ENDELEA KUKESHA!
Unawezaje Kuwa na Furaha Maisha Yanapokuwa Magumu?—Biblia Inasema Nini?
Katika nyakati hizi zenye misukosuko, hatuwezi kudhibiti mambo yote ambayo huenda yakatupata. Hata hivyo, licha ya hali tunazokabili tunaweza kuwa na furaha au kukosa furaha ikitegemea mtazamo wetu. Biblia inasema kwamba watu wenye furaha “huwa na karamu daima.” (Methali 15:15) Tunaweza kufanya nini ili tuwe na furaha zaidi? Chunguza jinsi ushauri wa Biblia unavyoweza kukusaidia.
Kukabiliana na mahangaiko
Biblia inasema: “Mahangaiko yaliyo moyoni mwa mtu huulemea moyo, lakini neno jema huuchangamsha.”—Methali 12:25.
Biblia inaweza kukusaidia kukabiliana na mahangaiko. Ili kujua jinsi inavyoweza kukusaidia, soma makala “Biblia Inasema Nini Kuhusu Mahangaiko.”
Kukabiliana na upweke
Biblia inasema: “Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”—Methali 17:17.
Biblia ina ushauri unaoweza kukusaidia kuimarisha urafiki pamoja na wengine, jambo ambalo litakusaidia kushinda upweke. Soma makala “Shinda Upweke kwa Urafiki—Biblia Inaweza Kusaidiaje.”
Sitawisha upendo kwa Mungu na kwa jirani
Biblia inasema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote. . . . Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.”a—Mathayo 22:37-39.
Sala inaweza kutusaidia kuwa karibu zaidi na Mungu. Ili ujifunze mengi zaidi soma makala “Je, Mungu Husikiliza Sala Zetu?”
Tunaonyesha tunawapenda wengine tunapowatendea kama Yesu alivyofundisha. Jifunze mengi zaidi katika makala “Yesu Alisema Tunapaswa Kuwatendeaje Wengine?”
Ili ujifunze zaidi kuhusu jinsi Biblia inavyoweza kukusaidia kuwa na furaha katika nyakati hizi ngumu, tunakualika ujifunze Biblia bila malipo.
a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.—Zaburi 83:18.