Je! Wewe Unachoshwa?
Mambo ya hakika ambayo vijana wanataka kujua
KUCHOSHWA ni ugumu wa kawaida kati ya vijana. Si kwamba wazee haiwapasi kupambana nao. Lakini mara kwa mara vijana wanajitamkia juu ya maisha ya nyumbani—au hata maisha kwa jumla—kama yenye kuchosha, yasiyopendeza. Sababu gani? Ni nini kinaweza kufanywa juu yake?
Kweli, taratibu ya mambo iliyopo sasa duniani imeondoa vitu vingi vya kupendeza, zaidi katika miji mikubwa. Hata hivyo, katika hali zile zile, kila mara kuna wengine wanaoweza kufurahia maisha, hali wengine wakichoshwa. Hii inaonyesha kwamba kuchoshwa zaidi kunategemea nia.
Chukua maisha ya nyumbani, kwa mfano. Kila jamaa ina utu. Kama vile mtu mmoja asivyoweza kuwa jamaa, vivyo hivyo, utu wa jamaa haufanyizwi na mtu mmoja lakini kwa njia ya kila mmoja kufanya jambo fulani kwa utu wote wa jamaa. Je! jamaa yako ikoje? Nyumba yako ni mahali penye uchangamfu? Je! mnafurahiana, mnakuwa na mazungumzo ya kupendeza nyakati za chakula, mnapata furaha katika kufanya mambo pamoja kwa kusaidiana? Au kila mmoja anafuata njia yake, bila kupendezwa na wengine? Je! ungetaka iweje?
Ni vyepesi kuwalaumu wengine kama mambo hayako namna tunavyotaka. Lakini mbele ya kulalamika, sababu gani usiulize: “Je! mimi mwenyewe ninaongeza nini kwa utu na roho ya jamaa? Je! ni bidii kadiri gani ninayoonyesha kuleta usitawi?” Ikiwa meli inajitahidi kwa nguvu kupita bahari zenye mawimbi baharia hasaidii cho chote kwa kuketi pembeni akilalamika. Ni shauri la wote katika meli kusaidiana ili meli ivuke bahari zenye mchafuko na kufika inakoelekea.
Mara kwa mara vijana waliochoshwa wanashindwa kuona faida ya mambo wanayopewa kufanya. Changanua migawo yako ya shule (masomo) na kazi unayogawiwa nyumbani. Elewa faida yake kwa kujaribu kuona namna yanavyokamatana na maisha yako (na maisha ya wengine) ya sasa na ya siku zijazo. Kama unaweza kufanya hivyo utaweza kufanya kazi katika migawo yako ukiwa na kusudi la kuitimiza. Hii inaweza kutofautisha kati ya kufurahia maisha na kuchoshwa.
Kwa kweli, kazi zile zile zinazoweza kutuchosha huenda zikatokeza sifa na tabia za maana—ambazo, mwishowe, zitasaidia sana katika matokeo mema kwetu ya siku zijazo katika maisha. Kwa mfano, je! kama kijana wa kiume umewahi kutengeneza ndege ya mfano? Kama ndivyo, ilikupasa kuunganisha sehemu zake zote kwanza halafu kuzifunika. Huenda zile sehemu hata zikakosa kuonekana nyuma ya kumaliza uunzi. Lakini bila nguvu na umbo lake, ndege ingekuwa haina maana. Au, kama msichana, je! umewahi kushona nguo? Mishono uliyoshona huenda haikuonekana nyuma ya kumaliza vazi lenyewe. Lakini bila nyuzi hizo zisizoonekana hilo lisingekuwa vazi.
Vile vile na mambo mengi tunayojifunza shuleni, au katika migawo yetu ya kazi nyumbani. Ni sehemu ya maoni kwa jumla na yanaweza kusaidia kuweka msingi kwa matokeo mema ya wakati ujao. Kwa kufanya kazi nyepesi zisizo za kusisimua, hata kwa kurudia-rudia, tunaweza kujifunza uvumilivu, ushupavu, na kupata nguvu za kindani.
Tusemeje basi? Kwamba kwa kweli hakuna jambo lo lote baya katika taratibu ya sasa inayoendelezwa na ulimwengu huu na kwamba ni shauri tu la kujipatanisha nayo? Sivyo hata kidogo. Kwa kweli, tumaini ambalo Biblia inatoa la kuona taratibu hii ya sasa ikimalizika na taratibu mpya yenye haki, yenye kuburudisha ikija—hili ndilo jambo linalotupa kichocheo kuvumilia. Vijana wanaweza kuwa na tumaini bora kuliko kuwa sehemu tu ya taratibu ya leo ya ulimwengu. Tumaini hili la taratibu bora ndilo vile vile linawazuia wazazi wengi wa Kikristo kutokuchoshwa na kazi yao ya kila siku, kwa kuwa wao, vile vile, wanakazwa na mikazo ya maisha ya siku hizi.
AKILI NA MAMBO MENGI YA KUPENDEZA
Mara kwa mara malalamiko yanayosikiwa nyakati za mapumziko ni, “Hakuna la kufanya.” Mara nyingi si kukosa mambo ya kufanya yenye kupendeza na yenye manufaa, bali ni kukosa akili, kuwaza. Au inaweza kuwa ni kupendezwa na mambo machache sana.
Taratibu iliyopo haitii moyo sana akili ya kutenda. Watu leo wamezoea kuwa watazamaji zaidi kuliko kuwa watendaji. Wanatazama sinema, vipindi vya televisheni, wanasikiliza muziki au kuwatazama wengine wakiwa katika mashindano ya michezo.
Hii ni vyepesi sana, kuliko kufanya mambo wewe mwenyewe, au kujifunza namna ya kufanya mambo. Lakini nyumaye vile vile kutazama kunaongeza kuchoshwa. Kunakufanya uwategemee sana wengine ufurahishwe; kunakufanya usiweze kujifanyia mambo mwenyewe ili maisha yako yawe ya kupendeza. Jambo hili ni sawa kwa vitoto—lakini si kwa vijana wa kiume na wa kike wanaoendelea kuwa watu wazima.
Je! kupendezwa kwako na mambo ni kwa kadiri gani? Kuna mambo mengi mazuri na namna za ujuzi zenye manufaa za kujifunza. Kusoma kunataka jitihada zaidi kuliko kutazama televisheni. Lakini kunaleta faida nyingi zaidi. Hakuna namna ya kazi, ujuzi au biashara, mahali au watu au wanyama ambayo haielezwi na vitabu. Kadiri unavyosoma ndivyo kupendezwa kwako kwa kusoma kunavyokuwa, ndivyo uwezo wako wa kushika ujuzi unavyokuwa. Lakini kusoma tu kuharakisha wakati (kwa sababu ni mwingi) hakutoshi. Inakupasa uamue jambo lenye manufaa. Ndipo unaweza kusoma ukiwa na shabaha akilini, ambayo inaweza kusitawisha siku za usoni katika maisha yako, kukutayarisha kufanya mambo.
Ndiyo, sisi tu watu mbalimbali. Si kila mmoja anayefurahia kufanya mambo yanayofurahiwa na wengine. Wengine wanafurahia kujifunza kufanya kazi kwa kutumia mbao, ngozi au chuma, hali wengine wanaweza kuchagua upigaji wa picha au kilimo cha mboga. Kati ya wasichana, wengine wanaweza kupenda kupika na kuoka mkate hali wengine wanapata furaha zaidi kutokana na kushona au kupamba nywele. Lakini kujifunza kufanya mambo mapya, halafu kusitawisha uwezo wa kufanya kazi bora, kunaleta uradhi wa kweli, kunaendeleza maisha ya kupendeza.
Unapoona ugumu kuwa mchangamfu juu ya kufanya jambo linalokupendeza, sababu gani usimfanyie mtu fulani jambo fulani? Kazi ambayo inaweza kuonekana kutokuvutia ikifanywa na wewe mwenyewe inaweza kuwa ya kupendeza kweli ukimfanyia mtu mwingine—mshiriki wa jamaa, rafiki au, zaidi ya hao, mtu anayetaka sana. Hii ni ya kuridhisha sana, na hakuna mwisho wa nafasi. Huenda jambo unalofanya halitazamiwi na yule mwingine. Mshangao wake utaongeza furaha yako katika kulifanya.
Kuwa ukipendezwa na wengine ni silaha yenye nguvu ya kushinda kuchoshwa. Watu wengi walio karibu nasi wana ujuzi wa kushangaza katika akili zao, vile vile na sifa nzuri mioyoni mwao—lakini hutajua isipokuwa unajitahidi kujua. Kama vile mithali isemavyo: “Mashauri ya moyoni ni kama kilindi; lakini mtu mwenye ufahamu atayateka.” (Mit. 20:5) Onyesha kupendezwa, uliza maulizo, chunguza kwa busara, zaidi kwa wale walio na miaka yenye ujuzi katika mambo yenye manufaa. Utathawabishwa kwa wingi na wakati utaenda kasi.—Mit. 27:9, 17.
Lakini zaidi ya unayoweza kupata kama faida kutoka kwa wengine, je! unaweza kupeana nini? Je! unajisemea mwenyewe, unashiriki na wengine uliyo nayo akilini na moyoni?
Vijana wanaoburudishwa kweli na ahadi ya Mungu ya mpango mpya na wanaoshiriki hizi habari njema na wengine wanaona kwamba hii inatoa maana zaidi kwa maisha zao. Ni jambo la kuthawabisha sana kuwapata watu, vijana au wazee, walio na njaa ya kweli na kuweza kuwasaidia. Ukweli wa kwamba ni wachache kuliko wale wanaoikataa kweli haupunguzi matokeo yenye kusisimua ya utendaji huu. Kuliko hivyo unaufanya uwe wenye kujaribu zaidi, hata wenye wasiwasi.
Washiriki wema vile vile wanasaidia kupambana na kuchoshwa. Lakini ikiwa washiriki wako ni wa namna ya wanaochoshwa wenyewe kwa sababu hawana lengo linalofaa katika maisha, watakuwa tu mzigo juu yako, wakikuzuia kuendeleza akili yako ya kutenda na nguvu za kindani. Wao ni kama wapumbavu wanaosemwa katika Mithali 17:24, walio na macho yao “katika ncha za dunia,” wakichukuliwa na mawazo mpaka kwenye mambo ya mbali, mawazo yao yakitangatanga hapa na pale, lakini bila lengo imara mbele yao.
Pamoja na akili ya kutenda, uvumilivu na imani ni misaada mikubwa kwa kushinda kuchoshwa. Kama vile mtume Paulo anavyosema juu ya utumishi wetu kwa Mungu na kwa wale wanaomtumikia, “Tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.” (Gal. 6:9) Vivyo hivyo, tunapojaribu kuendeleza uwezo ulio na kusudi fulani la kweli na wenye faida, inatupasa kuendelea mpaka tuanze kuvuna mengine ya matunda ya kazi zetu.
Ndipo, kadiri wakati unavyopita, tutakapoweza kuongeza uchunguzi wetu wa uwezo mwingine zaidi wa kusitawishwa, tukiwa na uongozi wa wazazi unaofaa na kibali, na tutakuwa watu bora, wenye kupendeza zaidi na wanaofaa zaidi kama matokeo. Tukiwa wenye tumaini angavu kwa wakati ujao, maisha hayatakuwa ya kuchosha.