Ukarimu Unatokeza Ukarimu
ROHO ya ukarimu imejaa katika shughuli zote za Mungu na viumbe vyake vya kidunia. Miaka elfu tatu iliyopita mwanamume mwenye ufahamu aliandika: “[Yehova] huwategemeza wote waangukao, huwainua wote walioinama chini. Macho ya watu wote yakuelekea Wewe [Yehova], nawe huwapa chakula chao wakati wake. Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” (Zab. 145:14-16) Je! unakubaliana na ungamo hilo lililoongozwa na roho ya Mungu?
Kuna wale ambao hawangekubali. Kwa kweli jamaa yote ya kibinadamu imemsahau Mungu. Wanasahau kukumbuka yeye na kanuni zake za haki katika maisha zao. Umati mkubwa unakana kuwako kwa Yehova na wanakataa kulifikiria Neno lake kwa uzito, Biblia Takatifu. Hata hivyo, mwendo wao haukanushi kwamba Mungu ni mkarimu. Kwa kweli unafunua kina cha ukarimu wake, kwa kuwa hata watu wasioshukuru wanafaidika kutokana nao. Yehova Mungu “huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.”—Mt. 5:45.
Na kuna mengi zaidi. Mungu anapendekeza na kusisitiza kwa waabudu wake roho ile ile nzuri—ile ya kuwa mkarimu na tayari kutoa. Mfano wa fundisho lake kwa watumishi wake wa kidunia ni maneno haya: “Nafsi ya mtu mkarimu itawandishwa; anyweshaye atanyweshwa mwenyewe.” (Mit. 11:25) Na katika sheria ambayo Mungu alitoa kupitia kwa Musa kama mpatanishi shauri hili lilitiwa ndani: “Mpe [ndugu yako aliyepatwa na umaskini] kwa kweli, wala moyo wako usisikitike utakapompa; kwa kuwa atakubarikia [Yehova], Mungu wako, kwa neno hili katika kazi yako yote, na katika utakalotia mkono wako.”—Kum. 15:10.
Halafu, alipokuwa akimtuma Mwana wake mwenyewe ulimwenguni kuwapa wanadamu wenye dhambi nafasi ya uzima, Yehova Mungu aliendelea kusisitiza lazima ya wema na ukarimu. Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliwasihi wanafunzi wake: “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa, kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.” (Luka 6:38) Mbali na kupitisha fundisho la ukarimu alilokuwa amepokea kutoka kwa Baba yake, Yesu alionyesha kushikamana kwake imara nalo. Alijitolea kwa kupenda katika kazi ya kuwavuta watu kwa Mungu, mwishowe akiutoa uhai wake wa kibinadamu kama dhabihu kwa ajili ya wanadamu wote.
Je! habari hiyo ya kutoa kwa ukarimu ilikuwa ya bure kwa watu walioishi wakati huo? Kwa umati mkubwa, Ndiyo. Lakini mitume na wanafunzi wa Yesu kwa hiari walikubali kukaribisha kwake kufuata mfano wake, ndiyo, kuiga ukarimu wake. Tunajuaje? Kwa sababu ya lililotukia katika Yerusalemu nyuma ya umwagaji wa roho takatifu ya Mungu siku ya Pentekoste katika mwaka wa 33 C.E. Makutano ya Wayahudi na waongofu waliokuwa ziarani Yerusalemu kutoka nchi za mbali wakawa waamini katika Kristo Yesu. Walipoamua kubaki katika mji kadiri iwezekanavyo kupata ufahamu bora zaidi wa Njia ya Kikristo ya kweli, kulitokea takwa kati yao kwa lazima za maisha. Hawakuwa na fedha ya kutosha kuendelea kukaa zaidi. Na hali waliwezeshwa kubaki Yerusalemu kwa ukarimu wa waamini wenzao walioishi humo na katika Uyahudi. Wakristo hao wa Yerusalemu na Uyahudi kwa furaha walitoa cho chote walichoweza kwa faida ya ndugu zao na dada katika Kristo.—Matendo 4:32-35.
Je! msaada huo ulitolewa kwa sababu ya kuwasaidia tu si kwa kupenda? Hapana, lilikuwa tendo la ukarimu kwa faida ya kueneza “habari njema” za Ufalme ambazo Kristo aliagiza wafuasi wake wapeleke katika mataifa yote. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Wonyesho huo wa ukarimu ulitimiza kusudi lake. Maelfu mwishowe walirudi katika nchi zao wenyewe wakiwa na maarifa ya kutosha na ufahamu ili kushiriki “habari njema” na wengine. Namna walivyokuwa wenye furaha kuwa walipokea bure na kuweza kutoa bure!
Lakini namna gani juu ya hali leo? Katikati ya idadi ya ulimwengu inayosukumwa sana na roho ya ushupavu, je! kuna watu wanaojaribu kuwa kama Mungu wao mkarimu? Ndiyo, wengi wameona roho hii ya ukarimu kati ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova. Inawashangaza kuwaona mashahidi wa Yehova wakitoa wakati wao na mali ili kwamba wengine waweze kupata maarifa ya Biblia.
Kwa sababu ya utendaji wao, miaka 30 iliyopita tangazo la habari ya Ufalme limeenezwa sana. Nyuma katika mwaka wa 1941 C.E. watu 106,137 walikuwa wakishiriki katika kazi hii. Lakini katika mwaka wa 1972, kulikuwa na watu 1,658,990 waliofanya hivyo. Waliotiwa ndani katika hesabu hii walikuwa maelfu ya wamisionari waliokuwa wamezoezwa na kufundishwa kusema lugha fulani nyingine na kupewa mgawo kwenye maeneo mapya ili kufungua kazi ya Ufalme. Mpanuko wenyewe umekuwa na maana ya kupata na kuendelea kutunza maelfu ya sehemu za mikutano au Majumba ya Ufalme duniani kote. Maafisi ya tawi zaidi ya Watch Tower Bible and Tract Society (chombo halali cha mashahidi wa Yehova) imekuwa lazima yaanzishwe katika nchi nyingi. Majumba mapya na makubwa zaidi ya tawi na viwanda vya uchapaji vimepangwa na vingali vinapangwa.
Mpanuko huu wote umegharimu kadiri kubwa ya fedha. Je! fedha hii ilipatikana kwa njia yo yote tofauti na fundisho la Yesu kwamba kutoa kusifanywe ‘kusudi kutazamwe na watu’? (Mt. 6:1-4) Hapana, ilikusanywa kutoka kwa michango midogo-dogo inayotolewa kwa faragha na watu zaidi wasio na mali nyingi. Michango hii iliwekwa katika visanduku vya michango bila jina la aliyetoa vinavyopatikana katika Majumba ya Ufalme mahali pengine pa mikutano pa mashahidi wa Yehova. Vile vile ilitia ndani na michango iliyotumwa moja kwa moja kwa maafisi ya tawi ya Sosaiti. Michango hii yote ilikuwa ya kujitolea. Ilichangwa na watu walioona lazima ya kushiriki kwa ukarimu katika gharama ya kuanzisha kazi ya Ufalme na kutunza kazi hiyo katika nchi mpya duniani kote.
Kwamba michango hiyo kila mara imekuwa ya kutosha ni lazima sifa imwendee Yehova Mungu. Amewajaza watumishi wake roho ya ukarimu.
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba kuhubiri kwa habari ya Ufalme ni kazi yenye uongozi wa Mungu. Wanafahamu kwamba Yehova angeweza kuitimiza kwa njia ya mwujiza. Na hali, kwa ukarimu, amewapendelea wanadamu wasiokamilika kwa nafasi ya kushiriki katika hiyo kama “wafanya kazi pamoja na Mungu.” (1 Kor. 3:9) Kwa hiyo mashahidi wa Yehova wana sababu nzuri kuona kama pendeleo kutoa wakati wao, nguvu na fedha kwa kazi ya kueneza “habari njema” za ufalme wa Mungu, wakiwafariji maelfu wanaopiga kite kwa sababu ya taabu, udhalimu na maonezi ambayo wakazi wengi wa dunia wanaona.