Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 9/15 kur. 411-415
  • Wanadamu Wanahitaji Mtawala wa Namna Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wanadamu Wanahitaji Mtawala wa Namna Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WATAWALA WA KRISTENDOMU HAWAFAI
  • MATENDO YA YEHOVA YAHAKIKISHA KWAMBA ANAWEZA KUMTOA MTAWALA MWEMA
  • MTAWALA WA YEHOVA ALIYECHAGULIWA
  • BARAKA KUTOKANA NA UCHUNGAJI MWEMA
  • Wazee, Chukueni kwa Uzito Madaraka Yenu ya Uchungaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • “Aliyepotea Nitamtafuta”
    Mrudie Yehova
  • Wao Huwachunga Kondoo Wadogo kwa Huruma
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Kuchunga Pamoja na Muumba Wetu Mtukufu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 9/15 kur. 411-415

Wanadamu Wanahitaji Mtawala wa Namna Gani?

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1. Kwa sababu gani utawala wa kibinadamu haukuwa baraka kwa wanadamu?

MMOJA wa watawala wenye hekima zaidi wa nyakati za kale, Mfalme Sulemani, alisema kwamba “mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa hasara yake.” (Mhu. 8:9, NW) Hii ni kwa kuwa, mara nyingi mno, watawala wa kibinadamu wamekuwa wenye kiburi, wasio na huruma na waonezi. Wao hawakuwaonyesha raia zao huruma na kupendezwa ambako mchungaji wa Mashariki anako kwa kundi lake. Kwa kweli, wamekuwa wenye kudhulumu.

2, 3. Yehova anawaonaje watawala wa kibinadamu wasio wenye huruma?

2 Bila shaka wanadamu wangekuwa na hali njema zaidi bila ya watawala hao wenye kudhulumu ama “wachungaji.” Ndivyo Yeye Aliye Mkuu Zaidi, Mwenye Enzi Yote wa ulimwengu wote, Yehova Mungu, aonavyo juu yake. Kwa mfano, wakati “wachungaji” wa Israeli wa kale walipokuwa wasio na huruma kwa raia zao, Yehova, kupitia kwa nabii wake Ezekieli, aliwafunua wazi, akisema:

3 “Mwanadamu, toa unabii juu ya wachungaji wa Israeli, toa unabii, uwaambie, naam, hao wachungaji, Bwana [Yehova] asema hivi; Ole wao wachungaji wa Israeli, wanaojilisha wenyewe; je! haiwapasi wachungaji kuwalisha kondoo? Mnawala walionona, mnajivika manyoya, mnawachinja walionona; lakini hamwalishi kondoo. Wagonjwa hamkuwatia nguvu, wala hamkuwaponya wenye maradhi, wala hamkuwafunga waliovunjika, wala hamkuwarudisha waliofukuzwa, wala hamkuwatafuta waliopotea; bali kwa nguvu na kwa ukali mmewatawala. Nao wakatawanyika, kwa sababu hapakuwa na mchungaji; wakawa chakula cha wanyama-mwitu, wakatawanyika. Kondoo zangu walitanga-tanga katika milima yote, na juu ya kila kilima kirefu; naam, kondoo zangu walitawanyika juu ya uso wote wa dunia; wala hapakuwa na mtu aliyewaulizia, wala kuwatafuta.”​—Eze. 34:2-6.

WATAWALA WA KRISTENDOMU HAWAFAI

4. Ni katika mambo gani watawala wa Kristendomu wamekuwa kama “wachungaji” wabaya wa Israeli wa kale?

4 Je! watawala wa Kristendomu hawa-kutenda kama wachungaji wabaya wa Israeli katika kushughulika na raia zao wanaojidai kuwa “kondoo” za Mungu? Je! watawala hawa hawakuwatendea watu kana kwamba ndio wenyewe wao kuliko kama mali ya Mungu waliyejidai kuabudu? Je! wao, vile vile mapapa, makardinali na maaskofu wakuu ambao wameshika vyeo vya kisiasa, hawakuwa wakali kuliko kuwa wenye huruma? Je! hawakujinenepesha wenyewe kwa njia ya kimwili kwa “kondoo” hawa maskini na wakaishi katika “anasa chafu”? (Ufu. 18:7, NW) Hatujawaona watawala wa kisiasa wa Kristendomu wakitoa uhai wao kwa ajili ya “kondoo,” kama vile alivyofanya Bwana Yesu Kristo. (Yohana 10:9-11) Lakini kunao ushuhuda tele wa kihistoria kwamba watawala wa kisiasa wa Kristendomu wamekuwa waonezi.

5. “Wachungaji” wa kisiasa wa Kristendomu wamewafanyia nini raia zao wenye mfano wa kondoo, na kama matokeo nini kimetukia kwa raia zao?

5 “Wachungaji” wa kisiasa wa Kristendomu wamepigana wao kwa wao, mtawala mmoja anayejidai Mkristo na mwingine anayeitwa mtawala wa Kikristo. Wamewatoa dhabihu watu wao wenye mfano wa kondoo juu ya madhabahu ya utukuzo wa taifa ama madhehebu ya kidini. Waonezi wengine hata wamekuwa wapenzi wakubwa wa viongozi wa kidini. Mashahidi wa Kikristo wa Yehova wamepatwa na mateso makali sana mkononi mwa waonezi hawa na watawala wenye kufuata utukuzo wa taifa kupita kadiri na wasiowataka. Kwa sababu ya udhalimu usioondolewa, wengi wa watu walioonewa wameyakimbilia matengenezo mbalimbali yaliyoundwa karibuni yenye uasi, nao wakapatwa na siasa za mambo ya kimwili na Ukomunisti usioamini kuwako kwa Mungu. Hakuna umoja katika Kristendomu, wala wa kisiasa wala wa kitaifa wala wa kidini. Kama kondoo waliopotea wasio na mchungaji, watu wametawanyika kama mateka kwa “wanyama-mwitu.” Hali iliyomo katika Kristendomu ni sawa na ile inayosimuliwa katika Ezekieli 34:7-10, na hii inatoa uhakika kabisa kwamba Yehova Mungu atahakikisha kwamba watawala wa Kristendomu watapoteza cheo chao. Twasoma hivi:

6, 7. Katika wakati wa Ezekieli, Yehova aliwaokoaje “kondoo” zake kutoka kwa “wachungaji” waonezi wa Kiisraeli?

6 “Enyi wachungaji, lisikieni neno la [Yehova]; Kama mimi niishivyo, asema Bwana [Yehova], kwa sababu kondoo zangu walikuwa mateka, kondoo zangu wakawa chakula cha wanyama-mwitu wote, kwa sababu hapakuwa na mchungaji, wala wachungaji wangu hawakutafuta kondoo zangu, bali wachungaji walijilisha wenyewe wala hawakuwalisha kondoo zangu; kwa sababu hiyo, enyi wachungaji, lisikieni neno la [Yehova]; Bwana [Yehova] asema hivi; Tazama, mimi ni juu ya wachungaji; nami nitawataka kondoo zangu mikononi mwao, nami nitawaachisha hiyo kazi ya kuwalisha kondoo; nao wachungaji hawatajilisha wenyewe tena; nami nitawaokoa kondoo zangu vinywani mwao, wasiwe tena chakula chao.”

7 Kwa habari ya Israeli wa kale wa siku za Ezekieli, Yehova aliwakomboa “kondoo” zake vinywani mwa “wachungaji” wenye kujilisha wenyewe katika mahali pa kiserikali kwa kuacha Yerusalemu uharibiwe na nchi ya Yuda iachwe ukiwa. Mfalme na wakuu walipaswa waviache vyeo vya kiserikali, wakitekwa nyara na Wababeli na kuhamishwa. Wengine waliuawa kama adhabu ya uasi wao. Katika Babeli watawala waliotekwa nyara waliwekwa gerezani ama wakawekewa vizuizi, wakinyang’anywa utawala.​—2 Fal. 25:18-30; Yer. 52:24-34.

8. Kulingana na kilichowapata “wachungaji” wabaya wa Kiisraeli, nini kitakachotukia kwa “wachungaji” wa kisiasa wa Kristendomu?

8 Kwa kupatana na mfano huo wa kale, Yehova Mungu atahakikisha kwamba waangalizi wa kiserikali wa taratibu nzima ya mambo ya ulimwenguni pote, kutia na wenye kujidai watawala wa Kikristo wa Kristendomu, wameondoshwa. Hii itawaweka huru “kondoo” za kweli za Yehova na uonezi na utendaji wa kujitumikia wenyewe wa “wachungaji” wa kisiasa. “Wachungaji” hao wasio waaminifu hawatajilisha wenyewe tena kwa hasara ya kundi la Yehova la mashahidi wa Kikristo. Hata ingawa hawa wawe wanajiona wenyewe kuwa wenye kutawanyika kwa sababu ya kupinga na mateso yanayoendeshwa na vyombo vya kisiasa, Yehova anajua ambako “kondoo” zake wa kweli wametawanywa. Kama Mchungaji mwenye upendo, yeye atawatafuta na kuwakusanya tena katika kundi moja. Ahadi yake nzito kama ilivyofanywa kupitia kwa nabii wake Ezekieli inatumika leo. Namna ambavyo aliitimiza ahadi hii kwa Israeli wa kale katika mwaka wa 537 B.C.E. na tangu wakati huo ulikuwa uhakika wa unabii wa kwamba yeye angeitimiza ahadi yake wakati ujao. Twasoma hivi:

9. Yehova aliahidi kufanya nini kwa ajili ya “kondoo” zake waliotawanyika?

9 “Maana, Bwana [Yehova] asema hivi; Tazama, mimi mwenyewe, naam, mimi, nitawatafuta kondoo zangu, na kuwaulizia. Kama vile mchungaji atafutavyo kondoo zake, siku ile anapokuwa kati ya kondoo zake waliotawanyika; ndivyo nitakavyowatafuta kondoo zangu; nami nitawaokoa katika mahali pote walipotawanyika, katika siku ya mawingu na giza. Nami nitawatoa katika watu wa mataifa, na kuwakusanya katika nchi zote, nami nitawarudisha katika nchi yao wenyewe; nami nitawalisha juu ya milima ya Israeli, kando ya mifereji ya maji; na katika mahali pote pa nchi panapokaliwa na watu. Nami nitawalisha malisho mema, na juu ya milima ya mahali palipoinuka pa Israeli litakuwa zizi lao; huko watalala katika zizi jema; nao watakula malisho mema, juu ya milima ya Israeli.”​—Eze. 34:11-14.

MATENDO YA YEHOVA YAHAKIKISHA KWAMBA ANAWEZA KUMTOA MTAWALA MWEMA

10, 11. (a) Utimizo wa kwanza wa Ezekieli 34:11-14 ulianza lini? (b) Nini kilichotukia nyakati za kisasa kinacholingana na utimizo wa kale?

10 Katika mwaka wa 537 B.C.E., kupitia kwa Mfalme Koreshi Mwajemi, Yehova aliyawezesha mabaki yenye uaminifu ya Kiyahudi warudie Yerusalemu na nchi ya Yuda. Vivyo hivyo katika karne hii, Yehova Mungu ameonyesha uwezo wake wa kuyakusanya mabaki yaliyotawanyika ya Israeli wa kiroho katika ujamaa na Yeye, wenye uhuru kwa kidini, na wenye kulisha kwa kiroho. (1 Pet. 2:25) Kwao nyakati zenye msukosuko za Vita ya Kwanza ya Ulimwengu (1914-1918 C.E.) zilikuwa zimekuwa “siku ya mawingu na giza.” (Eze. 34:12) Siku hiyo ilitiwa giza kwa sababu ya mateso ya kidini ambayo Kristendomu (sehemu iliyo kuu ya Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo) aliwalundikia mabaki ya Israeli wa kiroho. Kwa sababu hiyo mabaki ya Waisraeli wa kiroho yalitawanyika na wakaingia katika utumwa mkubwa sana wa Babeli Mkuu.

11 Lakini Babeli Mkuu alishindwa kuuendeleza mshiko wake wenye uonezi juu ya mabaki ya Waisraeli wa kiroho. Katika masika ya mwaka wa 1919 Babeli Mkuu alipatwa na anguko kubwa kutoka kwa cheo chake cha uwezo wa kidini juu ya watu wa Yehova, nazo pingu za utumwa wao kwake zilivunjika. Kwa kadiri ambavyo haki zao za kidini na mapendeleo kutoka kwa Mungu yalivyopaswa, mabaki haya hawakujiacha tena wawe mateka ama “chakula” cha “wachungaji” wa kiserikali wa Kristendomu. Kwa uhodari wa Kikristo walikwenda katika ulimwengu uliofuata vita kama mashahidi wa ufalme wa Yehova wa Kimasihi.​—Mt. 24:14.

12-14. Kulingana na ahadi ya Yehova katika Ezekieli 34:15, 16, Yehova atawafanyia nini “kondoo” wanaokuwa waonezi kwa wengine katika kundi?

12 Mabaki haya yameuona utimizo wa Ezekieli 34:15, 16:

13 “Mimi mwenyewe nitawalisha kondoo zangu, nami nitawalaza, asema Bwana [Yehova]. Nami nitawatafuta waliopotea, nitawarudisha waliofukuzwa, nitawafunga waliovunjika, nitawatia nguvu wagonjwa; nao wanono na wenye nguvu nitawaharibu; nitawalisha hukumu.”

14 Yehova Mungu amefanya ongezeko kwa mabaki ya kwanza waliookoka kwa uaminifu “siku ya mawingu na giza” mnamo Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Maelfu ya watu ndani na nje ya Kristendomu waliusikia ujumbe wa Ufalme kama ulivyohubiriwa na mabaki yaliyorudishwa ya Yehova na mwishowe wakawa wanafunzi waliojiweka wakf na waliobatizwa wa Bwana Yesu Kristo. Kati ya “kondoo” hawa wote Yehova hamruhusu ye yote atumie nguvu zake vibaya pasipo woga wa kuadhibiwa. Kama ye yote anakuwa mkatili na mwonezi kama kondoo mnono, mkali kwa “kondoo” wengine katika kundi, Yehova ‘anamharibu’ huyo “kondoo” asiyependa na mchoyo. Yeye anamkatilia mbali huyo kutoka zizini kama yeye aliyekufa kwa kiroho. Yeye ‘anamlisha hukumu’ huyo, yaani, hukumu ya kutengwa na ushirika sasa na uharibifu wa kweli katika “dhiki kubwa” inayokuja.

15, 16. Ni “kondoo” wa namna gani asiowavumilia Yehova, na ni mgawanyiko gani katika vikundi hakuuruhusu uingie kati ya mabaki yaliyorudishwa ya kondoo za kiroho?

15 Yehova amewaondosha kati ya mabaki yake yaliyorudishwa ya kondoo za kiroho wale ambao ni wenye pupa na wenye kujitafutia faida zao wenyewe. Hakuna hata mmoja anayevumiliwa anayewaharibia wengine mambo na anayetumia nguvu za kikatili na pembe za uwezo kusudi ayafurahie yaliyo bora mwenyewe bila ya “kondoo” walio dhaifu ama walio wagonjwa. Yehova hakuruhusu “kondoo” zake wagawanywe katika jamii ya viongozi wa dini na jamii ya watu wa kawaida. Yeye ameifikiliza amri iliyowekwa kupitia kwa Mwanawe Yesu Kristo: “Ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. Wala msimwite mtu baba [wa kiroho] duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni. Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo. Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu.” (Mt. 23:8-11) Alichofanya Yehova kinalingana na masimulizi ya unabii yanayopatikana katika Ezekieli 34:17-22:

16 “Na kwa habari zenu, Enyi kundi langu, Bwana [Yehova] asema hivi; Tazama, nahukumu kati ya mnyama na mnyama, kondoo waume na mbuzi waume pia. Je! mwaona ya kuwa ni neno dogo ninyi kulishwa malisho mema, hata mkawa hamna budi kukanyaga kwa miguu yenu yaliyosalia? na kuwa mmekunywa maji yaliyo safi, nanyi hamna budi kuyatibua kwa miguu [maji] yaliyobaki? Na kwa habari za kondoo zangu, wao wanakula hayo mliyoyakanyaga kwa miguu yenu, nao wanakunywa maji mliyoyatibua kwa miguu yenu. Kwa sababu hiyo, Bwana [Yehova] awaambia hivi; Tazama, mimi, naam, mimi, nitahukumu kati ya wanyama walionona na wanyama waliokonda. Kwa kuwa mmesukuma kwa ubavu, na kwa mabega, na kuwapiga wenye maradhi kwa pembe zenu, hata mkawatawanyia mbali; basi mimi nitaliokoa kundi langu, wala hawatakuwa mateka tena; nami nitahukumu kati ya mnyama na mnyama.”

MTAWALA WA YEHOVA ALIYECHAGULIWA

17, 18. Je! Yehova amewachagulia wanadamu mtawala?

17 Kwa sababu ya kupendezwa kwake kwingi na “kondoo” zake, twaweza kubaki na uhakika wa kwamba uchaguzi wake wa mtawala wa wanadamu utakuwa baraka kuu kweli kweli. Lakini je! Yehova amechagua mtawala? Ndiyo. Ezekieli 34:23, 24 anatuambia:

18 “Nami nitaweka mchungaji mmoja juu yao, naye atawalisha, naam, mtumishi wangu, Daudi; yeye atawalisha, naye atakuwa mchungaji wao. Na mimi, [Yehova], nitakuwa Mungu wao, na mtumishi wangu, Daudi, atakuwa mkuu kati yao.”

19, 20. Nani ‘mtumishi wa Mungu Daudi,’ na kwa sababu gani?

19 Haitupasi tuazimie kutokana na ahadi hii kwamba Yehova atamwinua Mfalme Daudi wa kwanza kutoka kwa wafu kusudi amweke katika cheo hiki kinachofanana na uchungaji. Bali, ‘mtumishi wa Mungu Daudi’ ni yeye aliyeirithi haki ya kifalme kutoka kwa Mfalme Daudi. Yeye ndiye Bwana Yesu Kristo. Uhakika wa kwamba jina Daudi maana yake ni “Mpendwa” unalingana vizuri na tangazo la Yehova juu ya Yesu: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu.” (Mt. 3:17; 17:5) Halafu, tena, Yesu alijifananisha mwenyewe na mchungaji, akisema: “Mimi ndimi mchungaji mwema; . . . nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo.”​—Yohana 10:14, 15.

20 Yesu Kristo aliutoa uhai wake kwa ajili ya “kondoo.” Lakini, Yehova Mungu alimfufua kutoka kwa wafu. Ndiyo sababu Waebrania 13:20 inamsema Yehova kama “Mungu wa amani aliyemleta tena kutoka kwa wafu Mchungaji Mkuu wa kondoo, kwa damu ya agano la milele, yeye Bwana wetu Yesu.” Akiwa amefufuliwa kwenye uzima wa kiroho tena kama ule aliokuwa nao mwanzoni, Yesu Kristo sasa ni Mchungaji wa kimbinguni. Kwa sababu hiyo kungekuwako “mchungaji mmoja” tu ambaye Yehova angeinua awe juu ya mabaki ya Israeli wa kiroho, yaani, Yesu huyu aliyefufuliwa aliye Masihi.

21. Ni lini Yehova alipomtokeza ‘mtumishi wake Daudi’ kama “mchungaji” juu ya Israeli wa kiroho, na hii imemaanisha nini kwao?

21 Yehova alifanya hivyo lini? Katika mwaka wa 1914 C.E. wakati ambapo “nyakati zilizowekwa za mataifa [yasiyo ya Kiyahudi]” zilimalizika, karibu Oktoba 4/5. Kulingana na daraka lake kama mfalme, Yesu Kristo alitabiriwa kuyachunga mataifa yote kwa fimbo ya chuma au fimbo ya enzi, akiyavunja-vunja vipande vipande. (Zab. 2:8, 9; Ufu. 12:5) Lakini, Waisraeli wa kiroho wameona namna nyingine ya uchungaji. Yesu Kristo amewalisha kwa chakula cha kiroho. Yeye amekuwa mkuu wao ambaye wanazifuata nyayo zake kama “kondoo.” Mungu wake, Yehova, amekuwa Mungu wao. Kwa kufahamu hivyo, mabaki yaliyotiwa mafuta, katika mwaka wa 1931, walilikubali kwa moyo jina lenye msingi wa Maandiko “mashahidi wa Yehova.”​—Isa. 43:10-12.

22, 23. (a) Nani mbali na mabaki waliotiwa mafuta wanaofaidika kutokana na uchungaji wa Yesu? (b) Yehova anaisimuliaje hali hii yenye amani kupitia kwa Ezekieli?

22 Mashahidi wa Kikristo wa Yehova hawa waliotiwa mafuta hawakuwa peke yao katika kufaidika kutokana na uchungaji mwema wa Yesu. Yesu mwenyewe alisema: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) Zaidi tangu mwaka wa 1935 hawa “kondoo wengine” wamekuja kwenye ushirika na mabaki. Na pamoja na Waisraeli hawa wa kiroho, wanaifurahia amani na ulinzi ambao Yehova aliuahidi kupitia kwa nabii wake Ezekieli:

23 “Nami nitafanya agano la amani nao, nami nitawakomesha wanyama wakali kati yao; nao watakaa salama jangwani, na kulala misituni. Nami nitawafanya wao, na mahali palipo pande zote za mlima wangu, kuwa baraka, nami nitaleta manyunyu kwa wakati wake; yatakuwako manyunyu ya baraka. Na mti wa kondeni utazaa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake, nao watakuwa salama katika nchi yao; nao watajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova], nitakapovunja vifungo vya kongwa lao, na kuwaokoa katika mikono ya watu wale waliowatumikisha. Hawatakuwa mateka ya makafiri tena, wala mnyama wa nchi hatawala; bali watakaa salama salimini, wala hapana mtu atakayewatia hofu.”​—Eze. 34:25-28.

BARAKA KUTOKANA NA UCHUNGAJI MWEMA

24. Kwa utimizo wa maneno ya Yehova katika Ezekieli 34:25-28, ni hali gani iliyomo kati ya “kondoo” zake?

24 Kulingana na “agano” la Yehova la amani ya Kikristo, yeye amewafukuza na kuwazuia watu wote wabaya wenye ukatili walio hatari kwa Wakristo wenye mfano wa kondoo. Kwa roho yake inayotenda juu ya wanafunzi wa kweli waliobatizwa wa Kristo yeye ameugeuza utu wao kuwa wenye amani, mfano wa kondoo usiodhuru. Kwa upendo wanatafuta kulindana wenyewe kwa wenyewe kwa kiroho na vile vile kwa kimwili katikati ya ulimwengu wenye uadui. Matokeo yake yamekuwa kama yalivyotabiriwa: Wao wamekuja kujua kwamba Mungu aliyeyavunja makomeo ya nira yao ya utumwa wa kidini na kuwakomboa kutoka kwa watu wenye kuwatumikisha wa Kibabeli ni Yehova. Wanaufurahia uchungaji ambao Yehova ametoa kupitia kwa Mwanawe Yesu Kristo.

25, 26. Ni paradiso ya namna gani wanayofurahia “kondoo”za Yehova, na hii inasimuliwaje katika Ezekieli 34:29, 30?

25 Chini ya uchungaji wa Yesu Kristo, Waisraeli wa kiroho wamekuwa wakifurahia paradiso ya kiroho. Hii ni kwa utimizo wa tangazo la Yehova katika Ezekieli 34:29, 30:

26 “Nami nitawainulia miche iwe sifa njema, wala hawataangamizwa kwa njaa katika nchi yao tena, wala hawatachukua tena aibu ya makafiri. Nao watajua ya kuwa mimi, [Yehova], Mungu wao, ni pamoja nao, na ya kuwa wao, nyumba ya Israeli, ni watu wangu.”

27. Ni matunda gani yaliyozaliwa katika paradiso ya kiroho inayofurahiwa na watu wa Mungu, na shamba lao limekuwaje lenye “sifa njema”?

27 “Miche” ambayo Yehova amewainulia Waisraeli hawa waliorudishwa wa kiroho imeendelea kuwako hata siku hii nayo inazaa kwa wingi zaidi kupita wakati wo wote tangu mwaka wa 1919. Chini ya baraka za Yehova, kama mvua zenye kumiminika, makao yao ya kidunia yamezaa kwa wingi sana “matunda” ya ufalme wa Mungu. (Mt. 21:43) Shamba hili lenye mazao limekuwa kwao ‘miche ya sifa njema,’ shamba maarufu. Neno la Yehova lililoandikwa, Biblia Takatifu, limefunuliwa wazi wakalielewa. Si kwamba tu wanakishiriki chakula cha kiroho kinachofuata kati yao wenyewe, lakini vile vile wanakitoa katika vitabu katika lugha nyingi iwezekanavyo. Kwa kweli wao ni ‘kondoo za malisho ya Yehova’ na wale wanaolishwa na mfalme wake aliyechaguliwa, Bwana Yesu Kristo.​—Eze. 34:31.

28. Kwa sababu gani twaweza kuwa na uhakika wa kwamba baraka hata zaidi zitafurahiwa nyuma ya uharibifu wa taratibu iliyopo ya mambo?

28 Ni za ajabu baraka ambazo mabaki yaliyotiwa mafuta na “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wamezipata kupitia kwa uangalizi wenye upendo wa Yesu Kristo. Ikiwa wanaweza kuzifurahia baraka hizo katika ulimwengu wenye uadui, bila shaka zitakuwa baraka za ajabu hata zaidi wakati Yesu Kristo atakapotawala dunia isiyo na taratibu iliyopo ya mambo ya kidini, ya kisiasa na ya kibiashara. Kwa kweli, Yesu Kristo ndiye Mtawala ambaye wanadamu wanahitaji. Je! wewe umesimama upande wake kwa kuyapatanisha maisha yako na mfano wake?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki