Njia ya Kumfikia Yehova au Mashetani—Njia Gani?
“Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”—Ebr. 4:16.
1, 2. Eleza njia ambayo kwa hiyo inampasa mtu amfikie Mungu.
YEHOVA MUNGU katika makao yake ya kimbinguni ametayarisha njia ya kumfikia yeye mwenyewe. Yeye anayo NJIA. Kumfikia lazima kuwe kupitia kwa njia inayofaa, imani katika Yesu Kristo na kukubali dhabihu yake ya ukombozi.
2 Yesu mwenyewe alisema hivi: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6) Hakuna njia za mkato. Si shauri la kuishi katika njia yo yote ambayo mtu anataka kuishi, ijapokuwa awe mtu wa dini fulani. Wala mtu hawezi kutumia njia yo yote tu, kama yoga (namna ya njia inayotumiwa na mabanyani katika kutafakari ili kupata maono ya mwujiza na umoja wa nafsi ya mtu na ile roho ya ulimwengu wote), unajimu, maisha ya kujinyima au dawa zenye kulevya, na kustahili kumfikia Mungu. Yampasa mtu awe na tamaa sana ya kumfikia Mungu katika njia inayofaa, na kuomba kutokana na moyo wake apate ujuzi wa kweli wa Neno la Mungu. Na hakuna mtu anayefanywa kumfikia au kumtumikia Yehova pasipo kutaka kwake mwenyewe. Mungu anakubali uaminifu wa kupenda, wa moyo wote tu.
3-5. (a) Tukiisha kumfikia Mungu, twawezaje kuendeleza hali ya kuwa karibu na yeye? (b) Ni “misaada” gani ambayo sisi hatuna haja nayo ili tumfikie Mungu?
3 Halafu, akiisha kuyajua mapenzi ya Mungu, inampasa mtu aufuate uongozi wa Neno la Mungu. Kusimama mbele za Mungu kunataka mikono safi na moyo safi. Mtunga Zaburi anasema hivi: “Ni nani atakayepanda katika mlima wa [Yehova]? Ni nani atakayesimama katika patakatifu pake? Mtu aliye na mikono safi na moyo mweupe.”—Zab. 24:3, 4.
4 Kuna “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja,” na juu ya kuhani mkuu ambaye kupitia kwa yeye tunamfikia Mungu tunasoma hivi: “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. . . . Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”—Efe. 4:5; Ebr. 4:14-16.
5 Mungu anatupenda sisi; kwa hiyo si vigumu kumfikia yeye. Mtume Paulo anasema hivi: “Hawi mbali na kila mmoja wetu.” Sisi hatuna haja ya misaada au vitu vya kutegemea kama sanamu au makuhani wa kidunia au kawaida zo zote zenye sherehe za kidini au sala zilizoandikwa, wala matendo yenye kutia usingizi wala namna yo yote ya dawa zenye kulevya. Adamu hakumfikia Mungu kwa njia za sanamu au dawa zenye kulevya, wala “Adamu wa mwisho,” Yesu Kristo.—Matendo 17:27; 1 Kor. 15:45.
6, 7. Ni kwa njia gani mmoja wa watu wa Mungu anaweza kuja chini ya utawala wa mashetani?
6 Kwa upande mwingine, Shetani na mashetani wenzake, wanataka kuwatawala wanadamu. Shetani ni mungu wa uongo. Yeye vile vile anazo njia ambazo kwa hizo anaweza kufikiwa, mambo fulani yanayotuweka sisi wazi kutawaliwa na mashetani.
7 Sasa, Yehova anawalinda watu wake wasitawaliwe na mashetani isipokuwa wanatumia njia ya kuwafikia mashetani. Walakini, mtu anapovutwa na tamaa mbaya au ya kipumbavu anageuzwa upesi kwenye njia fulani ambayo mashetani wanatayarisha. Ndipo anapokuja chini ya utawala wao. Huenda mtu huyo asipagawejaa mashetani, lakini yeye atakuwa akiyafanya mambo ambayo mashetani wanamtaka ayafanye, mambo yanayopingana na Mungu. Yakobo, ndugu mzazi mmoja na Yesu, alisema hivi: “Kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti.”—Yak. 1:14, 15.
8, 9. Kwa sababu gani ni jambo la hatari sana kushirikiana na watu wa ulimwengu?
8 Kujaribu kuchukua mfano au kuwa washiriki wa watu wa ulimwengu, au watu wanaofuata fikira za kilimwengu, ni hatari sana. Kufuata njia zao au kujaribu kuwapendeza ndiyo njia moja ambayo mwishowe inaongoza kwenye kutawaliwa na mashetani. Bila kujali watu hao waonekane kuwa wazuri, hawaongozwi na roho ya Mungu, bali “kulingana na taratibu ya mambo ya ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewani, roho inayotenda sasa katika wana wa kutokutii.” Ndiyo sababu imetupasa tulitii sana onyo la Maandiko: “Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.”—Efe. 2:2; 1 Kor. 15:33, NW.
9 Mtu akiisha kupagawa na mashetani anaweza kuingia kwa haraka katika ufasiki kamili na mauti ya mapema. Hilo ndilo jambo ambalo mashetani wanataka kuona, zaidi wanapendezwa na uharibifu wa mtu ambaye alimtumikia Mungu zamani.—Linganisha Mathayo 8:28-32.
NAMNA GANI DAWA ZENYE KULEVYA?
10-12. Kwa sababu gani hatuwezi kuepuka ulizo hili, Je! dawa zenye kulevya zinafungua njia ya kuwafikia mashetani?
10 Basi, namna gani dawa zenye kulevya? Je! katika habari hii zinatupasa sisi katika njia moja au katika njia nyingine? Kwa kweli dawa zenye kulevya zimekuwa ulizo kubwa. Matumizi ya dawa zenye kulevya yameenea katika vyuo vikuu na shule zenye masomo ya juu na yanaenea kwa haraka katika shule za misingi. Vijana wenye kufanya biashara wanavuta bangi au kasumba (marijuana) kwa starehe.
11 Je! kama wanavyodai ni ‘kiburudisho tu kisichodhuru, njia ya kustarehe, njia ya kuondolea mikazo ya ulimwengu wa kisasa’? Huenda mwingine akasema, ‘Ndivyo hasa; haishughuliki na mashetani; ni kwa kusudi la starehe tu.’
12 Ndiyo, huenda mtu fulani akasema hivyo, lakini hakuna ye yote kati yetu awezaye kuepa ulizo hili la maana, Dawa zenye kulevya zinafungua njia ya kumfikia nani? Kwa sababu gani? Kwa sababu watumiaji wa dawa zenye kulevya wenyewe wanasema kwamba dawa zenye kulevya ni ‘njia ya kuwa karibu zaidi na Mungu.’ Wanasema, dawa zenye kulevya ‘zinatoa hali ya kuwa macho,’ ‘ni paradiso ya mara hiyo’ au ‘zinatoa mchanganuo wa binafsi wa mara hiyo.’ Basi, je! kweli dawa zenye kulevya zinapanua akili? Je! zaweza kutusaidia sisi tuichanganue mioyo yetu kwa faida? Ni mambo gani ambayo inatupasa tuangalie katika habari hii, na mambo ya hakika yanaonyesha nini?
AKILI TIMAMU NI ZA LAZIMA
13-15. Kwa sababu gani ni lazima Mkristo aulinde utimamu wake wa akili?
13 Katika shauri la kumfikia Yehova na kupata thawabu ya uzima wa milele, Yesu alitaja akili wakati aliposema hivi: “Inakupasa umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na [tafadhali angalia] kwa akili zako zote.”—Mt. 22:37, NW.
14 Kwa hiyo, ni wazi kwamba njia ya kumfikia Mungu inataka matumizi kamili ya akili zenye afya, kuufanya uwezo wetu wa kufahamu na uwezo wetu wa kufikiri uwe waziwazi na mwepesi sana. Hivyo inataka akili timamu. Tena, Paulo anakazia kwamba Wakristo, Wakristo wote wanapaswa wawe na akili timamu. Anatia moyo kwamba wanaume wazee wawe timamu katika akili, kwamba wanawake wazee wawasaidie wanawake vijana wawe timamu katika akili, na kwamba Tito mwenyewe aendelee kuwatia moyo wanaume vijana wawe timamu katika akili.—Tito 2:2-6.
15 Kwa hiyo, kama Wakristo, hatuwezi kufanya lo lote ambalo lingehatirisha utimamu wa akili zetu za Kikristo. Tunaambiwa hivi: “Itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na uwezo wenu wa kufikiri.” (Rum. 12:1, NW) Kufanya vingine kungekuwa kushindwa kumfikia Yehova na kungetuweka sisi katika hatari kubwa ya kupagawa na mashetani.
16. Kwa sababu gani Mkristo ahangaike kwa sababu ya matokeo yanayofanywa na bangi katika akili?
16 Kwa kuwa matokeo ya bangi si yenye kudhuru sana kama ya dawa kali, matumizi yake yameenea zaidi katikati ya watu wa ulimwengu. Hata watu wa Yehova, zaidi wale walio shuleni, huenda wakashawishwa katika kuitumia. Jambo hili latokeza ulizo: Je! kwa kutumia bangi, au hata kufikiria kuitumia, Mkristo angekuwa akionyesha akili timamu, akili zenye afya? Hili ni ulizo zito sana, kwa maana matumizi ya bangi yanaongezeka sana.
MATOKEO YA BANGI KATIKA AKILI
17, 18. Je! matumizi ya bangi yalionekana kuwa ‘kiburudisho kisichodhuru’ kwa kijana fulani wa kike mwenye umri wa miaka kumi na sita?
17 Ili kuonyesha matokeo yenye kudhuru ya bangi katika akili za mtu, adili, maisha na mwili, msomaji na ayaangalie pamoja nasi mambo fulani ya hakika kama yalivyotolewa na madaktari wa utabibu ambao uchunguzi wao uliripotiwa katika gazeti JAMA, Journal of the American Medical Association, la Aprili 19, 1971.
18 “Mtoto wa kike mwenye umri wa miaka 16 ambaye zamani hakuwa na tatizo la akili alivuta bangi . . . kwa muda wa miaka miwili. Alianza kutopendezwa na masomo ya shule . . . Mtoto wa kike mtulivu, mwenye urafiki na mwenye kupendwa na wengi, akageuka akawa mwenye uadui na mwenye kutukana waalimu na watu wenye vyeo pasipo kufikiri. . . . Baada ya kuacha bangi, . . . Kwa muda wa miezi kumi ya uchunguzi wa daktari aliendelea kuonyesha kuharibika kwa kumbukumbu na kuchafuka kwa mawazo . . . yeye . . . hakuweza kuandika wala kusema kama alivyokuwa anaweza kufanya zamani kwa vyepesi sana.”
Bangi kiburudisho kisichodhuru? Pahali pa kuwa hivyo, ni uharibifu wa afya ya moyoni na utimamu wa akili.
19. Ni tukio gani linalofunua kwamba matumizi ya bangi yanaweza kutokeza ubaya katika mtu anayeitumia?
19 “Mwanamume mwenye umri wa miaka 20 alirukwa akili na akaanza kufikiri kwamba alikuwa mwenye uwezo wote na mwenye fahari miezi sita alipokwisha kuanza kuvuta bangi. Yeye akaona kwamba alikuwa mkuu wa Mafia (chama cha siri cha waasi) na ya kwamba alikuwa mtawala wa Masharikini wa Ku Klux Klan. Alianza kuzikusanya bunduki na visu kutia na kumzoeza mbwa wake wa Kijeremani kuwashambulia wengine.”
Akili za mtu huyu ziliharibika sana. Zikawa si timamu, zenye ugonjwa. Je! alikuwa akiitii amri ya Mungu ‘kuzifua panga kuwa majembe’ na kumpenda jirani yake? Alikuwa akimfikia nani—Yehova au mashetani?
20. Ni matendo gani yenye tabia mbaya yaliyofanyizwa katika mtumiaji wa bangi mwenye umri wa miaka kumi na minne?
20 “Upesi kijana wa kiume mwenye umri wa miaka 14 alipokwisha kuanza kuvuta bangi, alianza kuonyesha uvivu, ubaridi, huzuni. . . . hali yake ikawa mbaya zaidi mpaka akaanza kupotewa akili na kuwa na mawazo yaliyochafuka. Wakati uo huo, akawa mlawiti mwenye bidii. . . . akajaribu kujiua kwa kuruka kutoka katika motokaa inayoenda ambayo alikuwa ameiba.”
Tunauliza: Bangi, je! ‘ni njia ya kufikia paradiso’? Ulawiti na kujiua—paradiso ya mara hiyo?
21, 22. Ni ukamatano gani wa kidini na wa uchawi ambao tunaona katika mambo yaliyowapata vijana wawili wenye kutumia bangi?
21 Mara nyingi inachukua muda mfupi tu wa kutumia bangi na kunakuwa na matokeo yenye kuharibu, kama kijana mwingine alivyoona:
“Kijana wa kiume mwenye umri wa miaka 19 alivuta bangi kwa muda wa miezi minne, . . . Akisadiki ya kwamba alikuwa na akili zisizo za kibinadamu, aliona kwamba alikuwa na uwezo wa kuongea na kuongoza akili na matendo ya wanyama, zaidi mbwa na mapaka. . . . [yeye alisadiki] kwamba alikuwa Masihi.”
Kuongea na mbwa na mapaka na kwa kiburi kudhani wewe u Masihi kunafanya isiwezekane kumfikia Yehova.
22 “Kijana wa kiume mwenye umri wa miaka 18 aliyevuta bangi kwa kawaida kwa muda wa miaka mitatu alianza kujitenga polepole, kuchafuka akili, kuhuzunika. Kupendezwa kwake na unajimu na dini za Mashariki kuliongezeka. Akawa mlaji wa mboga tu na kujizoeza yoga. Alidhani alikuwa guru (mwalimu wa dini ya Kibanyani) na mwisho akadhani ya kwamba alikuwa mwana wa Mungu. . . . akahamia upande wa pwani ya magharibi akaendelea kuishi maisha yasiyo na matokeo, yasiyo na kusudi, akipatiwa msaada wa fedha na wazazi wake.”
Tena, twaulizwa ulizo: Njia ya kumfikia Yehova au mashetani—njia gani? Hawa wawili wanaotajwa mwisho wanaonyesha waziwazi kwamba namna ya uchawi ilitiwa ndani.
23. (a) Kwa sababu gani mtu hawezi kuwategemea washauri wa kilimwengu? (b) Taja mfano wa kuhakikisha.
23 Kama katika mambo mengine yanayotupasa kwa kiroho imetupasa tusiwasikilize washauri wa ulimwengu huu, ulio na ugonjwa wa akili, kwa habari ya matumizi ya dawa zenye kulevya. Imetupasa tulikubali shauri hili: hekima ya ulimwengu huu ambao mungu wake ni Shetani Ibilisi. Chunguza ubora wa shauri hilo lililopewa kwa mwanafunzi wa chuo kikuu.
“Kijana wa kiume mwenye umri wa miaka 19 aliingia katika chuo kikuu akiwa anafanya masomo yake vizuri zaidi. Alianza kuvuta bangi mapema katika mwaka wake wa kwanza wa chuo kikuu, na katika muda wa miezi miwili ya kuanza kuvuta bangi, alianza kuwa mwenye ubaridi, mwenye kuchafuka akili, na mwenye huzuni. Wakati wa kumalizika kwa muda wa shule, akawa ameshindwa masomo yote na kukosa uamuzi mzuri katika karibu mambo mengine yote. . . . Kama vile wagonjwa wetu wengi sana, kijana huyu wa kiume alimwambia daktari wake wa akili kwamba alikuwa ameona mageuzi wakati alipokuwa akivuta bangi; hata alimwendea mshauri wa chuo kikuu na kumwambia mshauri kwamba alijiona mwenye taabu ya kufikiri kwa sababu ya kuvuta bangi. Mshauri akamtumainisha kwamba bangi ilikuwa isiyodhuru na ya kwamba uchunguzi wa daktari haukuonyesha taabu kama matokeo ya kuvuta bangi.”
Walakini, kijana huyu aliacha kuvuta bangi, polepole ule ubaridi wake ukamtoka, nia yake ikarudi, sura yake ikawa nzuri zaidi. Alipata kazi na mwisho aliandikwa katika chuo kikuu kingine.
24. Yalikuwa matokeo gani fulani kwa wale waliokuwa wakitumia bangi?
24 Matukio mengine mengi yangeweza kutajwa. Labda itaongezwa kwamba kati ya watumia bangi, zaidi wanawake, ilionekana tabia isiyo ya kawaida ya kulalana mwanamume na mwanamke na vile vile wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake. Jambo hili lilionekana kuwa hivyo katikati ya wale ambao mbele ya kutumia bangi walikuwa hawajashiriki katika kulalana. Magonjwa ya kaswende na kisonono yalitokea kwa wingi.
DAWA ZA KULEVYA, UCHAWI NA IBADA YA MASHETANI
25. Wale wanaotumia dawa zenye kulevya wanashirikiana na nani?
25 Basi, dawa zenye kulevya zinatusaidia tumfikie nani? Ni nani anayependelea ufasiki wa wanadamu, uchafu, wote wa kimwili na wa adili, uwazimu na mauti ya mapema? Ni nguvu za giza ambazo watumiaji wa dawa zenye kulevya wanafikia na ambazo wanashirikiana nazo. Kwa kweli, kwa habari ya dawa yenye kulevya inayoitwa heroin, mtumiaji mmoja anasema hivi: “Ina faida zote za mauti bila kikomo chake.” Ndiyo, matumizi mabaya ya dawa zenye kulevya yanaongoza kwenye hatari ya kufisha ya uchawi, mazoea ya mashetani, ibada ya mashetani, na hata yanaweza kutokeza kupagawa na mashetani. Tofauti na hali ya kiroho ya kimungu na hali ya kuwa karibu na Mungu, yanaleta hali ya kuwa karibu na mashetani.
26, 27. Onyesha kwamba matumizi ya dawa zenye kulevya kweli yanaongoza kwenye uchawi.
26 Ama tunafanya ambayo mashetani wanatamani tuyafanye ama tunapagawa na wao, ikiwa tunatumia dawa zenye kurusha akili. Angalia hili, kwamba, mara nyingi, kuna kumwongoza mtu kwenye unajimu au kwenye dini za kipagani zenye mambo ya siri zinazozoea namna ya uchawi na kushirikiana na mashetani. Kuna ushirikiano wa moja kwa moja. Mtumiaji mmoja wa dawa zenye kulevya alisema kwamba lilikuwa jambo linalojulikana sana katikati ya watumiaji wa dawa zenye kulevya ambao alishirikiana nao kwamba (kama walivyosema) ‘walijua mtu alikuwa amerukwa akili alipoanza kufikiri kwamba yeye alikuwa mungu.’ Basi vijana wa kiume waliofikiri walikuwa Mwana wa Mungu hawakuwa hao tu. Sasa, wao walikuwa wakitaka kuwa kama nani—Yehova Mungu na Mwana wake Yesu Masihi, au miungu ya kishetani?
27 Wakiifuata njia yao ya kuwafikia mashetani kwa matumizi ya dawa zenye kulevya, vijana hawa ambao tumeangalia habari zao hawakuachia hapo. Hapana. Waliendelea na wakaonyesha kazi za mashetani: uadui, kuelekea kufanya jeuri, uhanithi na wakajaribu kujiua.
UCHAWI TENDO LA MWILI
28, 29. Kwa sababu gani uchawi unapangwa na Biblia kama tendo la mwili?
28 Lakini si lazima tuwe na mifano ili tujue mambo haya juu ya dawa zenye kulevya. Tunalo neno la mamlaka iliyo ya maana kuliko mamlaka zote, Yehova Mungu. Katika Wagalatia 5:19-21 tunasoma juu ya matendo ya mwili hivi: “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo.” Ni jambo gani kati ya haya ambalo matumizi ya dawa zenye kulevya hayaongozi kwalo?
29 Mambo haya yenye kuharibu tabia nzuri si matunda ya roho. Si mambo ya kiroho. Uchawi wenyewe si wa kiroho, bali unapangwa na Biblia kama tendo la mwili. Kama mfano: Mtu anayelala na mnyama ni mwanadamu anayefanya tendo, lakini si tendo la kibinadamu. Ni tendo la mnyama, la uhanithi, lenye tabia mbaya kwa mwanadamu kulifanya. Vivyo hivyo, uchawi, ujapodaiwa kuwa wa kiroho, ujaposaidiwa na viumbe vya kiroho, mashetani wabaya sana, ni wa uhanithi, wenye tabia mbaya, tendo la mwili, si la roho.
30, 31. (a) Mbele ya Gharika, mashetani walionyeshaje tamaa yao ya kuwa na ushirika wa kimwili? (b) Onyesha kwamba tendo la malaika waliooa wanawake wa kibinadamu lilikuwa uhanithi.
30 Kwa uhanithi mashetani wanatamani ushirika wa kimwili. Ebu ikumbuke habari ya wakati uliotangulia Gharika. Biblia inasema hivi: “Ikawa wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, wana wa Mungu [malaika] waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua.”—Mwa. 6:1, 2.
31 Tendo hili la malaika lilikuwa la uhanithi kwa sababu wao hawakuumbwa kwa kusudi hili. Mwandikaji wa Kikristo Yuda analinganisha tendo lao na uhanithi wa Sodoma na Gomora, akiandika hivi: “Malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu, amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku ile kuu. Kama vile Sodoma na Gomora, na miji iliyokuwa kando-kando, waliofuata uasherati kwa jinsi moja na hawa, wakaenda kufuata mambo ya mwili yasiyo ya asili, imewekwa kuwa dalili, wakiadhibiwa katika moto wa milele.”—Yuda 6, 7.
32. Mashetani wangali wanatafutaje kutosheleza tamaa yao ili wawe na ushirika wa kimwili?
32 Malaika hawa waliofanya dhambi hawawezi sasa kujivika mwili kama walivyofanya mbele ya Gharika, kwa sababu ya kizuizi cha Mungu. Walakini, kwa kutawala akili na miili ya watu wanaona kwamba, kwa kadiri fulani, wanakuwa na ushirika wa kimwili.
33. Neno la Kigiriki kwa “uchawi” linaonyeshaje ukamatano kati ya dawa zenye kulevya na uchawi?
33 Ni jambo lenye kupendeza kwetu kwamba neno la Kigiriki linalotumiwa kwa “uchawi” au “ulozi” ni phar·ma·kiʹa, linalokamatana sana na neno la Kiingereza “pharmacy.” Neno phar·ma·kiʹa maana yake ni “matumizi ya dawa.” Kwa sababu gani neno hili linatumiwa kwa uchawi au ulozi? Mwandikaji mmoja mwenye kutumainika anasema hivi:
“PHARMAKIA . . . (Kiingereza, pharmacy, n. k.) kwa msingi lilimaanisha matumizi ya dawa, uramali; halafu, kutia sumu; halafu, ulozi, . . . Tazama tena Ufu. 9:21; 18:23. . . . Katika ulozi, matumizi ya dawa, kwamba ni zile zisizo na sumu ama zenye sumu, kwa desturi yalifuatana na maneno ya kunuizia uchawi na maombi ya nguvu za kisiri, kwa kutolewa kwa matalasimu ya namna nyingi, hirizi, n. k., zinazodaiwa kuwa zinakusudiwa kumlinda mwombaji au mgonjwa asifikiwe na nguvu ya mashetani, bali kwa kweli kumfanya mwombaji adhani mlozi anao uwezo na nguvu za mwujiza.”—Vine’s Expository Dictionary of New Testament Words.
34. Watumiaji wa dawa zenye kulevya wanadanganywa namna gani, na mwisho matumizi ya dawa zenye kulevya yatatokeza nini kwa wenye kuzitumia?
34 Je! hali hiyo hailingani na ya leo? Watumiaji wengi wa dawa zenye kulevya wanajidai ‘wanamfikia Mungu,’ ‘wanapanua akili zao.’ Lakini kwa kweli kusudi ni kumfanya mtumiaji arukwe akili na kuwa na maono ya mwujiza, yakiwaongoza kwenye mashetani, kwa kudhani kwamba dawa yenye kulevya inapanua zaidi akili na fikira zao. Mtu akiongozwa katika mazoea ya uchawi anakuwa mtu mwenye kupatwa na namna zote za mazoea mabaya, kupagawa na mashetani, uwazimu tia mauti ya milele. Uchawi, tendo la mwili, utamzuia mtu asiingie katika ufalme wa Mungu, ndivyo yanavyosema Maandiko katika Wagalatia 5:21.
35. Ni onyo gani ambalo mtume Paulo anatoa juu ya kufanya cho chote kinachotufanya sisi tuache kuwa waaminifu kwa Mungu wa kweli, Yehova?
35 Mtume Paulo anasimulia mambo ambayo watu wanafanya wakati wanaposhiriki katika tendo lo lote la kidini au mazoea yanayofanya njia ya kumfikia mwingine ye yote kuliko Mungu wa kweli, Yehova. Anasema hivi: “Vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, walasi kwa Mungu; nami Sipendi ninyi kushirikiana na mashetani. Hamwezi kunywea kikombe cha [Yehova] na kikombe cha mashetani. Hamwezi kushirikiana katika meza ya [Yehova] na katika meza ya mashetani.” Ikiwa tunatumia dawa zenye kulevya, imetupasa tuyafikirie kwa makini sana maneno yafuatayo ya Paulo: “Au twamtia [Yehova] wivu?” anauliza, kisha anaonya hivi, “Je! tuna nguvu zaidi ya yeye?”—1 Kor. 10:20-22.
36. Mungu anampatia nini mtu anayemfikia kwa unyofu wa moyo?
36 Yehova anawapatia wale wanaomfikia kwa unyofu wa moyo kila kitu wanachohitaji ili wafurahi. Kwa habari ya kumfikia na kumtumikia Mungu, mtume anasema: “Walakini utauwa pamoja na kuridhika ni faida kubwa.” Tafuta utauwa kwa kumtii Yeye peke yake awezaye kuutoa, na ufurahi “pamoja na wale wamwitao Bwana kwa moyo safi.”—1 Tim. 6:6; 2 Tim. 2:22.
[Picha katika ukurasa wa 417]
Kuvuta bangi kunaweza kuharibu afya ya moyoni na utimamu wa akili. Je! ndivyo unavyotaka?
[Picha katika ukurasa wa 421]
Watumia bangi wengi wanajidai ‘wanamfikia Mungu.’ Kumbe wanajiweka wenyewe chini ya mashetani