Maandishi ya Utawala wa Kibinadamu
JE! KUMEKUWA na namna yo yote ya serikali ya kuwazika na mwanadamu ambayo hakuijaribu? Serikali zetu za kisasa kwa kadiri kubwa ni matokeo ya “sayansi ya kisiasa.” Hili ni funzo gumu la yaliyoonwa na mwanadamu katika jitihada zake za kujaribu-jaribu kujitawala mwenyewe, kwa kusudi la kutia katika serikali njia zilizo na matokeo mazuri zaidi.
Kwa hiyo, inatupasa tuwe na serikali—walau serikali fulani—zinazotosheleza mahitaji ya watu, zinazotoa ambacho watu wanataka kutoka kwa serikali. Je! tuna yo yote? Maandishi ya kisasa ya utawala wa kibinadamu yanafunua nini?
OMBI LA SERIKALI YA ULIMWENGU
New York Times la Jumapili, Mei 21, 1972, lilikuwa na ukurasa mzima wenye tangazo lililofanywa na kikundi cha raia wajulikanao sana wa nchi 32 wakijiita “Raia za Kwanza za Sayari.” “TANGAZO LA KIBINADAMU” hili lilikuwa mashtaka juu ya jitihada za utawala wa mwanadamu mpaka wakati uliopo za kuleta vitu vinavyotamaniwa zaidi. Lilifanya madai yafuatayo yenye nguvu:
“Uhai wa kibinadamu katika sayari yetu umo hatarini.
“Umo katika hatari ya vita ambayo ingeweza kuharibu kabisa makao ya kibinadamu.
“Umo hatarini kutokana na matayarisho ya vita yanayomaliza matumaini ya maisha yanayofaa.
“Umo hatarini kwa sababu ya kunyimwa haki za kibinadamu.
“Umo hatarini kwa sababu hewa inaendelea kuchafuliwa na maji na udongo vinatiwa sumu.
“Umo hatarini kwa sababu ya ongezeko la idadi ya watu lisilozuilika.”
Nini, basi, lililokuwa kusudi la tangazo hili? Lilielezwa katika ombi la kutia jitihada zaidi za kibinadamu kwa kutegemeza Umoja wa Mataifa.
Lakini je! maandishi ya utawala wa kibinadamu yanategemeza kuweka tumaini katika Umoja wa Mataifa?
VITA
Maandishi yanaonyesha nini juu ya ‘hatari kutokana na vita’? Je! utawala wa kibinadamu umefanya maendeleo kwa habari ya kuhakikisha ahadi ya amani?
Kama ilivyoripotiwa katika Western Producer, chuo kinachoitwa Norwegian Academy of Sciences kilifanya uchunguzi wa wingi na uzito wa vita tangu wakati wa nyuma zaidi unaoelezwa na historia. Walivumbua kwamba, “tangu mwaka wa 650 B.C. kumekuwa na uundaji wa zana za vita 1656, kati ya huo 16 peke yake ndio haukuleta vita. Unaobaki ulileta hasara ya uchumi kwa nchi zilizopaswa.”
Nyuma ya miaka 25 ya historia ya Umoja wa Mataifa, uchunguzi wa maandishi yake ulifanywa. Sunday Bulletin la Oktoba 18, 1970, lilimtaja U Thant, aliyekuwa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa wakati huo, akisema:
“Nasikitika sana kwamba ingawa tumeweza kufika mwezini, mara nyingi tunaonyesha choyo ajabu mno bila busara, ukinaifu na ubaridi tunapopambana na ugumu mkubwa hapa duniani.”
Na Lester P. Pearson, aliyekuwa waziri mkuu wa Canada wakati huo, alieleza matokeo ya jitihada za kuleta amani za Umoja wa Mataifa katika maneno haya: “Amani inategemea kwa mashaka makombora ya hydrogen. Ni jambo la kusikitisha kwamba Umoja wa Mataifa haukupata mahali pema zaidi kwa tegemeo lake.”
Kwa kweli, basi, je! utawala wa kibinadamu una lo lote la kutoa kutegemeza tumaini la kwamba wakati fulani utaleta amani?
UCHAFU
Tisho jingine lililo baya kama vita ni hali ya uchafu. Kama mfano mdogo tu wa magumu makubwa sana katika kila sehemu ya kupambana na uchafu, angalia hatari ya takataka. Reader’s Digest, katika habari iliyofupishwa kutoka kwa National Civic Review la Machi 1972, kinataja jibu la wakuu zaidi ya 20 wa United States juu ya usimamizi wa takataka, kwa ulizo “Shida ya takataka ni nzito kadiri gani”? Walieleza wazi:
“Kadiri ya takataka tunayokusanya kila mwaka ni kubwa ajabu—mikebe bilioni 80, chupa bilioni 38, tani milioni 40 za karatasi na vibweta, mipira mikuukuu ya magurudumu ya gari milioni 180, vyombo vikubwa vya nyumbani milioni 21, motakaa kuukuu milioni 7. Kuiondoa takataka hii sasa kunatugharimu shilingi milioni 31 na nusu kwa mwaka—hesabu ambayo huenda ikaongezeka maradufu kizazi kinachokuja.”
Labda iliyo hatari zaidi kupita zote ni takataka inayotumbukizwa katika maji yetu. “Mwaka wa 1980,” National Academy of Sciences kinaonya, “tutakuwa tukifanyiza takataka ya kuchafua maji ya kutosha kumaliza oksijeni (hewa) yote katika mito yote 22 ya United States.”
Je! ugumu huu ni wa taifa moja tu? Editorial Research Reports la Desemba 1, 1971, linaonya:
“Ulizo kubwa kwa mkutano wa Umoja wa Mataifa [uliofanyiwa Stockholm Juni 1972], na kwa majaribu yote yafuatayo ya kumaliza uchafu wa ulimwengu pote, ni kama kupendezwa na mazingira kumechelewa mno kutoweza kusaidia cho chote. Kwa kweli je!, mwanadamu amekwenda mbali mno kutoweza kurudi tena? Je! mataifa yanaweza kufanya maamuzi magumu ya kisiasa yaliyo ya maana ili kuleta ushirikiano ulimwenguni pote katika hatari iliyopo? Jambo lo lote lisilo jitihada ya mataifa yote linaelekea kuwa la bure. Mazingira ya ulimwengu ni mamoja; ni ya namna ambayo taifa moja peke yake haliwezi kuyasafisha. Hewa inachukua uchafu wa viwandani na madawa ya kuua madudu duniani kote. Kwa kweli kila bomba la maji limechafuliwa.”
Je! maandishi haya yanatia moyo, au kutia matumaini katika utawala wa kibinadamu?
UHALIFU
Uhalifu ni jambo jingine linaloharibu ambalo hakuna serikali yo yote imeweza kulimaliza. Kwa kweli, ambukizo hili baya sana linaenea kwa kadiri ya kuogofya ulimwenguni pote. Katika mataifa fulani uhalifu karibu uwe kama serikali ya kichinichini ya adui. Uhalifu umeitwa “ambukizo la ulimwenguni pote,” “msiba wa mataifa yote.”
Katika nchi iliyo tajiri kupita zote katika ulimwengu, United States, uhalifu unaelekea kuenea zaidi. Gharama ya kitaifa sasa ni karibu shilingi bilioni 357 kwa mwaka, sawa na zaidi ya kadiri ya 5 kwa mia ya mavuno mengi ya kitaifa ya shilingi bilioni mia saba elfu. Na uhalifu haufanywi na “magenge” tu. Kadiri kubwa (shilingi bilioni 56 kwa mwaka) inaibwa na wakuu na wafanya kazi wanaoaminiwa.
Lakini wa kutia hofu ni uhalifu wa kutumia jeuri juu ya mali. Inaendelea kuwa hatari kutembea katika barabara za miji ya United States, na uchunguzi unaonyesha wazi kwamba hatari kama hiyo inayoletwa na uhalifu inaongezeka karibu kila mahali.
Katika United States, tarakimu za Federal Bureau of Investigation (idara ya uchunguzi wa uhalifu) zinaonyesha, uhalifu uliongezeka mara kumi na moja upesi kuliko idadi ya watu ilivyoongezeka. Uhalifu mbaya sana (uuaji, kunajisi, unyang’anyi, mashambulio mabaya zaidi, uvunjaji wa nyumba, wizi wa motakaa, wizi [wa shilingi 350 na zaidi]) uliongezeka kwa kadiri ya 148 kwa mia, kutoka 2,014,600 mwaka wa 1960 kufika 4,989,700 mwaka wa 1969.
Katika London, mji ambao umejulikana kwa muda mrefu kama usio na jeuri barabarani, Waingereza wanaogofishwa kwa kuwa mashambulio, unyang’anyi na uoteaji wa barabarani vimezidi. Kundi la kipekee la mapolisi limepewa kazi katika reli zilizo chini ya ardhi kwa sababu ya hatari ya uhalifu. “Si salama wakati wa usiku katika Birmingham,” alisema afisa wa polisi. Uhalifu wa kutumia nguvu katika Uingereza ulipanda kutoka 26,000 mwaka wa 1966 kufika 41,000 mwaka wa 1970. Na hali kama iyo hiyo inazipata nchi nyingine.
Je! ni dalili gani za kumaliza magumu haya unazoona kutokana na utawala wa kibinadamu?
UGUMU WA DAWA ZA KULEVYA
Kutumia dawa za kulevya kumeitwa “ugonjwa ulio mbaya zaidi kuliko yote katika historia ya Kiamerika,” na kwa kasi inakuwa hivyo katika mataifa mengine. Imekuwa ndiyo sababu kubwa ya kadiri ya uhalifu unaoongezeka kwa kasi sana. Art Linkletter, mtu anayesema katika radio na televisheni, ambaye kijana wake wa kike alitumia dawa za kulevya, alifanya ombi kali tendo lichukuliwe na serikali, katika hotuba mbele ya wasikilizaji wa pekee wa Umoja wa Mataifa katika mji wa New York, Septemba 14, 1971. Hotuba yake ilionyesha waziwazi kwamba utawala wa kibinadamu ulikwisha shindwa kwa njia fulani kutimiza matakwa ya watu, matumaini na tamaa. Linkletter aliuliza:
“Ikiwa maisha matupu, yenye taabu yanawaelekeza watu kwenye dawa za kulevya, je! tutayageuzaje maisha hayo? Sababu gani watu wanajiua wenyewe kwa wingi namna hiyo katika ulimwengu? Sababu gani watu wengi namna hiyo wanafikia hatari yao wenyewe wasiweze kuishinda? Sababu gani kutumia vibaya dawa za kulevya kunakuwa sehemu ya msiba huo mara nyingi hivyo?”
Katika ombi lake la mwisho Linkletter alionya kwamba utawala wa kibinadamu ulikuwa umeelekeza makusudi yake upande usiofaa. Alisema:
“Kwa ajili ya jamaa ya kibinadamu, Umoja wa Mataifa lazima uwafikie walio katika taabu. Ulimwengu wetu umetenganishwa na mashindano makubwa, lakini matokeo yatakuwa si kitu ikiwa watoto wetu wanatupwa. Wanasayansi wetu wanaonyesha njia yetu katika mbingu, lakini hakuna haja ya kufunga safari hiyo tukiuacha ulimwengu ukiwa katika maumivu.”
HALI YA KUTOPATA CHAKULA KINACHOFAA
Robert S. McNamara, Rais wa International Bank for Reconstruction and Development, anaonyesha namna ulimwengu ulivyo katika hali ya kutopata chakula kinachofaa jambo linalopaswa kumwamsha mtu aone utawala wa kibinadamu usivyoweza kuleta matakwa ya wanadamu kwa furaha. Katika hotuba iliyotolewa Washington, D.C., mbele ya baraza inayoitwa Board of Governors of the World Bank Group, Septemba 27, 1971, alisema kwamba katika nchi zenye nafuu kidogo hali ya kutopata chakula kinachofaa imeenea pote, ndiyo sababu kubwa ya vifo vingi vya watoto wachanga na hivyo ni kizuizi kikubwa kwa maendeleo ya kibinadamu.
“Na hali,” McNamara anasema, “ijapokuwa kuna uhakika wa kwamba kwa kadiri ndogo ya matumizi ya uchumi faida kubwa zinaweza kupatikana, ni vigumu sana kupata taifa katika ulimwengu unaoendelea ambapo mpango unafanywa wa kuumaliza ugumu huu.”
Bw. McNamara aliendelea kueleza wazi kwamba hesabu ya vifo vya watoto ni kubwa sana katika nchi zilizo fukara zaidi. Kwa mfano, India kuna maeneo makubwa ambapo vifo katika mwaka wa kwanza wa kuishi vinatukia 150 mpaka 200 kwa kila vitoto 1,000 vinavyozaliwa vikiwa hai.
Katika United Arab Republic, kadiri ya watoto wa miaka kati ya mmoja na miwili wanaokufa ni zaidi ya mara 100 ya kadiri ya wanaokufa Sweden. Vital Speeches of the Day, Oct. 15, 1971.
Hata mapema zaidi katika Reader’s Digest, Februari 1969, mwanasayansi anayejulikana sana alisema: “Ni jambo lililo wazi sana kwamba, katika jitihada ya kuwalisha wanadamu, upande wetu umeshindwa. . . . imekwisha kuwa kuchelewa mno kuzuia ongezeko kubwa katika kadiri ya vifo vinavyoletwa na njaa kali.”
UFUKARA NA USITAWI WA HALI YA JAMII YA WATU
Kwanza sababu ya msingi ya hali ya kutopata chakula kinachofaa ni ufukara, ugumu ambao kwa sasa haushindiki na kumalizwa, hata katika nchi zilizo tajiri zaidi. Dr. John E. Reilly, Mkuu wa Overseas Development Council, anaripoti:
“Kulingana na Benki ya Ulimwengu, mapato kwa mwaka katika bara changa ya mwaka wa 1968 yalikuwa kama ifuatavyo: Asia shilingi 770; Afrika shilingi 910; Latin Amerika shilingi 2,590; Mashariki ya Kati shilingi 2,310. Hii inalinganishwa na wastani ya mapato kwa kila mtu katika United States ya shilingi 28,000; Canada shilingi 17,500; Ujeremani shilingi 13,300; Uingereza shilingi 12,600.
Dr. Reilly anaendelea kusema kwamba nchi zenye mapato ya chini zina mamilioni ya watu wanaoishi kwa sehemu iliyo nusu ya wastani. Je! jitihada za utawala wa ulimwengu, hata kwa msaada wa Umoja wa Mataifa, zinashinda hali hii yenye huzuni? Hapana, kwa kuwa Dr. Reilly anasema: “Kuna woga wa kwamba kanuni ya maisha ya mamilioni ya watu iko chini zaidi mwaka wa 1971 kuliko ilivyokuwa mwaka wa 1960.” Anaendelea kusema:
“Hii inatoa dokezo fupi la hali za nchi changa, mfano usioonyesha kabisa njaa inayoenea pote, hasara, kukosa nafasi ya masomo, ugawaji wa mali usio sawa, kuenea pote kwa maradhi, bila kutaja vizuizi vya kisiasa.”
Hata katika nchi iliyo tajiri kupita zote ulimwenguni, United States, miji mizima inapatwa na upungufu wa fedha, kwa sababu ya ongezeko la kasi la gharama za usitawi wa hali ya jamii ya watu. Mwaka wa 1970, karibu shilingi bilioni 90 zilikuwa gharama za usitawi wa hali ya jamii ya watu.
Hali hii ni ya namna ambayo wataalamu wa mambo ya uchumi hawaoni njia ya kuepukia, kama ilivyoonyeshwa na mtaalamu wa mambo ya uchumi Wakili Thomson wa Claremont Men’s College katika Califomia. Anaeleza kwamba, katika jamii iliyo tajiri, fedha zaidi na zaidi inapotolewa kwa usitawi wa hali ya jamii ya watu, wale wanaopokea msaada wanafanya maombi yanayoongeza gharama. Kwa hivyo, anasema, “ufukara unaifuatia-fuatia jamii ya watu kama kivuli kinachomfuata mtu anayekimbia.”
IDADI YA WATU INAYOONGEZEKA KASI
Idadi ya watu ikiwa ilipo, serikali zi karibu na hatari, magumu yakiwa kila upande na kila njia inaonekana haina matokeo. Hilo ni baya sana, lakini sasa idadi ya watu inayoongezeka inaonyesha msiba kwa mipango yao kwa wakati ujao. Katika ripoti ya Victor-Bostrom Fund ya International Planned Parenthood Federation, Rudolph Peterson, Msimamizi wa United Nations Development Program, alisema:
“Kuongezeka kwa kushangaza kwa idadi ya ulimwengu hakutoi tumaini zuri juu ya jitihada zetu zote kuendeleza usitawi wa mataifa yote. Kuendeleza hali za maisha katika nchi ambapo idadi ya watu inaongezeka maradufu kila miaka 20 ni kama jitihada ya mfalme wa Korintho katika hadithi, ambaye daima anajaribu kusukuma jiwe lifike juu kilimani ila kuliona likibingirika likirudi chini.”
Na A. H. Boerma, Msimamizi-Mkuu wa Food and Agriculture Organization, anatoa ombi la haraka sana:
“Hainipasi kuendelea kusema juu ya uhakika wa kwamba ongezeko lililoko lisilozuilika la idadi ya watu katika sayari hii linaelekeza magumu makubwa ya ulimwengu—njaa, ufukara na ukosefu wa kazi—kwenye hatari. Hainipasi kueleza maafa ambayo yangetokea na si juu yangu kueleza kila kitu juu ya linalopaswa kufanywa. . . . Lakini kutoka katika jukwaa hii ningependa kutoa ombi kwa wote wanaopaswa wakubali uhitaji wa kuzuia idadi ya watu isizidi.”
Ni nini, basi, linaloweza kusemwa juu ya maandishi ya utawala wa kibinadamu? Je! umemaliza hata mojawapo la magumu ya msingi ya kuishi pamoja kwa amani, uhuru bila ufukara, woga, njaa, hasara na uhalifu? Je! umewapa wanadamu wanayotamani sana kutoka kwa serikali?
Basi, mbele kuna nini kwa utawala wa dunia wa mwanadamu unaoendelea? Kila ugumu—uchafu, vita, njaa, dawa za kulevya, au lo lote la mengine mengi—unaelekea kuleta msiba mkuu wa dunia yote. Yote haya pamoja yanafanyiza hali ngumu ambayo hekima na jitihada za binadamu vimeshindwa kabisa kupunguza, licha ya kuyamaliza.
Je! huu si wakati kwa mwanadamu kutafuta shauri la juu zaidi, ndiyo, wakati wa kumsikiliza Mtawala wa Kimungu wa ulimwengu wote? Anayosema na anayokusudia juu ya utawala wa dunia ni shauri la uzima au kutoweka kabisa, kama itakavyozungumzwa katika makala inayofuata.
[Grafukatika ukurasa wa 462]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
UHALIFU
Uhalifu mbaya sana katika U.S.A, umeongezeka kwa haraka sana mara kumi na moja kuliko idadi ya watu, miaka ya 1960-1969.
UHALIFU
IDADI YA WATU
[Picha katika ukurasa wa 460]
VITA Maandishi ya historia yanaonyesha uundaji wa silaha ama umetokeza vita ama hasara ya uchumi.
[Picha katika ukurasa wa 461]
UCHAFU “Ulizo kubwa . . . ni kama kupendezwa na mazingira kumechelewa mno kutoweza kusaidia cho chote”
[Picha katika ukurasa wa 462]
DAWA ZA KULEVYA Matumizi ya dawa za kulevya ndio “ugonjwa” ambao ndiyo sababu kubwa ya kadiri ya uhalifu unaoongezeka kwa kasi sana.
[Picha katika ukurasa wa 463]
UFUKARA “Ufukara unaifuatia-fuatia jamii ya watu kama kivuli kinachomfuata mtu anayekimbia.” Gharama za kila mwaka kwa usitawi wa hali ya jamii ya watu katika U.S.A.—shs 89,600,000,000