Msaada kwa Ajili ya Wanawake Wanaotendewa Vibaya
“ MAMILIONI ya wanawake na wasichana ulimwenguni pote wametendewa vibaya kimwili, kingono, au hata kwa maneno. Je, wewe ni mmoja kati yao? Ona kwa nini usalama wako ni muhimu kwa Mungu na kile ambacho atafanya kuhusu dhuluma ambayo wanawake wamekabili.”
Hayo ndiyo maneno ya utangulizi kwenye makala, “Usalama wa Wanawake—Maoni ya Biblia,” inayopatikana kwenye jw.org. Kiunganishi kilicho mwishoni mwa makala kinakuwezesha kupakua makala hiyo katika mfumo wa PDF, ambayo inaweza kuchapishwa na kukunjwa mara nne. Dada nchini Marekani anayeitwa Stacy, anasema hivi: “Nilichapisha nakala kadhaa, na nikiwa pamoja dada mmoja, tulipeleka nakala hizo katika makao ya wanawake walio hatarini yaliyo katika eneo la kutaniko letu.”
Mfanyakazi mmoja katika makao hayo, aliniomba nakala zaidi ili aweze kuwapatia watu walioishi hapo. Matokeo ni kwamba trakti 40 zaidi na kadi 30 za mawasiliano zilisambazwa. Baadaye, msimamizi wa makao hayo aliwaomba Mashahidi wawaonyeshe wanawake hao jinsi ambavyo funzo la Biblia la kibinafsi linafanywa.
Stacy na dada wengine wawili walipata pia matokeo kama hayo katika makao mengine ambapo nakala tano za trakti hiyo zilitolewa na nyingi zaidi ziliombwa. Mfanyakazi mmoja alisema hivi: “Kijitabu hiki kitawasaidia wanawake wanaoishi hapa.” Akaongezea hivi: “Tunahitaji habari hizi.” Katika ziara nyingine, wanawake kadhaa katika makao hayo walikusanyika pamoja ili kuona jinsi ambavyo funzo la Biblia la kibinafsi linafanywa, na wanawake wawili walisema wangependa kuhudhuria mkutano uliofuata wa mwisho juma katika Jumba la Ufalme.
Stacy anasema hivi: “Tulishangazwa na jinsi ambavyo makala hiyo nzuri ilipokelewa. Makala hiyo inapochapishwa na kukunjwa, ni njia inayovutia ya kushiriki ujumbe wa Ufalme na watu hao walio na hali za pekee. Tuliguswa moyo sana na itikio lao zuri, na tunatazamia kwa hamu kuona jinsi Yehova atakavyobariki jitihada zetu za kuwafikia wanawake hao na habari njema.”