Dunia Iliyosafishwa
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1, 2. Hali ya dunia ni nini, na kwa sababu gani wanadamu hawawezi kuisafisha?
WATU wachache watakana kwamba hatuishi katika dunia iliyochafuliwa, iliyonajisiwa. Hii ni kweli si kutokana na maono yenyewe tu, maziwa, mito, bahari na hewa vikichafuliwa, lakini vile vile katika maana ya adili. Kuna uchafu katika sehemu za juu, ufisadi, ugonjwa, na kunajisiwa kwa nchi kwa kumwaga damu na kuua na vita.—Linganisha Hesabu 35:33, 34.
2 Nini kinachohitajiwa kwa kusafishwa kwa dunia? Wanadamu wanashindwa kwa sababu hawawezi kufikia chanzo cha uchafu. Nini chanzo hiki kisichoweza kufikiwa? Biblia inaelekeza kwenye taabu kama ikitoka katika makao yasiyoonekana yanayoitwa “nchi ya Magogu.” Gogu, yaani, Shetani Ibilisi tangu alipotupwa kutoka mbinguni, anatajwa kama kiongozi wa makao haya. Wao ni akina nani? Ni mashetani washiriki wa Ibilisi, watu waovu wa kiroho. Ni malaika ambao walimwasi Mungu nao wamehukumiwa uharibifu. (1 Pet. 3:19, 20; 2 Pet. 2:4; Yuda 6) Twapata ushuhuda wa hawa wakisumbua wanadamu wakati Yesu alipokuwa duniani.—Luka 4:33-35; 8:27-33.
3. Kupinga kwa mashetani kunafikia upeo namna gani?
3 Leo kupinga kwao Mungu na kusumbua kwao dunia kunafikia upeo. Kwa sababu gani? Kwa sababu uharibifu wao u karibu sana, na vile vile kwa sababu sasa wamewekewa mipaka katika kazi zao wasitoke katika dunia hii. Eneo hili lililozuiwa, lisiloonekana na wanadamu, linaitwa na Biblia “nchi ya Magogu,” mkuu wake akiwa ni Shetani Ibilisi. Ufalme wa Mungu uliposimamishwa mikononi mwa Yesu Kristo mwishoni mwa “nyakati zilizowekwa za mataifa” katika mwaka wa 1914, mashetani ‘walitupwa chini duniani’ pamoja na mkuu wao, Shetani. Katika kukata tamaa kwao wanapinga yote yaliyo haki nao wanauleta ulimwengu katika hali chafu, katika jaribio la kuondoa kabisa yote yanayokamatana na ibada ya kweli ya Mungu. Biblia yasema: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”—Ufu. 12:5, 7-12.
4-6. (a) Kwa sababu gani Yehova ameiruhusu hali ifikie kadiri ambayo imefikia? (b) Yeye anasimuliaje atakachofanya?
4 Maongozi ya “Gogu” ni yenye nguvu sana hivi kwamba anaitwa katika Biblia “mungu wa hii taratibu ya mambo.” (2 Kor. 4:4, NW; linganisha Yohana 12:31; 14:30.) Mtume Yohana aliandika: ‘Dunia yote hukaa katika yule mwovu.’ (1 Yohana 5:19) Kwa hiyo utawala kwa njia ya wanadamu katika serikali mbalimbali zilizofanyizwa na mwanadamu umekuwa ukiongozwa na Ibilisi, ijapokuwa huenda watawala wenyewe wasijue hivyo. Kwa hiyo, serikali hizi zilizofanyizwa na mwanadamu lazima ziharibiwe na Mungu, lakini Yehova anangoja mpaka Gogu, Ibilisi, atakapozileta hizi serikali katika shambulio moja, la moja kwa moja, la waziwazi juu ya mashahidi wake wa Kikristo. Kwa njia hii yaonyeshwa wazi kwa watazamaji wote kwamba serikali hizi zinastahili uharibifu. Kwa hiyo, Yehova amwambia Gogu:
5 “Bwana [Yehova] asema hivi; Tazama, mimi ni juu yako, Ewe Gogu, mkuu wa Roshi, Mesheki, na Tubali; nami nitakugeuza na kukuongoza, nami nitakupandisha toka pande za mwisho za kaskazini; nami nitakuleta juu ya milima ya Israeli; nami nitaupiga upinde wako, utoke katika mkono wako wa kushoto, na mishale yako nitaiangusha, itoke katika mkono wako wa kulia. Utaanguka juu ya milima ya Israeli, wewe, na vikosi vyako vyote, na watu wa kabila nyingi walio pamoja nawe; nami nitakutoa na kuwapa ndege wa kila namna walao nyama, na wanyama wa nchi, uliwe na wao. Utaanguka katika uwanda; kwa maana mimi nimenena.”—Eze. 39:1-5.
6 Yehova anamkamata Gogu pale pale, kana kwamba ilikuwa, anapolileta tengenezo lake lote la kidunia juu ya Yehova kwa kushambulia mawakili wake duniani. Wote duniani wataweza kuona hili. Wote wanaojipatanisha wenyewe na Gogu lazima wafe. Hakutakuwako mahali pa kukimbilia, hata mahali pa mbali kama visiwa pakiwa si kimbilio.
7, 8. Namna gani juu ya wale wanaokaa katika makao yasiyoonekana, “nchi ya Magogu”?
7 Namna gani, hata hivyo, juu ya makao yasiyoonekana ambamo Shetani anakaa, “nchi ya Magogu”? Hata mahali hapa palipo peke yake, panapoitwa “pande za mwisho za kaskazini,” hapataokoka. Yehova anasema:
8 “Nami nitapeleka moto juu ya Magogu; na juu ya watu wote wakaao salama katika visiwa; nao watajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova]. Na jina langu takatifu nitalifanya kuwa limejulika kati ya watu wangu Israeli; wala sitaliacha jina langu takatifu kutiwa unajisi tena; nao mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova], na Aliye Mtakatifu katika Israeli.”—Eze. 39:6, 7.
9, 10. Ni kupitia kwa nani, na kwa njia gani, Yehova ‘atapeleka moto juu ya Magogu’?
9 Yesu Kristo, Jemadari Mkuu wa Yehova, ni mtu wa kiroho, mwenye uwezo wa kumharibu Ibilisi. (Ebr. 2:14) Kupitia kwake Yehova anapeleka “moto juu ya Magogu.” Hii inafuata mara tu nyuma ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” penye Har–Magedoni, iliyotangulia kusemwa katika Ufunuo 16:14, 16; 19:11-21. Nyuma ya vita hii Kristo anachukua tendo kwa kipekee juu ya Gogu, kama vile habari ya Ufunuo inavyoendelea:
10 “Kisha nikaona malaika akishuka kutoka mbinguni, mwenye ufunguo wa kuzimu, na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; akamtupa katika kuzimu, akamfunga, akatia muhuri juu yake, asipate kuwadanganya mataifa tena, hata ile miaka elfu itimie; na baada ya hayo yapasa afunguliwe muda mchache.”—Ufu. 20:1-3.
11-13. Unabii unasema nini juu ya matumizi ya vifaa vya vita vya majeshi ya Gogu?
11 Lo! ni kitulizo kama nini kwa wale wanaobaki duniani! Lakini je! hesabu kubwa ya ajabu ya waliouawa na vita ya tengenezo la kidunia la Gogu, na vifaa vyao vya vita, itaondolewaje? Unabii wafunua wazi:
12 “Tazama, linakuja, nalo litatendeka, asema Bwana [Yehova]; hii ndiyo siku ile niliyoinena. Hao wakaao katika miji ya Israeli watatoka, nao watafanya mioto kwa silaha za vita na kuziteketeza, ngao, na vigao, na pinde, na mishale, na mafumo, na mikuki, nao watazitumia kama kuni kwa muda wa miaka saba; hata hawataokota kuni mashambani, wala hawatakata kuni msituni; maana watafanya mioto kwa silaha zile; nao watawateka nyara watu waliowateka wao, na kunyang’anya vitu vya watu walionyang’anya vitu vyao.”—Eze. 39:8-10.
13 Nyuma ya ushindi wa Yehova ambamo analitukuza jina lake juu ya yote mengine katika ulimwengu wote, waokokaji duniani, wanaoitwa hapa “hao wakaao katika miji ya Israeli,” bila shaka hawataweka vyo vyote vya vyombo vya vita vinavyochukiza na vyenye kufisha kama vitu vya ukumbusho. Wataviondosha, wakitumia vitu hivyo kwa makusudi yenye kufaa.
14-16. Nini kinachofananishwa na unabii kwa kusema itachukua “miezi saba” kuwazika wafu?
14 Nyuma ya ‘ndege walao nyama’ na ‘wanyama wa kondeni’ kushiba mizoga ya adui za Mungu waliouawa, je! kutakuwako kazi kubwa sana ya kuzika kwa waokokaji? Je! tutaifahamuje sehemu ifuatayo ya unabii wa Ezekieli? Kwa maana inasema:
15 “Tena, itakuwa katika siku hiyo, nitampa Gogu pa kuzikia katika Israeli, bonde la wapitao, upande wa mashariki wa bahari; nalo litawazuia wapitao; na huko watamzika Gogu na watu wake jamii yote; nao wataliita, Bonde la Hamon-Gogu. Na kwa muda wa miezi saba nyumba ya Israeli watakuwa wakiwazika, wapate kuisafisha nchi. Naam, watu wote wa nchi hiyo watawazika; itakuwa ni sifa kwao katika siku ile nitakapotukuzwa, asema Bwana [Yehova].”—Eze. 39:11-13.
16 Wakiwako wafu wengi namna hiyo, ingekuwako hatari kubwa ya ugonjwa. Vile vile, kazi ingekuwa kubwa mno kwa wachache kwa kulinganisha walioachwa duniani. Kwa hiyo usemi “miezi saba” kwa wazi unatumika tu kuonyesha ukubwa wa kundi la watu wasiomcha Mungu watakaotoweka. Zaidi ya hayo, kwa kuwa mizoga ilionwa michafu katika Israeli, ‘kuzikwa’ kwayo kwamaanisha kwamba dunia hii itasafishwa unajisi wote ambao Gogu na watumishi wake wasiomcha Mungu wameleta.—Hes. 19:11-13; 2 Pet. 3:13.
17. Wafu waliomo katika Bonde la Hamon-Gogu ‘watawazuiaje wapitao’?
17 Kumbukumbu la wale walioinajisi dunia na wakamwunga Gogu katika shambulio lake lenye kumkaidi Mungu litakuwa lenye kutapisha kwa wale watakaookoka kama uvundo unaotoka kwenye mizoga inayooza ya kundi la Gogu. Kwa usemi wa mfano ‘litaziba pua zao.’ Wale waliouawa wamejipatia wenyewe aibu ya milele. Hakuna kumbukumbu lao kama mashujaa wa vita. Ili kutoa mfano wa wazi wa ukamili wa kusafishwa kwa dunia chini ya ufalme wa Kimasihi, Yehova anaendelea kusema juu ya waokokaji wa shambulio la Gogu:
18, 19. Nini kinachofananishwa na mji Hamona?
18 “Nao watawachagua watu wa kufanya kazi ya daima, watakaopita kati ya nchi, ili kuwazika waliosalia juu ya uso wa nchi, ili kuisafisha; miezi saba itakapokwisha kupita watatafuta. Na hao wapitao kati ya nchi watatafuta; na mtu ye yote aonapo mfupa wa mtu, ndipo atakapoweka alama karibu nao, hata wazishi watakapouzika katika bonde la Hamon-Gogu. Tena, Hamona litakuwa jina la mji. Hivyo ndivyo watakavyosafisha nchi.”—Eze. 39:14-16.
19 Mji Hamona utakaliwa na wale watakaookoka ‘waisafishe nchi.’ Haielekei kuwa busara kwamba kutakuwako mji wa kweli unaoitwa Hamona, kwa maana waokokaji watakuwako duniani pote, shambulio la Gogu na uharibifu wa majeshi yake vikiwa vimekuwa vya duniani pote. Bali, mji Hamona (maana yake “kundi”) wa watu walio hai kando ya Bonde la Kundi la Gogu waonekana kufananisha tengenezo la walio hai kwa kutofautisha na makundi yaliyokufa ya kundi la Gogu.
20-23. Yaelekeaje kuwa maiti za watakaoharibiwa zitaondolewa nyuma ya Har–Magedoni?
20 Malipo yanayofaa yanakuja kwa wale kati ya kundi la kidunia la Gogu, ambao hawakuua watu tu lakini waliua wanyama vile vile kwa mchezo tu au katika njia yenye pupa kwa ajili ya biashara. Yehova anaendelea kusema:
21 “Sema na ndege wa kila namna, na kila mnyama wa kondeni, Jikusanyeni, mje; jikusanyeni pande zote mwijilie sadaka yangu niifanyayo kwa ajili yenu, naam, sadaka kubwa juu ya milima ya Israeli, mpate kula nyama na kunywa damu. Mtakula nyama yao walio hodari, na kunywa damu ya wakuu wa dunia, ya kondoo waume na ya wana-kondoo, na ya mbuzi, na ya ng’ombe, wote ni wanono wa Bashani. Nanyi mtakula mafuta na kushiba, mtakunywa damu na kulewa, na sadaka yangu niliyoifanya kwa ajili yenu.
22 “Nanyi mtashibishwa mezani pangu kwa farasi, na magari ya vita, na mashujaa, na watu wote wa vita, asema Bwana [Yehova].”—Eze. 39:17-20.
23 Unabii wa Ufunuo vile vile unasimulia uharibifu wa majeshi ya kidunia ya Shetani, ukitoa karibisho kwa ndege waje “kwa karamu ya Mungu iliyo kuu.” (Ufu. 19:17) Wakati fulani uliotangulia adui ya Mungu wa wazi alitafunwa na mbwa, ikiachwa mifupa michache tu ya kuzikwa. (2 Fal. 9:30-37) Lakini wanyama hawawezi kumaliza wote watakaouawa penye Har–Magedoni. Kwa hiyo, Mungu Mwenye Nguvu Zote bila shaka atatumia njia za juu za kisayansi katika mikono yake kuyaondoa masalio ya miili inayooza katika njia ya haraka na isiyodhuru afya. Twakumbuka kwamba Nuhu na waokokaji saba wenzake wa gharika ya dunia yote hawakulemezwa na kuzika wanadamu waliopatwa na maangamizi hayo ya ulimwengu nyuma ya walipotoka katika safina na kufanya ibada ya Yehova upya duniani.—Mwa. 8:18-22.
24. Kwa sababu gani haitupasi kuogofishwa na habari ya Ezekieli ya uharibifu mkubwa wa kundi la Gogu?
24 Je! turudi nyuma katika woga mwingi kwa kuufikiria uharibifu huo mkubwa? Ikiwa mtu anaelekea kuona hivyo, amepaswa ajiulize mwenyewe, Je! nilionyesha itikio hili kuelekea Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na ya Pili, au nilivitegemeza vita hivi vyenye damu kwa bidii au bila kusema, ambavyo havikupiganwa kwa ajili ya ushuhuda wa Yehova, na havikutokeza dunia iliyosafishwa, ambamo haki yakaa? Jambo tunalopaswa kukumbuka ni kwamba Yehova, kwa pigano hili, anairudisha dunia chini ya enzi yake kabisa ya ulimwengu wote na kuuondoa uovu kusudi kwamba usiwatawale wanadamu tena. Wale wanaoharibiwa ni wamchukiao Mungu. Ikiwa twampenda Mungu kwa kweli, tutasimama upande wake na upande wa Israeli wake wa kiroho, kusudi kwamba tuweze kufurahia kile ambacho Yehova anafuata kumwambia Ezekieli:
25-27. Wakiona wako huru kuwatesa watu wa Mungu, mataifa wamesahau nini?
25 “Nami nitauweka utukufu wangu kati ya mataifa, na mataifa wote wataiona hukumu yangu niliyoitekeleza, na mkono wangu niliouweka juu yao. Basi, nyumba ya Israeli watajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova], Mungu wao, tangu siku hiyo na baadaye. Nao mataifa watajua ya kuwa nyumba ya Israeli walihamishwa, na kwenda kifungoni, kwa sababu ya uovu wao; kwa sababu waliniasi, nami nikawaficha uso wangu; basi nikawatia katika mikono ya adui zao, nao wakaanguka kwa upanga, wote pia. Kwa kadiri ya uchafu wao, kwa kadiri ya makosa yao, ndivyo nilivyowatenda, nami nikawaficha uso wangu.”—Eze. 39:21-24.
26 Hivyo Yehova anaondoa maoni yo yote yenye makosa waliyochukua mataifa wakati walipoweza kutendea watumishi wa Mungu duniani bila woga wa kupata adhabu kama ilivyoonekana. Mataifa haya yalishindwa kujua kwamba Yehova alikuwa anaruhusu watu wake waadhibiwe na kuzoezwa. Hawakufahamu uhakika wa kwamba Mungu alikuwa mkali kwa watu wake wa agano, kwa sababu waliliwakilisha jina lake mbele ya mataifa. Vile vile, aliwaruhusu waadhibiwe kwa sababu ya makosa yao, hata kwa sababu ya makosa yao yasiyo ya kukusudia, kwa sababu aliwapenda naye alikuwa akishughulika nao kusudi kwamba waweze kutumiwa nyumaye kama mbaraka wa kweli kwa watu. (Ebr. 12:7-11; Mwa. 22:18) Si kwamba tu walileta habari njema za Ufalme kwa wale ambao wangesikia, lakini walikuwa wakisafishwa wawe wafalme na makuhani washirika pamoja na Yesu Kristo wakati wa utawala wake wa miaka 1,000 juu ya dunia iliyosafishwa.—Ufu. 20:4, 6.
27 Wale waliofafanuliwa kama wapiga vita juu ya Mungu vile vile walishindwa kuona kwamba mwishowe Yehova alimaliza adhabu yake kwa watu wake katika mwaka wa 1919 C.E. naye akaugeuza uso wake wa kibali kuwaelekea, akiwaweka katika amani ya kiroho na usalama, kama ilivyosimuliwa mapema katika unabii wa Ezekieli. (Eze. 38:8, 11) Mahali pake, mataifa yaliendelea kuwachukia na kuwadharau, mwishowe yakijiunga na Gogu katika jaribio lake lenye msiba la kuwaangamiza watu wa Yehova kabisa. (Mt. 24:9) Ni wachache tu wenye mioyo yenye haki kati ya mataifa haya waliofahamu shughuli ya Mungu na watu wake na kushirikiana nao. Kwa hiyo Mungu anasema:
28, 29. Yehova ameonyeshaje ibada ya pekee kwa jina lake takatifu kwa matendo yake kwa Israeli wa kiroho?
28 “Sasa nitawarejeza watu wa Yakobo waliohamishwa, nitawahurumia nyumba yote ya Israeli; nami nitalionea wivu jina langu takatifu. Nao watachukua aibu yao, na makosa yao yote waliyoniasi, watakapokaa salama katika nchi yao wenyewe, wala hapana mtu atakayewatia hofu; nitakapokuwa nimewaleta tena kutoka kabila za watu, na kuwakusanya kwa kuwatoa katika nchi za adui zao, na kutakaswa kati yao mbele ya macho ya mataifa mengi. Nao watajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova], Mungu wao, kwa kuwa naliwahamisha, waende utumwani kati ya mataifa, na mimi nikawakusanya, na kuwaingiza katika nchi yao wenyewe; wala sitawaacha tena huko kamwe, hata mmojawapo; wala sitawaficha uso wangu tena; kwa maana nimemwaga roho yangu juu ya nyumba ya Israeli.”—Eze. 39:25-29.
29 Kwa kupatana na ambayo Yehova ametabiri, washiriki wa Israeli wa kiroho wamefurahi katika kukusanywa kwao pamoja na Mungu. Kwa umoja wameweza kufanya habari njema za ufalme wake wa Kimasihi zihubiriwe ulimwenguni pote. Ni wachache walioko, zaidi katika nchi zinazoitwa “Kristendomu,” ambao hawalijui jina Yehova. Wanajua kwamba mashahidi wa Yehova wanasimama upande wa ufalme wa Yehova wa Kimasihi kwa imara, wakiwa wenye kutokuwamo kwa habari ya mapigano yote ya kilimwengu na mafarakano ya kisiasa.
30. (a) Kusafisha kwa Yehova mashahidi wake waliotiwa mafuta kumetimiza nini kati ya mataifa? (b) Israeli wa kiroho na wenzi wao wanaliona shambulio la Gogu kwa maoni na matumaini gani?
30 Hawa mashahidi wa Yehova waliotiwa mafuta, wakiwa wamejisafisha kulingana na kanuni za Neno la Mungu na kutokeza matunda ya roho ya Mungu, sasa wanaishi kwa ajili ya taratibu mpya ya Mungu. (Gal. 5:22, 23; Efe. 4:20-24) Mamia ya maelfu kutoka kati ya mataifa wamekuja mbele nao wakakaa pamoja nao katika ‘paradiso ya kiroho’ yao. Hawa watafanyiza “mkutano mkubwa” utakaookoka vita ya Har–Magedoni na kushindwa kwa Gogu, waishi duniani kwa umilele. (Ufu. 7:9-17; Mt. 25:31-40, 46; Yohana 10:16) Sasa wanatenda kulingana na onyo la shambulio la Gogu na wanatazamia ushindi wa Yehova na kushuhudiwa kwa jina lake. Wanatazamia kwa bidii tumaini la kuishi katika dunia iliyosafishwa uchafu wenyewe wa hewa, maji na chakula, na vile vile isiyo na ufisadi, kwa maana wanajua kwamba imeandikwa juu ya Mfalme na Mchungaji Yesu Kristo: “Kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili; . . . Na haki itakuwa mshipi wa viuno vyake, na uaminifu mshipi wa kujifungia.”—Isa. 11:4, 5.
—Kutoka Kitabu “The Nations Shall Know that I Am Jehovah”—How?