Kutoka Kwa Uvulana Kuwa Mwanamume
Mambo ya hakika ambayo vijana wanataka kujua
KUTOKA kwa uvulana kuwa mwanamume ni mwendo wa taratibu. Hakuna kivulana cho chote kinachokwenda kulala usiku na asubuhi yake kujikuta kimekuwa mwanamume. Kugeuka kunachukua miaka mingi. Sio wakati ulio mwepesi zaidi sana katika maisha ya kijana, lakini ni kipindi cha maana sana sana. Kipindi hiki cha kugeuka ni msingi wa kuhakikisha madaraka yako ya wakati ujao.
Hiki kipindi cha kutoka kwa utoto kuwa mtu mzima kinaonyeshwa na mwanzo wa ubalehe (mwanzo wa kuweza kuzaa). Katika wavulana, sehemu hii ya maisha inaanza karibu na umri wa miaka kumi na minne hivi, na kipindi cha kutoka kubalehe mpaka kupevuka kinaendelea, kwa kawaida mpaka katikati ya miaka 20 na 23 hivi.
MAGUMU YA MWANZO WA UBALEHE
Ni nini mengine ya magumu unayoweza kutazamia katika sehemu hii ya kuanza kubalehe? Kwanza, pengine utapitia katika wakati ambao unaelekea kuwa mwenye mashaka, hata kuwa mjinga. Huenda ukaelekea kuangukia viti, kuangusha bilauri zilizo mezani juu. Hili linaweza kuwa jambo la kutia haya. Kwa sababu gani linatukia?
Ni kwa kuwa mwili wako unaendelea kurefuka (na labda kupanuka penye mabega na kifua). Mifupa yako inarefuka na inakuwa lazima misuli ipanuke pamoja nayo. Lakini katika mpanuko huu sehemu nyingine za mwili zinaelekea kukua kasi, hali nyingine huenda zikakawia. Hii inaweza kuleta kukosa usawa. Kwa hiyo, katika sehemu ya kwanza ya kugeuka huku kijana anaweza kuwa mjinga kidogo. Lakini hii inapita na si jambo la kushughulikia sana—ingawa uangalifu wa ziada bila shaka unafaa, kwa kuwa unaweza kukuepusha na dhara linaloweza kutokea kwa ajali. Sio wakati wa kujihatirisha. Wala kipindi cha mashaka sio wakati bora kwa mtu kujifunza kuendesha motokaa, kwa kuwa kukosa usawa wakati wa hatari kunaweza kuleta maafa.
Kati ya sehemu za mwili zinazopanuka ni mishipa ya sauti. Urefu ulioongezeka unaifanya sauti iwe nzito. Lakini wakati wa kurefuka huenda sauti yako mara nyingi ikaalika, kwa ghafula ikiwa sauti yenye kelele sana ambapo hukutazamia hivyo. Tena, hii ni sehemu ya kipindi tangu kuanza kubalehe mpaka kupevuka. Kwa hiyo, linapotukia na wengine wakachekeshwa, wewe tabasamu tu pamoja nao na kuona haya ko kote kutakwisha.
Chanzo cha mageuzi haya ya mwili ni vifuko vyako mnamofanyiziwa maji yenye dawa, kutia ndani na kikoromeo, vifuko vya kufanyiza namna ya majimaji vilivyo karibu na figo pamoja na mapumbu. Hivi vinaleta hata mageuzi zaidi. Mojawapo ni ukuzi wa nywele zilizo uvunguni wa tumbo—kando kando ya viungo vya uzazi, vile vile makwapani mwako na kifuani. Kiasi chake ni tofauti kutoka kwa mtu huyu hata kwa mwingine na sio kionyesho cha namna ulivyo mwanamume kwa vyo vyote. Nywele vile vile zinaanza kuonekana usoni, kwa kawaida kuanzia na mdomo wako wa juu. Ndiyo, ingawa ni ndevu kidogo, unakaribia sana kuanza kunyoa.
Mara kwa mara vifuko vya mafuta vinavyotumikia ngozi ya uso vinashindwa kufanya kazi namna vinavyopaswa kufanya wakati ulio katikati ya mwanzo wa kubalehe na kupevuka. Ndiyo sababu unaweza kutopendezwa kwa sababu ya magumu yanayokamatana na sura. Kuumbuka usoni huenda kukaelekea kuiharibu sura yako na huenda ukajisikia kuchukizwa. Lakini imekupasa kujua kwamba wengine hawakuangalii sana kama wewe unavyofanya na, wakiijua sehemu ya maisha unayopitia, pengine wataelekea kutoliona kama jambo kubwa. Njia bora ya kuyaangalia magumu haya ya sura ni (1) kuwa na ulaji wenye vitu vyote vya maana, kutia ndani na mboga nyingi na matunda, pamoja na maji ya kunywa, (2) tumia sabuni nyingi na maji—si kwa uso wako peke yake bali na kwa kuweka kichwa chako chote na mwili kuwa safi, na kisha (3) iondoe mikono yako, usifinye au kuushika uso wako sana. Walau hii itayazuia magumu. Kama sivyo, basi huenda ukapaswa kutafuta shauri la daktari.
KUKUA KWA VIUNGO VYA UZAZI
Pengine geuzi ambalo mara nyingi sana linakuwa chanzo cha kusumbua kwa wavulana wanaoelekea kuwa wanaume ni lile linalovipasa viungo vya uzazi. Wakati wa ubalehe si kwamba tu hivi vinaanza kufikia ukubwa wake wote lakini vile vile vinaanza kufanya kazi. Biblia, katika Mambo ya Walawi 15:16, 17, inataja ‘kutokwa na shahawa.’ Ikiwa wazazi wake kwa kutowaza wameshindwa kuzungumza jambo hili pamoja na yeye mapema, huenda kutoka kwa shahawa ya kijana kukawa maono ya kufadhaisha. Ni nini kinachofanya shahawa hiyo itoke?
Mwili wa kijana, unapofikia sehemu ya ubalehe, unaanza kutokeza chembechembe za shahawa na vile vile namna ya majimaji inayoitoa nje ya mwili. Mara kwa mara mwili unaitoa shahawa hiyo, jambo ambalo inatukia mtu anapokuwa amelala na anaota.
Je! hii yote ina maana gani? Maana yake ni kwamba mwili wako sasa unaweza kuzalisha watoto. Huu ni mpango wa Muumba na unapaswa utumiwe, ndiyo, katika njia yake iliyopangwa, kwa ndoa yenye heshima.
Jambo fulani linaweza kuangaliwa hapa, hata hivyo. Ingawa kutoka kwa shahawa ni jambo la kawaida, unaweza kuzuia kutoka huku kwa kadiri fulani. Unayofikiria, zaidi mawazo yako mbele ya kwenda kulala, yanaweza kuwa na matokeo sana juu ya hili. Kama ukiyaacha mawazo yako yakae katika mambo yanayowapasa wanaume na wanawake, inaelekea hii itajionyesha yenyewe katika ndoto zako na kufanya shahawa itoke mara kwa mara, labda mara nyingi kwa mwezi mmoja. Kwa kuonyesha kujiweza unaweza kuyaondoa mawazo yako kwenye tamaa za mwili na hivyo uendelee kwa kipindi kirefu bila usingizi wako kukatizwa na kutoka huko kwa shahawa na bila masumbuo mengi yanayofuata kwa kawaida. (Zab. 119:9; Flp. 4:8) Ingawa kwa bahati, takwa la sheria ya Musa kwamba mtu amepaswa aoge nyuma ya kutokwa na shahawa halitendi kazi kwa njia ya kidini kwa Wakristo, yangali ni mazoea mazuri yanayoipasa afya kuoga upesi inavyofaa.
JE! UTENDEJE KAMA MATOKEO?
Uhakika wa kwamba mwili wako unakua katika njia hii huenda ukakufanya uone ajabu na kujisikia mwenye kutaka kufanya upekuzi. Je! utatoshelezaje upekuzi huo? Ni kwa kufanya jaribio kwa tumia viungo vyako vya uzazi? Au ni kwa kuwauliza wavulana wengine wa rika lako mwenyewe au walio wazee kidogo? Wengi wanafuata mwendo huo, lakini mara nyingi sana kwa matokeo yasiyopendeza. Kwa sababu gani?
Basi, wanalofanya linamkumbusha mtu juu ya mtoto mdogo ambaye anapewa zawadi ya kitu chenye sehemu nyingi kilicho kigumu kufahamika, kama vile saa ya mkono. Akitamani kupekua, mvulana huyo anataka kujua kinachofanya saa ifanye mlio, kinachoifanya mikono yake iende. Kwa hiyo anafungua nyuma yake na kuanza kuichezeachezea. Matokeo ni nini? Saa iliyoharibika, kwa kuwa, ingawa anaweza kujua namna ya kuifungua au hata kuondoa sehemu zake moja moja, yeye hana ujuzi unaotakiwa ili kuiunganisha tena. Wala haielekei mtoto mwingine wa umri wake atajua.
Ingawa huenda usijidhuru kwa kimwili kwa kufanya jaribio, bila shaka unaweza kujifadhaisha akilini, moyoni na kwa njia ya kimwili. Lililo baya zaidi, unaweza kujitia katika mazoea mabaya yanayoweza kuchukua miaka mingi kuyavunja na yanayoweza kuharibu furaha yako ya wakati ujao. Na, hata ingawa msisimko wa kwanza kwa sababu ya kujisikia kupatwa na matokeo ya mageuzi haya ya mwili unaweza kukufanya utake kuzungumza na wavulana wengine na kulinganisha maono, ni vema kufahamu kwamba mazungumzo haya yanaweza kwa wepesi kuongoza kwenye kujitia katika matendo yasiyofaa, kwenye kupiga punyeto au kujichua, au hata kwenye mazoea ya mwanamume kumlala mwenzake na mwanamke kumlala mwenzake.—Rum. 1:27, 28.
Njia bora ya kupata majibu ya kuridhisha kwa maulizo yako juu ya ukuzi wa viungo vya uzazi ni kuwauliza wazazi wako, zaidi baba yako. Wewe, na wavulana wengine katika kundi la rika lako, ndio mnaanza kufikia hali ya kuwa mwanamume mzima kabisa. Lakini baba yako tayari amekwisha pitia katika kila jambo ulilopitia na mengine mengi. Vile vile, ingawa wavulana wengine wanaweza kukupa habari zinazoelekea kuwa za kweli, baba yako anaweza kufikiwa kwa matumaini ya kwamba atakupa habari zinazofaa, mambo ya hakika yatakayokusaidia na kukuletea furaha. Ikiwa haiwezekani baba yako akupe habari au mashauri yenye msingi wa Neno la Mungu, ingekuwa bora kwako kujua vile Neno la Mungu linavyosema. Utaona kwamba ye yote wa wazee katika kundi la mashahidi wa Yehova atafurahi kukusaidia.—Mit. 4:1; 13:20; Mt. 7:9, 10.
KUJIONYESHA MWENYEWE KUWA MWENYE KUTEGEMEWA
Muumba wako amekupa wewe zawadi ya ajabu kwa kukupa uwezo wa kuwa baba. Lakini sasa ni juu yako kuitunza zawadi hiyo kwa njia ya kutegemewa, si kama mtoto asiyeweza kuaminishwa na kitu chenye ubora. Na ndivyo na mambo mengine mengi. Unapoelekea kuwa mwanamume ni jambo la kawaida kwamba unajisikia ukitaka kujulikana kama mtu anayeweza kujitegemea na vile vile kama mtu mzima mwenye uhuru kadiri fulani wa kujifanyia mambo. Inaelekea wazazi wako wataanza kukutayarisha kwa wakati utakapokuwa mwenye uhuru wa kujifanyia maamuzi. Namna gani? Kwa kukupa madaraka zaidi kidogo kidogo na pendeleo la kushiriki katika kufanya maamuzi fulani kwa habari ya mambo utakayofanya. Huenda wakakukaribisha uonyeshe chaguo lako kwa habari ya masomo fulani utakayojifunza shuleni au huenda wakakuruhusu ufanye kibarua. Huenda ukaruhusiwa kujinunulia vitu vyako mwenyewe. Lakini lo lote waonalo wazazi wako linafaa kufanywa kwa habari hii, itakuwa sasa juu yako kuonyesha unastahili daraka hilo. Ukitenda kwa utoto au kuwa mwenye “kichwa kikubwa,” basi huenda ikawa lazima wayapunguze mapendeleo yako tena mpaka utakapoonyesha u mtu mzima.
Tamaa hii ya kutaka kutegemewa zaidi na kuwa na kadiri fulani ya uhuru wa kujifanyia mambo inafuatana na tamaa nyingine za asili. Utajisikia ukitaka kufurahiwa na wengine kwa sababu ya namna ya mtu ulivyo na unayoweza kufanya. Ikiwa tamaa hizi haziongozwi vyema, zinaongoza kwenye kuunda “magenge,” ambamo wavulana wengi wanaridhisha tamaa yao ya kujiona wa katika genge fulani. Lakini magenge hayo yanafanyiza taratibu yao ya mwenendo, na mambo ya hakika yanaonyesha kwamba sikuzote hii inaelekea kuongoza kwenye kufanya mabaya, pengine hata kwenye uhalifu mbaya sana. Labda zaidi ya jambo moja jingine lo lote, ushirika mbaya ndio unakuwa chanzo cha ugumu vijana wanapoingia taabuni.—1 Kor. 15:33.
Mnamo kipindi hiki cha maisha unaanza kupata maoni kidogo juu ya utakavyoonekana kwa njia ya kimwili kama mtu mzima. Lakini imekupasa vile vile uanze kufikiri zaidi na zaidi juu ya namna utakavyokuwa kwa ndani, kinachoitwa na Biblia “utu wa moyoni usioonekana.” (1 Pet. 3:4) Sehemu hii ya maisha yako sio wakati wa kuiruhusu tamaa ya uhuru ulioongezwa ikuondoe kwa njia fulani kutoka kwa wazazi wako na wengine wa jamaa. Mageuzi unayoona wakati wa ubalehe, na vichocheo vipya unavyovisikia na ambavyo unavyopaswa kujifunza kuzuia, kwa kweli yanaongeza uhitaji wako wa upendo wao na maongozi yasiyogeuka. Pahali pa kuondoka kwa wazazi wako na kuacha pengo likue, wakaribie zaidi na ujifunze yote uwezayo kutoka kwao unapoelekea sasa kuwa mtu nzima. Hakuna wakati utakaposikitikia hili na utawaletea furaha ya kweli vile vile, ukiwafanya wakujivunie wewe kama mwana wao. (Mit. 23:24, 25) Halafu, tena, tamaa ya kujiona katika genge fulani inaweza kutoshelezwa si kwa kushiriki utendaji wa jamaa, tafrija na safari tu bali na kwa kushiriki pamoja na Wakristo wa kweli vile vile, kujikusanya pamoja nao na kutoa uwezo wako unaokua na nguvu ili kufanya kazi zinazotakiwa ndani ya kundi. Hivyo utakua si kwa kimwili tu, bali vile vile na kwa kiroho, na kutegemeka kwako kutaongezeka.