MACHI 30–APRILI 5, 2026
WIMBO 76 Unahisije?
Tumia Maneno Yenye Neema Unapofundisha Kweli
“ Yehova, Mungu wa ukweli.”—ZAB. 31:5.
JAMBO KUU
Jinsi ya kuwafundisha watu kweli kwa njia itakayowanufaisha zaidi.
1. Ni lazima tufanye nini ili tuwe sehemu ya familia ya Yehova?
TUNAPOKUTANA kwa mara ya kwanza na mwabudu mwenzetu wa Yehova, mojawapo ya maswali tunayouliza ni, “Uliipata kweli jinsi gani?” Wengine hujibu swali hilo kwa kusema kwamba “walilelewa katika kweli.” Huenda wengine wakasema kwamba “wameipata kweli” hivi karibuni. Tunajibu kwa njia hizo kwa kuwa kweli ya Neno la Mungu inaongoza maisha yetu yote. Kwa nini? Kwa sababu tunajua kwamba tunaweza kuwa sehemu ya familia ya Yehova ikiwa tu tutathibitisha kwamba tunaipenda kweli na kuishi kulingana nayo. Hilo linahusisha kuwa wanyoofu kupitia maneno na matendo yetu.—Zab. 15:1-3.
2. (a) Watu walikuwa na maoni gani kumhusu Yesu? (b) Kweli ambazo Yesu alifundisha zingekuwa na matokeo gani kwa watu?
2 Yesu alisema ukweli nyakati zote. Maadui wake walikiri kwamba Yesu alisema ukweli hata ingawa mara nyingine hawakupenda mambo aliyosema. (Mt. 22:16) Yesu alisema hivi kuhusu matokeo ya kweli alizofundisha: “Nilikuja kuleta mgawanyiko, mtu dhidi ya baba yake, binti dhidi ya mama yake, na binti mkwe dhidi ya mama mkwe wake.” (Mt. 10:35) Yesu hakutaka watu wapinge kweli ambazo yeye na wafuasi wake walifundisha, lakini alijua kwamba hilo lingeweza kutokea. (Mt. 23:37) Alijua kwamba ujumbe wake ungewagawanya watu katika makundi mawili—wale wanaiopenda kweli ya Biblia na wale wasioipenda.—2 The. 2:9-11.
3. Tutazungumzia nini katika makala hii?
3 Kama Yesu, tunajitahidi kuwa wanyoofu kwa kusema ukweli nyakati zote hata kama tutachukiwa na watu kwa kufanya hivyo. Pia, tunahubiri na kufundisha kweli ya Biblia hata ikiwa huenda baadhi ya watu wakakasirishwa na mambo tunayosema. Je, hilo linamaanisha kwamba hatuhitaji kufikiria jinsi na wakati tunaposema ukweli, kutia ndani tunapohubiri habari njema? La hasha! Katika makala hii, tutajibu kwanza swali hili la msingi: Tunaweza kuipata wapi kweli? Kisha tutajibu swali hili: Kwa nini, jinsi gani, na ni wakati gani tunapaswa kuwaambia wengine kuhusu kweli zinazopatikana katika Biblia? Majibu ya maswali hayo yatatusaidia kuboresha uwezo wetu wa kuhubiri habari njema na kusema ukweli kwa kutumia maneno yenye neema, yaani, kwa busara na kwa wakati unaofaa.
TUNAWEZA KUIPATA WAPI KWELI?
4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova ndiye Chanzo cha ukweli?
4 Yehova ndiye Chanzo cha ukweli. Kila anachosema ni ukweli. Kwa mfano, anatuambia ukweli kuhusu mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa. (Zab. 19:9; 119:142, 151) Atatimiza mambo yote anayoahidi kuhusu wakati ujao. (Isa. 55:10, 11) Havunji kamwe ahadi yoyote aliyoweka. (Hes. 23:19) Kwa kweli, Yehova hawezi kamwe kusema uwongo! (Ebr. 6:18) Hivyo, inapatana na akili kwamba Yehova anajulikana kuwa “Mungu wa ukweli.”—Zab. 31:5.
5. Kwa nini si vigumu kumpata “Mungu wa ukweli”? Eleza. (Matendo 17:27)
5 Tunaweza kumpata Yehova “Mungu wa ukweli,” licha ya baadhi ya watu kusema kwamba ni vigumu kufanya hivyo. Uumbaji wote unathibitisha kwamba Mungu yuko. (Rom. 1:20) Alipokuwa akizungumza na kikundi cha Wagiriki wenye elimu katika jiji la Athene, mtume Paulo alisema kwamba Mungu anataka “tumpate” naye “hayuko mbali na kila mmoja wetu.” (Soma Matendo 17:27.) Kwa kweli, Yehova anawavuta kwake watu wanyenyekevu ambao wanaitafuta kweli.—Yoh. 6:44.
6. Ni baadhi ya kweli gani zinazopatikana katika Biblia, na kwa nini unathamini kujua kweli hizo?
6 Njia moja ambayo tunaweza kumpata Yehova ni kwa kujifunza Biblia. Wanaume walioandika kitabu hicho waliongozwa na roho takatifu ya Mungu. (2 Pet. 1:20, 21) Hivyo, mambo yote yaliyo katika Biblia ni ya kweli na tunaweza kuyaamini. Kwa mfano, tunaweza kuamini kile inachosema kuhusu chanzo cha ulimwengu wetu na chanzo cha uhai duniani. (Mwa. 1:1, 26) Tunaweza kuamini kile inachosema kuhusu kwa nini sote tunatenda dhambi na kwa nini watu wanateseka sana na kufa. (Rom. 5:12; 6:23) Tunaweza kuiamini kabisa inaposema kwamba Yehova, kupitia Mwana wake, ataondoa kabisa madhara yote yaliyosababishwa na Shetani, “baba ya uwongo.” (Yoh. 8:44; Rom. 16:20) Na tunaweza kuamini ahadi inayopatikana katika Biblia kwamba Yesu atawaangamiza waovu, atawafufua wafu, ataifanya dunia iwe Paradiso, na kutusaidia tuwe wakamilifu. (Yoh. 11:25, 26; 1 Yoh. 3:8) Yehova ametupatia pendeleo kubwa sana! Ametufundisha kweli na kutupatia fursa ya kuwafundisha wengine kweli hiyo.—Mt. 28:19, 20.
KWA NINI TUNASEMA UKWELI?
7-8. Ni nini kinachotuchochea kusema ukweli? Toa mfano. (Marko 3:11, 12) (Tazama pia picha.)
7 Kama ilivyotajwa awali, tunapaswa kusema ukweli ili tuwe sehemu ya familia ya Yehova. Hata hivyo, ili tumpendeze Yehova, tunapaswa kufanya mengi zaidi ya kusema ukweli. Jambo la muhimu kwa Yehova ni nia yetu inayotuchochea kusema ukweli. Fikiria kilichotokea wakati wa huduma ya Yesu duniani. (Soma Marko 3:11, 12.) Yesu alipokuwa akihubiri karibu na Bahari ya Galilaya, umati mkubwa ulikusanyika. Kati yao, kulikuwa na baadhi ya watu waliokuwa na roho waovu ambao walianguka mbele ya Yesu na kupaza sauti wakisema: “Wewe ndiye Mwana wa Mungu.” Kwa nini roho hao waovu walisema ukweli kumhusu Yesu? Huenda lengo lao lilikuwa kuaminiwa na watu waliowasikiliza na kisha kusababisha waache kumtumikia Yehova. Mwanzoni, mambo waliyosema roho hao waovu yalikuwa ya kweli, lakini nia yao ilikuwa mbaya. Hawakumdanganya au kumfurahisha Yesu. Isitoshe, Yesu aliwaagiza roho hao waovu wasihubiri kumhusu.
8 Tunajifunza somo gani kutokana na simulizi hilo? Jambo la muhimu kwa Yehova ni nia yetu inayotuchochea kusema ukweli. Hivyo, ni muhimu sana kuwa na nia nzuri tunapofundisha kweli na kumwelekezea Yehova sifa zozote tunazopewa badala ya kujielekezea wenyewe sifa!—Mt. 5:16; linganisha Matendo 14:12-15.
Wewe humwelekezea fikira nani unapofundisha kweli? (Tazama fungu la 7-8)
9. Tunapaswa kuepuka kufanya nini, na kwa nini?
9 Fikiria hali nyingine ambayo tunahitaji kuepuka ili tusijielekezee sifa wenyewe. Tuseme kwamba ndugu mwenye mapendeleo anatupatia habari ya siri na kisha tunawaambia wengine habari hiyo. Ikiwa baadaye wale tuliowaeleza habari hizo watagundua kwamba zilikuwa za kweli, huenda wakavutiwa na mambo tunayojua na kuhisi kwamba tunajua habari nyingi za siri. Kufanya hivyo kunaweza kuwafurahisha watu, lakini hakutamfurahisha Mungu. (Met. 11:13) Kwa nini? Kwa sababu si tu kwamba tumefunua habari za siri, bali pia tumesema ukweli tukiwa na nia mbaya.
JINSI YA KUSEMA UKWELI
10. Unawezaje kufafanua kinachomaanishwa na maneno yenye “neema”? (Wakolosai 4:6)
10 Soma Wakolosai 4:6. Mtume Paulo aliwakumbusha Wakristo walioishi katika jiji la Kolosai kwamba maneno yao yanapaswa kuwa “yenye neema sikuzote.” Hilo linamaanisha nini? Neno la Kigiriki lililotumiwa hapa linatoa wazo la kwamba maneno yetu hayapaswi tu kumnufaisha msikilizaji wetu bali pia yawe yenye fadhili na yanayovutia.
11-12. Kwa nini ni lazima tufundishe kweli kwa uangalifu? Toa mfano. (Tazama pia picha.)
11 Tunahitaji kutumia shauri la Paulo la kuwa wenye neema tunapowafundisha wengine kweli. Biblia yenyewe inafananisha kweli zilizomo ndani yake na upanga mkali unaoweza kugawanya nafsi na roho yetu. Kwa maneno mengine, inaweza kufunua nia na hisia zetu za ndani kabisa. (Ebr. 4:12) Lakini tusipotumia Biblia kwa ustadi, huenda tukawakasirisha watu na kusababisha mabishano yasiyo ya lazima. Jambo hilo linaweza kutokeaje?
12 Wazia hali hii. Katika huduma yetu, tunakutana na mwanamume mnyoofu ambaye huabudu sanamu kwa ukawaida, na anafurahia kusherehekea Krismasi na Ista pamoja na familia yake. Kwa kutumia Biblia, tunaweza kumwonyesha mwanamume huyo jinsi lilivyo jambo la kipumbavu kuabudu sanamu zisizo na uhai, na kumthibitishia kwamba sherehe za Krismasi na Ista ni za kipagani. (Isa. 44:14-20; 2 Kor. 6:14-17) Ikiwa tutafanya hivyo tunapozungumza naye kwa mara ya kwanza kabisa, tutakuwa tukisema ukweli lakini hatutakuwa tukilitumia Neno la Mungu kwa ustadi.
Unawezaje kufundisha kweli kwa ustadi? (Tazama fungu la 11-12)a
13. Tunawezaje kukoleza chumvi maneno yetu?
13 Paulo alisema pia kwamba wasomaji wake walipaswa kukoleza chumvi maneno yao. Hakumaanisha kwamba tunapaswa kuficha ukweli. Badala yake, alikuwa akitusihi tutumie maneno “yaliyokolezwa” chumvi ili tufundishe kweli kwa njia ambayo itamvutia msikilizaji ‘atakapoionja.’ (Ayu. 12:11) Inaweza kuwa changamoto kufanya hivyo. Inapohusu chakula halisi, tunaweza kuwa na mtazamo wa kwamba watu wengine wanapenda chakula kilicho na ladha tunayoipenda. Vivyo hivyo, huenda tukafikiri kwamba njia yetu ya kuzungumza inawavutia watu wote. Lakini hilo si kweli. Kwa mfano, katika tamaduni fulani, ni jambo la kawaida kwa watu kutoa maoni yao moja kwa moja, hata wanapozungumza na watu waliowazidi umri. Huenda watu kutoka tamaduni tofauti wakaiona njia hiyo ya kuzungumza kuwa isiyofaa, au hata isiyo na heshima. Paulo alisema kwamba ni lazima tujue jinsi ‘tunavyopaswa kumjibu kila mtu.’ Hilo linamaanisha kuwa tunapaswa kukoleza chumvi mambo tunayosema, si kulingana na ladha au utamaduni wetu, bali kulingana na ladha ya msikilizaji wetu.
WAKATI WA KUSEMA UKWELI
14. Alipokuwa duniani, je, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake mambo yote aliyoyajua? Eleza.
14 Sikuzote Yesu alizungumza na wafuasi wake kwa neema, na aliwafundisha mambo mengi kwa fadhili. (Marko 6:34) Hata hivyo, bado walikuwa na mambo mengi ya kujifunza. Yesu hakujaribu kuwafundisha mambo yote aliyoyajua. Alijua kwamba uwezo wao una mipaka. Alitambua kwamba haukuwa wakati unaofaa kwao kujifunza kuhusu baadhi ya kweli. Isitoshe, alisema kwamba hawangeweza kustahimili kweli hizo. (Yoh. 16:12) Jambo hilo linatufundisha nini?
15. Je, ni lazima tuwafundishe wanafunzi wetu wa Biblia mambo yote tunayojua kwa wakati mmoja? Eleza. (Methali 25:11) (Tazama pia picha.)
15 Mfano wa Yesu unaonyesha kwamba kujua kweli hakumaanishi kwamba tunahitaji kufundisha mambo yote tunayojua kwa wakati mmoja. Tunawezaje kufuata mfano wa Yesu? Tunahitaji kufikiria hali za watu. Mfikirie tena yule mwanamume anayefurahia kusherehekea Krismasi na Ista pamoja na familia yake. Tunajua kuwa vyanzo vya sherehe hizo ni vya kipagani na Mungu hapendezwi nazo. Hata hivyo, wazia kwamba umeanza kujifunza Biblia na mwanamume huyo juma moja au majuma mawili kabla ya Krismasi. Je, tutakuwa tukizungumza kwa neema, ikiwa tutamwonyesha kile ambacho Biblia inasema kuhusu sherehe za kipagani, na kutarajia aache mara moja kusherehekea Krismasi? Ni kweli kwamba huenda baadhi ya wanafunzi wakatumia bila kukawia mambo yote wanayojifunza kutoka katika Biblia. Hata hivyo, wengine huchukua muda mrefu zaidi ili kurekebisha mtazamo na matendo yao. Tunaweza kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia kufanya maendeleo ikiwa tutawaambia mambo wanayohitaji kujua kwa wakati unaofaa, yaani, wanapokuwa na uwezo wa kuyastahimili.—Soma Methali 25:11.
Fuata mfano wa Yesu unapoamua ni wakati gani na ni kwa kiasi gani utasema kweli (Tazama fungu la 15)
16. Tunawezaje kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia ‘waendelee kutembea katika kweli’?
16 Si mambo mengi yanayotupatia shangwe kama ile tunayopata kwa kuwasaidia wengine wajifunze kweli kumhusu Yehova. Unaweza kuwasaidia “[waendelee] kutembea katika kweli” ikiwa utafanya mambo yafuatayo: Endelea kuwawekea mfano mzuri. (3 Yoh. 3, 4) Hakikisha kwamba njia yako ya maisha inathibitisha kuwa unaamini ahadi zilizo katika Neno la Mungu. Zungumza ukweli ukiwa na nia nzuri. Unapofundisha kweli, zungumza kwa wakati unaofaa ukitumia maneno yenye neema, wororo, na fadhili. Na umwelekezee Yehova sifa yoyote utakayopewa. Ukifanya hivyo, utathibitisha kwamba wewe ni wa Yehova, Mungu wa ukweli.
WIMBO 160 “Habari Njema”!
a MAELEZO YA PICHA: Katika picha ya kwanza, ndugu anaona mti wa Krismasi wa mwenye nyumba na anamwonyesha makala inayozungumzia vyanzo vya kipagani vya Krismasi. Katika picha ya pili, ndugu anamwonyesha mwenye nyumba makala iliyo na mapendekezo hususa kwa ajili ya akina baba. Ni njia gani itakayokuwa na matokeo zaidi kati ya njia hizo mbili?