Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Kulingana na yaliyoandikwa katika Kumbukumbu la Torati 22:5, je! inafaa kwa mwanamke kuvaa suruali ndefu zisizo za kubana?—U.S.A.
Kumbukumbu la Torati 22:5 linasema: “Mwanamke asivae mavazi yampasayo mwanamume, wala mwanamume asivae mavazi ya mwanamke; kwa maana kila afanyaye mambo hayo ni machukizo kwa [Yehova], Mungu wako.” Andiko hili halizungumzi mitindo ya mavazi. Katazo ni juu ya kuvaa kwa mtu vitu vilivyokusudiwa vivaliwe na mwanamume ama kuvaa kwake vitu vilivyokusudiwa vivaliwe na mwanamke.
Tofauti iliyoko kati ya mwanamume na mwanamke ina chanzo cha kimungu na sheria iliyowekwa katika Kumbukumbu la Torati 22:5 ilitumika kuhifadhi tofauti hiyo. Linapokuwa shauri la sura na mavazi, jambo la kawaida ni kwa mwanamume kutaka kuonekana kama mwanamume na kwa mwanamke kuonekana kama mwanamke. Kama Mwisraeli angalitenda tofauti na shauri hili kubwa la yanayofaa ingaliweza kumwongoza kwenye kumlala mwanamke mwenzake au mwanamume mwenzake. Hivyo sheria katika Kumbukumbu la Torati 22:5 iliikataza dhambi hii vile vile.
Wakati ilipotolewa sheria hii, wanaume na wanawake vile vile walivaa mavazi marefu (kama joho) ya heshima. Lakini ilikuwako tofauti ya wazi kati ya vazi la wanaume na lile la wanawake. Vivyo hivyo, katika sehemu nyingine za dunia leo wanaume na wanawake vile vile wanavaa suruali ndefu zisizo za kubana. Lakini mitindo ya suruali ndefu zisizo za kubana za wanawake ni tofauti na ile ya wanaume. Kwa hiyo, kanuni inayofundishwa katika Kumbukumbu la Torati 22:5 isingemkataza mwanamke kuvaa suruali ndefu zisizo za kubana.
Zaidi ya hayo, Wakristo hawamo chini ya sheria ya Musa. (Rum. 6:14) Kusisitiza kutumia maneno ya sheria hii basi kungekuwa kusikopatana na fundisho la Kikristo. Kwa hiyo kama mwanamke angevaa suruali ndefu iliyochakaa ya mumewe afanye kazi karibu ya nyumba au katika shamba, asingekuwa akitenda tofauti ya kusudi la waziwazi la sheria, yaani, kuzuia kushindwa kupambanua kati ya mwanamume na mwanamke na kuzuia mazoea mabaya.
Uhakika wa kwamba Wakristo hawamo chini ya sheria ya Musa lakini wanaongozwa na kanuni zake unawataka watumie ufahamu, busara na kutumia dhamiri yao. Mwanamke wa Kikristo anafahamu kwamba kama ingefaa kwake avae suruali ndefu zisizo za kubana inategemea mambo mengine yasiyo mapendezi yake mwenyewe. Yeye asingetaka kuwa sababu ya kuwakwaza wengine au kuliletea kundi la Kikristo suto. Huenda vazi linalotazamwa kwa kutolipendelea likivaliwa nyumbani mwa mtu au kazini likachukiza likivaliwa penye mikutano ya Kikristo na wakati wa kulitangaza Neno la Mungu waziwazi ama kuendesha kazi nyingine yo yote ya waziwazi. Hali, vile vile, huenda zikatofautiana eneo kwa eneo. Onyo la Biblia ni kwamba wanawake “wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi; . . . kwa matendo mema, kama iwapasavyo wanawake wanaoukiri uchaji wa Mungu.”—1 Tim. 2:9, 10.a
[Maelezo ya Chini]
a Kwa maelezo zaidi juu ya shauri la mavazi yanayofaa, tazama Mnara wa Mlinzi wa Desemba 15, 1972, kur. 574-576.