‘ Dumisha Roho ya Umoja’
MTUME Paulo aliwahimiza Wakristo katika jiji la Efeso waendelee ‘kuvumiliana kwa upendo, wakijitahidi sana kudumisha roho ya umoja katika kifungo cha muungano cha amani.’—Efe. 4:2, 3.
“Umoja,” tunaofurahia ni wa “roho.” Hilo linamaanisha kwamba unatokana na nguvu za utendaji za Mungu. Hata hivyo, kama Paulo alivyosema, umoja wetu unahitaji kudumishwa. Na nani? Kwa kweli, ni lazima kila Mkristo atimize sehemu yake ili “kudumisha roho ya umoja.”
Kwa mfano, tuseme kwamba mtu amekupatia gari jipya. Ni nani aliye na jukumu la kulitunza ili liendelee kuwa katika hali nzuri? Jibu liko wazi. Huwezi kumlaumu yule aliyekupa zawadi ya gari ikiwa litaharibika kwa sababu hukulitunza.
Vivyo hivyo, ingawa umoja wetu wa Kikristo ni zawadi kutoka kwa Mungu, kila mmoja wetu ana jukumu la kuudumisha. Ikiwa hatuna uhusiano mzuri na ndugu au dada fulani, tunahitaji kujiuliza, ‘Je, ninatimiza sehemu yangu ili kudumisha roho ya umoja kwa kutatua tatizo tulilo nalo?’
‘JITAHIDI SANA’ KUDUMISHA UMOJA
Kama Paulo alivyosema, huenda pindi fulani tukahitaji kujitahidi sana ili kudumisha roho ya umoja. Hilo ni kweli hasa ikiwa ndugu au dada ametukosea. Je, sikuzote kudumisha umoja kunamaanisha kwenda kwa mtu huyo ili kuzungumzia tatizo lenu? Si lazima iwe hivyo. Jiulize hivi, ‘Je, kwenda kuzungumzia tatizo hilo kutaendeleza umoja au kutasababisha ugomvi mkubwa zaidi?’ Nyakati nyingine, jambo la hekima ni kuachilia tu kosa au kusamehe.—Met. 19:11; Marko 11:25.
Jiulize, ‘Je, kwenda kuzungumzia tatizo hilo kutaendeleza umoja au kutasababisha ugomvi mkubwa zaidi?’
Kama mtume Paulo alivyoandika, acheni tuendelee ‘kuvumiliana kwa upendo.’ (Efe. 4:2) Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba msemo huo unaweza kutafsiriwa kuwa “kuwapokea jinsi walivyo.” Hilo linamaanisha kukubali kwamba waabudu wenzetu ni wenye dhambi kama sisi. Bila shaka, tunajitahidi kuvaa “utu mpya.” (Efe. 4:23, 24) Hata hivyo, hakuna yeyote kati yetu anayeweza kufanya hivyo kikamilifu. (Rom. 3:23) Ikiwa tutakubali ukweli huo, itakuwa rahisi zaidi kwetu kuvumiliana, kusameheana, na hivyo “kudumisha roho ya umoja.”
Tunapowasamehe wale wanaotukosea na kusuluhisha hali za kutoelewana—hata ikiwa ni moyoni mwetu tu—tutaendelea kuwa na “kifungo cha muungano cha amani.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kifungo cha muungano” kwenye Waefeso 4:3 linatafsiriwa kuwa “kano” kwenye Wakolosai 2:19. Kano ni mkusanyo wa tishu imara zinazounganisha mfupa mmoja na mwingine. Kwa njia hiyohiyo, sifa ya amani na pia upendo kwa ndugu zetu, zinatusaidia kuendelea kuwa karibu nao licha ya tofauti zozote ambazo huenda tunazo kati yetu.
Hivyo, mwabudu mwenzetu anapotukosea, anapotuudhi, au kutukasirisha, jitahidi kuwa na mtazamo wenye huruma kumwelekea, badala ya kumchambua. (Kol. 3:12) Kwa kuwa wanadamu wote si wakamilifu, huenda nyakati fulani wewe pia umemkosea mtu. Kukumbuka jambo hilo kutakusaidia kutimiza sehemu yako ili “kudumisha roho ya umoja.”