yake katika ulimwengu la kutukuza jina la Mungu na kanuni zake za haki? Hili ni ulizo zito sana. Linakamatana sana na ulizo kubwa la enzi ya Mungu. Usifikiri hata kidogo kwamba Ibilisi hafanyi vita vikali zaidi sana juu ya kundi. Na usifikiri kwamba hauko vitani, kwa maana yeye anapigana ili akuchafue WEWE, Mkristo peke yako.—Ufu. 12:17.
19. Ni njia gani ambayo Yehova ametayarisha ili kundi liendelee kuwa safi, na hii inataka nini upande wetu?
19 Kundi la Mungu litasimama, kama Biblia ilivyotabiri. (2 Tim. 2:19) Mungu amewaweka wanaume katika vyeo vyenye madaraka ili kuhakikisha kwamba linaendelea kuwa safi, na kwamba kila mmoja wa washiriki wa kundi analindwa kwa msaada wa wanaume hawa wa kiroho. Kwa hiyo, wanaume hawa wanapotoa shauri, wanapomkaripia mshiriki anayefanya dhambi, au hata kumfukuza mwasi kutoka katika kundi, imetupasa sisi sote tushirikiane. Imetupasa tufurahi kwa vile Mungu ameweka mpango huo wenye ulinzi.
20. Shauri katika Wakolosai 3:2 linatusaidiaje tushirikiane sana na kundi?
20 Tunaweza kushirikiana na kundi kwa ‘kuyafikiria yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi.’ “Yaliyo katika nchi” ni mambo ambayo mara nyingi yanatuvutia sisi. Huenda kwanza tukapata taabu katika kuona tofauti kati ya uhuru tunaoruhusiwa kuyafanya mambo haya na haki ya kuyafanya. Lakini tukijifunza, kutafakari na kukazia fikira juu ya “yaliyo juu,” mambo ya Mungu, tunaweza kuona waziwazi maoni yetu yapaswavyo kuwa.—Kol. 3:2.
21. Tunawezaje kuonyesha uaminifu kwa kundi wakati ndugu anapoadhibiwa au kukaripiwa na wale wenye vyeo vyenye madaraka?
21 Halafu, tunaweza tena kuonyesha uaminifu kwa kundi la Mungu kwa kutegemeza vita vyake ambavyo linaendesha ili lenyewe liendelee kuwa safi na kusaidia kwa kuwashauri au kuwaadhibu wanaofanya makosa. Kuliko kumfanya ndugu aone kwamba ile adhabu aliyopewa haikuwa nzuri, tunaweza kusema naye kwa upole, tukimwonyesha jambo lililofanya mwendo wake usiwe wa hekima, tukimkaripia, kumsaidia aone namna anavyoweza kuinyosha njia yake na kuwa mwenye furaha zaidi. Tunaweza kuwasaidia wazee katika jitihada zao za “kumtengeneza upya.” (Gal. 6:1, NW) Tutaepuka kumfanya mtu huyo kujiona anahesabiwa haki. Ikiwa tunapinga hatua hiyo ya kumwadhibu, kwa kufanya hivyo tunapinga faida zake. Kama Maandiko yanavyosema, sisi ‘tunamchukia ndugu yetu moyoni mwetu.’—Law. 19:17.
HATARI YA KULETWA CHINI YA MAMLAKA MBAYA
22, 23. Ebu eleza maneno ya mtume katika 1 Wakorintho 6:12, 13.
22 Kuna njia nyingine ya kulitazama ulizo juu ya kadiri ambavyo uhuru wetu kama Wakristo unavyoendelea na ni katika mambo gani kumtii Mungu kunauwekea mpaka. Ebu yaangalie maneno ya mtume: “Vitu vyote ni halali kwangu, lakini si vyote vifaavyo; vitu vyote ni halali kwangu, lakini mimi sitatiwa chini ya uwezo wa kitu cho chote.” Mtume anataja kama mfano kula chakula. Hakuna kitu ambacho kingeweza kuthibitishwa kwa wazi zaidi kama haki kuliko kula chakula. Lakini Paulo anaeleza kwamba ikiwa kula kwa vyakula fulani kwafanyiza ugomvi na wengine katika kundi, imempasa Mkristo awe na nia ya kuacha. Si kitu kwa sababu ya faida za Ufalme na kukilinganishwa na faida za ndugu zake. Paulo anasema: “Vyakula ni kwa tumbo, na tumbo ni kwa vyakula; lakini Mungu atavitowesha vyote viwili, tumbo na vyakula.”—1 Kor. 6:12, 13; 10:23.
23 Chakula kinaharibika wakati kinapoliwa. Hakiendelei kwa muda mrefu. Tena, kwa wakati wake mtu anayependa sana kutosheleza tu hamu au tamaa yake ya kimwili ataharibiwa na Mungu. Kwa kweli, basi, Mkristo anayesisitiza juu ya njia fulani ijapokuwa maoni ya kundi au ijapokuwa shauri la Biblia la kumkanya anafanya nini? Yeye analetwa chini ya kutii mamlaka mbaya kwa maoni yake, kwa azimio lake au kusisitiza juu ya kufanya mambo fulani ambayo kwa choyo anataka kuyafanya. Yeye anatenda kwa kutokumtii Mungu. Basi, yeye anamtolea nani utii na utumishi? Adui ya Mungu. Kwa hakika yeye ni mtumwa wa mwendo usio mzuri, na maoni yake yatamwongoza katika taabu kubwa maishani mwake akiendelea.
24. Maneno ya Paulo juu ya nyakati za hatari katika “siku za mwisho” yanawapasa nani, na hili limepaswa lituhangaishe namna gani?
24 Ndiyo sababu Paulo alimwandikia Timotheo, mwangalizi katika Efeso, akimwonya kwamba katika “siku za mwisho” watu wangekuwa “wakaidi,” “wenye kujipenda wenyewe,” “wenye kujisifu,” “wasiotaka kufanya suluhu.” Paulo alimwonya Timotheo kwamba mambo hayo yangeonekana sana katikati ya wale waliomo katika Kristendomu wanaojidai kuwa Wakristo. Lakini hali hizi hazipaswi ziruhusiwe kuingia katika kundi la kweli la Kikristo lenyewe. Hivyo, ikiwa mtu katika kundi anakuwa mkaidi, yu katika hali mbaya zaidi kuliko na wakaidi waliomo katika ulimwengu, kwa maana mtume Petro anasema kwamba ‘hukumu inaanza katika nyumba ya Mungu.’ Mtu huyo ana daraka zaidi kwa Mungu kuliko yule aliye nje ya kundi. Yeye yu katika hali yenye hatari sana.—2 Tim. 3:1-5; 1 Pet. 4:17.
JIHADHARI NA KUTAKA “BADILIKO”
25. Kwa sababu gani imewapasa Wakristo wasijiunge na wale wanaojaribu kuugeuza ulimwengu kuwa bora?
25 Kuna hatari kwa wote, zaidi vijana, kwa sababu kuna msukosuko kila mahali wa kutaka “badiliko.” Wengi wanaotaka mabadiliko ni watu wanyofu, wenye kuona uchafu na mambo yasiyo ya haki na wanataka kitu fulani kilicho bora, lakini wasijue namna kipaswavyo kuwa. Lakini wale wenye kupashwa habari juu ya ufalme wa Mungu na wanaoshirikiana na kundi la Mungu wanajua juu ya mwundo wake wa kitheokrasi; wanajua kwamba linapatana na kanuni za Neno la Mungu. Imewapasa watu hawa wakumbuke kwamba ulimwengu unajaa sana choyo kinachopingana kabisa na kanuni za haki, na hauwezi kugeuzwa uwe bora. Hakuna sababu ya kujaribu kufanya hivyo. Tena imewapasa wajue kwamba haiwapasi wajaribu kulibadili kundi kulingana na mawazo yao wenyewe ya kipekee, au kulingana na mawazo ya wale wanaotaka mabadiliko katika ulimwengu. Kufanya hivyo kungekuwa kuiingiza roho ya ulimwengu katika kundi, ambalo lazima liendelee kutokuwa upande wa ulimwengu huu.
26. Maandiko yanaonyaje juu ya hatari kwa wale wanaotaka kuleta mabadiliko katika kundi kulingana na mawazo yao wenyewe au yale ya ulimwengu?
26 Ni matokeo gani ya mwendo wenye hatari wa kutaka badiliko, kufikiri kwamba kundi la Mungu ni “la kikale,” au kwamba halifuati sana njia na mawazo ya kisasa? Labda maoni haya yatajitokeza yenyewe katika kujaribu kuweka “haki” fulani za kipekee katika kundi. Ebu angalia mwenye hekima alivyomwambia mwanawe, katika kitabu cha Mithali: “Mwanangu, mwogope Yehova na mfalme. Usijitie kati ya wale wanaotaka badiliko. Kwa maana msiba wao utatokea kwa ghafula sana, kwamba ni nani ajuaye kutoweka kwa wale wanaotaka badiliko?”—Mit. 24:21, 22, NW.
27. Yatakuwa matokeo gani kwa wale wanaojizoeza uhuru ambao Mungu anawapa, wakati uo huo wakikuhali matakwa ya utii kamili?
27 Yehova awapenda wale wanaomtii yeye. Ampenda mtu anayesoma Neno lake, anayelitafakari, na anafuata shauri lake jema, bila kujali namna shauri hilo linavyompasa yeye. Lo! uhuru ambao Yehova anawapa wale wanaomtii yeye! Yeye atabadili sura ya dunia hii kwa kuwafutilia mbali wanaoichafua. Mwisho wanadamu wote wataokolewa kuingia “katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” Ujamaa wa baba mwenye upendo na wana watiifu utarudishwa. Kupitia kwa upendo wake usiolinganishwa anaouonyesha kwa wana watiifu Yehova ataweza kutoa kwao mali nyingi mno za kiroho na za kimwili kwa umilele wote!—Rum. 8:21; Ufu. 11:18.
—Kutoka The Watchtower, March 1, 1973.