MACHI 23-29, 2026
WIMBO 18 Tunathamini Fidia
Utaonyeshaje Kwamba Unaithamini Fidia?
“Upendo alio nao Kristo hutuchochea.”—2 KOR. 5:14.
JAMBO KUU
Jinsi sisi sote tunavyoweza kuonyesha kwamba tunaithamini fidia.
1-2. Dhabihu ya fidia ya Yesu inapaswa kutuchochea kufanya nini, na kwa nini? (2 Wakorintho 5:14, 15) (Tazama pia picha.)
IKIWA umeokolewa kutoka katika kifusi cha jengo lililoporomoka, je, hutamthamini sana mtu aliyeokoa uhai wako? Hata ikiwa kuna wengine waliookolewa, inaelekea ungetaka kumweleza kibinafsi jinsi unavyothamini, ili kuonyesha kwamba huchukulii kivivi hivi tendo hilo la kuokolewa.
2 Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, hatuwezi kujiokoa wenyewe kutokana na madhara ya dhambi tuliyorithi. Hata hivyo, dhabihu ya fidia ya Yesu inaweza kutuokoa kwa kutupatia (1) msamaha wa dhambi tunazotenda, (2) tumaini la kuponywa kabisa kutokana na hali yetu ya dhambi, na (3) kupatanishwa na Mungu. Matokeo ni kwamba tuna tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Yehova. Kwa kweli, fidia inaonyesha upendo wa Yesu kwa watu—upendo ambao alikuwa nao muda mrefu kabla ya kuzaliwa akiwa mwanadamu mkamilifu. (Met. 8:30, 31) Mtume Paulo aliandika kwamba “upendo alio nao Kristo hutuchochea.” (Soma 2 Wakorintho 5:14, 15.) Hilo linamaanisha kwamba upendo wa Yesu unapaswa kutuchochea kuonyesha tunathamini na kwamba hatuchukulii kivivi hivi dhabihu yake ya fidia.
Iwe tumeokolewa kutoka katika kifusi cha jengo lililoporomoka au dhambi tuliyorithi, tunapaswa kumwonyesha shukrani yule aliyetuokoa (Tazama fungu la 1-2)
3. Kwa nini huenda kila mtu akaonyesha uthamini wake kuelekea fidia kwa njia tofauti?
3 Uandalizi wenye upendo wa fidia utakuchochea wewe kwa njia gani? Huenda jibu lako likatofautiana na jibu la mtu mwingine. Ili tuelewe kwa nini, fikiria mfano wa watu watatu wanaotaka kusafiri kwenda sehemu moja, lakini kila mmoja wao anaanza safari yake katika jiji tofauti. Njia watakazotumia zitatofautiana. Vivyo hivyo, njia utakayotumia ili kufikia lengo lako, yaani, kuonyesha kwamba unathamini fidia, inategemea mahali ulipo sasa katika uhusiano wako na Yehova. Tukiwa na hilo akilini, makala hii itazungumzia vikundi vitatu vya watu: (1) wanafunzi wa Biblia, (2) Wakristo waliobatizwa, na (3) kondoo waliopotea.
WANAFUNZI WA BIBLIA
4. Wanafunzi wa Biblia wanatambuliwa kwa njia gani na Yehova?
4 Ikiwa unajifunza Biblia, fikiria jambo hili: Kukubali kwako habari njema kunaonyesha kwamba wewe ni miongoni mwa watu ambao Yehova amewavuta katika uhusiano pamoja naye. (Yoh. 6:44; Mdo. 13:48) “Yehova ndiye mchunguzaji wa mioyo.” Hilo linamaanisha kwamba anatambua jitihada zako za kujifunza kumhusu na anashangilia kuona maendeleo yako unapofanya mabadiliko ili uishi kulingana na viwango vyake. (Met. 17:3; 27:11) Fidia inakuwezesha uwe na urafiki wa karibu pamoja na Yehova. (Rom. 5:10, 11) Kamwe usichukulie fidia kivivi hivi.
5. Wanafunzi wa Biblia wanawezaje kutumia mwongozo unaopatikana kwenye Wafilipi 3:16?
5 Ukiwa mwanafunzi wa Biblia, unawezaje kuonyesha unathamini fidia? Njia moja ni kwa kufuata shauri hili la mtume Paulo kwa Wafilipi: “Kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika mwendo huohuo.” (Flp. 3:16) Tafsiri nyingine ya Biblia inasema hivi kwenye mstari huo: “Ni lazima tuendelee kusonga katika njia ileile tunayoelekea.” Kupatana na shauri hilo, usiruhusu jambo lolote lizuie maendeleo yako katika barabara ya uzima.—Mt. 7:14; Luka 9:62.
6. Wanafunzi wa Biblia wanaweza kufanya nini ikiwa ni vigumu kwao kufanya mabadiliko? (Kumbukumbu la Torati 30:11-14) (Tazama pia picha.)
6 Namna gani ikiwa ni vigumu kwako kukubali fundisho la Biblia ulilojifunza karibuni? Fanya utafiti kuhusu fundisho hilo, na sali kwa Yehova ili akusaidie uweze kulielewa vizuri zaidi. (Zab. 86:11) Ikiwa bado ni vigumu kwako kuelewa fundisho hilo, liweke kando kwa sasa—lakini usiache kujifunza Biblia. Namna gani ikiwa ni vigumu kwako kuacha zoea ambalo Biblia inalishutumu? Kumbuka kwamba Yehova kamwe hawezi kuwaomba wanadamu wasio wakamilifu wafanye jambo ambalo hawawezi kutimiza. Unaweza kuishi kulingana na viwango vyake. (Soma Kumbukumbu la Torati 30:11-14.) Na Yehova anaahidi kwamba atakusaidia. (Isa. 41:10, 13; 1 Kor. 10:13) Hivyo, usikate tamaa. Badala ya kukazia fikira changamoto unayokabili, kazia fikira jinsi unavyothamini mambo yote ambayo Yehova amekuandalia—kutia ndani mpango wa fidia. Kadiri upendo wako kwa Yehova unavyozidi kukua, utajionea kwamba “amri zake si mzigo mzito.”—1 Yoh. 5:3.a
Yehova kamwe hawezi kutuomba tufanye jambo ambalo hatuwezi kutimiza. Atatusaidia tuishi kulingana na viwango vyake (Tazama fungu la 6)
7. Vijana wanaolelewa katika kweli wanaweza kutafakari kuhusu nini?
7 Namna gani ninyi vijana ambao mnalelewa katika kweli? Ninyi pia ni wanafunzi wa Biblia. Ukweli ni kwamba ninyi ni wanafunzi wa Biblia walio muhimu zaidi wa wazazi wenu. Biblia inasema hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8; 1 Nya. 28:9) Unapochukua hatua ya kwanza kumkaribia Yehova, yeye pia anakukaribia. Yehova hakuoni tu kuwa sehemu ya kikundi. Anatuvuta tukiwa mtu mmoja-mmoja—kutia ndani wale wanaolelewa katika kweli. Ni jambo gani lililokuwezesha kuwa na uhusiano wa kibinafsi na Yehova? Ni fidia—jambo ambalo hupaswi kulichukulia kivivi hivi. (Rom. 5:1, 2) Hivyo, kabla ya kuhudhuria Ukumbusho mwaka huu, kwa nini usitafakari kile ambacho kifo cha Yesu kinamaanisha kwako? Wazo hilo na likuchochee kujitahidi kufikia lengo lako linalofuata la kiroho—haidhuru ni lengo gani—ili kuonyesha jinsi unavyothamini fidia ambayo Yehova alituandalia kupitia Mwana wake.b
WAKRISTO WALIOBATIZWA
8. Wakristo waliobatizwa wameonyeshaje imani katika fidia?
8 Ikiwa wewe ni Mkristo aliyebatizwa, tayari umeonyesha imani katika fidia kwa njia kadhaa. Kwa mfano, ulichukua hatua ili umkaribie Yehova na kuishi kulingana na viwango vyake. Ulitii amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi kwa kushiriki imani yako na wengine. Ulijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Je, umekabili upinzani kwa sababu ya kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli? (2 Tim. 3:12) Kuvumilia kwako kwa uaminifu kunaonyesha upendo wako kwa Yehova na uthamini wako kuelekea fidia aliyotoa kupitia Mwana wake.—Ebr. 12:2, 3.
9. Wakristo waliobatizwa wanapaswa kuwa macho dhidi ya hatari gani?
9 Tukiwa Wakristo waliobatizwa, tunapaswa kuwa macho dhidi ya hatari fulani. Baada ya muda, tunaweza kuanza kuchukulia kivivi hivi fidia. Hilo linaweza kutokeaje? Wafikirie Wakristo wa karne ya kwanza katika jiji la Efeso. Yesu aliyefufuliwa aliwapongeza kwa sababu ya uvumilivu wao. Hata hivyo, alisema hivi: “Nina jambo hili dhidi yako, kwamba umeacha upendo uliokuwa nao mwanzoni.” (Ufu. 2:3, 4) Kama maneno ya Yesu yanavyoonyesha, bidii ya Mkristo kuelekea ibada inaweza kuanza kupungua hatua kwa hatua na ibada yake ikawa ya kidesturi. Mtu huyo anaweza kuwa anasali, anahudhuria mikutano, na kushiriki katika huduma lakini kidesturi tu. Mtu huyo hachochewi tena na upendo. Unaweza kufanya nini ikiwa unahisi kwamba upendo wako kwa Yehova hauna nguvu kama zamani?
10. Unawezaje ‘kutafakari’ na ‘kuzama katika’ utendaji wako wa Kikristo? (1 Timotheo 4:13, 15)
10 Mtume Paulo alimwambia Timotheo ‘atafakari’ na ‘kuzama katika’ utendaji wake mwenyewe wa Kikristo. (Soma 1 Timotheo 4:13, 15.) Kwa kupatana na shauri hilo, jaribu kufikiria njia za kufanya ibada yako kwa bidii zaidi ili uweze kuendelea ‘kuwaka roho.’ (Rom. 12:11; tazama habari za utafiti, “Be aglow with the spirit” nwtsty) Kwa mfano, huenda unaweza kuboresha usikivu wako kwenye mikutano kwa kujitayarisha vizuri zaidi. Au unaweza kuboresha zaidi funzo lako la kibinafsi kwa kuandaa mazingira yenye utulivu yatakayokuruhusu kutafakari mambo uliyojifunza. Kama tu jinsi ambavyo unachochea moto ili uendelee kuwaka, unaweza kuboresha mambo hayo ili uchochee tena uthamini wako kwa mambo yote ambayo Yehova amekuandalia, kutia ndani fidia. Pia, kwa nini usitenge wakati majuma machache kabla ya Ukumbusho ili kutafakari kuhusu baraka za pekee tunazofurahia tukiwa Mashahidi wa Yehova? Bila shaka, hilo litakusaidia kuongeza uthamini wako kwa fidia—msingi wa uhusiano wako mzuri pamoja na Yehova.
11-12. Je, kutokuwa na bidii kwa muda fulani kunamaanisha kwamba hauna roho ya Mungu? Eleza. (Tazama pia picha.)
11 Ikiwa kwa muda fulani hauna bidii ileile uliyokuwa nayo zamani kwa ajili ya ibada safi kama ambavyo ungependa, usivunjike moyo au kufikia mkataa kwamba umepoteza roho ya Mungu. Kumbuka kile ambacho mtume Paulo aliwaandikia Wakorintho kuhusu huduma yake: “Hata nikifanya hivyo bila kupenda, bado nimekabidhiwa usimamizi.” (1 Kor. 9:17) Alimaanisha nini?
12 Paulo alikuwa na mielekeo ambayo pindi nyingine ilipunguza tamaa yake ya kuhubiri. Hata hivyo, alikuwa ameazimia kuendelea na huduma yake bila kuacha licha ya jinsi alivyohisi wakati huo. Unaweza kuwa na azimio hilo pia. Azimia kufanya lililo sawa hata ikiwa hauna hamu ya kufanya hivyo. Hivyo, sali ili Yehova akupatie “hamu na nguvu za kutenda.” (Flp. 2:13) Uwe na mengi ya kufanya katika utendaji wako wa kiroho. Uwe na uhakika kwamba baada ya muda, matendo yako yatagusa hisia zako na utachochea upya upendo ambao bado upo moyoni mwako.
Uwe na mengi ya kufanya katika utendaji wako wa kiroho hata kama nyakati nyingine hauna hamu ya kufanya hivyo (Tazama fungu la 11-12)
13. Tunawezaje kuendelea kujijaribu kama tuko “katika imani”?
13 Pindi kwa pindi, itafaa tujichunguze wenyewe kulingana na mwongozo huu unaopatikana katika 2 Wakorintho 13:5: “Endeleeni kujijaribu kama mko katika imani, endeleeni kuthibitisha jinsi ninyi wenyewe mlivyo.” Pindi kwa pindi, tunaweza kujiuliza maswali kama vile: ‘Je, ninatanguliza masilahi ya Ufalme maishani mwangu?’ (Mt. 6:33) ‘Je, burudani ninazochagua zinaonyesha kwamba ninachukia maovu?’ (Zab. 97:10) ‘Je, ninaendeleza amani na umoja kati ya waabudu wenzangu?’ (Efe. 4:2, 3) Ukumbusho—pindi ambayo tunatumia hasa kutafakari kuhusu uandalizi wa Yehova wa fidia—unatupatia nafasi ya kujichunguza wenyewe na kuhakikisha kwamba tunaishi kwa ajili ya Kristo na si kwa ajili yetu.c
KONDOO WALIOPOTEA
14. Ni nini kinachoweza kusababisha baadhi ya Wakristo waliache kundi?
14 Baadhi ya Wakristo wameacha kushirikiana na kutaniko baada ya kutumikia kwa uaminifu kwa miezi kadhaa au miaka mingi. Kwa nini? Baadhi yao wamelemewa na “mahangaiko ya maisha.” (Luka 21:34) Wengine wamekwazwa na maneno au matendo ya mwabudu mwenzao. (Yak. 3:2) Ilhali wengine wamejihusisha katika mwenendo usiofaa na wanasita kuomba msaada. Haidhuru sababu ni nini, unaweza kufanya nini ikiwa umeliacha kundi? Uandalizi wenye upendo wa fidia unaweza kukuchochea wewe kufanya nini?
15. Yehova anaonyeshaje kwamba anawajali kondoo waliopotea? (Ezekieli 34:11, 12, 16)
15 Tafakari jinsi Yehova anavyohisi kuhusu wale waliopotea. Hawakatai. Badala yake, anawatafuta kondoo waliopotea. Anawalisha na kuwasaidia wamrudie. (Soma Ezekieli 34:11, 12, 16.) Je, Yehova anafanya hivyo kwa ajili yako? Ndiyo! Kwa kuwa unachunguza habari hii unaonyesha kwamba unapenda uadilifu. Kama tu ambavyo Yehova aliona moyo wako na kukuvuta katika kweli, je, inawezekana kwamba anakuvuta urudi kwake?
16. Ni nini kinachoweza kuwasaidia kondoo waliopotea wamrudie Yehova? (Tazama pia picha.)
16 Broshua Mrudie Yehova ina maneno haya yenye kutia moyo: “Uwe na hakika kwamba Yehova atakutegemeza unapojitahidi kumrudia. Atakusaidia kukabiliana na mahangaiko, kuondoa maumivu ya kihisia, na kupata amani ya akili na moyo kwa sababu ya kuwa na dhamiri safi. Kisha unaweza kuchochewa kumtumikia tena Yehova pamoja na waabudu wenzako.” Kumbuka pia kwamba wazee wana hamu ya kukusaidia. Wanaweza kuthibitika kuwa “kama mahali pa kujificha kutokana na upepo, na mahali pa kujisitiri kutokana na dhoruba ya mvua.” (Isa. 32:2) Ili kuonyesha kwamba unaithamini fidia, jiulize, ‘Ninaweza kuchukua hatua gani sasa ili “kunyoosha mambo” na Yehova?’ (Isa. 1:18; 1 Pet. 2:25) Kwa mfano, je, unaweza kuhudhuria mkutano katika Jumba la Ufalme? Je, unaweza kumfikia mzee mmoja na kumwomba msaada wa kiroho, ambao unaweza kutia ndani funzo la Biblia la ukawaida kwa muda fulani? Unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zako za kuonyesha uthamini kwa ajili ya fidia ya Mwana wake.
Jiulize hivi, ‘Ninaweza kuchukua hatua gani sasa ili “kunyoosha mambo” na Yehova?’ (Tazama fungu la 16)
UTAONYESHAJE KWAMBA UNAITHAMINI FIDIA?
17-18. Tunawezaje kutumia wakati wetu kwa hekima kabla ya Ukumbusho wa mwaka huu?
17 Yesu alisema kwamba fidia iliandaliwa “ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Fidia ni njia ya Yehova ya kutuokoa kutokana na madhara ya dhambi na kifo. Hatupaswi kuichukulia fidia kivivi hivi. (Rom. 3:23, 24; 2 Kor. 6:1) Siku chache kabla ya Ukumbusho, tumia wakati kutafakari kuhusu upendo ambao Yehova na Yesu wametuonyesha, na jinsi ambavyo upendo huo unapaswa kutuchochea kuonyesha uthamini.
18 Fidia itakuchocheaje kuonyesha uthamini? Huenda jibu lako likawa tofauti na jibu la mtu mwingine. Hata hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zako unapojiunga na mamilioni ya waabudu wenzako ambao ‘hawaishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yule aliyekufa kwa ajili yao.’—2 Kor. 5:15.
WIMBO 14 Kumsifu Mfalme Mpya wa Dunia
a Ili kukusaidia kufanya maendeleo unapoendelea kujifunza Biblia, tumia sanduku la “Lengo” linalopatikana mwishoni mwa kila somo katika kitabu cha Furahia Maisha Milele!
b Ili kupata mapendekezo ya jinsi unavyoweza kufanya maendeleo ya kiroho, tazama makala “Vijana—‘Endeleeni Kuufanyia Kazi Wokovu Wenu Wenyewe’” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 2017.
c Ili kupata mapendekezo ya jinsi ya kudumisha mtazamo wa kuonyesha uthamini, tazama makala “Ni Nini Hukuchochea Kumtumikia Mungu?” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1995.