Wenye Hatia ya Damu Hawawezi Kuokoka Hukumu ya Mungu
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1. Maoni ya Yehova ni nini juu ya wenye hatia ya damu, na kwa hiyo imempasa Kristendomu atazamie nini?
TANGU kutokea kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika mwaka wa 1914 C.E., wanaume, wanawake na watoto wameuawa kwa kadiri ambavyo haijapata kuonwa ikitukia hata kidogo zamani katika historia ya wanadamu. Kwa hakika hatia kubwa ya damu iko juu ya mataifa. Zaidi hii ni kweli juu ya wale watu wa Kristendomu, kwa maana wao ndio ambao wameongoza katika vita vyenye umwagaji wa damu vya karne hii. Kujidai kwao kuwa Wakristo hakutawaokoa na hukumu kali ya Yehova Mungu. Yeye anachukia, ndiyo, anachukia sana, wenye hatia ya damu.—Zab. 5:6; Mit. 6:16, 17.
2. Kwa sababu gani twaweza kuwa na hakika kwamba watu na mataifa yenye hatia ya damu hawawezi kuokoka hukumu kali ya Yehova?
2 Wanadamu na mataifa yenye hatia ya damu wajapositawi kwa muda, hawawezi wakaepuka milele kupatwa na kufikilizwa kwa hukumu ya Mungu juu yao. Kurasa za historia ya kale zinahakikisha hili. Ebu fikiria, kwa mfano, yaliyowapata wakaaji wa Yerusalemu wa kale kuelekea mwisho wa karne ya saba B.C.E.
UJAMAA WA KUJIDAI NA MUNGU SI ULINZI
3. Kwa sababu gani wakazi wa Yerusalemu walifikiri kwamba walikuwa salama, lakini walisahau nini?
3 Kwa sababu ya ujamaa wao wa pekee wa agano na Mungu, wakaaji wa Yerusalemu walijiona wako salama. Vile vile walijifikiria wenyewe kuwa salamini kwa sababu ya maboma yenye nguvu ya mji na mwungano wao pamoja na majeshi ya Misri. Basi mfalme wa Babeli Nebukadreza alipoanza kuuzunguka Yerusalemu kuelekea mwisho wa Desemba katika mwaka wa 609 B.C.E., hawakuogopa kwamba mji wao ungekuwa mahame kabisa. Jambo ambalo walikosa kujua lilikuwa kwamba Yehova Mungu alikuwa ameuacha Yerusalemu. Lilikuwa kusudi lake afanye hesabu pamoja na wakaaji wenye hatia ya damu.
4. Ezekieli alijuaje wakati ambapo mazingiwa ya Yerusalemu yalianza?
4 Siku yenyewe ambayo Nebukadreza alianza kuuzunguka Yerusalemu, Yehova Mungu, kupitia kwa nguvu yake ya utendaji isiyoonekana au roho, alimfunulia nabii wake Ezekieli hili, wakati huo akiwa katika uhamisho wa Kibabeli. (Eze. 24:1, 2) Vile vile Ezekieli aliagizwa afanye mfano wa jambo ambalo lingeupata Yerusalemu. Katika kitabu cha Biblia chenye jina lake tunasoma hivi:
5, 6. (a) Ni kwa mfano gani Yehova akafunua wazi matokeo ya mazingiwa ya Kibabeli juu ya wakazi wa Yerusalemu? (b) Ni nini kilichofananishwa na ‘vipande vyema’ na “mifupa iliyochaguliwa” ambayo ingetiwa ndani ya sufuria la mfano?
5 “Ukawatungie mithali nyumba ya kuasi, ukawaambie, Bwana [Yehova] asema hivi; Teleka sufuria, liteleke; ukatie maji ndani yake; vikusanye vipande vyake ndani yake, naam, kila kipande chema, paja na bega; lijaze mifupa iliyochaguliwa. Uwatwae wateule wa kundi la kondoo, ukafanye chungu ya [kuni katika mzunguko] chini yake; ukalitokose sana; naam, mifupa yake itokoswe ndani yake.”—Eze. 24:3-5.
6 Hivyo ndivyo Yerusalemu ulivyofananishwa na sufuria. Kufanywa kwa chungu ya kuni chini yake na kwa hiyo kuziwasha moto kungefananisha mazingiwa ya Yerusalemu. Polepole mazingiwa hayo yangefanya iwe moto kama maji yanayochemka kwa wale waliomo ndani ya mji. Vile vipande vya nyama vilivyowekwa katika sufuria vingefananisha wale waliomo ndani ya Yerusalemu, kutia na wakimbizi walioukimbilia mbele ya majeshi ya Kibabeli yenye kusonga. Vile vipande vyema vilivyotiwa ndani yake vingefananisha wale wenye vyeo bora wa mji, zaidi mfalme na wakuu wake. Kwa kuwa mifupa ndiyo inayofanyiza tegemeo linalotegemeza mwili wenye nyama, “mifupa iliyochaguliwa” ingefananisha wale waliotegemeza taifa zima, yaani, majemadari na maafisa wao. Iliwapasa wote ‘watokoswe’ wakati wa mazingiwa.
7-9. Yehova alikusudia kufanya nini juu ya maandishi ya Yerusalemu ya umwagaji wa damu?
7 Hali ya wakaaji wa Yerusalemu ya kuwa na hatia ya damu iliwafanya wastahili msiba huo. Kupitia kwa nabii Ezekieli Yehova alitangaza hivi:
8 “Ole wake mji wa damu! hilo sufuria ambalo kutu yake i ndani yake, ambalo kutu yake haikulitoka; litoe kipande kipande; hapana kura iliyoanguka juu yake. Maana damu yake imo ndani yake; aliiweka juu ya jabali lililo wazi; hakuimwaga juu ya nchi, apate kuifunika kwa mavumbi; ili ipandishe ghadhabu ya kulipa kisasi, nimeiweka damu yake juu ya jabali lililo wazi, isipate kufunikwa.”—Eze. 24:6-8.
9 Uchafu wa adili na takataka ndani ya sufuria ya mfano, Yerusalemu wenye hatia ya damu, ilishikamana sana pande zake na kufanyiza kutu. Lile povu na uchafu visingeweza kuondolewa au kusuguliwa. Yerusalemu hakujali sana damu ya kibinadamu hata akakosa kuimwagia damu ya wale aliowaua juu ya nchi na kuifunika kwa mavumbi. Yeye hakuwafanyia wanadamu alioua kulingana na ambavyo sheria ya Mungu ilivyoamuru ifanywe kwa habari ya damu ya mnyama aliyeuawa katika kuwinda. (Law. 17:13, 14) Bila aibu Yerusalemu aliimwagia damu iliyomwagwa kwa jeuri juu ya jabali lililo wazi ili ifunuliwe wazi kama ushuhuda wa uvunjaji wake wa sheria. Kudharau huku damu ya kibinadamu kulichochea hasira ya Yehova. Yeye aliazimia asiache hatia yake ya damu ifunikwe bali ifunuliwe wazi ipate kutazamwa na watu wote kama damu iliyo juu ya jabali lililo wazi, lisilo na mavumbi. Bila kupambanua, wavunja sheria katika Yerusalemu wangetolewa waletwe kwenye hukumu, “kipande kipande.” Hakuna kura ya uteuzi ambayo ingepigwa juu yao.
10-12. Kulingana na Ezekieli 24:9-12, mazingiwa ya Kibabeli yangekuwa na matokeo gani juu ya Yerusalemu?
10 Ili kutoa habari zaidi juu ya mazingiwa, neno la Yehova kupitia kwa Ezekieli linaendelea kusema:
11 “Ole wake mji wa damu! Mimi nami nitaiongeza chungu. Tia kuni nyingi, uchochee moto, itokose nyama sana, fanyiza mchuzi mzito, mifupa ikateketee. Kisha litie juu ya makaa yake, tupu, lipate moto, na shaba yake iteketee, uchafu uyeyushwe, na kutu yake iteketee. Amejidhoofisha kwa taabu, lakini kutu yake nyingi haikumtoka; kutu yake haitoki kwa moto.”—Eze. 24:9-12.
12 Yehova alijua jambo ambalo mji wenye damu, wenye uchafu ulilostahili. Lazima ufunikwe katika mwali mkubwa kana kwamba unatokana na chungu kubwa ya kuni. Kwa sababu ya kutokoswa kwa muda mrefu mpaka kuchemka lazima majemadari na maafisa wake wapate moto sana kwa mazingiwa ya Kibabeli yenye nguvu sana, na wakaaji wengine, kama nyama ambayo imepikwa mno, lazima wafanywe katika hali iliyo kama mchuzi mzito na kuwa chepechepe. Mji ungefanywa ukiwa kabisa wakati wa kuanguka kwake kwa Wababeli wenye kuuzunguka. Ungetelekwa kama sufuria la shaba lililo tupu katika moto wa uharibifu, kwa sababu ya kutu ya povu ambayo bado inashikamana katika kingo zake. Sufuria lote la mfano (Yerusalemu) lingeyeyushwa ili kuutenga uchafu nalo.
13-15. Lilipaswa jambo gani litukie kwa Yerusalemu ili kuukomesha uchafu wake?
13 Kulikuwa hakuna uwezekano kwa Yerusalemu kuokoka. Hatia yake ya damu na uchafu wake vilimshtaki. Kama Yehova alivyotangaza kupitia kwa Ezekieli:
14 “Katika uchafu wako mna uasherati, kwa maana nimekusafisha, ila wewe hukusafika; hutasafishwa tena uchafu wako ukutoke, hata nitakapokuwa nimeituliza hasira yangu kwako. Mimi, [Yehova], nimenena hili, nalo litakuwa; nami nitalifanya; sitaachilia, wala sitahurumia, wala sitajuta; sawasawa na njia zako, na sawasawa na matendo yako, ndivyo watakavyokuhukumu.”—Eze. 24:13, 14.
15 Mwanzo wa mazingiwa ya Kibabeli ulihakikisha kwamba Yerusalemu, mji mkuu wa Ufalme wa Yuda, alikuwa amekataa kusafishwa uasherati wake wa kiroho. Kwa kweli, uchafu wake usingekoma mpaka wakati ambapo Yehova angeituliza hasira yake kwa kuagiza mji wenye hatia ya damu uharibiwe. Yeye asingejuta asichukue hatua hii kali.
MATOKEO YENYE KUSHTUA YAFANYIZWA NA UHARIBIFU WA YERUSALEMU
16. Wahamishwa wenzi wa Ezekieli wangeuonaje uharibifu wa Yerusalemu, na kwa sababu gani?
16 Uharibifu wa Yerusalemu kweli ungekuwa na matokeo yenye kushtua juu ya wahamishwa wenzi wa nabii Ezekieli. Uharibifu huo ungemaanisha kuharibiwa kwa hekalu lenye fahari lililojengwa na Sulemani, jengo ambalo Wayahudi walitazama kama kitu cha kuwakinga na msiba. (Yer. 7:1-11) Vile vile ungemaanisha kwamba wengine kati ya wayahudi wazee katika Tel-abibu wangefiwa na wana na binti ambao walilazimishwa wawaache katika Yerusalemu wakati walipotwaliwa katika uhamisho. Nabii Ezekieli aliagizwa aonyeshe mfano wa ambavyo uharibifu wa Yerusalemu ungekuwa na matokeo juu yao. Aliambiwa hivi:
17. Ezekieli angeonyeshaje matokeo ya uharibifu wa Yerusalemu kwa wahamishwa wenzake?
17 “Tazama, [mimi Yehova] ninakuondolea kwa pigo moja tunu, mteule wa macho yako; walakini hutaomboleza wala kulia, wala yasichuruzike machozi yako. Ugua, lakini si kwa sauti ya kusikiwa; usifanye matanga kwa ajili yake yeye aliyekufa; jipige kilemba chako, ukavae viatu vyako, wala usiifunike midomo yako, wala usile chakula cha watu.”—Eze. 24:15-17.
18. Ni maono gani ya kusikitisha aliyopatwa nayo Ezekieli kwa utimizo wa neno la Yehova na alijiongozaje mwenyewe kwa habari hiyo?
18 Yeye ambaye ni mteule wa macho ya Ezekieli alikuwa mke wake mwenyewe, aliyekufa baadaye katika muda wa punde kuliko saa 24. Kwa kutii amri ya Yehova, Ezekieli mwenye umri wa miaka 34 alitumia kujiweza juu ya maono yake ya moyoni ya kibinadamu. Yeye hakutoa ishara yo yote ionekanayo au yenye kusikika ya kuhuzunikia kifo cha mke wake. Alivaa kilemba chake, akakifunga vizuri, na hakuacha yo yote ya sehemu yake ifunike uso wake na kufunika mdomo wake. Hakutembea bila viatu kwa kuhuzunika wala hakuwaacha wenye kumfariji wamtayarishie chakula cha kumpa rambirambi. Jambo hili lilileta mshangao kati ya wahamishwa wenzake. Waliuliza hivi: “Je! hutaki kutuambia maana ya mambo haya kwetu?” (Eze. 24:18, 19) Ezekieli alijibu hivi:
19. Ezekieli aliwaelezaje wahamishwa wenzake maana ya matendo yake nyuma ya kifo cha mkewe?
19 “Neno la [Yehova] lilinijia, kusema, Uwaambie nyumba ya Israeli, Bwana [Yehova] asema hivi; Angalieni, nitapatia unajisi patakatifu pangu, fahari ya uwezo wenu, mahali pa kutamaniwa na macho yenu, ambapo roho zenu zinapahurumia; na wana wenu na binti zenu, mliowaacha nyuma, wataanguka kwa upanga. Nanyi mtafanya kama mimi nilivyofanya; hamtaifunika midomo yenu, wala kula chakula cha watu. Na vilemba vyenu vitakuwa juu ya vichwa vyenu, na viatu vyenu miguuni mwenu; hamtaomboleza wala kulia; lakini mtafifia katika maovu yenu, na kuugua kila mtu pamoja na mwenziwe. Basi ndivyo Ezekieli atakavyokuwa ishara kwenu; ninyi mtatenda sawasawa na yote aliyoyatenda yeye; litakapokuja jambo hili, ndipo mtakapojua ya kuwa mimi ndimi Bwana [Yehova].”—Eze. 24:20-24.
20. Wahamishwa wenzi wa Ezekieli walikuja kumjua Yehova namna gani?
20 Kutokuaminika kwa wakaaji wa Yerusalemu na wahamishwa wa Kibabeli ndivyo kulivyokuwa hata kungetaka pigo kwa namna ya uharibifu wa mji mtakatifu, hekalu na watoto mbele ya wao kupata kujua kwamba Yehova asingevumilia hatia ya damu na uchafu wa adili. Wao wenyewe wasingesadiki ya kwamba Yehova angepatia unajisi patakatifu pake mwenyewe kwa kuwaacha Wababeli wapagani, wenye kuabudu sanamu walitwae, waliteke nyara na kuliharibu hekalu la Sulemani lililokuwa limesimama kwa muda wa miaka 420. Walakini, Yehova asingehurumia kile ambacho alisimulia kwa wahamishwa kama ‘fahari ya uwezo wao, kitu cha kutamaniwa na macho yao na ambacho nafsi zao zinahurumia’ (ama patakatifu pa Yehova katika Yerusalemu ama wana na binti zao huko). Wakati wa kutimizwa kwa neno lake katika njia yenye kushtua ingewapasa wahamishwa hawa wajue ya kwamba Yeye aliyesema angefanya jambo hilo na Yeye ambaye kweli alilifanya angekuwa mmoja na Mtu yule yule, Yehova.
KRISTENDOMU MWENYE HATIA YA DAMU HAWEZI KUOKOKA
21. Kwa sababu ya lililotukia kwa Yerusalemu, ni nini kitakachompata Kristendomu?
21 Kama vile Yehova Mungu hakuvumiliana Yerusalemu mwenye hatia ya damu kwa wakati usiojulikana, ndivyo hatamvumilia Kristendomu mwenye hatia ya damu. Kristendomu ajapojidai kuwa anamtumikia Mungu, matendo yake yanaonyesha vingine. Yeye si kundi la Mungu au hekalu anamokaa kwa njia ya roho. (1 Kor. 3:16) Kujidai kwake kuwa hekalu hilo hakutamwokoa hata kidogo kama kusivyoliokoa hekalu la Sulemani ati kwa sababu lilikuwa katika Yerusalemu. Kujidai huko kutafunuliwa kuwa kwa uongo wakati atakapoharibiwa kabisa.
22. Mambo ambayo mashahidi wa Yehova wa Kikristo waliotiwa mafuta wamekuwa wakitangaza juu ya Kristendomu yatahakikishwaje kuwa kweli?
22 Mtu asifikiri kwamba uharibifu huu hautakuja, kwa maana Yehova Mungu hakugeuza maoni yake juu ya hatia ya damu na uchafu wa adili. (Mal. 3:5, 6) Matukio ya wakati ujao na habari zitakazotokea zitaonyesha mambo ambayo mabaki ya mashahidi wa Yehova wa Kikristo wamekuwa wakitangaza juu ya mwisho wa Kristendomu kuwa ya kweli. “Dhiki kubwa” itakapoanza juu ya Kristendomu mabaki watiwa mafuta watajua na hawatakuwa na shaka juu ya matokeo yake. Yale ambayo watakuwa wamekwisha kutangaza wakati huo juu ya matokeo ya dhiki hiyo yatatosha. Hawatakuwa na ujumbe wenye tumaini kwa Kristendomu.
23-25. Ni kwa maana gani Ezekieli alikuwa bubu nyuma ya kuanza kwa mazingiwa ya Yerusalemu, na ububu huu ungeendelea mpaka lini?
23 Hali ya mabaki watiwa mafuta wakati huo italingana na ile ya Ezekieli aliyeambiwa hivi:
24 “Nawe, mwanadamu, je! haitakuwa hivi katika siku hiyo nitakapowaondolea nguvu zao, na furaha ya utukufu wao, na kilichotamaniwa na macho yao, ambacho walikiinulia mioyo yao, wana wao na binti zao, kwamba katika siku iyo hiyo yeye atakayeokoka atakuja kwako, akusikize jambo hili kwa masikio yako? Siku hiyo kinywa chako kitafumbuliwa kwake aliyeokoka, nawe utasema; hutakuwa bubu tena; ndivyo utakavyokuwa ishara kwao; nao watajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova].”—Eze. 24:25-27.
25 Wakati mazingiwa ya Yerusalemu yalipoanza, Ezekieli alikuwa amekwisha kusema ya kutosha kwa watu wake. Hakukuwa na haja ya yeye kuongeza zaidi ili kuufanya unabii wa kimungu uonekane kuwa wenye kusadikisha zaidi. Basi mpaka siku hiyo ya kutokea kwa taarifa au ripoti ya uthibitisho ilimpasa Ezekieli awe bubu, yaani, awe kimya kwa habari ya kutoa unabii tena juu ya msiba utakaoupata Yerusalemu na Ufalme wa Yuda. Mpaka wakati ambapo mmoja aliyeokoka mwishowe angefika akiwa na ripoti juu ya kuharibiwa kwa Yerusalemu, Wayahudi waliohamishwa katika Babeli wangeweza kuyafikiria yale ambayo Ezekieli alikuwa ametabiri kwao. Ikiwa wangechagua, wangeweza kuendelea kuwa wasiosadiki. Lakini mwishowe kutosadiki kwao kungevunjwa-vunjwa wakati mjumbe wa kweli aliyeona kuharibiwa kwa Yerusalemu angefika.
26. Ezekieli alikuwa mtu wa “ishara” ya nini?
26 Hapo ndipo Ezekieli angeweza kusema kutokana na msingi bora wa matukio. Angekuwa na ujumbe mpya. Mamlaka yake kama nabii wa kweli wa Yehova aliyeongozwa na roho yake ingalithibitishwa. Kama “ishara” ya jambo lililokuwa likikaribia sana sana, yeye hakuonekana kuwa mwongo.
27. Leo watu watakujaje kujua kwamba jamii ya Ezekieli wa kisasa ina “ishara” ya wakati unaofaa?
27 Kama vile uharibifu juu ya Yerusalemu wenye hatia ya damu ulivyokuja, ndivyo uharibifu juu ya Kristendomu mwenye hatia ya damu utakavyokuja bila shaka. Taarifa au ripoti zitazokuwa zikisikiwa kutoka sehemu zote za ulimwengu ambako sasa Kristendomu ameenea zitaonyesha ukweli kwamba jamii ya kisasa ya Ezekieli, mabaki watiwa mafuta wa mashahidi wa Yehova wa Kikristo, ilikuwa “ishara” inayofaa wakati kutoka kwa Mwenye Enzi Yote Bwana wa ulimwengu wote. Wakati huo itawapasa watu wamjue Yehova kama Mungu asiyeacha matendo ya jeuri na hatia ya damu bila kuadhibiwa. Kwa hiyo, je! usingekuwa mwendo wenye hekima sasa kusikia ambayo mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanatangaza ili mtu aepuke kujiletea mwenyewe msiba wakati Kristendomu atakapoufikia mwisho wenye jeuri?
—Kutoka Kitabu “The Nations Shall Know that I Am Jehovah”—How?
[Picha katika ukurasa wa 365]
Mazingiwa ya Yerusalemu kama yalivyofananishwa na Yehova