Je! Wewe Unamaliza Unachoanza?
Mambo ya hakika ambayo vijana wanataka kujua
NYINGI za furaha za kibinadamu zinakuja kupitia kwa utimilifu. Mtu anayeamua kujifunza kutumia chombo cha muziki, na kukaa nacho mpaka aweze, anapata furaha. Anayeacha mara tu nyuma ya kuanza hapati furaha hiyo.
Sawasawa na ufundi wa kazi za mikono, upasuaji wa mbao, useremala, ufundi wa mitambo, ushonaji wa cherehani, au kazi za kutumia akili, kama kujifunza lugha au hesabu. Katika kazi au mgawo wo wote, ukiutimiza, utapata uradhi na furaha kutokana nao.
Lakini, katika jambo hili la kumaliza tunachoanza, sisi sote tuna maelekeo ambayo tunapaswa tuyashinde.
PALIPO NA UGUMU
Kwa mfano, katika miaka yetu michache kama watoto tulikuwa tukikazia fikira jambo fulani kwa wakati mfupi tu. Hata katika mchezo fikira za mtoto hazikai pale kwa muda mrefu sana; zinavutwa kwa wepesi kuelekea upande mwingine.
Kadiri tunavyokua, uwezo wetu wa kukazia jambo fulani fikira unasitawi. Lakini zaidi ni sisi tunaopaswa kuusitawisha. Inafaa kwa sababu hii inaweza kugeuza kujifunza kwenye maumivu kuwe jambo lenye furaha.
Ili tuwe na uwezo wa kukazia jambo fikira inatupasa tuishinde tabia nyingine ya watoto wachanga: kutotulia. Kwa kawaida watoto wanataka vitu SASA! Na wanapojaribu kufanya jambo fulani mara chache, kwa jumla wanataka kuachana nalo ikiwa hawapati matokeo mema. Kufahamu kwamba mengine ya mambo yanayofaa zaidi yanachukua muda mwingi na bidii kuyapata kutakusaidia usikate tamaa kwa wepesi.
Tabia nyingine ya kushindwa ni ile ya kufanya mambo haraka haraka, kwa ghafula tu. Mithali 21:5 inatuambia: “Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu; bali kila mwenye pupa huuelekea uhitaji.” Kwa hiyo, mbele ya kuingilia kazi fulani au mgawo, kwanza hakikisha kwamba ni jambo linalofaa kabisa.
Nyakati nyingine jambo la busara kufanya ni kutomaliza unachoanza. Namna gani? Kwa sababu huenda yalikuwa maoni mabaya kutoka mwanzoni. Lengo linaweza kuwa baya, ambalo halipatani na kanuni za haki na mashauri ya Neno la Mungu.
Kwa upande mwingine, huenda lengo likawa si baya, lakini je! linakufaa wewe? Na je! lina ubora wa kutosha ili lichukue wakati na bidii kulitimiza? Je! wewe una sababu nzuri ya kuamini unaweza kulitimiza?
Yesu alisimulia juu ya mtu ambaye anaondoka akajenge mnara bila kwanza kufikiria gharama yake na kama anaweza kuitimiza au sivyo. Kama Yesu alivyosema, mtu huyo anaweza kuweka msingi halafu aone kwamba hawezi kuendelea, akiwafanya watazamaji wamcheke na kusema, “Mtu huyu alianza kujenga, akawa hana nguvu za kumaliza.” (Luka 14:28-30) Kwa hiyo, ikiwa unataka kumaliza unachoanza, hesabu gharama kwanza.
Linganisha faida zake na hasara zake. Waulize wengine maoni yao, zaidi wazazi wako. Jifaidi na ujuzi wao; wamekwisha kufanya makosa na wanaweza kukuepusha nayo. Biblia ni chanzo kikubwa cha mashauri yenye hekima na yanayofaa, Mfalme Sulemani, kwa mfano, alifanya karibu yote yawezayo kufanywa na mwanadamu kwa habari ya kutafuta furaha katika mambo ya kimwili. Anatupa matokeo: Ilikuwa ni “kujilisha upepo.” Kwa hiyo, sababu gani tufuate mwendo uo huo usiofaa?—Mhu. 2:3-11; linganisha 1 Timotheo 6:17-19.
Uhakika wa kwamba lengo lako kwa kweli linafaa unaweza kukusaidia kutokukata tamaa. Kupanga namna ya kutimiza lengo hilo ni kwa maana vile vile. Je! utatumia njia na hatua gani?
Vijana wengi wanashindwa kumaliza wanachoanza kwa sababu wanavunjika moyo. Wanaona kwamba kazi waliyoanza ni ngumu kuliko walivyodhani mbeleni. Au labda magumu au vizuizi visivyotazamiwa vinatokea kwa ghafula. Halafu nini?
Ni vyepesi kukata tamaa. Lakini hali hii inaonyesha wazi mtu ni mtu wa namna gani.
Ukiyaruhusu magumu yakujaze mawazo ya kutazamia mabaya, hii itakumaliza nguvu za kuendelea. Mithali 24:10 inasema: “Ukizimia siku ya taabu, nguvu zako ni chache.” Kuliko hivyo, ona hali yenyewe kama mwito. Ondoka upambane nayo kwa nguvu zaidi—fikira zaidi, jitihada na wakati zaidi. Mwito unaweza kuyafanya maisha yapendeze tusipoukimbia. Kwa kuushinda, unakua katika uhakika na busara. Ndipo unaweza kufanya kazi wakati ujao kwa uhakika na furaha zaidi.
Kwa hiyo epuka kukuza tabia mbaya au mfano wa utu wa kuacha kwa sababu tu inakuwa vigumu kuendelea. Ama sivyo, wakati mwingine mambo yatakapokuwa magumu, maelekeo yako yatakuwa ni kufanya vile vile, kuacha. Kwa kuzuia tabia hii isichipuke, unaweza kuyaepusha maisha yako yasiwe ya kushindwa kumaliza kazi.
MUNGU ANAWASHUKURU WANAOVUMILIA
Biblia inaonyesha kwamba Mungu anawatazamia watumishi wake waazimie kufanya mambo na kuyamaliza. Mfikirie Nuhu, Safina aliyoijenga pamoja na wanawe ilikuwa ni kitu kama sanduku lenye orofa tatu urefu wake ukiwa ni kama urefu wa nusu uwanja wa mpira. Haikuwa kazi ya kufanywa wakati wa mapumziko. Lakini kwa sababu aliitimiza kazi yenyewe, Nuhu na jamaa yake waliokoka Gharika na sisi, wazao wake, tunaishi leo.
Kati ya Wakristo, mtume Paulo anatupa mfano wa kweli wa kuazimia na wa busara. Kwake yeye, mgawo wake au utumishi ulikuwa ni hazina, wenye ubora wa kutosha kuvumilia namna zote za magumu ili kuutimiza. Yeye alikuwa na nia ya kuvumilia dhiki, taabu, mapigo, kupigwa mawe, kutiwa gerezani, kazi ngumu, kukosa usingizi, kiu, baridi na kukosa mavazi, kushitakiwa uongo, kuingia katika hatari, si kati ya adui wa kweli peke yao bali vile vile na kati ya wahalifu wa kawaida na hata wanyama wakali wa mwituni na nguvu za asili, alipokuwa akisafiri katika nchi kavu na baharini. (2 Kor. 6:3-10; 11:23-28) Kwa kuwa hakuwa mwoga, angeweza kweli kusema kwamba alikuwa ‘amevipiga vita vilivyo vizuri, kuumaliza mwendo, kuilinda imani.’ Alikuwa na uhakika wa kupata ushindi na kupokea thawabu iliyoahidiwa. (2 Tim. 4:6-8; Rum. 8:35-39) Je! wewe usingesema kwamba alikuwa mtu wa kufaa kuigwa?
KUKUZA UVUMILIVU UJANANI
Ujana ndio wakati wa kuanza kujenga mfano wa uvumilivu, wa kufanya mambo mpaka kuyamaliza. Katika shule, masomo mengine ni mepesi zaidi, mengine yanakupendeza zaidi kuliko mengine. Lakini ukitia bidii ile ile au hata zaidi kwa yale usiyoyapenda sana, unapata faida maradufu. Hupati ujuzi peke yake bali vile vile uwezo wako wa kukazia jambo fikira na kuazimia unauzidisha. Waalimu wengine wanasema kwamba jambo la maana zaidi tunalopata shuleni (masomoni) ni kujua namna ya kujifunza, namna ya kujitahidi wenyewe, kufanya uchunguzi wa habari, kuifahamu na kuizoelea.
Vile vile na kazi zo zote unazofanya usipokuwa shuleni. Kazi fulani zinavuta, nyingine hazivuti. Lakini unaweza kujifunza jambo fulani kutokana na kazi yo yote. Usiitazame kazi kwa juujuu kwa sababu ya faida unazoweza kupata papo hapo kama kuzoezwa, ufundi, au mshahara. Fikiria vile vile mageuzi inayoweza kukufanyia wewe kama mtu. Hata kazi ya ivi hivi, ya mshahara mdogo na ngumu inaweza kukufanya ukomae na kukuza nguvu zako za utu.
Jifunze uvumilivu vile vile katika ushirika wako mwenyewe. Ili kuwa wenye furaha kwa kweli imetupasa tuwe tunasikizana na wengine, kufanya kazi pamoja nao kwa matokeo mema, kuheshimiwa nao, na kuona kwamba wengine wanatufurahia. Huwezi kufanya hivyo ikiwa wewe u mwepesi wa kuchoshwa na watu, mwenye kuanza urafiki halafu kuuvunja mara tu usiposikizana na mwenzako au kuruhusu mkazo uvunje mipango ya kufanya kazi na wengine. Jichunguze mwenyewe. Je! wewe wakati mwingine huwakosei wengine? Je! unajichosha? Basi sababu gani uwe mwepesi wa kuchoshwa na wengine? Tumia wakati unaotakiwa kumaliza magumu kwa uvumilivu na nia, ukijikaza uyamalize kwa kutumia akili na busara. (Linganisha Mithali 14:29; 2 Timotheo 2:23, 24.) Kuweza kufanya hivyo ndiko kunaonyesha sababu ya kufanikiwa au kushindwa katika ndoa nyingi.
Ukihakikisha kwamba wewe si mwenye kushindwa upesi, kwamba wewe si mwoga, utatumainiwa na kuheshimiwa na wengine. Alipokuwa angali kijana, Timotheo “alishuhudiwa vema na ndugu” katika miji miwili mbalimbali. (Matendo 16:2) Hiyo ndiyo sababu mtume Paulo alimchagua kama msafiri mwenzake. Timotheo alikuwa na mapendeleo ya ajabu, kwenda pamoja na mtume katika sehemu nyingi za Milki ya kirumi. Nyuma ya karibu miaka kumi na miwili ya utumishi mwaminifu, alipewa madaraka mazito, akapewa uwezo wa kuwaweka waangalizi katika makundi. (Flp. 2:19-22; 1 Kor. 4:17; 1 Tim. 3:1-15) Hakuwa mwenye afya bora. (1 Tim. 5:23) Lakini alisikiza onyo la mtume ‘kudumu’ katika mambo aliyojifunza, ‘kutimiliza kabisa’ kazi aliyogawiwa, katika wakati ufaao na usiofaa, akijihakikisha mwenyewe askari wa kweli wa Kristo Yesu, mwenye nia ya kuvumilia magumu na masumbufu. (1 Tim. 4:11-16; 2 Tim. 4:2-5; 2:3) Ndiyo, Timotheo alikuwa wa kutegemewa kukaa katika mgawo wake na kufanya kazi mpaka kumaliza. Alikuwa mwanamume wa kutumainia. Lakini ilichukua muda na uvumilivu kutumainiwa vile.
Ndiyo, kwa kujihakikisha mwenyewe kuwa mtu anayefanya mambo na kuyatimiza, unaweza kupata mapendeleo na faida nyingi. Kwa kweli, uhai wenyewe uko hatarini kwa habari hii. Yesu alisema juu ya wafuasi wake: “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.” (Mt. 24:13) Tuko katika mbio za uzima wa milele kama watu wanaofurahia kibali cha Mungu. Tutapata zawadi hiyo kama tunasitawisha uwezo wa kufanya mambo na kuyamaliza, tukihakikisha uhodari wetu tunapokutana na magumu. Kwa kumaliza tunachoanza katika mambo madogo, tunaweza kuvumilia katika makubwa vile vile.—Luka 16:10; 1 Kor. 9:24-27; 2 Tim. 2:5.
Kwa hiyo ‘lo lote ufanyalo, fanya kwa moyo, kama kwa Yehova, wala si kwa wanadamu,’ kwa kuwa ni kutoka kwa Mungu utakakopokea zawadi iliyo ya maana kweli kweli.—Kol. 3:23, 24.