Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Ufunuo 14:3 unasema: “Na kuimba wimbo mpya mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele ya wale wenye uhai wanne, na wale wazee; wala hapana mtu aliyeweza kujifunza wimbo ule, ila wale mia na arobaini na nne elfu, walionunuliwa katika nchi.” Ikiwa wazee wanaotajwa hapa, na katika Ufunuo 4:4, wanafananisha jamii yote ya makuhani—wafalme 144,000, yawezekanaje hao 144,000 waimbe mbele ya wazee hawa?—Ecuador.
Jawabu la kukielewa kitabu cha Ufunuo limetolewa katika maneno yake yanayotangulia: “Ufunuo wa Yesu Kristo, aliopewa na Mungu awaonyeshe watumwa wake mambo ambayo kwamba hayana budi kuwako upesi; naye akatuma kwa mkono wa malaika akamwonyesha mtumwa wake Yohana kwa ishara.” (Ufu. 1:1, NW) Kwa wazi, jambo lisiloweza kuonekana kabisa kama lilivyo laweza kufananishwa kwa ishara na mifano. Kwa mfano, ijapokuwa mtu hawezi kuimba akiwa mbele yake mwenyewe, anaweza kusimama mbele ya picha yake mwenyewe na kuimba. Kwa hiyo kwa kweli hakuna jambo lenye kujipinga juu ya uhakika wa kwamba wale 144,000 wanafananishwa kama wamesimama mbele ya kitu ambacho kwacho wanafananishwa.
Hali zile zile za yeye aliyeiona njozi, mtume Yohana, zinatusaidia kuamua ni katika maana gani “wazee ishirini na wanne” wanaotajwa katika Ufunuo 4:4 ni mfano au ishara. Akiwa Myahudi, Yohana alijua kwamba “wazee wa Israeli” waliliwakilisha na kuzungumza kwa ajili ya taifa zima. (Kut. 3:16, 18; 19:7) Sasa, kundi zima la Wakristo waliotiwa mafuta linafanyiza “taifa takatifu” la Israeli wa kiroho, na “wazee” wa Kikristo wanaweza kulifananisha hilo “taifa” zima. (1 Pet. 2:9) Kwa kulingana na hilo, “wazee ishirini na wanne” walioketi juu ya viti vya enzi wangefananisha jamii zima ya 144,000. Hii hesabu ishirini na nne ingalimkumbusha Yohana migawanyiko ya kikuhani ishirini na minne iliyopangwa na Mfalme Daudi kutumikia katika hekalu la Yerusalemu. (1 Nya. (Sik.) 24:4) Hii inalingana vizuri na uhakika wa kwamba “taifa takatifu” la 144,000 watatenda kama “ukuhani wa kifalme.”
Vile vile angalia kwamba hapa Yohana alikuwa akipewa njozi ya matukio ya wakati ujao, “mambo ambayo hayana budi kuwako.” (Ufu. 4:1) Kwa hiyo, njozi ya “wazee ishirini na wanne” ilikuwa ya unabii wa mpango ambao Yehova Mungu angeusimamisha mbinguni. Wakati ambapo mtume Yohana aliiona njozi, hakuna hata mshiriki mmoja wa jamii ya 144,000 aliyekuwako mbinguni. Wale wa jamii hiyo waliokuwa wamelala katika mauti walikuwa wakingoja ufufuo. (1 Kor. 15:20-23, 51, 52) Lakini, uhakika wa kwamba “wazee ishirini na wanne” walionekana katika njozi ulihakikisha kabisa kwamba vyeo vya uzee vingejazwa na wale ambao kwa ajili yao vilikuwa vimewekwa.