Zaidi ya Yote Iweni na Juhudi Nyingi Katika Kupendana
KWA VILE “mwisho wa mambo yote” u karibu, ni jambo gani la kutokeza ambalo imewapasa wale wanaotamani uzima katika Taratibu Mpya iliyoko mbele wasitawishe? Katika 1 Petro 4:8-10, mtume aliyeongozwa na roho ya Mungu anaandika hivi:
1, 2. Kulingana na mtume aliyeongozwa na roho ya Mungu, imetupasa tusitawishe nini zaidi ya yote, ikiwa tunataka kuishi katika taratibu mpya ya Mungu?
2 “Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi. Mkaribishane ninyi kwa ninyi, pasipo kunung’unika; kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu.”
3, 4. Kwa sababu ya jambo tunalojua litakuwamo katika taratibu mpya bila shaka, imetupasa tupendezwe sana na nini sasa?
3 Hatuna njia ya kujua kama vitu kama motokaa, televisheni, vinanda au vitu vinavyofanana na hivyo, vikiwako, vitakuwa na sehemu gani duniani wakati wa taratibu mpya ya Mungu. Lakini kuna jambo moja tunalojua litakuwamo katika taratibu hiyo mpya, jambo ambalo kwa sasa tunashughulika nalo kila siku. Ni jambo gani hilo?
4 Watu; watu ambao, kama wewe mwenyewe, wanapenda yaliyo haki. Basi, kuliko kujenga kupendezwa na maisha zetu juu ya vitu vinavyotengenezwa na vifaa vya taratibu hii, vitu ambavyo havina uhakika kama vitaendelea, ni heri na ni jambo la hekima kupendezwa sana na watu na kujifunza namna ya kupata furaha ya kweli katika kuwatumikia wengine. Bila shaka maisha katika taratibu inayokaribia yatajaa sana utumishi huo wa upendo na “kuhudumiana.” Ikiwa tunaweza kuona furaha ya kweli na uradhi katika kufanya hilo sasa—kupenda kuwatumikia wengine, kuwa wenye msaada, kutumikia faida zao, kuwa wenye kufikiria na wakaribishaji—hapo tunaelekea kufaulu katika maisha ya Taratibu Mpya.
5. (a) “Juhudi nyingi katika kupendana” itatimiza nini, na kwa sababu gani hii ni ya lazima? (b) Tafadhali toa maelezo juu ya maandiko yaliyo mwishoni mwa fungu hili.
5 Kama mtume anavyosema, ili tufanye hivyo wapaswa upendo wetu uwe na “juhudi nyingi,” au, kama tafsiri nyingine zinavyosema, “uwe na nguvu nyingi,” “usiwe wa unafiki hata kidogo,” “mwingi.” (New English Bible; Jerusalem Bible; New World Translation) Katika maana halisi, neno la awali la Kigiriki lililotafsiriwa “juhudi nyingi” linamaanisha “uliokunjuka.” Kwa hiyo, upendo wetu hauwezi kuwa nusu, ukifanya tunayoona inatupasa tuyafanye tu, au tunayoona kwamba hayatatusumbua sisi, wala hauwezi kuwapendelea wachache tu. Unapaswa ukunjuke, uwafikie wengi kwa kadiri uwezavyo na vile vile ujifanyie juhudi nyingi. Upendo wa namna hiyo peke yake ndio utakaotuwezesha sisi tuendeleze umoja wa lazima pamoja na ndugu zetu chini ya hali nyingi za namna mbalimbali ambazo zingeweza kuharibu ujamaa wetu na kutufanya tuwe wenye kulaumu, au tuelekee kufunua na kuyafanya makosa ya ndugu zetu yawe sababu kubwa. Lakini “upendo mwingi” (NW) ‘utakunjuka’ ufunike hali hizo zo zote.—Linganisha Mithali 10:12; Wakolosai 3:12-14.
6, 7. (a) Ni maulizo gani tunayoweza kujiuliza wenyewe ili tujue kama tunakosa juhudi katika upendo wetu? (b) Upendo huo ‘husitirije wingi wa dhambi’? Kwa sababu gani hii itakuwa lazima hata kufuata “dhiki kubwa”?
6 Je! upendo wetu uko hivyo sasa? Katika saa chache ambazo kwa kawaida tunatumia tukiwa pamoja na ndugu zetu kila juma, je! upendo wetu unafunika makosa ya wengine? Au je! tunaelekea kuudhika na kukasirika kwa sababu ya makosa hayo? Wengine wanaona vigumu kupatana na wengine, na hivyo wanaruhusu tofauti zitokee, uadui unaanza. Lakini ikiwa mtu anaona vigumu kupatana na ndugu zake sasa kwa saa chache kila juma, namna gani, basi, ikiwa anaokoka na kuingia katika taratibu mpya ya Mungu na anajikuta mwenyewe amezungukwa na ndugu zake pande zote, kila siku na mchana kutwa?
7 “Juhudi nyingi katika kupendana” haitamruhusu mtu aendelee kuweka makosa moyoni, akiyakumbuka hata kuwaonea wengine uchungu, akiendelea na mawazo hayo mabaya bila kuyaondoa. Kwa kuyaondoa katika akili na moyo au kuchukua hatua za kusitawisha hali nzuri, upendo huo ‘husitiri wingi wa dhambi.’ Unatuongoza katika kutoa msaada wetu kwa wale wanaoelekea kudhoofika au kutumbukia katika makosa, bila kuwa wenye kuwalaumu au kuwasengenya. (Yak. 5:20) Kwa kuwa dhambi hazitatoweka duniani kwa siku moja katika taratibu mpya inayokuja, ni lazima tuwe na huo upendo mwingi ili tuhakikishe tunaendeleza ujamaa mwema na Yehova Mungu, ambaye “ni upendo,” na Mwana wake, ambaye upendo wake mwenyewe mwingi ulimwongoza autoe uhai wake mwenyewe kwa ajili ya wenye dhambi.—Rum. 5:6-8.
8. (a) Ni mwendo gani ambao tena Petro anasihi kuwa wonyesho wa upendo mwingi? (b) Hii itatusaidiaje katika kujitayarisha kuishi katika Taratibu Mpya?
8 Sisi vile vile tunaweza kuonyesha upendo huo kwa ukaribishaji wetu. “Mwe wenye kukaribishana”; “karibishaneni katika nyumba zenu bila kuguna.” (1 Pet. 4:9, New American Bible; Jerusalem Bible) Ndiyo, lo lote tulifanyalo kupatana na haya limepaswa liwe pasipo manung’unu, kwa maana “yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu” peke yake ndiye anayependwa na Mungu. (2 Kor. 9:7) Inaelekea kutakuwako kushiriki kwingi kwa mambo ya kimwili katika kipindi cha kwanza wakati “dhiki kubwa” itakapopita. Maelekeo yo yote ya kuwa mtu asiye mkarimu au mtu mwenye unyimivu yangeweza kutufanyia matata makubwa wakati huo. Lakini, ikiwa tunaonyesha roho kama ile ya Wakristo waliokuwa katika Yerusalemu waliozifungua nyumba zao wakawakaribisha na kuwalisha ndugu zao wapya kati ya wanafunzi wapya 3,000 waliobatizwa, hapo tunajitayarisha kwa maisha katika Taratibu Mpya. (Matendo 2:46; 4:32-35) Kama mtume Paulo anavyosihi: “Shirikini pamoja na watakatifu kulingana na mahitaji yao. Fuateni njia ya ukaribishaji.”—Rum. 12:13, NW.
MAWAKILI WEMA WA KARAMA ZA MUNGU
9. Kila mmoja katika kundi la Kikristo ‘aliipokeaje karama,’ na imempasa aifanyie nini?
9 “Kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana [jiwekeni wenyewe tayari kuwatumikia wengine, Je].” Katika njia hii sisi tunatenda “kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu.” (1 Pet. 4:10) Na, kwa kweli, hakuna wo wote kati yetu wasio na jambo la kutoa katika kuwahudumia ndugu zetu. Kila mtu anayekuja katika mpango wa kitheokrasi wa Mungu anapokea karama. Kila mtu anayo mambo ya kufanya, migawo ya utumishi au madaraka. Sisi sote hatuko namna moja, hatuna utu ule ule, uwezo, akili, nguvu, ujuzi au mali zile zile. Lakini cho chote tulicho nacho, tunawiwa na Mungu. (Rum. 12:6-8; 1 Kor. 4:7) Tukifahamu haya, hatutaifanya “karama” yetu ikae tu bila kutumiwa, kana kwamba imewekwa katika kasha la hazina. (Mt. 25:14-30) Inatupasa tuitumie, tuifanyie kazi, katika kuwatumikia wengine.
10. Kuwa kwetu “mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu” kunamaanisha nini?
10 Uhakika wa kwamba sisi tunaitwa “mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu” unaonyesha kwamba “karama” hii ni amana. Wakati wa kuipokea karama hiyo mpokeaji anakuja chini ya daraka kwa Mpaji, Yehova Mungu. “Wakili” au msimamizi wa nyumba katika nyakati za Biblia aliwekwa na mwenye nyumba na alitakiwa ashughulike na washiriki mbalimbali wa nyumbani. Alitakiwa awatendee katika njia yenye msaada. Watumishi wenzake walitiwa moyo na wakili wazitimize kazi zao wenyewe kwa uaminifu. Je! Mungu ametupendelea sisi kwa kutupa mapendeleo, nafasi, migawo au madaraka? Hii ni neema kwa upande wake nasi twataka tuitumie neema hiyo ili tuyatimize mapenzi yake, tutimize kusudi la kutuonyesha sisi neema au kibali hicho.—Linganisha Luka 12:42-44.
11. Neema ya Mungu ambayo kwa habari yake tunaweza kuwa mawakili, inajionyeshaje kuwa “mbalimbali,” na je! ndivyo na wazee vile vile?
11 Mungu katika hekima yake ametoa “tofauti za huduma” zenye kuongozwa kwa roho ile ile, na “tofauti za kutenda kazi, bali Mungu ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote.” Kwa roho yake, Mungu anaweza kumsaidia kila mmoja wa sisi atumie au kusitawisha alicho nacho, “kwa kufaidiana.” (1 Kor. 12:4-7) Ijapokuwa inawapasa wote wayatimize matakwa ya msingi, wazee, kama ‘mawakili’ wa Mungu (Tito 1:7), vile vile wanazo nguvu na uwezo wa pekee. Huenda wengine wakazidi katika kufundisha jukwaani, hali wengine huenda wakawa wenye nguvu zaidi katika kufundisha kwa bahati tu, labda katika kuwasaidia washiriki wa kundi au jamaa katika matatizo yao ya kipekee kwa kuwatembelea nyumbani au katika maongezi ya faragha.—Matendo 20:20.
12. (a) Tofauti iyo hiyo inaonekanaje katikati ya washiriki wote wa kundi katika kuzitumia kwao “karama” katika kuhudumia? (b) Tafadhali toa maelezo juu ya Warumi 12:6-8.
12 Vile vile, kila mshiriki wa kundi anazo karama tofauti-tofauti ambazo anaweza kutumia katika kuhudumiana na wengine. Wote wanaweza kushiriki katika mikutano, na tofauti ya maelezo na uwezo ina matokeo yenye kujenga. Katika kushiriki katika kazi ya kuzihubiri habari njema za Ufalme kwa watu nyumbani kwao, huenda wengine wakaweza kuweka mfano bora katika kuangusha vitabu vya Biblia au katika kuanzisha maongezi na katika kujibu vipingamizi. Huenda wengine wakafanya vema sana katika kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani. Huenda wengine wakawa na uwezo bora wa kuwakaribisha vizuri wapya katika mahali pa kukutania hata upesi wanajiona kama wako nyumbani. Au huenda mtu akawa na uwezo wa ajabu wa kushughulika na vijana au watoto, ambao vile vile ni lazima wajione kwamba ni wenye maana na wanastahili kuangaliwa. Huenda mwingine akafanya vizuri sana katika kuwatembelea washiriki wa kundi ambao ni wagonjwa au labda wanahuzunika, aweze kuwachangamsha na kuwatia moyo katika imani yao katika wema wa Yehova. Kama Paulo alivyowaandikia Wakristo katika Rumi juu ya karama ambazo Mungu aliwapa: “Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema tuliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia, kwa bidii; mwenye kurehemu, kwa furaha.”—Rum. 12:6-8.
13. Kuliko kuongoza kwenye kujikinai, tofauti ya kuonyeshwa kwa neema za Mungu imepaswaje itutie moyo, na hii imepaswa iwe na matokeo gani juu ya kundi?
13 Hivyo, ijapokuwa sisi sote tunaweza kuendelea kutafuta kufanya maendeleo na vile vile kujifunza kwa mifano mizuri ya wengine, si lazima tuvunjike moyo hata kidogo kwa sababu hatuwezi kutimiza yale ambayo wengine wanaweza kutimiza. Sisi sote tunaweza kupokea “neema mbali mbali za Mungu” na kutoa kile ambacho tumepokea. Ikiwa kila mtu anatoa kile alicho nacho, kundi linatajirishwa kwa kiroho kwa tofauti nyingi za karama na linakuwa kama mwili wenye afya, ambao viungo vyake vingi vinatenda kazi pamoja kwa kupatana kwa faida ya mwili wote. (Linganisha Warumi 12:3-5.) Utoaji huo usio wa choyo kwa ajili ya wengine hautakoma wakati Yehova Mungu atakapowapitisha watu wake katika “dhiki kubwa” kuingia katika taratibu yake mpya.
KUSEMA NA KUHUDUMU KWA UTUKUFU WA MUNGU
14. Ni “karama” gani ambayo imetupasa tuione kuwa bora sana kwa “kuhudumiana,” na imepaswa ituongoze tufanye nini?
14 Bila shaka imetupasa sote tuzijaze akili na mioyo yetu kweli ya Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake, tukilisoma kwa bidii. Ndipo tutakapokuwa na jambo linalofaa sikuzote kutoa kwa kiroho, jambo linalopita karama zo zote za vito vyenye bei au dhahabu na fedha, kwa sababu ya baraka za ajabu zinazotokea. (Mit. 2:1-6; 3:13-18) Hasa ambao imewapasa wafanye hivi ni wale walio na pendeleo la kutumikia katika makundi kama wazee. Imewapasa wapendezwe sana na kutimiza shauri jingine la mtume Petro:
15, 16. Tunawezaje ‘kusema kama mausia ya Mungu’ kupatana na shauri la Petro na Paulo?
15 “Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye hata milele na milele. Amina.”—1 Pet. 4:11.
16 Sasa, kwa kuwa mwisho wa taratibu ya kale unakaribia, kuna uhitaji sana wa kusema kwa kusadikisha na kwa imani. Je! ndivyo wewe unavyosema wakati unapopendelewa kutumikia mbele ya kundi au unaposema pamoja na ndugu zako juu ya mambo ya kiroho? Je! uko kama Paulo, ambaye ‘hakuja kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima ya kibinadamu,’ bali ambaye maneno yake na kuhubiri kwake kulikuwa “kwa dalili za [roho ya Mungu] na za nguvu,” ili imani ya wasikiaji wake “isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu”? (1 Kor. 2:1, 4, 5) Si akili ya mtu mwenyewe au ‘njia yenye maneno ya kushawishi,’ bali ujuzi kamili wa Neno la Mungu na kanuni zake na kufahamu sana haja ya kuwakilisha kwa uaminifu na kushikamana kwa ustahifu na Neno hilo ndiko kutakakotuwezesha tufanye hivi.
17. Kwa sababu gani imewapasa hasa wazee watafute kulitumia shauri hili kwa kuwa tunaikaribia Taratibu Mpya?
17 Huenda kati ya sasa na siku zilizo mbeleni watu wa Mungu wakapatwa na majaribu mazito sana, hatari na magumu. Imewapasa wale wenye pendeleo la ‘kulichunga kundi la Mungu’ waweze kuonyesha kwamba shauri lao, uongozi na hukumu viko juu ya Neno la Mungu lisilo na makosa. Kama Yesu, wanataka waweze kusema: “Imeandikwa.” (Mt. 21:13) Ndipo ndugu zao watakapojua kwamba tumaini lao limewekwa sawasawa—si katika wanadamu bali katika Mungu, ambaye, kupitia kwa Mwana wake na kwa roho yake, anawatumia wanaume hao kwa ajili ya watumishi wake. Maisha zi hatarini, na kukosa bidii au kufikiria katika neno hili kusingeweza kuleta hata kidogo kibali cha Mchungaji Mkuu, Yehova Mungu, na Mchungaji Mwema wake, Kristo Yesu. Na bila kujali utumishi wo wote ambao huenda wazee wa Kikristo wakatakiwa kuufanya katika wakati ujao katika taratibu mpya ya haki, kujitayarisha na kujizoeza kwao katika njia hii sasa bila shaka kutawategemeza wakati huo.—Yohana 10:11; Matendo 20:28-30; 1 Pet. 2:25; 5:1-4.
18. Sisi sote tunawezaje kufuata mfano mwema wa wazee katika kusema kwetu, na tunataka tujihadhari na nini?
18 Ndiyo, inawapasa wazee wawe “vielelezo kwa lile kundi,” na ndivyo na sisi sote inavyotupasa tuwe. (1 Pet. 5:3) Ikiwa kweli tunaziamini ahadi za taratibu mpya ya Mungu na inavyokaribia, jambo hili litaonekana katika usemi wetu. Tutaonyesha kwamba sisi ‘tunatazamia kuja kwa siku ile ya Mungu, na kuihimiza.’ (2 Pet. 3:12) Lakini kusema kunaweza kuwa maneno matupu, nasi hatutaki tusingizie kuwa na “juhudi nyingi katika kupendana” ‘kwa neno au kwa ulimi tu, bali tuionyeshe katika tendo na kweli.’ (1 Yohana 3:18) Na hivyo shauri la mtume lililoongozwa na roho ya Mungu linaongeza hivi:
19. (a) Kwa sababu gani kuhudumia katika kundi kunataka nguvu nyingi? (b) Wale wanaohudumia hivyo wanawezaje kutiwa moyo waendelee kufanya bidii na kujitahidi wenyewe?
19 “Mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu.” (1 Pet. 4:11) Ili waseme na kufundisha kwa mfano wa Yesu, Petro, Paulo, Yohana na wachungaji wengine waaminifu, inawapasa wazee katika makundi wafanye bidii, na wale wanaofanya hivyo wanapaswa “wahesabiwe kustahili heshima maradufu” na kuwastahi “sana katika upendo, kwa ajili ya kazi zao.” (1 Tim. 5:17; 1 The. 5:12, 13) Kujitaabisha kwao kwa ajili ya kundi, ‘kuonya wale wasiokaa kwa utaratibu; kuwatia moyo walio dhaifu; kuwatia nguvu wanyonge; kuwavumilia watu wote,’ kwaweza kuwachosha. (1 The. 5:14) Huenda wakaona kwamba, kama Paulo, ‘wanamiminwa juu ya dhabihu na ibada ya imani’ ya ndugu zao. Lakini baraka zinazoletwa na kufanya hivi zaweza ‘kuwafurahisha,’ wakati mfano wao wa bidii unapowatia moyo ndugu zao wamtumikie Mungu kwa moyo wote.—Flp. 2:17, 18; Ebr. 13:7.
20. Kwa sababu gani kusihi kwa Paulo wazee juu ya jambo ili hili kulikuwa na maana kubwa, na tunajifunza nini kutokana na shauri hilo?
20 “Wazee wa kanisa” la Efeso waliujua sana mwendo ambao mtume Paulo alikuwa ameweka kati yao wa kumtumikia “Bwana kwa unyenyekevu wote, na kwa machozi, na majaribu.” Hivyo maneno yake yangepaswa yawe na maana kubwa kwao wakati alipowasihi hivi: “Kesheni, mkikumbuka ya kwamba miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mtu kwa machozi. . . . Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu. Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumikia kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.”—Matendo 20:17-20, 31-35.
21. Sisi sote tunawezaje ‘kuhudumu kwa nguvu tunazojaliwa na Mungu,’ na kwa uhakika gani?
21 Katika rehema yake Mungu ametupa sote pendeleo la kuhudumu, la kutumikia kama “mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu.” Ikiwa katika imani tunazitegemea ‘nguvu tunazojaliwa na Mungu,’ ‘hatutachoka katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.’ (1 Pet. 4:10, 11; Gal. 6:9) Uhakika wa taratibu yake mpya iliyoahidiwa umepaswa utuhimize tuendelee mbele, na kukaribia kwake kumepaswa kututie azimio zaidi. Pamoja na mtume, tunaweza kusema: “Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa; lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku.” Ikiwa ‘tunahudumu kwa nguvu tunazojaliwa na Mungu,’ hakuna jambo ambalo Mungu ametupa tulifanye tusiloweza kulifanya. Yeye anatupa “uwezo usio wa kawaida” hata ‘tunayaweza mambo yote katika yeye atutiaye nguvu.’—2 Kor. 4:7, NW, 16; Flp. 4:13.
22, 23. Kwa sababu gani haitupasi tuvunjike moyo au kudhoofika hata kidogo katika kuhudumu kwetu bali, pahali pake, imetupasa tujitahidi kufanya zaidi?
22 Huenda yale ambayo tunatimiza yakaonekana madogo machoni petu na kutufanya tusijulikane sana. Hata hivyo Yehova hakosi kushukuru yale tunayofanya wala yeye “si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia.” Kwa kuwa wakati unaotamaniwa sana wa taratibu yake mpya u karibu sana, huu ndio wakati wa nyakati zote wa kuendelea kuionyesha “bidii ile ile, kwa utimilifu wa matumaini hata mwisho.”—Ebr. 6:10, 11.
23 Tukifanya hivi tutapata baraka za ajabu ambazo tumewekewa akiba. Na kwa njia hiyo tutakuwa tayari kushiriki sana na kwa furaha na kwa matokeo mema nyakati hizo bora katika taratibu mpya ya Mungu kwa sababu tumekaza fikira zetu juu ya mambo yaliyo ya lazima sana sasa.
24. “Ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo,” inatupasa tufanye nini sasa na katika taratibu mpya inayokuja?
24 Lo lote tulifanyalo, na katika yote tuyafanyayo—katika shughuli zetu za kila siku na mambo na maisha ya jamaa, katika kuwahudumia wale walio katika ulimwengu wa wanadamu kwa neno la uzima, na katika kuhudumiana katika kundi la Kikristo—na ‘tufanye yote kwa utukufu wa Mungu,’ tujionyeshe wenyewe kuwa wanafunzi wa kweli wa Mwana wake mpendwa, Yesu Kristo. (1 Kor. 10:31) Ndipo sisi sote pamoja, twaweza kutumikia kama kito chenye sifa kwa jina la Yehova katika dunia yote, kama watu walio tayari kwa uzima katika taratibu yake mpya. Kwa maana “utukufu na uweza una yeye hata milele na milele. Amina.”—1 Pet. 4:11.
—Kutoka The Watchtower, June 15, 1973.