Biblia Inasema Nini Kuhusu Vita vya Nyuklia?
Mataifa yenye nguvu ulimwenguni yana akiba ya silaha za nyuklia na yanaendelea kutengeneza silaha zaidi. Kwa sababu hiyo, tishio la kutokea kwa vita vya nyuklia linazidi kuongezeka. Watu wana wasiwasi kwamba silaha za nyuklia zikiendelea kuongezeka, uwezekano wa vita vya nyuklia kutokea utakuwa mkubwa hata zaidi. Wanahisi kwamba ikiwa nchi moja itatumia hata bomu moja dogo tu la nyuklia, hilo litaanzisha vita vya nyuklia ambavyo vitaangamiza ulimwengu wetu. Shirika la Bulletin of the Atomic Scientists linasema kwamba, leo “kuna uwezekano mkubwa wa vita vya nyuklia kutokea.”
Je, kuna uwezekano wa vita vya nyuklia kutokea? Ikiwa ndivyo, je, sayari yetu itaokoka? Tunawezaje kukabiliana na hofu ya kutokea kwa vita vya nyuklia? Biblia inasema nini?
Katika makala hii
Unawezaje kukabiliana na hofu ya kutokea kwa vita vya nyuklia?
Je, Biblia ilitabiri kwamba Har-Magedoni ni vita vya kinyuklia?
Je, kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinarejelea vita vya nyuklia?
Je, Biblia ilitabiri kuhusu kutokea kwa vita vya nyuklia?
Biblia haitaji kihususa kuhusu vita vya nyuklia. Hata hivyo, tishio la vita vya nyuklia linatokana na matukio na mitazamo ya watu ambayo Biblia ilitabiri.
Linganisha yale yanayotajwa katika mistari ifuatayo ya Biblia na matukio yaliyo ulimwenguni leo:
Mistari ya Biblia: Wanafunzi wa Yesu walimuuliza:“Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Naye Yesu akawajibu:“Taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.”—Mathayo 24:3, 7.
Matukio ya ulimwengu: Nchi mbalimbali mara nyingi huamua kujihusisha katika vita, na hili linatia ndani nchi zenye uwezo wa kinyuklia.
“Katika miaka ya hivi karibuni matukio ya ukatili yameongezeka ulimwenguni: migogoro pia imeongezeka sana.”—Shirika la Armed Conflict Location & Event Data Project.
Mstari wa Biblia: “Wakati wa mwisho mfalme wa kusini atasukumana [na mfalme wa kaskazini].”—Danieli 11:40.
Matukio ya ulimwengu: Mataifa yenye nguvu pamoja na mataifa mengine yanayoyaunga mkono yanashindania mamlaka kama tu Biblia ilivyotabiri. Ingawa mataifa yenye nguvu na yenye silaha za nyuklia yanaweza kuepuka migogoro ya moja kwa moja, bado yanaendelea kutengeneza na kuboresha silaha zao za nyuklia.
“Tumejionea ongezeko la migogoro kati ya mataifa katika miaka kumi iliyopita, kutia ndani mataifa yenye nguvu kuunga mkono pande tofauti.”—Shirika la Uppsala Conflict Data Program.
Mistari ya Biblia: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa . . . wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali.”—2 Timotheo 3:1-3.
Matukio ya ulimwengu: Kama ilivyo kwa watu wengi leo, viongozi wa mataifa pia hutofautiana. Hata hivyo, badala ya kusuluhisha tofauti zao kwa njia ya amani, wao wanatumia vitisho au nguvu. Wanapofanya hivyo, wanazidisha uwezekano wa vita vya nyuklia kutokea.
“Ikiwa mataifa hayatapata njia inayofaa ya kusuluhisha matatizo yao, migogoro inayoweza kusababisha uharibifu mkubwa itazidi kuongezeka.”—S. Saran na J. Harman wa Shirika la World Economic Forum.
Je, Mungu ataruhusu vita vya nyuklia vitokee?
Biblia haisemi. Hata hivyo, inataja kwamba “mambo yenye kuogopesha,” au mambo yenye kushtua yangetokea katika siku zetu. (Luka 21:11) Mfano wa matukio kama hayo ni mabomu ya atomu yaliyoangushwa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Biblia inafafanua kwa nini Mungu anaruhusu vita viendelee kuwepo. Ili kujifunza mengi zaidi, tazama video Kwa Nini Mungu Anaruhusu Kuteseka?
Je, Dunia itaokoka?
Ndiyo. Hata ikiwa wanadamu watatumia silaha za nyuklia tena, Mungu hataruhusu hali ziwe mbaya sana hivi kwamba waiharibu dunia kabisa. Biblia inasema kwamba sayari yetu haitaangamizwa bali wanadamu wataendelea kuishi humo milele.
Baadhi ya watu wanafikiri kwamba wakati ujao dunia itabaki na watu wachache tu watakaokuwa wakipambana kuishi katika hali ngumu kwa sababu ya madhara ya vita vya nyuklia. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba uharibifu wowote unaotokea duniani ambao unasababishwa na vita utaondolewa.
Mungu anataka tuishi kwa furaha katika dunia maridadi
Muumba wetu aliiumba dunia ikiwa na uwezo wa kujirekebisha. Isitoshe, tunajua kwamba Mungu atatumia nguvu zake kuirekebisha dunia ili iwe kama ilivyokuwa awali; dunia itakuwa maridadi na itakaliwa na wanadamu milele.—Zaburi 37:11, 29; Ufunuo 21:5.
Unawezaje kukabiliana na hofu ya kutokea kwa vita vya nyuklia?
Huenda baadhi ya watu wakawa na hofu kwamba vita vya nyuklia vitatokea na kusababisha madhara makubwa. Ahadi za Biblia zinaweza kuwasaidia wale ambao wameathiriwa na hofu hiyo kukabiliana na hisia hizo na kupunguza woga wao. Jinsi gani?
Biblia inaeleza kwamba wakati ujao hali zitakuwa nzuri duniani na wale watakaoishi humo watafurahia maisha. Kujifunza kuhusu tumaini hilo kunaweza kuwa kama “nanga ya uhai wetu” na kutupunguzia wasiwasi. (Waebrania 6:19, maelezo ya chini) Pia, tunaweza kupunguza wasiwasi kwa kukazia fikira mambo yaliyopo sasa badala ya kukazia fikira mambo yanayoweza kutokea wakati ujao. Kama Yesu alivyosema, “kila siku ina matatizo yake ya kutosha.”—Mathayo 6:34.
Ni muhimu pia tutunze afya yetu ya akili na ya kihisia. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuepuka kusoma, kutazama, au kusikiliza taarifa zinazosababisha wasiwasi kama vile mazungumzo, utabiri, au maoni ya watu kuhusu maendeleo ya karibuni zaidi ya kinyuklia. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba tunapuuza uhalisia wa mambo. Badala yake, tunafanya yote tunayoweza ili kuepuka kukazia fikira mambo ambayo yanaweza kutuletea wasiwasi. Ukweli ni kwamba, hatuwezi kudhibiti mambo hayo na huenda hata yasitokee.
Jipatie muda wa kufikiria mambo mazuri unayofurahia maishani mwako badala ya kukazia fikira habari mbaya tu kila wakati.
Biblia inatoa tumaini hakika kwamba kutakuwa na wakati ujao mzuri
Kujifunza mengi zaidi kuhusu ahadi za Mungu kutakupatia tumaini, shangwe, na amani ya moyoni.
Je, Biblia ilitabiri kwamba Har-Magedoni ni vita vya nyuklia?
Watu fulani hufikiri kwamba Har-Magedoni ni vita vya nyuklia vitakavyopiganwa ulimwenguni pote. Na wanahofia uharibifu unaoweza kutokana na tukio kama hilo.
Hata hivyo, Biblia inatumia neno “Har-Magedoni” kurejelea vita vya “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa,” au serikali za wanadamu, dhidi ya Mungu.a (Ufunuo 16:14, 16) Mabomu ya nyuklia yanawaangamiza watu wazuri na wabaya na kuharibu kila kitu katika sehemu ambayo yanaangushwa. Hata hivyo, katika vita vya Har-Magedoni, Mungu atawaangamiza watu waovu tu, na hilo litaleta amani na usalama wa kweli.—Zaburi 37:9, 10; Isaya 32:17, 18; Mathayo 6:10.
Biblia inatoa suluhisho gani kuhusu vita?
Yehovab Mungu ataonyesha mamlaka yake dhidi ya mataifa kwa kukomesha migogoro yao na kuharibu silaha zao. Atafanya hivyo kupitia Ufalme wake, ambao ni serikali ya mbinguni itakayotawala dunia yote.—Danieli 2:44.
Ufalme wa Mungu utawafundisha watu jinsi ya kuishi kwa amani na upatano. Kwa sababu dunia yote itatawaliwa na serikali moja tu, hakutakuwa na migogoro ya kimataifa na watu hawatajifunza vita tena kamwe! (Mika 4:1-3) Matokeo yatakuwa nini? “Kila mtu atakaa kwa amani chini ya mitini na mizabibu yake, bila kutishwa na mtu yeyote.”—Mika 4:4, Biblia Habari Njema.
a Ona makala yenye kichwa “Vita vya Har-Magedoni Ni Nini?”
b Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?”