Katika Kundi, Itikia Huruma za Yehova
1. Ni mpango gani katika kundi la mashahidi wa Yehova unaopatikana kwa wote, nao unawasaidiaje washiriki?
MMOJAWAPO wa mipango bora inayopatikana katika kila kundi la mashahidi wa Yehova ni Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ambayo wote katika kundi wanakaribishwa kushiriki. Kuhudhuria Shule hii kunawezesha washiriki wajitahidi wenyewe kujifunza habari maalum za Biblia. Je! wewe mwenyewe unashiriki? Ikiwa ndivyo, unaongeza elimu na ufahamu wako mwenyewe, sivyo? Tena, unaongeza ubora wa utoaji wako wa kweli kwa watu wengine, kuwa mwenye kujenga kwa kiroho kwa wengine katika kundi.
2. Ni mambo gani ya hakika juu ya Neno la Mungu yanayomtia moyo mtu afaidike sana na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi?
2 Ijapokuwa mpango uko, huenda watu wengine katika kundi wasishiriki katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Kwa sababu gani? Labda ni kwa sababu ya kujiona kukosa uwezo na wanaogopa kwamba hawawezi wakastahili hata kidogo. Je! isingefaa watu kama hao wafikirie uhakika wa kwamba Yehova awataka watu wake waseme kweli yake? Faida tele zinatokana na kusema yanayotoka katika Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu. “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa [1] mafundisho, na kwa [2] kuwaonya watu makosa yao, na kwa [3] kuwaongoza, na kwa [4] kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe [5] kamili, [6] amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.” (2 Tim. 3:16, 17) Ni faida bora kweli kweli!
3. Ni msaada gani unaotolewa na Shule ambao ni wenye kutia moyo vile vile?
3 Hakuna shaka juu ya kutaka kwa Yehova watu wake waseme kweli na kuisema waziwazi. Hii haina maana ya kwamba wote watafikia uwezo ule ule wa kusema kama wasemaji wa jukwaani; hata hivyo, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi itawasaidia wote waongeze elimu, ufasaha wa kusema na usahihi wa maneno na vile vile uwezo wa kuwafikia watu wengine. Kushiriki katika Shule vile vile kunasaidia kusitawisha upendo kwa ndugu na dada wengine katika kundi. Tena, inaonyesha imani upande wa washiriki wanaojitahidi kwa pekee katika uhakika wote na katika kumtegemea Yehova.
4. Ebu simulia tena mambo yaliyoonwa ambayo yamesimuliwa hapa na kuonyesha namna katika hayo imani inavyoonyeshwa.
4 Hii ni kweli hata kwa habari ya wengine ambao huenda wakawa si wenye ujuzi sana wa lugha inayosemwa katika eneo ambalo ndani yake wanaishi. Ijapo kizuizi kama hicho wanakuwa wenye ujuzi sana katika huduma kwa sababu wanajitahidi kweli kweli katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mambo yanayotimizwa na roho ya Mungu ni ya ajabu sana. Watu wasio na elimu wanashinda hali zao kwa msaada wa Shule hii, kama inavyoonyeshwa na habari ifuatayo iliyotolewa kutoka katika barua iliyopokewa kutoka afisi ya tawi ya Sosaiti katika Dahomey, Afrika Magharibi:
“Ndugu wanapata shida fulani. Karibu watu wote hawajui kusoma wala kuandika. Ushirikina wa kidini uko imara sana. Halafu kuna lugha nyingi, ijapokuwa hakuna lugha ya taifa. Kwa mfano, katika mji wa Cotonou sasa yako makundi matano ya mashahidi wa Yehova na mikutano yao inaongozwa katika lugha mbalimbali tano. Lugha nyingi haziandikwi, na hivyo inawapasa watu wafundishwe katika lugha inayoandikwa. Mwaka jana watu 108 walifundishwa kusoma. Hawa walikuwa wakihudhuria darasa la kusoma na kuandika kama lilivyoongozwa chini ya usimamizi wa makundi. Wangali wako ndugu 600 wasiojua kusoma, na mwaka ujao watakuwa wakifanya bidii zaidi juu ya shida hii. Kwa kweli, uhitaji wa kusoma ni mkubwa, kama ilivyosimuliwa na mhubiri aliyekuwa hajui kusoma.
“Ndugu huyu alikuwa mpya naye alikuwa akifanya utumishi wa nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza. Alimfikia Mprotestanti aliyejua kwamba asingeweza kusoma basi akasema hivi: ‘Usije kunihubiri mimi mpaka wewe mwenyewe utakapoweza kusoma Biblia.’ Ijapokuwa mhubiri mpya aliendelea kujaribu kusema na mtu huyo, hakusikiliza, akasema tena kwamba mtu asiyejua kusoma hangeweza kufundisha cho chote. Sasa mhubiri aliazimia kushinda shida hii. Pahali pa kuridhika na kuhudhuria darasa la kujifunza kusoma tu, alikuwa akijifunza zaidi kila siku kwa majuma sita. Kila alipokwenda alichukua kitabu chake na kuwaomba wale ambao wangeweza kusoma wamsaidie kutamka maneno. Yalipokwisha majuma sita alirudi katika utumishi, na unajua mtu wa kwanza ambaye alifikia alikuwa nani? Kumbe! ni mtu yule aliyekuwa amekataa kumsikiliza mara ya kwanza alipoanza kuhubiri. Wakati huu yule Mprotestanti hakushangaa kwa kumsikia mtu huyu ‘asiyejua kusoma’ akimsomea Biblia tu bali vile vile alipendezwa na yale aliyokuwa akifundisha.
‘‘Wakati wa mwaka ujao tunatumaini kwamba wengi zaidi wataona maana ya kuweza kusoma ili ‘habari njema’ zipate kuhubiriwa kwa matokeo zaidi katika sehemu hii ya shamba ili ‘kuwafanya wanafunzi zaidi.’”
5. Wanyenyekevu wanawezaje kulitegemeza tengenezo la watu wa Yehova?
5 Kama inavyoonyeshwa katika tukio hilo lililotangulia, na vile vile kama inavyoonyeshwa katika matukio yaliyoandikwa katika Maandiko, watu walio wanyenyekevu mara nyingi wanabarikiwa zaidi ikiwa wanaitikia mapendeleo na nafasi zao katika utumishi wa Yehova, wakifanya yale wawezayo katika imani. Ikiwa wanyenyekevu wanashirikiana na kundi, wamepaswa watiwe moyo washiriki katika huduma ya shambani, ikiwa wanastahili kufanya hivyo kulingana na Maandiko, na wamepaswa wasaidiwe wapanue utendaji wao. Itikio lao zuri katika neno hili ni tegemezo kwa tengenezo la watu wa Yehova wakati wanapojitahidi kwa kutumia uwezo waliojaliwa, wakati uo huo wakiutunza unyenyekevu wao. Mwendo huu utasaidia kuleta matokeo mazuri yanayotajwa katika Waefeso 4:2, 3: “Kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa [roho] katika kifungo cha amani.”
6. Ni matokeo gani yenye kufikia wote ambayo huenda yakapatwa kupitia kwa jitihada za uaminifu za mtu mnyenyekevu?
6 Habari ya Maandiko, inayoonyesha si kundi la watu wa Yehova lililo mahali pamoja tu kuwa likisaidiwa, bali vile vile taifa zima la kitheokrasi kuwa likitegemezwa na jitihada za uaminifu za mtu mmoja ambaye ni mnyenyekevu, imo katika maandishi yanayopasa ushindi juu ya majeshi ya adui za Israeli. Jemadari wa Israeli, Baraka, alipashwa habari kwamba Sisera, jemadari wa majeshi ya Kanaani, ‘angeuzwa’ au angetolewa, si mkononi mwa Baraka, bali mkononi mwa mwanamke. Na ndivyo ilivyotukia kwamba mwanamke Yaeli, mke mnyenyekevu wa mwanamume Mkeni, akapewa heshima hii kubwa. Yeye alikuwa na nia naye alijipa moyo, ijapokuwa aliogofishwa na hatari kuu katika kufanya hivyo. Alifanya kwa kadiri alivyoweza naye alithawabishwa kwa kutolewa kwa adui mbaya sana wa Mungu mkononi mwake. Vile vile, habari ya mambo aliyotimiza na jina lake imo katika Maandiko Matakatifu. Habari ya Maandiko inapatikana katika Waamuzi 4:8, 9, 21-23:
7. Katika masimulizi ya Biblia ya Waamuzi, sura ya 4, ni mambo gani hasa yanayokupendeza wewe?
7 “Baraka akamwambia [Debora nabii mke], Kama utakwenda pamoja nami, ndipo nitakwenda; bali kama huendi pamoja nami, mimi siendi. Basi akasema, Hakika nitakwenda pamoja nawe, lakini safari utakayoiendea haitakupatia heshima wewe; maana [Yehova] atamwuza Sisera katika mkono wa mwanamke. Debora akainuka, akaenda pamoja na Baraka mpaka Kedeshi. Ndipo Yaeli, mkewe Heberi, akatwaa kigingi cha hema, akashika nyundo mkononi mwake, akamwendea [Sisera] polepole, akamtia kile kigingi katika kipaji chake, nacho kikapenya, hata kuingia mchangani; kwa maana usingizi mzito ulikuwa umemshika; basi akazimia, akafa. Na tazama, Baraka alipokuwa akimfuatia Sisera; Yaeli akatoka ili kumlaki, akamwambia, Njoo, nami nitakuonyesha yule mtu unayemtafuta. Basi akamwendea, na tazama, Sisera amelala humo, amekufa, na hicho kigingi kilikuwa kipajini mwake. Basi hivyo Mungu akamshinda Yabini, mfalme wa Kanaani, mbele ya wana wa Israeli siku hiyo.” Ushindi wenye nguvu sana, kwa njia ya mnyenyekevu mwaminifu!
MSAADA NA UONGOZI WA KIMBINGUNI
8. (a) Ukristo ni zaidi ya imani ya vivi hivi namna gani? (b) 2 Timotheo 3:14 inapasaje shauri hili?
8 Bila kujali namna ya maisha ya watumishi walio wakf wa Yehova, wakati fulani zamani kila mmoja alianza kutembea katika njia ya Kikristo, ambayo si imani ya vivi hivi bali ni njia ya maisha, njia au barabara inayotia mwendo wa uaminifu. Mtume Paulo alimkumbusha Timotheo ‘akae katika mambo yale aliyofundishwa na kuhakikishwa.’ (2 Tim. 3:14) Basi, vile vile, tukiisha kuanza kuwa katika njia hii ya haki, tunaendelea katika uhakika kamili, tukikumbuka kwamba kwanza tuliichunguza kweli kwa uangalifu tulipoisikia. Mwisho, tulihakikishwa kabisa, na kuhakikishwa huku hakukuja kupitia kwa maono ya moyoni au kulazimishwa, bali kwa njia ya kweli isiyoweza kupingwa. Kwa hiyo, imetupasa tuendelee kuifuata njia ya kweli tuliyopangiwa katika Biblia. Katika kufanya hivyo tunahakikishwa kwamba Mungu Mwenye Nguvu Zote, Mwana wake Mfalme anayetawala na malaika zake wanatusaidia sisi!
9. Eleza namna Ufunuo, sura ya 7, unavyofunua tegemeo la kimbinguni la wale wanaomsifu Mungu duniani.
9 Unakumbuka kwamba “mkutano mkubwa” wa Ufunuo sura ya saba wanaendelea “wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.” (Mst. 10) Tegemezo la kimbinguni la huu “mkutano mkubwa” wa wasifaji wa Yehova linaonyeshwa katika maneno yafuatayo ya mistari 11 na 12: “Na malaika wote walikuwa wakisimama pande zote za kile kiti cha enzi, na za hao wazee, na za wale wenye uhai wanne, nao wakaanguka kifulifuli mbele ya kile kiti cha enzi, wakamsujudu Mungu, wakisema, Amina [Amina kwa yale ambayo “mkutano mkubwa” ulilia kwa sauti kuu;] Baraka na utukufu na hekima na shukrani na heshima na uwezo na nguvu zina Mungu wetu hata milele na milele. Amina.” Ndiyo, kweli, “mkutano mkubwa” unao msaada wa kimbinguni!
10. (a) Uongozi wa Yehova unatia nini? (b) Je! watu wanyenyekevu wahubiri na kufundisha kama wahudumu wa Mungu?
10 Kuna ushuhuda wa Maandiko vile vile kuonyesha kwamba watu wanyenyekevu wanao uongozi katika njia ya Kikristo ya uzima, kwa maana imeandikwa hivi: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.” (Zab. 119:105) Uongozi huo wa kimungu unatia ndani mwenendo, kufikiri, mazoea, maoni, na huduma ya watumishi wa Yehova walio wakf. Hata watu wanyenyekevu kati ya watumishi hao wanafaidika kwa kutimiza agizo hili: “Lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho . . . uwe na kiasi katika mambo yote, vumilia mabaya, fanya kazi ya mhubiri wa Injili, timiliza huduma yako.”—2 Tim. 4:2, 5.
11. (a) Ni nani, basi, anayepaswa kuzifuata kanuni za Mungu? (b) Eleza mwendo ambao ni bora kuufuata kwa habari ya nafasi za utumishi kwa Yehova.
11 Basi, je! si kweli kwamba “aina” zote za watu katika tengenezo la kitheokrasi inazipasa zifuate matakwa, madaraka na mapendeleo ya “Njia” ikiwa zitapata msaada na uongozi wa Yehova? Hii inatia ndani watu wengi waliomo katika “Njia” ambao ni aina ya watu walio wanyenyekevu na ambao mara nyingi wanajiona hawastahili yote yaliyomo katika “Njia.” (Matendo 19:9) Walakini, watu kama hao na wakumbuke, ikiwa daraka au mapendeleo makubwa zaidi yanatolewa, mwendo ulio bora ni kuitikia na kufanya hivyo kwa bidii sana. Mungu anajua uwezo wetu naye anaweza kutupa uwezo wa kutosha ili tutimize mgawo anaotupa sisi. “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu,” akaandika mtume Paulo. (Flp. 4:13) Hivyo tukiombwa tutumikie katika cheo cha pekee katika kundi, imetupasa tuitikie kwa tumaini, tukimwachia Bwana mambo, nasi tukijitahidi. Kama anavyosema mtunga zaburi: “Watu wako watajitoa wenyewe kwa moyo wa kupenda siku ya jeshi lako la vita.”—Zab. 110:3, NW.
ITIKIA KWA MOYO WA KUPENDA
12, 13. (a) Yehova anatumia ubaguzi gani? (b) Ni watu gani wanaopendwa sana na Yehova?
12 Mtu kuwa na “unyenyekevu” kunamaanisha kwamba yeye si mwenye kiburi, na hii ndiyo sifa inayotamanika. Walakini, mtu anayejiona mnyenyekevu kwa sababu ya namna ya maisha yake au hali zake za asili anahitaji amtumaini kabisa Yehova.
13 Kwa habari ya mwenye kiburi na mnyenyekevu, Yehova anatumia ubaguzi, Neno lake likisema hivi: “Ingawa [Yehova] yuko juu, amwona mnyenyekevu, naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali.” (Zab. 138:6) Ubaguzi huu unaonyeshwa tena katika Isaya 66:2, ambapo “asema [Yehova]” hivi: “Mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.” Vile vile, Wakristo wanashauriwa hivi: “Ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake.” “Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.” (1 Pet. 5:5, 6; Yak. 4:6) Kwamba “unyenyekevu” umepaswa uvaliwe kama vazi na kuvaliwa wakati wote ni wazi: “Jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu.” (Kol. 3:12) Kiongozi wetu, Kristo Yesu, yuko hivyo, kwa maana kwa habari yake mwenyewe anasema kwamba yeye ni “mpole na mnyenyekevu wa moyo.” (Mt. 11:29) Watu hao wanyenyekevu ndio anaowapenda sana Mungu.
14. Ni kusudi gani la Mungu kwa wale ‘waliotubu na kunyenyekea’?
14 Katika kuwapenda sana wanyenyekevu, kusudi la Yehova ni kuitia nguvu mioyo yao na roho zao. “Maana yeye aliye juu, aliyetukuka, akaaye milele; ambaye jina lake ni Mtakatifu; asema hivi; Nakaa mimi mahali palipoinuka, palipo patakatifu; tena pamoja na yeye aliye na roho iliyotubu na kunyenyekea, ili kuzifufua roho za wanyenyekevu, na kuifufua mioyo yao waliotubu.” (Isa. 57:15) Yehova angewafanya upya wale waliofanywa vibaya na kupondwa na mikazo ya namna ya maisha zao na hali zao za sasa.
15. Ni ubaguzi gani ambao inawapasa wanyenyekevu wautumie?
15 Hata kama vile Yehova anavyofanya ubaguzi kati ya wanyenyekevu na wenye kujikuza, vivyo inawapasa watu wanyenyekevu wafanye ubaguzi na inawapasa wapambanue kati ya unyenyekevu wa Kikristo wa lazima, unaofaa, na unyenyekevu wa uongo, kwa sababu huu wa pili sio unyenyekevu bali kwa kweli ni kiburi.
16. Ni uchunguzi gani utakaosaidia katika kufanya upambanuzi huu unaofaa?
16 Wanyenyekevu wanasaidiwa wafanye upambanuzi huu kwa kuchunguza tumaini lao katika Yehova. Tunafahamiana sana na mithali hii: “Mtumaini [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.”—Mit. 3:5, 6.
17. Maandiko yanapambanuaje kati ya unyenyekevu wa kweli na unyenyekevu wa uongo?
17 Katika kuwaandikia Wakristo katika Kolosai mtume Paulo anatusaidia tupambanue kati ya sifa ya unyenyekevu wa kweli na ambao huenda ukaonekana kuwa ni ukaidi tu. “Mtu asiwanyang’anye thawabu yenu, kwa kunyenyekea kwa mapenzi yake mwenyewe tu, na kuabudu malaika, akijitia katika maono yake na kujivuna bure, kwa akili zake za kimwili. Mambo hayo yanaonekana kwamba yana hekima, katika namna ya ibada mliyojitungia wenyewe, na katika kunyenyekea . . . lakini hayafai kitu.” (Kol. 2:18, 23) Inawapasa watu wanyenyekevu waepuke au waondoe ‘akili za kimwili.’ Ijapokuwa huenda hizo ‘zikaonekana kana kwamba ni za hekima,’ isingekuwa hekima ya kweli wala unyenyekevu wa kweli, kama Mithali 11:2 inavyoonya: “Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; bali hekima hukaa na wanyenyekevu.” Kwa kweli wanyenyekevu ndio wenye hekima, si wale ‘wanaojivunia akili.’ (Rum. 12:16) Kwa hakika hili linawapa wanyenyekevu mengi ya kufikiria, mashauri mengi ya kimungu wayafikirie sana, ili wasipate kuitikia huruma za Yehova na mipango yake yenye upendo tu bali vile vile wafanye hivyo kwa uhodari au ujasiri. “Wenye haki ni wajasiri kama simba.”—Mit. 28:1.
18. Ni mashauri gani mawili tuwezayo kukata kutokana na makala hii?
18 Kutokana na yote haya tunaweza kukata shauri kwamba ye yote anaweza, kwa kadiri kubwa, kusitawisha uwezo wa kufanya namna yo yote ya mgawo wa utumishi kwa msaada wa Yehova Mungu. Tunaweza vile vile kukata shauri kwamba Yehova awapenda sana wanyenyekevu na ya kwamba yeye atawatayarisha kwa mapendeleo makubwa zaidi ya utumishi ikiwa wanatafuta uongozi wake na kuliamini neno lake na kukubali mapendeleo ya utumishi wanayotolewa.
19. Kuna msaada na shauri gani kwa watu wanaojitumainia?
19 Tofauti na wale wanaojiona kutokuweza na unyenyekevu, huenda wengine, kwa sababu ya hali, mambo wanayotimiza au namna ya maisha, wakajitumaini sana. Watu hao, vile vile, wanapata shauri katika Neno la Mungu ambalo ni lenye msaada kwao. Watu wote wa Yehova ni “kondoo” wa kundi lake, na hilo ni kutia na wale walio na mapendeleo ya pekee na madaraka katika kundi la watu wa Mungu. Kutoka kati ya kondoo wa mfano, wanachukuliwa wachungaji ili waweze kuongoza na kulisaidia kundi, lakini inawapasa wajiangalie wenyewe wasije wakajiona wenyewe kuwa wakubwa mno na wakajivuna. Wakiwa wenye kujivuna, Yehova hawezi kuendelea kuwatumia, kwa sababu yeye hawapendelei wenye kiburi na wenye kujivuna. “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo miongoni mwake roho takatifu imeweka ninyi kuwa waangalizi, kuchunga kundi la Mungu, ambalo yeye alinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.”—Matendo 20:28, NW.
20. Ni mfano gani ambao Yesu aliwawekea wafuasi wake?
20 “Mwana wake mwenyewe,” hata Yesu Kristo, hakujitegemea mwenyewe, bali alisema hivi: “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile.” (Yohana 5:19) Mitume wangaliweza kujiona wadogo mno mbele ya Yesu, lakini unyenyekevu wa Yesu na upendo wake ulitokeza sifa bora ndani yao. Watu hao wote walio katika vyeo vyenye madaraka katika kundi la watu wa Mungu imewapasa wawe hivyo, yaani, kama Yesu alivyokuwa katika unyenyekevu na upendo wake, akionyesha huruma na rehema za Baba yake.
21. Ni shauri gani ambalo Maandiko yanawapa watu wenye kiburi, na kwa sababu gani?
21 Ikiwa baraka na mapendeleo ya mtu yamemfanya awe na kiburi amepoteza sifa inayohitajiwa ya unyenyekevu wa akili na moyo naye ataanguka isipokuwa anageuka, “kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi.” (1 Pet. 5:5) “Kiburi hutangulia uangamivu; na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko. Afadhali kuwa na roho ya unyenyekevu pamoja na maskini, kuliko kugawanya nyara pamoja na wenye kiburi.”—Mit. 16:18, 19.
22. Ni maoni gani yanayofaa kwa: (a) Wale walio na hali nzuri na uwezo? (b) Wale wanaotaka wakati na mazoezi ili wafanye maendeleo?
22 Maoni ya Mungu kwa wanyenyekevu ni wazi, na imewapasa wote wayasitawishe. Wengine walio na hali nzuri na uwezo wa asili wanajitahidi na kufanya maendeleo mazuri ya Kikristo. Maendeleo haya yapaswa yasifiwe. Mtu aliye na uwezo huo, daraka na mapendeleo amepaswa afahamu kwamba watu wengine hawana mambo haya. Wako wengine wanaofaidika na mazoezi na utendaji wa roho ya Yehova, na mwishowe wanafanya maendeleo na kupokea mapendeleo zaidi ya kitheokrasi. Hilo ni jambo zuri sana na vile vile laonyesha maendeleo yanayofaa ya Kikristo. Tena, wengi hao waliomo katika kundi la Kikristo ambao ni wapya au ambao hali zao hazijawaruhusu bado wafanye maendeleo vile vile yatupasa tuwatazame kwa maoni ya Mungu. Kungekuwa ni kuwaza kwa kibinadamu kwenye makosa kuwaona hawa wasiofanya maendeleo kama watu tu wasio na maana. Mungu anapendezwa na wao naye aweza kuwatumia watu hao katika njia nyingi zenye maana sana, naye anafanya hivyo.
23. (a) Nani wamepaswa wasaidiwe, na nani? (b) Katika kukubaliana na Yakobo, jambo gani ambalo sisi sote tumeona kuwa la kweli?
23 Basi, kwa kuwa na maoni haya yanayofaa, waacheni wote, wanyenyekevu na vile vile wengine, wasaidiane. Hii ingetia kuwasaidia wale ambao kwa kweli ni watoto, wachanga. Vile vile wale ambao ni watu wenye makamu, labda wenye udhaifu wa kimwili, na labda hata watu wenye makamu, labda wenye udhaifu wa kimwili, na labda hata watu wanaojiona kuwa wadogo mno wamepaswa wasaidiwe. Wote wanaweza kufaidika kwa kiroho kutokana na wanyenyekevu ambao, wanapoitikia mipango yenye upendo ya Yehova, wanategemeza na kulitia nguvu tengenezo la kundi la watu wa Yehova. Ushirika wa kundi na ushirika wa kipekee ni wa maana sana katika hili, ukiwafanya wote waone ukweli wa dai la Maandiko kwamba “Mungu ameungamanisha mwili, na kukipa heshima zaidi kile kiungo kilichopungukiwa.” (1 Kor. 12:24) Kwa hakika, watumishi wote wa Yehova wanakubaliana na maneno ya mwandikaji wa Biblia Yakobo, aliposema: “Mmeuona mwisho wa [Yehova aliompa Ayubu] ya kwamba [Yehova] ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.”—Yak. 5:11.
—Kutoka The Watchtower, Feb. 15, 1973.