Mungu ‘Hakufariki’
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1. Waalimu wa dini wanasema wana maana gani kwa kusema, “Mungu amefariki”?
WEWE unafikirije wakati unaposikia mapadre wakisema “Mungu amefariki”? Wengine kati ya waalimu wakubwa wa dini wanaosema hivyo wanaeleza kwamba kwa kusema hivyo hawamaanishi kwamba Mungu hajapata kuwako wakati wo wote. Ila, kusema kwao hivyo kuna maana ya kwamba Mungu ‘hayumo katika historia ya kisasa.’ Waalimu hawa wa dini wanasema kwamba yeye hapendezwi na mambo ya wanadamu na anaridhika kuwaacha wakifuata njia yao wenyewe bila kizuizi au msaada kutoka kwake Yeye.
2. Filosofia hii inageuza namna gani mwendo wa tendo wa wale wanaoiamini?
2 Wale wanaosadiki filosofia hiyo basi wanaona kwamba, hata wafanye nini, Mungu hatawahukumu. Wanafikiri kwamba Mungu haoni wanayofanya, au ikiwa anaona, yeye hajali sana kuchukua hatua yo yote.
3, 4. Sababu gani hakuna msamaha kwa mapadre wanaosema “Mungu amefariki”?
3 Inaonekana kama jambo lisilosadikika kwamba viongozi wa kidini katika mataifa yanayojiita yenyewe ya “Kikristo” wanakuwa na moyo huu. Wanayo Biblia, na wako karibu na maandishi ya historia. Wanaweza kutazama vitu vya asili vilivyoumbwa. Bila shaka wanajua kwamba Mungu anayetumia uangalifu huo katika kuumba na aliyetoa kitabu chenye kweli na chenye kanuni bora, kama Biblia, ni Mungu ambaye anapendezwa sana na kuumba kwake. Tena, Biblia inatoa mifano mingi ya kushughulika kwake na wanadamu na ahadi nyingi na unabii mwingi unaoonyesha namna anavyoangalia na kupendezwa na watu wanaoishi leo.
4 Ili wale wanaomwamini Mungu wasitumbukie katika moyo wa upumbavu wa viongozi hawa wa kidini, Yehova kupitia kwa nabii wake Ezekieli anatoa masimulizi juu ya watu wa zamani waliofikiri kama mapadre hawa wanavyofikiri. Anaonyesha matokeo mabaya ya kufikiri huko—mambo mabaya sana ambayo kwa hayo kufikiri huko kuliongoza.
NJOZI YA PILI YA EZEKIELI JUU YA YEHOVA
5, 6. (a) Ni wakati gani na ni wapi ambako Ezekieli aliona njozi yake ya pili ya Yehova? (b) Wakati wazee wa Yuda walipokuwa wakingojea, Ezekieli aliona nini katika njozi?
5 Ezekieli alikuwa katika Babeli. Ulikuwa mwaka wa 612 B.C.E., zaidi ya mwaka mmoja tangu njozi yake ya kwanza, ambayo katika hiyo aliona gari la kimbinguni la Yehova likielekea Yerusalemu. Ezekieli alikuwa katika nyumba yake katika Telabibu, na wazee wa Yuda wameketi mbele yake, ili wajue ujumbe ambao angekuwa nao ili kuwaambia. Wakati watu hawa walipokuwa wakingojea, Ezekieli aliona njozi ifuatayo:
6 “Ndipo nikaangalia, na tazama, kana kwamba ni mfano wa moto; tangu mfano wa viuno vyake na chini, moto; na tangu mfano wa viuno vyake na juu, kana kwamba ni mfano wa mwangaza, kama rangi ya kaharabu. Naye akanyosha mfano wa mkono, akanishika kwa kishungi kimoja cha nywele za kichwa changu; nayo roho ikaniinua kati ya dunia na mbingu, ikanileta katika maono ya Mungu mpaka Yerusalemu, mpaka mlango wa kuingilia ua wa ndani uelekeao upande wa kaskazini; mahali palipokuwa pamewekwa sanamu ya wivu, itiayo wivu. Na tazama, huo utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwapo hapo, sawasawa na maono yale niliyoyaona katika uwanda.”—Eze. 8:2-4.
7. Je! kusafirishwa kwa Ezekieli Yerusalemu kulikuwa kwa kweli au kwa njozini?
7 Ilikuwa vigumu kwa Ezekieli kueleza namna Yehova alivyoonekana katika njozi hii, maana kuonekana huko hakukuwa kule kwa mfano wa mwanadamu, lakini kulikuwa kwa kuogofya na utukufu mwingi. Ezekieli aliinuliwa kwa nywele za kichwani akapelekwa kwa roho yenye uongozi apate kuona, katika njozi hii, yaliyokuwa yakitukia katika Yerusalemu mamia ya maili kuelekea magharibi.
8. (a) Ezekieli alipelekwa wapi katika njozi? (b) “Sanamu ya wivu” ilikuwa nini?
8 Ezekieli alifikishwa penye lango la ua wa ndani wa hekalu, penye lango la kaskazini. (Hekalu lenyewe lilielekea mashariki.) Lilikuwa lango lenye kuongoza kwenye madhabahu ya dhabihu. Mahali hapa aliona kitu cha kuchukiza sana: “sanamu ya wivu” isiyo na uhai, isiyotembea. Hii ilikuwa namna fulani ya sanamu ya kuabudiwa. Labda ilikuwa “ashera” au nguzo takatifu ikiwa mfano wa mungu mke wa uongo—mungu mchafu wa kike wa mambo ya kiume na ya kike—aliyekuwa mke wa mungu Baali wa Wakanaani.
“SANAMU YA WIVU”
9, 10. Halafu Yehova alisema kwa Ezekieli kutoka wapi, na alisema nini?
9 Ndipo Yehova alipoanza kusema kutoka gari lake, ambalo sasa lilikuwa limesonga kwa kuogofya kuelekea Yerusalemu ili kutekeleza hukumu juu ya mji ule. Ezekieli anatuambia hivi:
10 “Ndipo akaniambia, Mwanadamu, inua macho yako sasa, uangalie upande wa kaskazini. Basi nikainua macho yangu, nikaangalia upande wa kaskazini, na tazama, upande wa kaskazini wa mlango, ilikuwako sanamu ile ya wivu, mahali pale pa kuingilia. Akaniambia, Mwanadamu, je! unayaona wanayoyafanya, yaani, haya machukizo makubwa wanayoyafanya nyumba ya Israeli hapa, hata niende zangu mbali na patakatifu pangu? lakini utaona tena machukizo makubwa mengine.”—Eze. 8:5, 6.
11. Sababu gani tendo la viongozi wa dini wa Yerusalemu lilikuwa ‘chukizo,’ na kwa hiyo Mungu aliona lazima ya kufanya nini?
11 Viongozi wa kidini wa Yerusalemu walikuwa wamevunja za kwanza mbili za Amri Kumi, na walikuwa wakifanya ‘chukizo.’ Hekalu lilikuwa mahali ambapo kwa mfano Mungu alikaa pamoja na Israeli kama taifa lililojitoa kwa ibada yake. Na hekalu likiwa limetiwa unajisi kwa ibada yenye kutapisha ya hii “sanamu ya wivu” ambayo kwa hiyo Wayahudi walimtia Yehova wivu, je! hekalu hilo lilikuwa mahali panapofaa yeye kukaa? Hata kidogo! Yehova hakuwa na lazima ya kukaa humo. Kuliko kukaa humo, aliona lazima aondoe kuwapo kwake kwa kiroho; kama alivyosema, “niende zangu mbali na patakatifu pangu.”
12-14. Toa mfano wa Kristendomu akifanya “machukizo” mahali ambapo wanajidai kuwa patakatifu pa Mungu.
12 Je! Kristendomu, ambaye ndani yake wamo wale wanaosema, “Mungu amefariki,” amefanya vivyo hivyo? Ebu angalia yaliyotukia katika kanisa la St. Clement’s Episcopal Church mjini New York, katika Desemba wa 1971. Katika toleo lake la Januari 3, 1972, gazeti la Time lilitoa ripoti hivi:
13 “Maonyesho yaliendelea katika orofa ya mahali patakatifu. Upande mmoja, vijana watatu walio uchi walijitupa kwa furaha majini katika kiziwa cha maji cha watoto wachanga. Upande mwingine, Mchezaji Kevin O’Connor (Tom Paine) alifanya mchezo wa chombo cha kuogea kutokana na mchezo Chicago wa Sam Shepard, mchezo wenye kukatisha tamaa na wa kuzaliwa upya. Penye birika ya maji, akina mama wawili walizungumza juu ya sabuni gani iliyokuwa safi kuliko zote.”
14 Lo! mzaha gani! Uharibifu gani wa mafundisho safi, yenye unyofu ya Kristo! Haya ndiyo matokeo ya kudharau Neno la Mungu Biblia na ya kutumia sanamu, mifano na mafundisho yanayoondoa washiriki wa kanisa kutoka katika kumwabudu Mungu peke yake ambaye wanajidai kutumikia.
YEHOVA YUKO HAI NA ANAONA SANA YANAYOTENDEKA
15-17. (a) Maneno ya Yehova kwa Ezekieli: “Lakini utaona tena machukizo makubwa mengine,” yanatumikaje kwa Kristendomu vile vile? (b) Viongozi hao wa Kiyahudi walisema nini juu ya kujua kwa Mungu waliyotenda? (c) Ni juu ya msingi gani walitoa udhuru kwamba Yehova hakuwaona?
15 Wakati Ezekieli alipochukuliwa katika utalii wa njozini wa kutazama, Yehova alimwambia hivi, “Lakini utaona tena machukizo makubwa mengine.”
16 Vile vile, katika Kristendomu, mtazamo huo mfupi hauwezeshi kuona machukizo yote yanayofanyika katika makanisa ya Kristendomu. Huko nyuma katika njozi ya Ezekieli, mambo haya yalifanywa na wakuu wa watu waliowekwa. Kama mapadre leo wanaosema, ama kwa matendo ama kwa maneno, “Mungu amefariki,” viongozi hao walifikiri hivi, “[Yehova] hatuoni; [Yehova] ameiacha nchi hii.”—Eze. 8:12.
17 Labda viongozi hao wa Kiyahudi walidhani ya kwamba Yehova alikuwa ameonekana kama “ameiacha nchi hii” kwa sababu Yerusalemu na Ufalme wa Yuda ulikuwa umepata taabu nyingi mno majuzi mikononi mwa Wababeli. Kwa kweli walikuwa wakisema jambo lile lile ambalo mapadre wanasema sasa.
18. Mungu alijua waliyokuwa wakifanya, na aliangalia nini juu yao?
18 Kwa sababu watu hawa wa Yuda hawakumwona Mungu akichukua hatua katika mambo yao, je! walikuwa na maana kwamba Mungu hakujua? Hapana. Alijua sana waliyokuwa wakifanya. Kwa sababu tu hakufanya walilofikiri lilipaswa lifanywe, yaani, kutenda ili kuokoa Yerusalemu, hiyo haikuwa na maana kwamba yeye alikuwa haangalii. Bali, yeye aliangalia hukumu yake kwamba waharibiwe kwa matendo yao yenye kuchukiza sana!
19. Matukio yaliyofuata yalifunuaje kwamba Yehova aliona na aliangalia?
19 Hata wakati huo, Yehova alitumia uvumilivu. Lakini miaka mitano iliyofuata alimwongoza mfalme wa Kibabeli Nebukadreza kwenda kushambulia Yerusalemu. (Eze. 21:18-23) Ikiwa unasoma kitabu cha Biblia cha Maombolezo ya Yeremia, zaidi sura ya pili na ya nne, utaona kwamba msiba uliokuja juu ya Yerusalemu unasemekana kuwa hukumu ya Yehova kwa sababu ya matendo yake yenye kuchukiza sana. Kwa hakika Wayahudi, wale waliookoka mazingiwa na vile vile wale waliokuwa katika Babeli, hawakusema wakati huo, “[Yehova] hatuoni, [Yehova] ameiacha nchi hii.”
20. Mungu anapendezwa na nini zaidi wakati huu?
20 Kutokana na habari hii ya kihistoria tunaweza kufahamu kwamba kuna hatari kubwa inayokaribia kwa kuogofya juu ya Kristendomu. Mungu anaishi, na anapendezwa sana na jina lake na ibada yake mwenyewe ya kweli. Vile vile anapendezwa na watu wote ‘wanaoamini kwamba yeye yuko, na kwamba anawapa thawabu wale wanaomtafuta yeye.’—Ebr. 11:6.
21. Watu wanaochukizwa na yanayotendeka katika Kristendomu imewapasa wafanye nini?
21 Je! wewe unachukizwa sana na mambo yenye kutapisha ambayo mapadre, wakifuatwa na washiriki wengi wa kanisa, wamefanya? Basi usishirikiane hata kidogo na watu hao bali mpe Mungu ibada ya pekee. Utahakikisha kwamba yeye anaona na kweli atawapa zawadi wale wanaomtumaini yeye kama Mungu aliye hai.
—Kutoka Kitabu “The Nations Shall Know that I Am Jehovah”—How?