AGOSTI 3-9, 2026
WIMBO 113 Amani Tuliyo Nayo
Heshimu Maamuzi ya Wengine
“Msihukumu kuhusu maoni yanayotofautiana.”—ROM. 14:1.
JAMBO KUU
Jinsi ya kuwaonyesha heshima waabudu wenzetu wanapofanya maamuzi ambayo hatukubaliani nayo.
1-2. Kwa nini maamuzi yetu ya kibinafsi mara nyingine yanatofautiana na ya Wakristo wenzetu?
JE, UMEWAHI kuhisi kwamba watu wamekuhukumu vibaya kwa sababu ya uamuzi uliofanya? Je, umewahi kumhukumu Mkristo mwenzako kwa sababu ya uamuzi aliofanya? Bila shaka, wengi wetu tunaweza kujibu ndiyo inapohusu maswali hayo mawili.
2 Hatupaswi kushangazwa kwamba mara nyingine maamuzi yetu yatatofautiana na ya Wakristo wenzetu waaminifu. Kwa nini? Kwa sababu sisi sote tuko tofauti. Kila mmoja wetu ana maoni tofauti. Njia yetu ya kufikiri imeathiriwa na utamaduni wetu, malezi, na mambo tunayopitia maishani. Lakini hatupaswi kuruhusu maoni yetu tofauti yahatarishe amani na umoja kutanikoni.—Efe. 4:3.
3. Ni nini ambacho kinaweza kufanya tuhukumu uamuzi ambao Mkristo mwenzetu amefanya?
3 Mkristo mwenzetu anapofanya uamuzi ambao hatukubaliani nao, huenda tukahisi tunahitaji kumshawishi abadili uamuzi wake au huenda tukawaeleza wengine maoni yetu kuhusu jambo hilo. Huenda tuna nia nzuri. Tunawapenda ndugu na dada zetu, na tunawatakia mema. (Met. 17:17) Hivyo, hatungependa wafanye uamuzi ambao watajutia baadaye au ambao utawadhuru kiroho.
4-5. Tunapaswa kufanya nini ikiwa Mkristo mwenzetu anaamua kufanya jambo linalotofautiana na jambo ambalo sisi tungefanya?
4 Je, tunapaswa kuzungumzia hangaiko letu na mwabudu mwenzetu ikiwa hatukubaliani na uamuzi wake? Hilo linategemea mambo kadhaa. Kwa mfano, ikiwa tutajua kwamba anafikiria kufanya jambo lisilopatana na amri fulani ya Biblia, basi kwa kuwa tunampenda, tunapaswa kujaribu kumsaidia arekebishe mtazamo wake. (Met. 27:5, 6) Hata hivyo, tunapaswa kufanya nini ikiwa ndugu ataamua kufanya jambo ambalo halivunji mojawapo ya sheria za Mungu, lakini linatofautiana tu na jambo ambalo sisi tungefanya? Tunapata jibu katika andiko letu la msingi. ‘Hatuhukumu kuhusu maoni yanayotofautiana.’—Rom. 14:1.
5 Hata hivyo, inaweza kuwa vigumu kwetu kuheshimu uamuzi wake. Katika makala hii, tutazungumzia kwa nini tunapaswa kuheshimu maamuzi ya wengine na jinsi ya kufanya hivyo. Lakini kwanza, acheni tuzungumzie baadhi ya hali zinazohusu maamuzi ya kibinafsi ambazo zinaweza kutufanya tuwahukumu ndugu na dada zetu.
KWA NINI HUENDA TUKAHUKUMU MAAMUZI YA KIBINAFSI YA WENGINE?
6-7. Elezea hali ambazo huenda tukawahukumu wengine kwa sababu ya maamuzi yao.
6 Kama tulivyotaja awali, tunaweza kuwa na maoni thabiti kuhusu mambo fulani kwa sababu ya malezi yetu au mambo tuliyopitia maishani. Huenda tukahisi kwamba wengine wana maoni kama yetu. Lakini huenda isiwe hivyo. Fikiria hali zifuatazo. Hali ya 1: Kabla ya kujifunza kweli, ndugu alilelewa na baba ambaye alitumia kileo kupita kiasi. Kwenye tafrija, ndugu huyo anawaona Wakristo wengine wakinywa kileo. Anakwazika na kuwaeleza kwamba wanachofanya si sawa. Hali ya 2: Dada amefanikiwa kupambana na ugonjwa mbaya. Baadaye, anagundua kwamba dada mwingine amegunduliwa na ugonjwa huohuo. Dada yule wa kwanza anataka kusaidia, hivyo anamshinikiza rafiki yake afuate matibabu yaleyale aliyopata—iwe ni aina fulani ya chakula, dawa za hospitali, au tiba za asili. Hali ya 3: Awali ndugu alikuwa mshiriki wa dini ya uwongo. Anachukia maisha yake ya awali na hataki tena kujihusisha na dini hiyo. Anapojua kwamba Mkristo mwenzake amehudhuria ibada ya mazishi kanisani, anakwazika.a
7 Fikiria hali hizi nyingine zaidi. Hali ya 4: Ndugu amelelewa wakati ambapo watu wengi waliona ni jambo lisilofaa kwa wanaume kufuga ndevu na wanawake kuvaa suruali (suruali ndefu) katika matukio yaliyo rasmi. Ingawa ndugu huyo anajua kuhusu marekebisho ya karibuni kuhusu jambo hilo, anasisitiza kwa wengine kwamba wanaume Wakristo hawapaswi kufuga ndevu na kwamba wanawake Wakristo wanapaswa kuvaa gauni (rinda) wanaposhiriki katika utendaji wa kitheokrasi. Hali ya 5: Mzee mmoja wa kutaniko anamfahamu ndugu aliyefuatia elimu ya ziada na baadaye akaacha kweli. Sasa, ndugu kijana katika kutaniko la mzee huyo ameamua kufuatia elimu ya ziada. Mzee huyo anahangaishwa na jambo hilo na anaamua kumchochea ndugu huyo kijana na wazazi wake wabadili uamuzi wao.
8. (a) Ni jambo gani linaloweza kusababisha mzazi awahukumu wazazi wengine? (b) Kuwa na mtazamo wa kuwachambua wengine kunaweza kuathirije kutaniko?
8 Fikiria hali hii ambayo inaweza kuwaathiri wazazi. Hali ya 6: Ukiwa mzazi, unajitahidi sana kuwalea watoto wako “katika nidhamu na maagizo ya Yehova.” (Efe. 6:4) Lakini wazazi wengine Wakristo wanawaruhusu watoto wao wafanye mambo ambayo wewe huwaruhusu watoto wako wafanye. Kwa mfano, wanawaruhusu watoto wao wachelewe zaidi kurudi nyumbani, wacheze michezo ya video isiyo na ukatili, au wawe na simu ya mkononi wakiwa na umri mdogo. Kwa sababu hiyo, mtoto wako anahisi kwamba wewe ni mkali sana. Huenda mtoto wako akakuuliza, “Kwa nini usiwe kama wazazi wa marafiki wangu?” Hali kama hiyo inaweza kufanya uanze kuwachambua wazazi wengine. Ukweli ni kwamba uamuzi wowote wa kibinafsi wa Mkristo unaotofautiana na wetu, unaweza kusababisha hali za kutoelewana. Kwa mfano, huenda tusikubaliane na jinsi anavyotumia pesa zake, anaenda likizo mara ngapi, au burudani anayochagua. Lakini hatupaswi kuruhusu hisia zetu ziwe muhimu zaidi kuliko umoja wetu kutanikoni.
9. Tunapaswa kukumbuka nini? (Tazama pia picha.)
9 Wakati uamuzi wa Mkristo mmoja unapotofautiana na wa Mkristo mwingine, si lazima hilo limaanishe kwamba mmoja yuko sahihi na mwingine hayuko sahihi. (Rom. 14:5) Ingawa Wakristo wanaagizwa ‘wafikiri kwa upatano’ inapohusu viwango vya Yehova, jambo hilo halimaanishi kwamba tunapaswa kufikiri kwa njia ileile katika mambo yote ya kibinafsi. (2 Kor. 13:11) Tunaweza kulinganisha maamuzi yetu ya kibinafsi tunayofanya na njia tunayoamua kutumia tunaposafiri kuelekea eneo fulani. Mara nyingi, kuna njia mbalimbali zinazoweza kutufikisha katika eneo hilo. Tunachagua njia tunayoipenda na inayotufaa. Vivyo hivyo, huenda Wakristo wakafanya maamuzi tofauti inapohusu mambo ya kibinafsi, lakini lengo letu ni moja: Tunataka kumfurahisha Yehova. Hivyo, hatuwahukumu wengine kwa sababu ya maamuzi yao ya kibinafsi.—Mt. 7:1; 1 The. 4:11.
Wasafiri wanaweza kuchagua njia mbalimbali ili kufika katika eneo fulani; vivyo hivyo, Wakristo wanaweza kufanya maamuzi tofauti inapohusu mambo ya kibinafsi wanapoendelea kumtumikia Yehova (Tazama fungu la 9)
KWA NINI TUHESHIMU MAAMUZI YA KIBINAFSI YA WENGINE?
10. Kulingana na Yakobo 4:12, hatuna mamlaka ya kufanya nini, na kwa nini?
10 Biblia inatoa sababu kadhaa kwa nini tunapaswa kuheshimu maamuzi ya kibinafsi ya wengine. Fikiria baadhi ya sababu hizo. Hatuna mamlaka ya kuwahukumu wengine inapohusu mambo ya kibinafsi. (Soma Yakobo 4:12.) Yehova ni Mpaji-sheria na Mwamuzi mwadilifu. Ni yeye tu aliye na haki ya kuweka viwango na sheria kuhusu maisha yetu. Hivyo, ndugu na dada zetu watatoa hesabu mbele za Yehova, na si kwetu sisi. (Rom. 14:10) Hatuna haki ya kuhukumu au kuchambua maamuzi ya wengine kwa kutegemea maoni au viwango vyetu.b
11. Tunaweza kuchangiaje umoja kutanikoni? (Tazama pia picha.)
11 Yehova anataka waabudu wake wawe na umoja, na si wafanane kabisa. Kwa kweli, Mungu wetu anapenda unamna-namna! Tunajionea uthibitisho wa jambo hilo katika uumbaji. Kwa mfano, hakuna chembe mbili za theluji zinazofanana. Na fikiria kuhusu wanadamu. Kati ya watu zaidi ya bilioni nane duniani, hakuna watu wawili wanaofanana kabisa inapohusu mwonekano au utu wao. Yehova alituumba tuwe tofauti. Hataki tufanane kabisa. Lakini anataka tuwe na umoja. Hivyo, badala ya kuruhusu tofauti tulizo nazo zitutenganishe, tunaendeleza amani. Tunathamini zaidi amani na umoja wa kutaniko kuliko maoni na mapendezi yetu.—Rom. 14:19.
Yehova alituumba tuwe tofauti, lakini anataka tuwe na umoja (Tazama fungu la 11)
JINSI YA KUHESHIMU MAONI YA WENGINE
12-13. Tunapaswa kukumbuka nini ikiwa tunahisi kwamba mtu amechukua “hatua isiyofaa”? (Wagalatia 6:1; tazama pia sanduku “Ikiwa Hukubaliana na Uamuzi wa Wengine.”)
12 Wengine wanapofanya maamuzi kuhusu mambo ya kibinafsi. Jiulize hivi, ‘Je, mtu huyo anachukua “hatua isiyofaa” au ni kwamba tu anachukua hatua tofauti?’ Ikiwa anachukua hatua isiyofaa, ambayo inavunja amri ya Biblia, jiulize hivi: ‘Je, nina sifa za Kimaandiko zinazohitajika ili kumrekebisha, au mtu mwingine anastahili zaidi kufanya hivyo?’ Ikiwa unastahili kumsaidia, jitahidi kufanya hivyo kwa roho ya upole. (Soma Wagalatia 6:1.) Hata hivyo, mara nyingi huenda ukagundua kwamba ameamua tu kufanya jambo tofauti—ambalo halipatani na maoni yako. Ikiwa ndivyo, usimtilie shaka au kuzungumza kwa njia isiyofaa kuhusu uamuzi wake. Heshimu haki yake ya kujiamulia mambo, na usimhukumu.—Rom. 14:2-4.
13 Fikiria mfano huu: Ikiwa utaenda kwenye mkahawa pamoja na rafiki yako, je, utasisitiza aagize chakula kinachofanana na chako? Hapana. Utaheshimu haki yake ya kuchagua chakula anachotaka. Isitoshe, kile anachochagua kula hakitakuathiri kwa njia yoyote. Na ingekuwa ni wewe, huenda usingetaka rafiki yako akuagizie chakula kulingana na mapendezi yake. Vivyo hivyo, tunaweza kuwaonyesha wengine heshima kwa kuwaruhusu wafanye maamuzi ya kibinafsi bila kujaribu kuwalazimisha wafuate maoni yetu.
14. Unawezaje kuchangia umoja unapofanya maamuzi ya kibinafsi? (1 Wakorintho 8:12, 13)
14 Unapofanya maamuzi kuhusu mambo ya kibinafsi. Unaweza kuchangia umoja kwa kujitahidi kadiri uwezavyo kuepuka kuwakwaza wengine. (Soma 1 Wakorintho 8:12, 13.) Pindi fulani, huenda ukajua kwamba uamuzi unaotaka kufanya ni “halali,” yaani, unakubalika. Lakini ikiwa uamuzi huo utamkwaza ndugu yako, je, utakuwa na “faida”?c (1 Kor. 10:23, 24) Katika hali hizo, badala ya kusisitiza haki yako, fikiria kuweka mapendezi yako kando na kutanguliza ya wengine. (Rom. 15:1) Lakini je, si tumesema kwamba wengine wanapaswa kuheshimu maamuzi yetu ya kibinafsi? Ndiyo. Wanapaswa kuheshimu maamuzi yetu, kama tu ambavyo sisi tunapaswa kuheshimu maamuzi yao. Lakini tunapaswa kukumbuka shauri la Biblia linalopatikana katika Waroma 12:18, linalosema hivi: “Kwa kadiri inavyowategemea ninyi, fanyeni amani na watu wote.” Hivyo, tunafanya yote tunayoweza ili kudumisha amani na wengine na kuepuka kuwakwaza wengine isivyo lazima.
15. Wazee wanawezaje kuchangia umoja kutanikoni? (1 Wakorintho 4:6)
15 Wazee wa kutaniko huheshimu maamuzi ya wengine. Wazee huchangia umoja wa kutaniko kwa kutoweka sheria kuhusu mambo ya kibinafsi na kwa ‘kutopita mambo yaliyoandikwa’ katika Biblia. (Soma 1 Wakorintho 4:6.) Hilo linamaanisha kwamba hawapiti shauri la Biblia linalopatikana katika machapisho yetu. Kwa kuongezea, Mkristo mwenzao anapoomba msaada, wazee wanakuwa waangalifu ili wasitegemee tu uzoefu wao wanapotoa ushauri. Badala yake, wanategemea Neno la Mungu wanapotoa shauri.—Isa. 48:17, 18.
16. Mzee anawezaje kuheshimu maamuzi ya baraza la wazee?
16 Mzee anaonyesha pia heshima anapounga mkono maamuzi ya pamoja ya baraza la wazee. Baada ya baraza la wazee kusali ili kupata roho takatifu, kupitia na kutumia mwongozo wa Kimaandiko, na kufikia uamuzi, kila mzee anapaswa kuunga mkono uamuzi huo, hata ikiwa maoni yake hayatakubaliwa na wengi. (Efe. 5:17) Kwa kuongezea, wazee wanapaswa kuwa waangalifu wasijaribu kulazimisha kutumia mwongozo wa kitheokrasi kwa njia inayopatana na maoni yao. Kwa mfano, mzee hatachukua sentensi moja kutoka kwenye mojawapo ya machapisho yetu bila kuzingatia muktadha ili kuunga mkono maoni yake ya kibinafsi.
17. Tunanufaikaje tunapoheshimu maamuzi ya wengine?
17 Kama tulivyojifunza, kila mmoja wetu yuko tofauti. Kila mmoja wetu ana maoni na mapendezi yake. Lakini unamna-namna huo ni jambo zuri! Malezi na utu wetu tofauti-tofauti unafanya kutaniko liwe mahali penye kuvutia. Hivyo, badala ya kuruhusu tofauti zetu zitugawanye, tunaendeleza amani. Tunakuwa waangalifu ili tusiwakwaze wengine. Tunaheshimu maamuzi ya wengine inapohusu maamuzi ya kibinafsi. Tunapofanya hivyo, jitihada zetu zitathawabishwa. Tutafurahia kuwa kwenye kutaniko lenye furaha na umoja.—Zab. 133:1; Mt. 5:9.
WIMBO 89 Sikiliza, Tii, Upate Baraka
a Mkristo anapaswa kuzingatia mambo kadhaa anapofikiria ikiwa atahudhuria mazishi au harusi kwenye kanisa. Tazama makala “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2002.
b Pindi fulani, wazee wanahitaji kuwahukumu wale wanaovunja amri za Biblia. Hata hivyo, wazee wanakumbuka kwamba wanahukumu kwa ajili ya Yehova kwa msingi wa viwango vyake vya uadilifu, na si vyao.—Linganisha 2 Mambo ya Nyakati 19:6.
c Ili kupata mifano, tazama kitabu Furahia Maisha Milele!, somo la 35, jambo kuu la 5.