Kushirikiana Kabisa na Waliowekwa wa Mungu
“Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya [nafsi] zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.”—Ebr. 13:11.
1. Wapenda haki wote wanatamani sana kuona nini? Jambo hili linawezekanaje?
JE! WEWE ni mtu anayependa haki? Kama ndivyo, moyo wako hautamani sana kuona chuki na uvunjaji wa sheria vikitoweka, amani ikienea na furaha ikija pahali pa huzuni? Yote haya na mengine zaidi yanawezekana kupita kwa ufalme wa Mungu, ambao kwa huo mambo ya dunia hii yatarekebishwa kabisa. (Isa. 11:3-5; Mt. 6:9, 10; Ufu. 21:1-4) Je! si hilo wewe mwenyewe ungetaka kuona, taratibu mpya kabisa ikichukua nafasi ya taratibu hii ya kale, inayokufa ambapo choyo na dhambi vinazidi? Je! unaweza kumfikiria mtu mwingine ye yote akilini mwako ila Mungu Mwenyezi akifanya kazi kubwa ya kujenga taratibu mpya kabisa juu ya majivu ya ile ya kale, akifanya hivyo katika muda wa kizazi chetu?—Dan. 2:44; Mit. 29:2.
2. Twajuaje kwamba taratibu mpya i karibu sana? Tunaweza kwenda wapi kwa maelezo zaidi?
2 Kusudi letu wakati huu si kuzungumza elimu ya tarehe, lakini hata hivyo usisite kumwuliza ye yote wa mashahidi wa Yehova akuonyeshe katika Maandiko uhakika wa kwamba imebaki miaka michache tu tufikie mwisho wa miaka elfu sita ya kuwako kwa mwanadamu duniani, na waulize hiyo maana yake ni nini kwa habari ya uhuru wa kweli kulingana na maoni ya Mungu. Watafurahi kushiriki habari hii pamoja nawe.a
“TARATIBU MPYA” ITATAKA USHIRIKIANO
3. Eleza kazi fulani kubwa zitakazokuwa za lazima katika taratibu mpya.
3 Ebu tuliza akili kidogo, tafadhali, ufikirie kazi kubwa zitakazotakiwa kufanywa katika taratibu hiyo mpya ya mambo, ya kimungu. Kwanza, orodha kubwa ya kuelimisha itatakiwa kuwafundisha lugha mpya mamilioni ya wafu watakaofufuliwa wanapotoka makaburini. (Yohana 5:28, 29) Na, zaidi, fikiria kazi inayotakiwa kufanywa ili kugeuza mioyo na akili za watu hawa, wengi wao wakiwa hawajasikia hata kidogo habari ya Biblia, au juu ya sheria za Mungu na makusudi kwa wanadamu. Kisha, fikiria mpango utakaoanzishwa ili kuigeuza hii dunia yetu kuwa bustani ya kupendeza iliyokusudiwa na Mungu. Mtu anapofikiria wakati unaomalizika kufyeka eka moja tu ya ardhi, kulima udongo na kupanda kwa njia ambayo utatokeza vijiti na miti na mimea mingine kwa njia itakayofanya sehemu yenyewe ifae kuitwa bustani ya kupendeza, anapata maoni kidogo juu ya kazi kubwa itakayofanywa kugeuza dunia yote kuwa paradiso ikiwa na sehemu za kutosha zenye kuzaa chakula cha kuridhisha umati wenye starehe duniani.—Mwa. 1:28; Zab. 72:16; 67:6; Eze. 34:27.
4, 5. (a) Ili 1 Wakorintho 15:24-28 litimizwe, ni lazima utawala wa kifalme wa Kristo ufanye nini bila kushindwa’ (b) Eleza uradhi ambao Mfalme bila shaka atakuwa nao wakati huo,
4 Na, ebu fikiri, kazi hiyo yote ni lazima ifanywe katika muda wa miaka elfu moja ili unabii utimizwe: “Hapo ndipo mwisho, atakapompa Mungu Baba ufalme wake; atakapobatilisha utawala wote, na mamlaka yote, na nguvu. Maana sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti. Kwa kuwa, Alivitiisha vitu vyote chini ya miguu yake. Lakini atakaposema, Vyote vimetiishwa, ni dhahiri ya kuwa yeye aliyemtiishia vitu vyote hayumo. Basi, vitu vyote vikiisha kutiishwa chini yake, ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote, ili kwamba Mungu awe yote katika wote.” (1 Kor. 15:24-28) Kwa wazi, ili unabii huu utimizwe, dunia yote ni lazima igeuzwe kuwa paradiso, sawasawa na ilivyokusudiwa mwanzoni, katika muda wa miaka elfu moja.—Ufu. 20:2-6.
5 Fikiria, vile vile, furaha na uradhi utakaokuwa na Yesu Kristo kama msimamizi na msawazishi wa kazi hizi zote kusema kwa Baba yake wa kimbinguni, kweli: ‘Tazama, Baba. Mgawo ulionipa umemalizika. Dunia imefanywa kuwa paradiso kama Edeni. Wafu waliokuwa katika Sheol wote wamefufuliwa, wakazoezwa na kuadibishwa. Wanadamu wamefikishwa kwenye ukamilifu. Mambo yote uliyoniagiza nifanye sasa yametimizwa, na yote yametimizwa katika wakati wake!’
6, Tunaweza kukata shauri gani kutoka katika njozi hii fupi juu ya wakati ujao?
6 Sasa, njozi hii fupi inatufundisha nini? Kati ya mambo mengine, inatia mkazo kwamba kazi kubwa iliyo mbele yetu inayotakiwa kufanywa itataka utaratibu, umoja, wafanya kazi wenye ujuzi, mioyo yenye hiari, wasimamizi wazuri na, zaidi ya yote, roho na baraka za Yehova ili imalizwe wakati unaofaa. Je! si hii ni mojawapo ya sababu za Mungu kutoa uangalizi wenye upendo kwetu leo, yaani, ili uangalizi huo ututayarishe kufanya kazi na kupata mazao katika taratibu mpya ya wakati ujao inayokaribia sana?—Yohana 15:5, 8; Kol. 2:19.
IWENI WATII KWA WALE WANAOWAONGOZA
7. Ni ulizo gani linalotokea juu ya nia yetu kuelekea uangalizi na adabu sasa na wakati ujao?
7 Hivyo, nia ya watumishi wote wa Mungu inapaswa kuwa nini kuelekea uongozi, uangalizi na adabu inayotolewa kupitia kwa kundi la Kikristo leo? Na tujifunze si inayopaswa kuwa nia yetu tu, bali na zawadi zitakazopatikana kwa kuwa na maoni yanayofaa kuelekea uongozi na adabu sasa na wakati ujao.—Ebr. 12:5-11.
8. (a) Ingawa waangalizi wote wa kibinadamu wanafanya makosa, sababu gani twaweza kuwatumaini waliowekwa kuwa waangalizi katika kundi la Kikristo? (b) Waebrania 13:17 linatupaje chakula cha mawazo na maongozi kupatana na haya? (c) Eleza maana ya “kuwa na wajibu” na matokeo yake.
8 Kwanza, tukumbuke kwamba sisi tu wanadamu, na wanadamu wote wanafanya makosa. (Zab. 51:5) Hata hivyo, Wakristo waliojiweka wakf, zaidi waangalizi na watumishi wa huduma, wanafunzwa kuwa wenye fadhili, wenye upendo, wenye kusaidia, wakati ule ule wakiwa imara. Sifa hizi za fadhili yenye upendo, rehema na haki ni alama za kuwajulisha Wakristo waliokomaa. (Yohana 13:35; Mik. 6:8) Je! mioyo yetu haipaswi kutaka kuwatumaini wanaume kama hao? Kwa kweli, mtume Paulo anatusihi tuwatii, akiandika katika Waebrania 13:17: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya [nafsi] zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.” Sasa, tunapolifikiria andiko hili, tunaona kwamba waangalizi hawa ni lazima watoe hesabu kwa nafsi zetu, yaani, maisha zetu. Mtu anapojua kwamba ana wajibu kwa mtu mkubwa kumpita kwa anayofanya, kwa kawaida huyo anafikiri mbele ya kusema au kutenda. Bila shaka hataki kutenda kwa ujinga.
9. 2 Mambo ya Nyakati 19:6, 7 linawafundisha nini wale walio na madaraka ya kuhukumu na kutoa mashauri?
9 Yehova, tangu nyakati za kale, amewasihi wanadamu waliopewa madaraka ya kuhukumu, kuongoza na kusimamia, kufikiri mbele ya kutenda. Namna kanuni hii inavyotamkwa wazi katika 2 Mambo ya Nyakati 19:6, 7: “Akawaambia hao makadhi, Angalieni myafanyayo; kwa kuwa hammfanyii mwanadamu hukumu, ila [Yehova]; naye yupo pamoja nanyi katika neno la hukumu. Basi sasa hofu ya [Yehova] na iwe juu yenu; angalieni mkaifanye; kwa maana kwa [Yehova], Mungu wetu, hapana uovu, wala [upendeleo au kukubali rushwa].” Hivyo uangalifu, kupima mambo, kuamua uhakika wote kila mara kunatangulia kutenda, yaani, kukata hukumu.
10. (a) Je! ni vyepesi kuwa mwangalizi? Eleza. (b) Sababu gani haitupasi tuwe na hofu juu ya uangalizi unaotolewa katika kundi la Kikristo? (c) Ni jambo la maana namna gani kuwa na uangalizi wenye upendo kama huo?
10 Si vyepesi kuwa mzee, mchungaji, mwangalizi, au mwamuzi. Kufanya maamuzi yenye hekima kwa faida ya watu wa Mungu kunataka ufahamu na ujuzi. (Mit. 2:3-5) Na nyakati nyingi, kwa sababu ya umbo la mwanadamu, si watu wote walio wepesi kushughulika nao. Huenda ikawa wewe unaudhika kwa kadiri fulani unapopewa mashauri. Labda hujashirikiana na tengenezo la Yehova kwa muda mrefu sana. Au, huenda ikawa unajifunza na watu wa Yehova, na kwa njia fulani una hofu juu ya kutiwa adabu na rekebisho unaloagizwa ufanye katika maisha yako yanayolingana na kanuni ya kibinadamu ambayo umezoea. Usiogope uangalizi wenye upendo unaozoewa na tengenezo la Yehova. Si kwamba tu linatutayarisha kwa maisha katika taratibu mpya ya mambo; ni la maana sana katika kutusaidia sasa tupatane wenyewe kwa wenyewe katika hali yetu isiyo ya ukamilifu leo. (Zab. 141:5) Wakati tunapofikiria mikazo inayotujia katika taratibu hii ya kale, ambapo hasira zinapanda, ambapo wengine wanatumia ndimi zao kupiga domo, ambapo kujiweza kunadharauliwa na kutumiwa kidogo, tunaweza kushukuru namna lilivyo jambo la maana kuwa na uangalizi wenye upendo na mashauri ya moja kwa moja kutoka kwa wale walio wazee zaidi kwa kiroho. (Mit. 1:22, 30, 33) Uongozi wenye hekima na msaada wenye upendo wa wazee vinakuwa na matokeo ya mchanganyiko wa ajabu wa namna mbalimbali za ujuzi na utu zilizounganishwa ili kutimiza kazi iliyo ya maana zaidi duniani leo, yaani, kuhubiri kwa habari njema za Ufalme mbele ya kuchelewa sana.—Mt. 24:14.
NAMNA YA KUWARUDISHA WALE WANAOCHUKUA HATUA MBAYA
11. (a) Sababu gani ni lazima walio na madaraka kama waalimu watumie ndimi zao kwa hekima? (b) Je! inampasa mwangalizi asite kutoa shauri anapoona kosa? Eleza.
11 Kumbuka, vile vile, si vyepesi kutoa mashauri. Aliyepewa madaraka, akiitwa afundishe au atoe mashauri, ni lazima aangalie anayosema. (Yak. 3:1) Ulimi unaweza kujeruhi na kuumiza na kuponya vile vile. (Yak. 3:5-10) Lakini ni lazima waangalizi wa watu wa Mungu wasisite wanapoona kosa. Bila shaka ndiyo sababu Paulo aliandika: “Ndugu zangu, mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi mlio [na sifa za kiroho] mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe.”—Gal. 6:1.
12. (a) Je! Wagalatia 6:1 linaandikiwa waangalizi peke yao? Eleza. (b) Tukigundua dhambi nzito, tutatendaje katika hali hiyo? (c) Ni ushirikiano gani unaoweza kutazamiwa kutoka kwa wale walio waaminifu kwa kweli kwa Mungu wanapoona mwenendo wenye dhambi ndani ya kundi la Kikristo?
12 Je! andiko hili limeandikiwa waangalizi au wazee peke yao? Hapana, kwa maana mtu ye yote akimwona mfanya kazi mwenzake ameghafilika katika hatua mbaya, ni wajibu wake kujaribu kumrudisha mtu kama huyo kwa roho ya upole. Kwa kweli, lingekuwa jambo la upendo kwa upande wetu kufanya hivyo. Ikiwa dhambi yenyewe ni nzito, labda tungemwambia aliyeitenda aieleze mara moja kwa waangalizi wanaopaswa katika kundi, na asipofanya hivyo, kwa sababu ya kushirikiana kwetu kwa uaminifu na tengenezo la Yehova ingetupasa tulieleze jambo hili kwa halmashauri ya hakumu ya kundi. (1 Kor. 5:9-13; Zab. 31:23) Anayependa haki na aliye mwaminifu kweli kwa Mungu atajitokeza kihodari na kueleza waziwazi mwenendo wo wote mbaya sana wa dhambi ambao ameshuhudia katika kundi na atahakikisha bila kusita ukweli wa jambo lenyewe anapoitwa afanye hivyo.—Law. 5:1; Efe. 4:24; Luka 1:74, 75.
13. Eleza namna upendo unavyotusaidia katika kundi la Kikristo.
13 Kweli, tunapofikiria jambo hili la kushirikiana wenyewe kwa wenyewe na kushirikiana na wale wenye vyeo vya uangalizi, mara kwa mara tunakumbuka nia yenye upendo tunayopaswa kuwa nayo sote kila mmoja kumwelekea mwenzake. Kwa kweli, upendo unapaswa ufunike wingi wa dhambi, na mtu anapokuwa na nia yenye upendo kumwelekea mwenzake, anaweza kusamehe na kusahau. Kwa kweli upendo unafanya maajabu. (1 Pet. 4:8; 1 Kor. 13:4, 5) Lakini, nyakati nyingine upendo unawafanya Wakristo waliojiweka wakf wasitupilie mbali kosa lakini wajaribu kumsaidia mkosaji kwa sababu gumu lenyewe linaweza kuwa zito sana. Basi, je! kanuni ya kumaliza ugomvi mzito kati ya mtu na mwenzake ni ipi?
‘FUNUA KOSA LA NDUGU YAKO’—WAKATI GANI NA KWA NJIA GANI?
14. (a) Ni hatua gani zilizowekwa na Yesu za kushughulika na mambo ya dhambi anayotendewa mtu, mambo ambayo ni mazito sana kutostahili kusahauliwa? (b) Maana yake ingekuwa nini kwa mtu kuonwa “kama mtu wa mataifa na kama mtoza kodi”?
14 Yesu alitoa mashauri juu ya dhambi zinazoweza kutendwa kwa mtu na zinazodhaniwa kuwa nzito sana zisiweze kusahauliwa. Alisema: “Ikiwa ndugu yako anafanya dhambi, nenda ukafunue kosa lake kati yako na yeye peke yenu. Ikiwa anakusikiliza wewe, umempata ndugu yako. Lakini ikiwa yeye hasikilizi, chukua pamoja na wewe mtu mmoja au wawili zaidi, ili kwa kinywa cha mashahidi wawili au watatu kila shauri lipate kuthibitika. Ikiwa yeye hawasikilizi, sema kwa kundi. Ikiwa hasikilizi hata kundi, mwache yeye awe kwako kama mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi.” (Mt. 18:15-17, NW) Wasikilizaji wa Yesu, wakiwa Wayahudi, walijua kuwa kwa watu wengine wa taifa lake kumdharau Myahudi “kama mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi” ingekuwa na maana ya kwamba ametupwa nje ya kundi la Kiyahudi.
15. Kosa dogo analotendewa mtu linaweza kwa faida kushughulikiwaje, lakini hii ndiyo namna ya kosa ambalo Yesu alikuwa akizungumza hapa?
15 Kwa kuwa hatua alizoweka Yesu zingeongoza kwenye matokeo mazito kama hayo, kwa wazi hakuwa akiweka kanuni ya kushughulika na kila kosa dogo analofanyiwa mtu. Kweli, mara nyingi ni jambo linalofaa na la hekima na la msaada sana kwenda na kusema na mtu ambapo kuna ugumu wa mtu mwenyewe kwa sababu ya kosa fulani dogo, ukifanya hivyo kwa kusudi la kumaliza ugomvi unaoelekea kukua. (Mt. 6:14, 15; Mit. 12:18) Kutopatana kwingi kunamalizwa kwa njia hii. Lakini kwa hakika Yesu hakuwa akisema juu ya jambo hili wakati huo. Alielekeza, si kwenye kutopatana tu kwa kibinafsi kwa kawaida, lakini kwenye makosa yaliyo mazito kadiri ya kustahili kwa mtu kufukuzwa katika kundi.
16. Mbele ya kuanza taratibu iliyowekwa katika Mathayo 18:15-17, ni shauri gani linafaa?
16 Mbele ya wewe kuanza taratibu inayoonyeshwa katika Mathayo 18:15-17, basi, inakupasa uwe na uhakika wote kwamba dhambi nzito kama hiyo ulitendewa kabisa. Yesu hakusema, ‘Ikiwa unafikiri ndugu yako amefanya dhambi.’ Inakupasa ufikirie shauri lililo katika Mithali 25:8-10 ili kwamba usianzishe kitu ambacho kitakuletea mwenyewe aibu na kukuvunjia heshima. Hata wakati ambao kuna uhakika, haikupasi kueneza jambo lenyewe, ukipiga domo juu yake, bali inakupasa umwendee aliyekukosea kwa faragha na “ukafunue kosa lake kati yako na yeye peke yenu.”
17. Maana ya ‘kumpata’ ndugu yako katika andiko hili ni nini?
17 Ikiwa ndugu yako “anakusikiliza,” akikubali karipio lako, basi “umempata ndugu yako.” Je! hii maana yake ni kufanya mapatano ya kibinafsi tu? Hapana, lakini kama linavyoonyesha shauri la Yesu lililobaki, ni lazima iwe na maana ya ‘kumpata’ kwa njia ya kumsaidia akae katika kundi, kumwondoa katika mwendo unaoweza kumfanya afukuzwe humo, pamoja na kupoteza kibali na baraka za Mungu. Kwa hiyo ‘kumpata’ ndugu yako kuna maana inayoelezwa katika Yakobo 5:19, 20, Wagalatia 6:1 na Yuda 22, 23. Hili, kwa kweli, linapaswa liwe ndilo kusudi na hamu yako—si kujipatia mwenyewe faraja au uradhi kwa sababu ya kosa fulani.
18. Ni makosa gani ambayo hayakumaanishwa na maagizo yaliyotolewa hapa na Yesu, na sababu gani sivyo?
18 Mtenda dhambi anapokubali karipio na kutaka msamaha, Yesu anasema, hakuna sababu ya kuendelea mbele na jambo lenyewe. Hii inaonyesha kwamba, ijapokuwa ni mazito, makosa yanayozungumzwa hapa yalikuwa ya namna ya kumalizwa kati ya watu wanaopaswa tu. Hii haitii ndani makosa kama uasherati, uzinzi, kulalana kwa wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake, kukufuru, kuasi imani ya kweli, ibada ya sanamu na dhambi mbaya sana za namna hiyo, kwa kuwa chini ya agano la Torati lililokuwapo wakati huo, dhambi hizi zilitaka zaidi ya msamaha kutoka kwa mtu aliyekosewa.—1 Kor. 6:9, 10; Gal. 5:19-21.
19. Dhambi zinazozungumzwa hapa zilikuwa za namna gani, na ni jambo gani linaonyesha hivyo?
19 Kwa sababu hiyo, na kwa sababu ya mfano ambao nyumaye Yesu alitoa, kama ilivyoandikwa katika Mathayo 18:21-35, dhambi zilizoangaliwa hapa kwa wazi zilikuwa dhambi kama zile za mambo ya fedha au mali—kushindwa kulipa sawasawa kitu fulani, tendo fulani lililokamatana na udanganyifu wa kadiri fulani—au labda kuharibu sifa ya mtu kwa kumsengenya, au dhambi kama hizo. Katika mambo kama hayo, ikiwa mkosaji alikubali kosa lake, akaonyesha nia ya kulirekebisha awezavyo, na kuomba msamaha, jambo lenyewe lingeweza kumalizwa kwa aliyekosewa kutoa msamaha.—Linganisha Mathayo 5:25, 26; Luka 12:58.
20. (a) Ikiwa mkosaji haitikii vyema unaposema naye peke yenu, ni hatua gani zaidi lazima ichukuliwe? (b) Ni akina nani “mtu mmoja au wawili” zaidi utakaoenda pamoja nao?
20 Lakini namna gani ikiwa unachukua hatua hii ya kwanza na anayefanya dhambi haitikii? Kwa sababu ya uzito wa dhambi yenyewe, huwezi tu kuachana na jambo hilo. Shauri la Yesu linaonyesha kwamba inakupasa umtafute mtu mwingine au wengine wawili na kurudi kusema na mkosaji. Kwa kweli inawapasa hawa wawe mashahidi wa kosa lenyewe. Hawaendi kama watazamaji tu wasio ndani au wapatanishi wanaojaribu kuleta mapatano. Kuliko hivyo, unaenda pamoja nao ili kwamba kwa sababu walishuhudia kosa lenyewe, waweze kuongeza ushahidi wao kwa wako. Wanaweza vile vile kuwa wasikilizaji wa yanayosemwa wakati huo. Ikiwa jambo lenyewe linasonga mbele na kuja mbele ya “kundi” na mkosaji anakana au anageuza maneno fulani au mambo fulani yaliyokiriwa, hawa wengine wanaweza kutoa ushuhuda wao na kuonyesha kweli zenyewe. Kwa tumaini hatua hii nyingine haitatakiwa na mtu huyo ataitikia jitihada zote zinazofanywa ili kumrudisha katika mwendo wa haki. Ikiwa hivyo, basi jambo hilo linamalizwa.
21. Ni hatua gani zaidi huenda bado ikawa ya lazima, na huenda matokeo yakawa nini?
21 Je! ikiwa bado mkosaji anakataa kukubali ni mwenye hatia, basi namna gani? Jambo lenyewe sasa linapaswa kukaziwa fikira za washiriki wanaopaswa wa kundi, wale wa baraza ya wazee walioagizwa kutumikia katika nafasi ya kuhukumu. Inatumainiwa kwamba sasa mtu huyo atasikiza hukumu yao rasmi na ‘kupatwa’ kama mtu anayestahili kubaki katika kundi. Kama sivyo, basi anatengwa na ushirika, na nyuma ya hapo kutendewa kama mtu wa nje.—Mt. 18:17.
USHIRIKIANO KATIKA MAMBO MENGINE
22. Taja mambo fulani yenye fadhili ambayo kila mhudumu katika kundi anaweza kufanya kwa hiari yake mwenyewe. Matendo kama hayo yatalisaidiaje kundi?
22 Ushirikiano na waliowekwa wa Mungu ni wa namna nyingi, zote ambazo zinaleta umoja na upatano katika kundi la Kikristo. Kufikia hapo inaweza kuwa vizuri kutaja mambo fulani ambayo kila mhudumu anaweza kufanya kwa hiari yake mwenyewe. Si vigumu kuelewa kwamba kila Mkristo ana wajibu kumwelekea mtu aliye mgonjwa, mtu anayetaka kutiwa moyo, au labda mtu aliye hospitalini. Je! tumwendee mwangalizi-msimamizi kumwuliza kama kuna jambo tunaloweza kufanya hali kama hizo zinapotokea? Ikiwa, kwa mfano, mwanamke wa Kikristo amekuwa mgonjwa na akatoka hospitalini karibuni na ndio anapata nafuu, je! si wazi kwamba anataka msaada wa namna fulani? Huenda akataka aletewe vyakula vya moto. Huenda akataka mtu fulani amsafishie nyumba yake, au amsomee na kumtia moyo, au kuipa jamaa yake msaada wa kimwili au wa kiroho. Namna jambo hili linavyotufanya tujisikie kuwa karibu karibu wenyewe kwa wenyewe, na namna matendo kama hayo kwa upande wetu yanavyoweza kuwa ya Kikristo!—Yak. 1:27; 2:14-17.
23. Taja kazi nyingine tunazoweza kufanya kwa kupenda, tukionyesha upendo wetu kwa wale walio katika kundi la Kikristo.
23 Halafu, tena, fikiri juu ya kuliweka Jumba la Ufalme kuwa safi na katika hali njema. Nyakati nyingine madaraka haya yanachukuliwa na wachache katika kundi. Je! unaweza kushirikiana, ukisaidia kwa upande huu, labda hata kujitolea kufanya hivyo? Au kunaye mtu fulani mgonjwa kwa kiroho unayeweza kutia moyo au kusaidia? Je! kuna mtu fulani anayekosa mikutano au anayeelekea kutokuwa na furaha ile ile aliyokuwa nayo katika huduma ya shambani? Je! ni wazee tu wanaopaswa kupendezwa na watu kama hao? Kwa wazi hapana. Bila kuchungulia mambo ambayo ni ya mtu mwenyewe peke yake, je! unaweza kuwa mwenye kutia moyo kwa kiroho na mwenye msaada kwa mtu kama huyo? Nyakati nyingine kuwatembelea watu kama hao nyumbani mwao, bila kwenda huko ili kuchungulia lililo baya, ni jambo la kufariji, na nyuma ya mazungumzo mara nyingi ugumu wenyewe unajulikana, kisha msaada unaofaa wa kiroho unaweza kutolewa. Ni mambo mengi namna gani tunayoweza kufanya tukivutwa na upendo kwa wote katika kundi!
24. (a) Inapaswa iwe tamaa gani ya kila mpenda haki leo? (b) Kuna faida gani zinazotokana na kujizoeza na uongozi na uangalizi wenye upendo wa waliowekwa wa Yehova leo?
24 Bila kutia shaka, tunashi katika nyakati zisizo za kawaida. Wakristo waliojiweka wakf na wale wanaojifunza Biblia pamoja nao wanajua kwamba “dhiki kubwa” inakuja. (Mt. 24:21, 22) Wakati huo u karibu sana. Tunaona kibali cha Mungu juu ya kundi lake. Kwa kweli inapaswa iwe tamaa ya kila mpenda haki kujipatanisha kabisa na kundi la Kikristo. Lakini, inaelekea kwamba wengine wanaoshirikiana na kundi la Kikristo hawatumikii kwa moyo wote au kuwa watiifu kwa Yehova inavyotakiwa. Mambo mengi yanawavuta watu tu kama hao “nyuma ya miaka michache mmoja katika taratibu ya kale,” kama tunavyoweza kusema. Namna gani juu ya watu kama hao nyuma ya miaka michache tu kutoka sasa? Je! watakuwapo? Wakati huo hakutakuwako taratibu ya kale yo yote hata kidogo, lakini ufalme wa Mungu utakuwa ukiongoza dunia kabisa na mambo yake. Tunaposhughulika na watu wakati huo, wote watakuwa ndugu zetu au watu wanaofundishwa kuishi katika taratibu mpya ya mambo. Sote tutaongozwa na sheria ya Yehova ya upendo. (Yak. 2:8) Kwa tumaini la uzima wakati huo, ni jambo la hekima kujizoeza na uchungaji na uangalizi wenye upendo wa waliowekwa wa Yehova katika kundi la Kikristo leo. (1 The. 5:12, 13) Hii kwa kweli itatupa mwanzo mzuri ajabu katika taratibu mpya ya mambo, ambapo hapatakuwa na masazo yo yote ya taratibu hii ya mambo hata kidogo. Kwa kweli, basi, kuna sababu za lazima kwa kila mmoja wetu kuja chini ya uangalizi wenye upendo wa kundi la Kikristo leo, kufanya kazi pamoja, kugeuza mioyo yetu na akili, kufanya rekebisho lo lote la kimwili, la moyoni au akilini na la kiroho linalotakiwa ili kumpendeza Yehova.—Rum. 12:1, 2.
25. Ni jambo gani linalowafanya watu wa Yehova kuwa umati wenye furaha namna hiyo leo?
25 Kwa kweli, kundi la Kikristo la Yehova ni la ajabu. Si kamilifu kabisa, lakini bila shaka limejitoa kabisa kwa Yehova na linaonyesha sifa zake za fadhili yenye upendo, rehema na haki. Hali chafu ya taratibu ya kale ya mambo ni ya kufisha. Hali safi ya taratibu mpya ya mambo ni ya kutoa uzima. Namna inavyotupasa sote kufurahi, vile vile na watu wanaopendezwa wanaopenda haki, kujua kwamba kupitia kwa uangalizi wenye upendo wa Yehova, Mwanawe-Mfalme Yesu Kristo, na kundi la “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” tunafundishwa, kutolewa makosa na kulindwa tunapotembea pamoja na kushirikana mmoja na mwenzake, tukisaidiana wenyewe kwa wenyewe kuingia katika taratibu mpya ya mambo kwa fadhili isiyostahili ya Yehova!
—Kutoka The Watchtower, Aug. 1, 1972.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa maelezo zaidi tazama sura ya kwanza, “Why Human Creation Will Yet Be Set Free,” katika kitabu cha Life Everlasting—in Freedom of the Sons of God.
[Picha katika ukurasa wa 66]
Kusaidia kusafisha Jumba la Ufalme ni mojawapo ya njia nyingi za kushirikiana na waangalizi waliowekwa