Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 6/1 kur. 243-250
  • Hekalu la Kweli Moja Mahali pa Kuabudu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Hekalu la Kweli Moja Mahali pa Kuabudu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “HEMA”
  • HEKALU LA KWELI LATOKEA
  • MADHABAHU ILIYOFANANISHWA
  • Kukusanywa kwa Mataifa Yote Kwenye Hekalu Moja kwa Ibada
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • “Nyumba ya Sala kwa Mataifa Yote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Ni Katika Hekalu Gani Anamoweza Kupatikana Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Thamini Pendeleo Lako la Kuabudu Katika Hekalu la Kiroho la Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 6/1 kur. 243-250

Hekalu la Kweli Moja Mahali pa Kuabudu

“Na mahali patakatifu pa hekalu la Mungu Uliloko mbinguni palifunguliwa, na sanduku la agano lake lilionwa katika mahali pake patakatifu pa hekalu.”​—Ufu. 11:19, NW.

1. Habari za mambo ya ulimwengu zinatolewa namna gani?

HABARI za leo zinakuja kwa wingi sana kutoka sehemu zote za dunia hata sisi tulio watu wa vivi hivi hatuwezi kuzisikia zote. Ziko kwa namna nyingi hata tunatatizwa nazo. Habari za mambo ya kidunia ya ulimwengu zinatolewa sana kupitia kwa njia za mawasiliano, kama magazeti, simu, radio na televisheni.

2. Ni habari gani ya maana sana ambayo kwa kawaida haiangaliwi na njia hizi za kisasa za mawasiliano?

2 Walakini, kuna habari ambayo ni ya maana zaidi kupita zote ambayo sikuzote haiangaliwi na njia hizi za mawasiliano. Habari hii inastahili sisi tuiangalie kwa uzito zaidi. Imetukia katika mfululizo wa matukio ambao umetukia mbele ya wanadamu katika muda huu wa vita vya kati ya mataifa yote na mageuzi katika serikali za kisiasa tangu mwaka wa maana sana wa 1914 katika huu Wakati wetu wa Kawaida. Habari hii ya maana sana ilikusudiwa mapema itolewe katika kipindi chetu cha karne ya ishirini cha historia ya kibinadamu. Katika historia iliyoongozwa na roho ya Mungu iliyotangulia kuandikwa, yaani, katika unabii wa kimungu, ilitabiriwa na kusimuliwa kwetu karibu karne kumi na tisa zilizopita. Tunaposoma sasa maandishi haya ya unabii, tunaweza kuona kukamatana kwa habari hii na jambo ambalo limekuwa likitukia katika mambo ya ulimwengu.

3. Tunaivumbua habari hii kutoka wapi, na inasema nini?

3 Habari hii tunaivumbua kutoka katika kitabu cha mwisho cha Biblia Takatifu, kiitwacho Ufunuo, sura ya kumi na moja, na mistari ya kumi na tano mpaka kumi na tisa, NW. Kinasomwa hivi: “Na malaika wa saba akapiga tarumbeta yake. Na sauti kuu zikatukia mbinguni, zikisema: ‘Ufalme wa ulimwengu ukawa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atatawala kama mfalme milele na milele.’ Na wazee ishirini na wanne walioketi mbele za Mungu katika viti vyao vya enzi walianguka kifudifudi na wakamwabudu Mungu, wakisema: ‘Asante, Yehova Mungu, Mwenye Nguvu Zote, wewe uliyeko na uliyekuwako, kwa sababu wewe umechukua uwezo wako mkuu na kuanza kutawala kama mfalme. Lakini mataifa wakawa wenye hasira kuu, na hasira kuu yako mwenyewe ilikuja, na wakati uliowekwa kwa wafu wahukumiwe, na kuwapa zawadi watumwa wako manabii na watakatifu na wale wanaoliogopa jina lako, wadogo na wakubwa, na kuwaharibu wale wanaoharibu dunia.’ Na mahali patakatifu pa hekalu la Mungu lililoko mbinguni palifunguliwa, na sanduku la agano lake lilionwa katika mahali pake patakatifu pa hekalu. Na kukatukia umeme na sauti na ngurumo na tetemeko la dunia na mvua ya mawe.”

4. (a) Katika kueleza juu ya habari hiyo, jambo gani lapaswa lisemwe juu ya utawala wa Ufalme wa ulimwengu? (b) Kuwapo kwa “sanduku la agano lake” katika mahali patakatifu pa hekalu kunafananisha nini?

4 Basi, ni maelezo gani yanayostahili kutolewa juu ya habari hiyo ya unabii leo? Haya: Bila kujali vita tangu mwaka wa 1914 kati ya mwungano wa mataifa ya kidemokrasi na mwungano wa mataifa yenye serikali ya mtawala mwenye amri peke yake, kwa utawala wa ulimwengu wa wanadamu, ni Yehova Mungu, Mwenye Nguvu Zote, aliye hai sikuzote, ndiye amechukua uwezo wake mkuu na kuanza kutawala kama mfalme tangu mwaka huo wa 1914. Katika mwaka huo “ufalme wa ulimwengu ukawa ufalme wa Bwana [Mungu] wetu na wa Kristo wake,” yaani, wa Yesu Kristo Mwana wa Mungu. Yehova Mungu, Mwenye Nguvu Zote, ambaye sasa ndiye Mwenye “ufalme wa ulimwengu,” amekuja mahali pake patakatifu pa hekalu. Kuwapo kwake mahali hapo patakatifu kulifananishwa na kasha takatifu, liitwalo “sanduku la agano lake.” Ukubwa na mwundo wa “sanduku” hili mtazamaji, mtume wa Kikristo Yohana hatuelezi sisi; lakini lilifananisha kuwapo kwa Bwana Mungu, ambaye haiwezekani kwetu kumwona na kusimulia kabisa katika usemi wa kibinadamu. “Sanduku” hili la mfano ni sanduku la “agano jipya” la Mungu pamoja na wanadamu, ambalo limekuwa likitumika tangu mwaka wa 33 C.E.

5. Kulingana na historia, hekalu ni nini, na ni penye hekalu gani ambapo mataifa yote yanapaswa kuabudu ili wapate uzima usio na mwisho?

5 Maandishi ya historia yanaonyesha kwamba hekalu ni jengo au mahali palipowekwa wakf kwa utumishi na ibada ya mungu au miungu. Kwa habari ya lile “sanduku la agano lake” la mfano, mahali patakatifu pa hekalu ni pa Yehova Mungu, Mwenye Nguvu Zote. Ni kwenye hekalu hili la kimungu kwamba mataifa yote bado wanapaswa waje kwa ibada ya umoja, hata ingawa lazima kuwarudisha watu wa mataifa kutoka kwa wafu kwa njia ya ufufuo ulioahidiwa wa wenye haki na wasio haki. (Ufu. 11:18; Matendo 24:15) Hii ndiyo njia moja peke yake ambayo kwa hiyo watu wa mataifa yote wanaweza kupata uzima wa milele katika dunia yetu, itakayogeuzwa kwa kufaa kuwa paradiso ya dunia yote. Inawapasa wote wakubali na kumwabudu na kumtumikia Mwenyewe wa kimungu wa “ufalme wa ulimwengu,” atakayetawala kama Mfalme katika mahali pake pa hekalu milele na milele.​—Ufu. 11:15.

6, 7. Kunatokea maulizo gani kwa habari ya kuabudu penye hekalu hili kwa wakaaji wa Paradiso, na Sulemani alisema nini juu ya kukaa kwa Mungu katika jengo la hekalu?

6 Je! ina maana kwamba watu wa mataifa hawatakwenda mbinguni, kwa sababu ibada hii inaendeshwa katika dunia ya paradiso? Wasipokwenda, je! wanawezaje kwenda kwenye hekalu la Mungu, kwa kuwa Ufunuo 11:19, NW unasema “mahali patakatifu pa hekalu la Mungu lililoko mbinguni”? Hilo ni ulizo linalofaa hapa, lakini je! ni kwa sababu tunafikiria mahali patakatifu pa hekalu la Mungu kama pakiwa jengo au jumba katika mbingu zisizoonekana lililo na kuta na milango? Basi, na tukumbuke yale ambayo mjenzi mkubwa wa hekalu wa karne ya kumi na moja mbele ya Wakati wetu wa Kawaida alisema wakati wa kufungua hekalu. Huyu alikuwa Mfalme Sulemani mwenye hekima, aliyejenga hekalu la kwanza la namna yake juu ya Mlima Moria wa Yerusalemu. Akimtaja Mungu, Sulemani alisema hivi:

7 “Lakini Mungu je! atakaa kweli kweli juu ya nchi? Tazama, mbingu hazikutoshi, wala mbingu za mbingu; sembuse nyumba hii niliyoijenga!”​—1 Fal. 8:27.

8. “Sanduku la agano” lilikuwa wapi, lilifananisha nini, na hivyo Patakatifu Zaidi pa hekalu palifananisha nini?

8 Katika mahali patakatifu pa hekalu palipojengwa na Mfalme Sulemani, chumba cha ndani kiliitwa Patakatifu Zaidi na palikuwa mahali penye miraba sita iliyo sawasawa kwa ukamilifu, urefu, upana na urefu wa juu ni mikono ishirini. Kwa hakika kilikuwa chenye nafasi kubwa kutosha kukaa “sanduku la agano la Yehova” la kidunia linaloonekana, sanduku hili ndani yake mkiwa mbao mbili za mawe ambazo kidole cha Mungu kilikuwa kimeandika Amri Kumi. (1 Fal. 6:19, 20; 8:6-9; Kut. 34:1, 27, 28; 40:20) Lakini chumba hicho cha ndani au Patakatifu Zaidi pa hekalu hapakuwa na nafasi kubwa kumtosha Yehova Mungu mwenyewe, Muumba wa mbingu na dunia kuwamo. Sanduku la agano lilikuwa kitu kitakatifu ambacho kuelekea hicho kuhani mkuu wa Mungu alinyunyizia damu ya dhabihu zenye kufunika dhambi Siku ya Upatanisho ya kila mwaka. Katika njia hii lile sanduku lilifananisha kiti cha enzi cha Yehova Mungu katika mbingu. Kupatana na uhakika huu, Patakatifu Zaidi pa hekalu, ambapo sanduku lilipokuwa, palifananisha ile sehemu ya mbingu zisizo na mpaka ambapo Mungu ana maskani yake takatifu. Mahali hapo pana nafasi kubwa kumtosha Yeye.

“HEMA”

9. Hekalu la Sulemani lilifanywa kwa kiolezo cha jengo gani, na walioingia katika vyumba vya jengo hilo walikuwa akina nani?

9 Mahali patakatifu pa hekalu ambalo Mfalme Sulemani alikuwa mjenzi palifanywa kwa kiolezo cha hema takatifu ambayo nabii Musa alijenga katika jangwa la Mlima Sinai katika Arabuni. Hema hiyo ilikuwa na vyumba viwili, hivi vilitengwa kimoja kwa kingine kwa pazia la ndani. Chumba cha kwanza, ambacho makuhani waliingia kwa kupita pazia la nje lililoelekea ua, kiliitwa Patakatifu. Chumba cha ndani ndani, ambacho kuhani mkuu aliingia kwa kupita pazia la ndani, kiliitwa Patakatifu Zaidi. Wakati kuhani mkuu alipoingia Patakatifu Zaidi alichukua chetezo au chombo cha kufukizia uvumba ili kupajaza Patakatifu Zaidi uvumba. Hii ilifanywa ili kuandalia hali kwa kuhani mkuu kunyunyizia damu ya dhabihu za Siku ya Upatanisho kuelekea sanduku la agano la dhahabu. Mtume wa Kikristo Paulo anasimulia hili, katika Waebrania 9:2-10, NW, akisema:

10. Kulingana na Waebrania 9:2-10, yalikuwa mambo gani yaliyokuwamo katika vyumba hivyo, na ni nani walioingia katika vyumba hivyo, na wakati gani?

10 “Kulijengwa chumba cha kwanza cha hema ambacho ndani yake kilikuwamo kinara cha taa na pia meza na wonyesho wa mikate; na kiliitwa ‘Mahali Patakatifu.’ Lakini nyuma ya pazia la pili kilikuwako chumba cha hema kinachoitwa ‘Patakatifu Zaidi.’ Hiki kilikuwa na chetezo cha dhahabu na sanduku la agano lililofunikwa pande zote kwa dhahabu, ambalo ndani yake ulikuwamo mtungi wa dhahabu wenye mana na fimbo ya [Kuhani Mkuu] Haruni iliyochipuka na mbao za agano; lakini juu yake walikuwapo makerubi wenye utukufu wakifunika kwa kivuli funiko la kupatanisha. Lakini sasa sio wakati wa kusema mengi juu ya mambo haya. Mambo haya yakiisha kujengwa katika njia hii, makuhani huingia katika chumba cha kwanza cha hema nyakati zote ili kufanya utumishi mtakatifu; lakini katika chumba cha pili kuhani mkuu peke yake ndiye anayeingia mara moja kwa mwaka, si bila damu, ambayo yeye huitoa kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya dhambi za ujinga wa watu. Hivyo roho takatifu inaonyesha wazi kwamba njia ya kuingia katika mahali patakatifu ilikuwa bado haijafunuliwa wakati hema ya kwanza ilipokuwa ikisimama. Hema yenyewe hii ni mfano kwa wakati uliowekwa ambao ndio sasa, . . . wakati uliowekwa ili kunyosha mambo.”

11. Je! “hema” hiyo lilikuwa mfano wa jambo fulani la zamani au jambo fulani la wakati ujao?

11 Na tufahamu kwamba mwandikaji anasema kwamba ile hema takatifu iliyojengwa na Musa ilikuwa “mfano kwa wakati uliowekwa ambao ndio sasa,” na kwa habari ya mwandikaji, ilikuwa kama mwaka wa 61 C.E., au miaka tisa mbele ya kuharibiwa kwa hekalu katika Yerusalemu na majeshi ya Kirumi katika mwaka wa 70 C.E. Tena ilikuwa miaka ishirini na minane baada ya kufa na kufufuka kwa Yesu Kristo na kupaa kwake mbinguni. Basi ile hema iliyojengwa na Musa ilikuwa “mfano” wa jambo fulani la wakati ujao na si jambo fulani mbele ya siku za nabii Musa. Katika siku za Kuhani Mkuu Eli “hema” hiyo ya mfano ilikuja kuitwa “hekalu.” (1 Sam. 1:9; 3:3; tazama tena 2 Samweli 22:7; Zaburi 18:6; 27:4) Hivyo hema au hekalu lililojengwa na Musa halikuwa mfano wa hekalu lililokuwa limekuwako mbele ya wakati wa Musa.

12. Je! mashahidi waaminifu wa Yehova waliomtangulia Musa walikuwa wamejenga mahekalu duniani, na je! Yehova mwenyewe alikuwa na hekalu mbinguni wakati huo?

12 Tukitazama nyuma kwa wakati ambao Musa alikuwa bado kuzaliwa, hatupati maandishi yanayoonyesha kujengwa kwa hekalu duniani na mwabudu ye yote mwaminifu wa Yehova Mungu, wala hata na mwabudu Melkizedeki, aliyekuwa “mfalme wa Salemu, kuhani wa Mungu aliye juu.” (Ebr. 7:1; Mwa. 14:18-20) Ijapokuwa mashahidi waaminifu wa Yehova Mungu kama Habili, Nuhu, Ibrahimu, Isaka, Yakobo na Ayubu walitoa dhabihu kwa Mungu, hawakumjengea Yeye hekalu. Vema, basi, je! Yehova Mungu alikuwa na hekalu mbinguni, ijapokuwa hakuwa na hekalu lionekanalo duniani? Sivyo’ Yaani, si hekalu kama lile lililofananishwa na hema iliyojengwa na Musa na hekalu lililojengwa na Mfalme Sulemani.

13. Sababu gani kulikuwa hakuna haja ya hekalu mwishoni mwa siku ya sita ya utendaji wa uumbaji wa Mungu, na mitajo ya hekalu la Yehova katika maandishi ya unabii ifahamike namna gani?

13 Bila shaka, wakati Yehova Mungu alipowaumba Adamu na Hawa katika ukamilifu wa kibinadamu katika bustani ya Edeni, kulikuwa hakuna lazima ya kuwa na hekalu hilo mbinguni. Sababu gani? Kwa sababu wakati huo mwanamume na mwanamke wakamilifu walipokwisha kuumbwa mwishoni mwa siku ya sita ya kuumba, wakati ambao “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana,” kulikuwa hakuna dhambi katika kuumba kote, ama mbinguni ama duniani. Haikuwa lazima kwa Mungu kuwa na kuhani mkuu wa kutoa dhabihu za kuondoa dhambi, wala haikuwa lazima kuwa na madhabahu katika ua wa hekalu pa kutolea toleo la dhambi. (Mwa. 1:26-31; 2:7-24) Mitajo ya hekalu kama inavyopatikana, kwa mfano, katika Zaburi 11:4, Mika 1:2 na Habakuki 2:20, ilikuwa ya unabii na iliandikwa wakati Musa alipokuwa amekwisha kujenga hekalu la hema au Sulemani alipokuwa amekwisha kujenga hekalu Yerusalemu. Hii ilifananisha hekalu la kiroho lililokuwa bado likitazamiwa kuwako.

14. Kwa sababu gani tunauliza kama hekalu la kweli la Yehova lilitokea siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E.?

14 Sasa, basi, hekalu la kweli lililofananishwa na hema iliyojengwa na Musa na hekalu lililojengwa na Sulemani lilitokea wakati gani? Je! ilikuwa wakati wa siku-kuu ya Pentekoste katika mwaka wa 33 C.E., wakati kundi au kanisa la Kikristo lilipoanzishwa? Sababu ya kuuliza ni kwa vile mtume Paulo aliandikia kundi la Kikristo la wakati wake akasema hivi: “Je! ninyi hamjui kwamba ninyi watu ni hekalu la Mungu, na kwamba roho ya Mungu inakaa ndani yenu? Ikiwa ye yote anaharibu hekalu la Mungu, Mungu atamharibu yeye; kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, hekalu ndiyo ninyi watu.” (1 Kor. 3:16, 17, NW) Kutokana na maneno hayo ingefikiriwa kwamba hema iliyojengwa na Musa na mahekalu yaliyojengwa Yerusalemu na Mfalme Sulemani na Gavana Zerubabeli na Mfalme Herode Mkuu yalifananisha kundi la Kikristo kama hekalu la mfano. Lakini je! hii ni kweli? Ni jibu gani ambalo Paulo mwenyewe anatupa juu ya ulizo hili?

15. Waebrania 9:11, 12 inasema nini juu ya Yesu Kristo kama kuhani mkuu?

15 Basi tunarudia Waebrania, sura ya tisa, mahali tulipoachia, na kuendelea kusoma maneno haya yenye maelezo ya Paulo: “Walakini, wakati Kristo alipokuja kama kuhani mkuu wa mambo mema ambayo yametukia, kupitia kwa hema kubwa zaidi na lililo kamilifu zaidi lisilofanywa kwa mikono, yaani, si la kuumba huku, aliingia, la, si na damu ya mbuzi na ng’ombe dume wachanga, bali na damu yake mwenyewe, mara moja tu katika mahali patakatifu na akapata wokovu wa milele kwa ajili yetu.”​—Ebr. 9:11,12, NW.

16. Katika Siku ya Upatanisho ya Kiyahudi, je! Yesu aliingia katika Patakatifu Zaidi pa hekalu la Yerusalemu akiwa na damu yake mwenyewe au ilikuwa katika kundi la Kikristo kama hekalu ndimo alimoingia?

16 Yesu Kristo hakufa kama dhabihu katika Siku ya Upatanisho ya Kiyahudi (Tishri 10) na kuingia akiwa na damu yake mwenyewe katika Patakatifu Zaidi pa hekalu la Herode katika Yerusalemu. Hakuweza kufanya hivyo hata kidogo. Yeye hakuwa kuhani mkuu wa Kilawi. Kuhani mkuu wa Kilawi wakati huo alikuwa Kayafa, naye aliingia akiwa na damu ya ng’ombe dume mchanga na mbuzi katika Patakatifu Zaidi pa hekalu la Yerusalemu Siku ya Upatanisho. Lakini Yesu Kristo hakufanya hivyo. Vema, basi, ni katika “mahali patakatifu” gani ambapo yeye aliingia akiwa na damu yake mwenyewe? Si katika kundi la Kikristo duniani, maana hilo halikuwa limeanzishwa bado siku ya kufufuka kwa Yesu wala siku ya kupaa kwake mbinguni siku kumi mbele ya sikukuu ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E. Basi palikuwa “mahali patakatifu” gani ambapo Yesu Kristo aliingia mbele ya siku hiyo ya Pentekoste? Na tufungue tena Waebrania, sura ya tisa, na kumwacha Paulo atoe jibu:

17. Kulingana na Waebrania 9:23, 24, Yesu Kristo kama Kuhani Mkuu aliingia wapi?

17 Yeye anasema hivi: “Kwa hiyo ilikuwa lazima kwamba mifano ya mambo yaliyo katika mbingu itakaswe kwa njia hizi, lakini mambo ya kimbinguni yenyewe yenye dhabihu zilizo bora kuliko dhabihu hizo. Kwa maana Kristo aliingia, si mahali patakatifu palipofanywa kwa mikono, ambapo ni mfano wa uhakika, bali katika mbingu yenyewe, sasa aonekane mbele za Mungu kwa ajili yetu.”​—Ebr. 9:23, 24, NW.

HEKALU LA KWELI LATOKEA

18, 19. (a) Mungu anakaaje katika Patakatifu Zaidi hapo pa kweli ambapo Yesu Kristo aliingia? (b) Ilimpasa Yesu Kristo apite kizuizi gani ili aingie, na hii ilifananishwaje kulingana na Waebrania 6:18-20?

18 Asante, Paulo, maana tunafurahia kujua kwamba mahali patakatifu ambapo Yesu Kristo aliyefufuka alipoingia akiwa na bei ya damu yake mwenyewe ya dhabihu hapakuwa mahali patakatifu duniani ambapo wakati huo wanafunzi wake wachache walipokuwa, bali palikuwa “mbingu yenyewe,” “mbele za Mungu,” ambako Mungu mwenyewe anakokaa kuliko kukaa huko kwa njia ya roho. Walakini, “mahali patakatifu” hapo pa kweli, yaani, “mbingu yenyewe,” hapakuwa ndilo jambo peke yake kwa hekalu la kweli. Sababu gani? Kwa sababu Patakatifu Zaidi pa hema ya kidunia na mahekalu yaliyofanywa kwa mikono na ambapo Mungu alikaa kwa njia ya roho yake hayakuwa ndiyo mambo peke yake kwa majengo hayo matakatifu. Patakatifu Zaidi palikuwa chumba tu cha ndani ndani cha majengo hayo, na kilitengwa kwa chumba cha kwanza kwa pazia. (Mt. 27:50, 51) Pazia hili la ndani lilifananisha kizuizi cha kimwili ambacho ilimpasa Yesu akipite ili aingie katika Patakatifu Zaidi pa kimbinguni, yaani, mwili wake mwenyewe, ubinadamu wake. Akizungumza juu ya tumaini lake, Paulo anasema hivi:

19 “Sisi ambao tumekimbilia kwenye kimbilio tupate kuwa na kutia moyo kwa nguvu ili kushikilia tumaini lililowekwa mbele yetu. Tumaini hili tunalo kama nanga kwa nafsi, lililo hakika na imara, nalo linaingia ndani ya pazia, ambamo mtangulizi ameingia kwa ajili yetu, Yesu, ambaye amekuwa kuhani mkuu kulingana na jinsi ya Melkizedeki milele.”​—Ebr. 6:18-20, NW.

20. Patakatifu pa hema palitengwa namna gani na ua, na ni kitu gani cha shaba kilichokuwa katika ua huo?

20 Tunakumbuka kwamba chumba cha kwanza cha hema kiliitwa Patakatifu na kwamba kilitengwa kwa pazia na ua wa nje ya mahali patakatifu pa hekalu. Katika ua huo na mbele (au mashariki) ya mahali patakatifu pa hekalu ilikuwako madhabahu kubwa ya shaba.

21. Ni kutoka kwenye madhabahu gani makuhani wa Kiyahudi hawana haki ya kula, na madhabahu hii inashughulika na dhabihu ya nani?

21 Kama mahali patakatifu pa hekalu penyewe, madhabahu hii ilikuwa ya mfano. Mtume Paulo anaonyesha hili, wakati anaposema juu ya tofauti kati ya makuhani wa Kiyahudi na wanafunzi waliobatizwa wa Kristo na kusema: “Sisi tunayo madhabahu ambayo kutoka kwa hiyo wale wanaofanya utumishi mtakatifu penye hema hawana ruhusa ya kula. Kwa maana miili ya hao wanyama ambao damu yao inapelekwa katika mahali patakatifu na kuhani mkuu kwa dhambi inateketezwa kabisa nje ya kambi. Kwa hiyo Yesu naye, ili apate kuwatakasa watu kwa damu yake mwenyewe, aliteswa nje ya lango [yaani, nje ya lango la Yerusalemu].” (Ebr. 13:10-12, NW) Kwa hiyo madhabahu ya Kikristo inashughulika na dhabihu ya kibinadamu ya Yesu. Lakini madhabahu hii ni nini? Tena, ni kitu gani kilichofananishwa na chumba cha kwanza au Patakatifu pa hema au hekalu la kidunia? Na tuchunguze hili kwa msaada wa Biblia.

22. (a) Jambo gani lilifananishwa na pazia la ndani la hekalu, na Yesu alilipita namna gani? (b) Hivyo, kila kitu nje au mashariki ya pazia hilo kilifananisha mambo ya namna gani?

22 Pazia lile la ndani kati ya Patakatifu Zaidi na Patakatifu pa hekalu linafananisha mgawanyo. Linafananisha kizuizi cha kimwili ambacho ilimpasa Yesu Kristo akipite kwa kutoa mwili wake mkamilifu wa kibinadamu katika dhabihu, kuuacha huu milele. Sasa, kwa kuwa chumba cha Patakatifu Zaidi katika pazia la ndani kinafananisha “mbingu yenyewe,” anakokaa Mungu, si kwa njia ya roho bali katika kuwapo mwenyewe, kila kitu kilicho nje ya pazia hilo (au upande wake wa mashariki) kingefananisha jambo fulani si katika mbingu zisizoonekana bali chini hapa duniani. Lingeshughulika na mwili wa wale wanaomwabudu na kumtumikia Yehova Mungu hapa duniani. Kwa hiyo kanuni hii ilitumika kwa madhabahu ya shaba. Kwa habari ya mahekalu ya Sulemani na ya Herode, madhabahu ilikuwa katika ua wa ndani au wa makuhani, ambamo kuhani mkuu na makuhani wake wadogo walimofanyia kazi zao za dhabihu. Madhabahu hii ilikuwa mfano wa nini?

MADHABAHU ILIYOFANANISHWA

23, 24. (a) Yesu alipokuja “katika ulimwengu,” alisema nini juu ya maoni ya Mungu juu ya dhabihu, na kwa sababu gani? (b) Basi ni nini kilichoondolewa, na Wakristo wanatakaswa na nini kupitia kwa dhabihu ya Kristo?

23 Hii imeonyeshwa wazi kwa ajili yetu na mtume Paulo katika Waebrania, sura ya kumi. Akiisha kusimulia namna Yesu Kristo kama Kuhani Mkuu wa Mungu alivyoingia katika mbingu yenyewe ili aonekane akiwa na bei ya damu yake mwenyewe mbele za Mungu kwa ajili yetu, Paulo anaendelea kusema:

24 “Kwa kuwa Sheria ina kivuli cha mambo mazuri yatakayokuja, lakini si maana yenyewe ya mambo, wanadamu hawawezi kamwe kwa dhabihu zile zile kila mwaka ambazo wanatoa sikuzote wawafanye wale wanaokaribia kukamilika. . . . kwa maana haiwezekani kwa damu ya ng’ombe dume na ya mbuzi kuondoa dhambi. Kwa hiyo wakati anapokuja katika ulimwengu anasema: ‘“Dhabihu na toleo wewe hukutaka, bali wewe ulinitayarishia mwili. Wewe hukukubali matoleo ya kuteketezwa na toleo la dhambi.” Ndipo niliposema, “Tazama! naja (katika kitabu cha kukunja imeandikwa juu yangu) kufanya mapenzi yako, Ee Mungu.”’ Baada ya kusema kwanza: ‘Wewe hukutaka wala wewe hukukubali dhabihu na matoleo na matoleo ya kuteketezwa na toleo la dhambi’​—dhabihu zinazotolewa kulingana na Sheria​—ndipo kwa hakika anaposema: ‘Tazama! naja nifanye mapenzi yako.’ Anaondoa cha kwanza ili aimarishe cha pili. Kwa hayo ‘mapenzi’ sisi tumetakaswa kupitia kwa kutolewa kwa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu.”​—Ebr. 10:1-10, NW.

25. Basi, ilikuwa madhabahu gani ambayo juu yake Yesu alikuja na akajitoa mwenyewe ili atolewe kama dhabihu?

25 Kutokana na hili ni wazi kwamba mfano unaolingana wa madhabahu ya dhahabu katika ua wa hekalu ni “mapenzi” ya Mungu, kutaka kwake kuikubali dhabihu kamilifu ya kibinadamu ambayo kwa hiyo alikuwa ametayarisha, “mapenzi” haya ya Mungu yakiwa yametabiriwa katika yale yaliyoandikwa katika kitabu cha kukunja. (Zab. 40:6-8) Mungu hakuwa akitaka kuikubali dhabihu ya kibinadamu isiyokamilika ya mwana wa Ibrahimu Isaka, bali yeye alikuwa akitaka kuikubali dhabihu kamilifu ya kibinadamu ya Mwana wake mzaliwa wa pekee, Yesu Kristo. Yeye hakutaka na hakukubali dhabihu za wanyama za Siku ya Upatanisho ya kila mwaka milele, bali, kulingana na mapenzi na kusudi Lake, alitaka dhabihu kamilifu ya kibinadamu ambayo ingepatanisha dhambi za kibinadamu, “kuondoa dhambi” kabisa. Yesu Kristo alikuja kufanya mapenzi ya Mungu, na ilikuwa juu ya msingi wa mapenzi ya Mungu kama penye madhabahu kwamba kutolewa kwa Yesu mkamilifu kwa dhabihu ya kibinadamu kulikubaliwa na mwili wake wa kibinadamu uliotayarishwa, mkamilifu ulitolewa. Dhabihu hii kamilifu ya kibinadamu katika madhabahu ya “mapenzi” ya Mungu ilileta kweli utakaso kwa wanafunzi wa Kristo. Ndiyo sababu Paulo aliongeza hivi: “Kwa hayo ‘mapenzi’ sisi tumetakaswa kupitia kwa kutolewa kwa mwili wa Yesu Kristo.”​—Ebr. 10:10, NW.

26. Ni kwa sababu gani makuhani wa Kiyahudi hawakuwa na ruhusa ya kula katika “madhabahu” ambayo kutoka hiyo makuhani wadogo wa Kikristo wanakula?

26 Ndiyo sababu, tena, Paulo wakati uliofuata alisema hivi: “Sisi tunayo madhabahu ambayo kutoka kwa hiyo wale wanaofanya utumishi mtakatifu penye hema hawana ruhusa ya kula . . . Kwa hiyo Yesu naye, ili apate kuwatakasa watu kwa damu yake mwenyewe, aliteswa nje ya lango.” (Ebr. 13:10-12, NW) Yaani, sisi Wakristo tulio makuhani wadogo wa kiroho tunayo dhabihu yenye kupatanisha dhambi katika madhabahu ya “mapenzi” ya Mungu ambayo kutoka kwa hiyo makuhani wanaotumikia katika hekalu la Herode katika Yerusalemu hawana ruhusa ya kula dhabihu kwa sababu ya kukosa kwao imani katika Kuhani Mkuu wa kweli wa Yehova, Yesu Kristo, Mpatanishi wa agano jipya la Yehova.

27. Yesu alijitoa mwenyewe kwa dhabihu wakati gani, na ni msingi gani wa dhabihu uliotokea wakati huo, na ni “siku” gani iliyofananishwa iliyoanza wakati huo?

27 Yesu kama binadamu mkamilifu alijitoa mwenyewe dhabihu wakati gani katika madhabahu ya “mapenzi” ya Mungu kama ilivyoandikwa katika kitabu cha kukunja? Hii ilikuwa wakati alipojitoa mwenyewe kwa Yohana Mbatizaji katika mwaka wa 29 C.E. ili azamishwe katika Mto Yordani. Kwamba Yehova Mungu aliikubali dhabihu ya kujitoa kwa Yesu ni wazi, kwa maana Yesu alipobatizwa katika maji Yehova aliimimina roho yake takatifu juu ya Yesu akamfanya kuwa Kristo au Mtiwa Mafuta na akasema hivi kwa sauti kuu: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” (Mt. 3:13-17; Yohana 1:29-34) Kwa hiyo ilikuwa wakati huo kwamba “madhabahu” ya mfano ikatokea na kukawa toleo la dhambi lenye kukubalika juu yake. Tangu wakati huo Yesu Kristo alikuwa akitembea katika ua wa mfano wa kikuhani akisimamia dhabihu yake ya kibinadamu mpaka kufa. Ile Siku ya Upatanisho iliyo kubwa ya mfano ilikuwa imeanza, naye Yesu Kristo kama Kuhani Mkuu wa Mungu alikuwa akitumikia katika “madhabahu” ya kweli ya kiroho ya Mungu katika njia inayofanana na ile ya kuhani mkuu wa Kiharuni katika hekalu la Yerusalemu Siku ya Upatanisho ya kila mwaka, Tishri 10.​—Ebr. 8:1-6.

Mchoro katika ukurasa wa 245]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

RAMANI YA MSINGI WA HEMA

KASKAZINI

MAGHARIBI

KUSINI

MASHARIKI

PATAKATIFU ZAIDI

Sanduku

Pazia

PATAKATIFU

Meza

Madhabahu ya Uvumba

Kinara cha Taa

Ua

Birika

Madhabahu ya Sadaka ya Kuteketezwa

Kiwambo

[Picha katika ukurasa wa 246]

Hekalu la Sulemani, na vile vile hema, vilifananisha hekalu la kiroho la Mungu​—mpango wa kumkaribia Yehova katika ibada juu ya dhabihu ya upatanisho ya Yesu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki