Je, Harakati za Kulinda Amani Zinaweza Kuleta Amani ya Kudumu Duniani?
Vita na migogoro kati ya mataifa inaendelea kuongezeka ulimwenguni. Umoja wa Mataifa na mashirika mengine yamekuwa yakiendeleza harakati za kulinda amani.a Kwa mfano, wamewaweka wanajeshi katika maeneo ambayo yana migogoro. Wanatumaini kwamba kwa kufanya hivyo, wataleta amani katika maeneo haya. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, alisema kwamba, “Vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Mataifa vinafanyiza sehemu muhimu zaidi ya jitihada za Umoja wa Mataifa za kuleta amani ulimwenguni.”
Harakati za kulinda amani zimekuwepo kwa miaka mingi na zimekuwa na mafanikio kwa kiasi fulani. Kwa mfano, vikosi vya kulinda amani vimelinda raia, vimewarudisha wakimbizi katika nchi zao, vimetoa misaada, na kujenga upya miundo-mbinu ambayo ilikuwa imeharibiwa. Hata hivyo, harakati za kulinda amani zimekumbwa na changamoto kubwa ambazo zinafanya iwe vigumu kuendelea kulinda amani. Je, inawezekana kupata suluhisho la kudumu ambalo litaleta amani ya kweli katika ulimwengu wetu? Je, Biblia ina majibu?
Changamoto za kulinda amani, na suluhisho ambalo Biblia inatoa
Changamoto: kukosa ushirikiano. Katika visa vingi, inakuwa vigumu kwa wanajeshi na mashirika mbalimbali yanayotoka nchi tofauti kushirikiana. Nyakati nyingine inakuwa vigumu kwa mashirika hayo kufanya kazi kwa upatano kwa sababu masilahi yao yanatofautiana au hawaelewani.
Suluhisho la Biblia: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme . . . na kuzikomesha falme hizi zote [serikali za wanadamu], nao pekee utasimama milele.”—Danieli 2:44.
Hivi karibuni, Mungu atakomesha vita na kuleta amani katika dunia yote. (Zaburi 46:8, 9) Ataondoa serikali zote za wanadamu duniani na kusimamisha serikali moja: Ufalme wa Mungu. Serikali hiyo kamilifu itakapoanza kuitawala dunia, hakutakuwa na migogoro tena, na hivyo hatutahitaji mashirika ya wanadamu ya kulinda amani.
Changamoto: uwezo mdogo na rasilimali chache. Mara nyingi mashirika yanayolinda amani hayana watu wa kutosha wa kufanya kazi, pesa za kutosha, au vitu vingine vinavyohitajika ili kufanikisha kazi yao. Isitoshe, watu wanaofanya kazi ya kulinda amani wanafanya kazi katika mazingira yanayoendelea kuwa magumu zaidi na hatari zaidi.
Suluhisho la Biblia: ‘Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo . . . alimketisha [Yesu] kwenye mkono wake wa kuume katika mahali pa kimbingu, juu kuliko kila serikali na mamlaka na nguvu.’—Waefeso 1:17, 20, 21.
Mungu Mweza-yote, Yehova,b amempatia Yesu, Mfalme aliyechaguliwa wa Ufalme wa Mungu, vitu vyote anavyohitaji ili atawale kwa mafanikio. (Danieli 7:13, 14c) Mungu amempatia Yesu ujuzi, hekima, utambuzi, na nguvu nyingi. Hakuna serikali au shirika lolote la wanadamu lililo na uwezo kama huo. (Isaya 11:2) Yesu pia ana jeshi kubwa la malaika analoweza kulitumia. (Ufunuo 19:14) Hakuna hali yoyote ngumu inayoweza kumshinda.
Yesu atatumia vitu vyote na uwezo wote ambao Mungu amempatia ili kuondoa migogoro, na kuleta utulivu, usalama, na amani ya kudumu kwa wote watakaoishi chini ya Ufalme wa Mungu.—Isaya 32:17, 18.
Changamoto: vikwazo vya kisheria. Nyakati nyingine, watu wanaofanya kazi ya kulinda amani wanakabili wakati mgumu kwa sababu wanapewa maagizo yasiyo ya wazi. Kwa hiyo, huenda wasijue wanachoruhusiwa kufanya au wanachotazamiwa kufanya. Maagizo hayo yanafanya iwe vigumu kwao kutimiza majukumu na malengo yao kikamili na kuwalinda wengine.
Suluhisho la Biblia: ‘[Yesu] amepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.’—Mathayo 28:18.
Mungu amempatia Yesu jukumu la kuleta amani duniani na mamlaka kamili ya kuhakikisha hilo linatendeka. (Yohana 5:22) Kamwe, Yesu hatatenda isivyo haki au kuwa mfisadi. (Isaya 11:3-5) Hiyo ndiyo sababu Biblia inamwita Yesu “Mkuu wa Amani” ambaye msingi wa Ufalme wake ni “haki na uadilifu.”—Isaya 9:6, 7.
Ufalme wa Mungu utaleta amani ya kweli
Mashirika ya wanadamu ya kulinda amani yanaweza kuleta amani kwa kiwango fulani, au hata kuzuia vita visiendelee katika eneo fulani. Hata hivyo, hayawezi kuondoa chanzo halisi cha migogoro, yaani, chuki ambayo watu wanahisi kuwaelekea wengine.
“Changamoto ya msingi ni kwamba amani inayopaswa kulindwa haipo.”—Dennis Jett, balozi wa zamani wa Marekani.
Kwa upande mwingine, Ufalme wa Mungu ni serikali inayoweza kuleta amani ya kweli kwa sababu inawasaidia watu kuondoa chuki moyoni mwao. Kwa mfano, Yesu alipokuwa duniani, aliwafundisha wafuasi wake kwa maneno na matendo jinsi ya kufanya amani na kuwaonyesha wengine upendo:
Yesu alisema kwamba raia wa Ufalme wa Mungu watajulikana kwa upendo wanaowaonyesha wengine. Biblia inaonyesha wazi kwamba wale wanaowachukia wengine hawataishi chini ya Ufalme wa Mungu:
Yehova Mungu, aliyewaumba wanadamu, anajua njia bora—njia pekee—ya kuleta amani duniani. Ufalme wake utafanya mambo yote ambayo wanadamu wameshindwa kufanya, kutia ndani kuleta amani.
a Umoja wa Mataifa na mashirika mengine hutumia maneno mengine kama vile, “kurejesha amani,” “kuleta amani,” “kurudisha amani,” na “operesheni za ulinzi wa amani” kuwasilisha wazo hili.
b Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?”
c Kwenye Danieli 7:13, 14, neno “mwana wa binadamu” linamrejelea Yesu Kristo.—Mathayo 25:31; 26:63, 64.