Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w73 1/1 kur. 14-19
  • “Katika Makusanyiko Nitamhimidi (Yehova)”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Katika Makusanyiko Nitamhimidi (Yehova)”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUTOA KWA NAFSI YOTE KATIKA MAKUSANYIKO
  • KWA KUJITAYARISHA
  • KWA KUWAKARIBISHA NDUGU NA WAGENI WETU
  • KUSIKILIZA SANA
  • KWA KUIMBA
  • KWA SALA YA UMOJA
  • Wasaidie Wale Wanaohudhuria Mikutano
    Huduma Yetu ya Ufalme—1988
  • Ratiba ya Familia—Mikutano ya Kutaniko
    Huduma ya Ufalme—2005
  • Watu Wanakukosa!
    Huduma Yetu ya Ufalme—1997
  • Kwa Nini Tunapaswa Kukutanika Pamoja kwa Ajili ya Ibada?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1973
w73 1/1 kur. 14-19

“Katika Makusanyiko Nitamhimidi (Yehova)”

1. Ni makusanyiko gani ambayo katika hayo Daudi alisema, “Nitamhimidi [Yehova],” na kwa sababu gani aliweza kusema hivi? (b) Imepaswa iwe tamaa gani yetu ya moyo?

DAUDI alikuwa akisema juu ya tamaa yake ya moyo wakati aliposema hivi: “Katika makusanyiko nitamhimidi [Yehova].” (Zab. 26:12) Daudi alijulisha waziwazi makusanyiko hayo kama waabudu wa Yehova Mungu, kwa maana alisema hivi: “Sikuketi pamoja na watu wa ubatili, wala sitaingia mnamo wanafiki. Nimelichukia kusanyiko la watenda mabaya, wala sitaketi pamoja na watu waovu.” (Zab. 26:4, 5) Je! tamaa yetu ya moyo ni ile ile kama ya Daudi? Ikiwa ndivyo, basi tutamhimidi Yehova kati ya makusanyiko, maana yake kushiriki kwa uaminifu katika mikutano ya kundi ya mashahidi wa Yehova kila juma kwenye Jumba la Ufalme na vile vile kuhudhuria kila mwaka makusanyiko ya mzunguko na ya wilaya, ya taifa au ya mataifa yote.

2. Ni sababu gani fulani imetupasa kukusanyika kwa kawaida pamoja na watu wa Yehova?

2 Lakini sababu gani imetupasa tukusanyike pamoja na watu wa Yehova? Tunapata faida gani? Tunaweza kufikiria sababu ngapi zenye nguvu za kuhudhuria kwetu kila mkutano wa kundi kila juma, kwamba ni katika nyumba ya faragha au kwenye Jumba la Ufalme? Basi, na tuangalie chache za sababu hizi ili tuweze kuona ubora wa kukusanyika kwetu pamoja. Kukutana kwetu pamoja ni sehemu ya ibada yetu, inaamriwa katika Maandiko, na tunazoezwa penye mikutano kutoa dhabihu ya sifa yenye kukubalika. Tena, tunaonyesha kwamba sisi ni wanafunzi wa Kristo, na roho ya Yehova inakuwapo penye mikutano. Tunajengwa na washiriki wetu wa Kikristo, halafu na sisi, tunawajenga. Mikutano ya kundi ni chanzo cha chakula tele cha kiroho na vile vile mahali pasalama.

3, 4. (a) Ni msingi gani wa Maandiko tulio nao kwa kukusanyika pamoja, na kwa kukumbuka kusudi gani? (b) Kwa sababu gani ni jambo la lazima zaidi sasa kwamba tukusanyike pamoja kuliko wakati wo wote zamani?

3 Kukusanyika pamoja kama kundi ni sehemu ya lazima ya ibada yetu. Hili si jambo jipya. Imekuwa hivi sikuzote pamoja na Wakristo. Kitabu cha Matendo kinafunua namna kukusanyika pamoja kulivyokuwa sehemu ya maana ya ibada kwa Wakristo wa kwanza. Tunaambiwa hivi: “Na sikuzote kwa moyo mmoja walidumu ndani ya hekalu, . . . wakimsifu Mungu, na kuwapendeza watu wote.” (Matendo 2:46, 47) Basi, kufuata mfano wa Wakristo wa kwanza inatupasa sisi vile vile tukusanyike pamoja ili kumsifu Mungu.

4 Tena, kumsifu Yehova kati ya Wakristo wenzetu si wazo tu lililotokana na wanadamu, bali inaamriwa katika Maandiko. Tunaona amri hiyo imeelezwa waziwazi na Paulo: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” (Ebr. 10:24, 25) Siku hiyo imekaribia! Tunaiona! Na hivyo tunaamriwa tukusanyike pamoja, kumhimidi Yehova na kujengana.

5. Ni katika njia gani huduma yetu ya wazi inavutwa na kukutana kwetu pamoja na watu wa Yehova?

5 Halafu kuna shauri la sifa. Kila mkutano ambao tunahudhuria unatuzoeza sisi tutoe dhabihu ya sifa yenye kukubalika zaidi kwa Yehova. Kila wakati tunapokusanyika, tunapewa mazoezi yanayofaa katika kufanya tunda la midomo yetu, huduma yetu ya wazi, kuwa yenye kupendeza hata zaidi kwa Yehova. Kila mkutano unaongeza tamaa yetu kumhimidi Yehova kupitia kwa huduma hiyo.​—1 Pet. 3:15.

6. Tuna mfano wa nani kututia moyo tushirikiane na makusanyiko, na kwa kufanya hivyo tunaonyesha nini?

6 Je! ungefikiria kutohudhuria mkutano wakati unapojua kwamba Kristo Yesu angekuwako? Kristo Yesu alitupa sababu yenye nguvu kwa nini imetupasa tushirikiane na makusanyiko wakati aliposema: “Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.” (Mt. 18:20) Ndiyo, Kristo Yesu hakosi kuhudhuria mikutano wakati wo wote pamoja na wanafunzi wake wanaokusanyika duniani kwa kuwa anahudhuria mikutano yote mitano ya kundi inayofanywa na mashahidi wa Yehova wa Kikristo kila juma kupitia kwa kuwapo kwake kwa kiroho. Kwa hiyo je! tusihudhurie? Hii ndiyo njia ya maana sana kuonyesha kwamba sisi ni wanafunzi wake. Mahali ambapo watu wa Yehova wanapokusanyika, ndipo na roho Yake inapokuwa. Kujua hili kunatuongoza sisi tutake kuwa pamoja na watu wa Yehova. Hapo ndipo tunapoona roho ya Yehova, kama kurunzi yenye nguvu, yenye kutoa mwanga mahali fulani, ikitoa nuru na uongozi kwa wale wanaokusanyika hapo.

7. Tuna sababu gani nzuri kwa kukusanyika pamoja? Toa mfano.

7 Katikati ya makusanyiko tunajengwa kwa ushirika mzuri wa ndugu zetu, halafu, na sisi tunawajenga wengine. Kila mkutano unatoa nafasi ya kutiana moyo, na nafasi ya kuonyesha upendo wetu kwa ushirika mzima wa Wakristo wenzetu na kuona upendo wao kwetu. Lo! hii ni sababu nzuri kwa kukusanyika pamoja namna gani! Shahidi mmoja wa Yehova kipofu na kiziwi ambaye hakukosa hata kidogo nafasi ya kukusanyika pamoja na Wakristo wenzake alisema hivi: “Sikuzote mimi ninatazamia mikutano ya kundi ili kukutana pamoja na ndugu zangu kwa sababu ninajisikia vizuri zaidi, na kuwa na ndugu wakinipa mkono au kunigusa inanitia nguvu sana.” Ikiwa mtu ambaye ni kiziwi na kipofu, asiyeweza kusikia na kuona yanayotukia jukwaani, anajengwa hivyo, je! sisi tunaoweza kuona na kusikia, hatutajengwa zaidi wakati tunapokuwa kati ya wasifaji wa Yehova?​—Rum. 1:12.

8, 9. Mwito wa Maandiko kunywa maji ya kweli unatoka kwa nani na nani wanaokaribishwa, na ni faida gani ya mara hiyo ambayo tunapokea katika kuwa kati ya makusanyiko?

8 Vile vile mikutano ni chanzo cha chakula tele cha kiroho kwetu, na hivyo ni ya maana sana kwa ukuzi wetu wa kiroho. Yehova ndiye Mkaribishaji wetu penye kila moja ya wakaa hizi za chakula. Yeye Ndiye ambaye ametuandalia chakula, na kupitia kwa roho yake yeye anaendelea kutukaribisha tuje tunywe maji ya kweli. Ni kama ilivyoandikwa na Yohana: “Na [roho] na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.”​—Ufu. 22:17.

9 Mwisho, Yehova anabariki kwa amani watu wake wanaokusanyika. Mikutano ya kundi ni mahali penye utulivu sana katika ulimwengu wenye vita. Hapo ndipo tunapochangamana pamoja na ndugu na dada za Kikristo walio na amani ya Mungu inayopita wazo lote. Ikiwa tunapenda amani na tunaitaka, tutakuwamo kati ya makusanyiko.​—Flp. 4:7.

KUTOA KWA NAFSI YOTE KATIKA MAKUSANYIKO

10. Ni ulizo gani ambalo tunaweza kujiuliza wenyewe juu ya kushirikiana na Wakristo wenzetu, na ni kanuni gani ya Maandiko ambayo ingetumika?

10 Mpaka sasa tumeangalia sababu gani imetupasa tumhimidi Yehova katika makusanyiko. Sasa tunakuja kwenye sehemu nyingine ya shauri hili, nayo ni hii: Kutoa kwa nafsi yote katika makusanyiko. Katika maneno mengine, mimi mwenyewe naweza kutoa nini kwa kusudi la kumhimidi na kumsifu Yehova wakati ninaposhirikiana na ndugu zangu? Bila shaka kanuni hii, “Ni heri kutoa kuliko kupokea” inatumika hapa. Ikiwa tunatoa kwa nafsi yote, tutapokea baraka tele vile vile.

KWA KUJITAYARISHA

11. (a) Ni mashauri gani yawezayo kufuatwa ili kufaidika na mikutano ya kundi, na ni mfano wa nani ulio mzuri kufuata katika hili? (b) Sababu gani kutangulia kujitayarisha ni kwa lazima? Onyesha mfano.

11 Njia ya kwanza ya kutoa ni kwa kujitayarisha kabisa kwa mikutano yote mitano. Hii inamaanisha nini? Inamaanisha kutangulia kuweka wakati wa kusoma kwanza habari ambayo imepangwa kwa funzo la mkutano ujao. Tunaweza kufanya hivi mmoja mmoja au kama jamaa, labda kupiga mistari chini ya mawazo makuu kwa funzo la Mnara wa Mlinzi au kwa funzo la kitabu, au labda kwa kurudia habari ya Mkutano wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi au Mkutano wa Utumishi ili tuweze kuona mambo yaliyomo katika habari tutakayojifunza. Jamaa za Betheli katika ulimwengu wote ni mifano mizuri ya kuwa na orodha kwa kutangulia kujitayarisha kwa mikutano. Kila jioni ya Jumatatu inawekwa kwa funzo lao la jamaa la gazeti la Mnara wa Mlinzi na kuangalia habari ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Labda tuonyeshe mfano wa maana ya kutangulia kujitayarisha katika njia hii: Ninyi waume mnafurahia sana kurudi nyumbani mkiisha kufanya kazi sana siku nzima, ili mkapate chakula kizuri cha moto kilichotayarishwa na wake zenu. Namna gani ikiwa jioni moja unarudi nyumbani ukiwa na hamu kubwa ya kula na unaingia jikoni unakuta penye sahani yako pana kiazi kisichoambuliwa, kisichopikwa pamoja na kipande cha nyama ambayo bado kupikwa. Haielekei kama ungekila, ijapokuwa, kikitayarishwa vizuri, hiki ni chakula kizuri, chenye kuleta afya na nguvu. Sisi sote tunapenda kukifanya chakula chetu kuwa kizuri zaidi kwa kutayarishwa vizuri, kupikwa sawasawa. Kwa kweli, miili yetu inatumia zaidi vyakula fulani wakati vimepikwa. Akili zetu zinafanya kazi katika njia ile ile. Ikiwa hatutangulii kutumia wakati kutayarisha chakula cha kiroho kitakachopakuliwa kwetu penye mikutano, ikiwa hatutangulii kuziamsha akili zetu, tutaona vigumu zaidi sana kwa akili zetu kufahamu kabisa mawazo yanayotolewa penye mikutano. Lakini tukitangulia kusoma kwanza habari itakayotolewa, ndipo akili zetu zitakapopokea na kutumia kwa vyepesi zaidi chakula cha kiroho kinachopakuliwa.

12. Ni katika njia gani tunaweza kujitayarisha, na kwa sababu gani ni vizuri kwa wahubiri vijana vile vile kuwa na kutumia vitabu vyao wenyewe vya funzo penye mikutano ya Kikristo?

12 Njia nyingine ya kujitayarisha kwetu ni kwa wote katika jamaa kuviweka vitabu vyao vya funzo tayari kwa kutumiwa kwenye mikutano. Je! wewe umepata kuwapo penye mkutano na ukaona kwamba ulikuwa umekosa kuchukua nakala yako ya Huduma ya Ufalme, au kitabu chako cha nyimbo, au Biblia yako? Ndiyo, imetukia hivi kwa karibu sisi sote. Wahubiri wengine wanaepuka jambo hili kutukia kwa kuwa na mifuko miwili, mfuko mmoja ambao wanatumia kwa huduma ya shambani na mfuko mwingine ambao wanautumia kwa mikutano una vitabu vinavyotakiwa. Kuchunguza kwa haraka mfuko wa vitabu wakati haujaondoka kwenda kwenye mikutano kunaweza kukuonyesha kuwa umejitayarisha vizuri. Inapendekezwa kwamba wahubiri wetu vijana wawe na vitabu vyao wenyewe vya kutumia kwenye mikutano na wanaweza kuzoezwa na wazazi wao waone daraka lao kuvileta na kuvitumia wakati wa programu.

13. Akina baba, mama na watoto wanawezaje kushirikiana ili jamaa iweze kufika mapema kwenye mikutano, na jambo gani linakoswa tunapofika tumechelewa?

13 Ushirika mzuri wa jamaa katika kujitayarisha ni wa lazima katika kufika mapema kwenye mikutano. Hii ina maana kwamba ni lazima wake wahakikishe kwamba vyakula vimepikwa mapema, kuruhusu wakati unaofaa kwa jamaa kujitayarisha na kuanza safari kwenda kwenye mikutano. Hii ina maana kwamba imewapasa akina baba waweke wakati fulani wa kuondoka, wakifikiria mwendo ambao watasafiri kufika kwenye Jumba la Ufalme bila haraka yo yote au mwendo ulio salama ikiwa unaendesha motokaa. Hii ina maana kwamba watoto wamepaswa washirikiane na akina baba na mama zao kwa kuvaa upesi ukiwa ni wakati wa kujitayarisha kwenda kwenye mikutano. Kila mtu katika jamaa ana daraka la kusaidia kufika mapema kwenye mikutano. Ikiwa tunakosa wimbo au sala au sehemu ya mwanzo ya mkutano, chakula hicho cha kiroho kimetupotea sisi, na tunaweza vile vile kuwazuia ndugu zetu wasijifurahishe programu kwa kufika kwetu tumechelewa.

14. Hivyo, basi, jambo gani linatakiwa ikiwa tutamhimidi Yehova kwa kufaa katika makusanyiko?

14 Basi kama vile ilivyokuwa lazima kujitayarisha kabisa mbele ya kutolewa kwa dhabihu za sifa na kuhimidi kwa Yehova katika Israeli wa kale, vivyo kujitayarisha kwa kila mtu mapema ni kwa lazima ikiwa tutamhimidi Yehova katika makusanyiko kwa nafsi yetu yote.​—Law. Sura za 1, 2.

KWA KUWAKARIBISHA NDUGU NA WAGENI WETU

15. Tunawezaje kuwasalimu wapya, wageni na ndugu zetu wenyewe wa Kikristo tunapokusanyika pamoja, na kwa sababu gani hili ni la lazima?

15 Njia ya pili ambayo sisi sote tunaweza kutoa kwenye mikutano ni kwa kuwakaribisha kwa uchangamfu ndugu zetu za Kikristo, wapya, na wageni kwenye Jumba la Ufalme la mashahidi wa Yehova. Wengine kati yetu ambao asili yao ni watu wa kimya huenda wakaona kwamba hivi ni vigumu kidogo kufanya. Je! wewe umepata kumwuliza ndugu mwingine hivi: “Yule ni nani? Sijui kama ni Shahidi.” Basi, je! si afadhali ingekuwa bora kumwendea mtu huyo na kupata habari? Si vigumu ikiwa tunakumbuka kwamba jambo kubwa kupendezwa katika wengine. Jijulishe mwenyewe kisha umwulize mpya huyo maulizo machache ya kirafiki hivi: Anaishi wapi? Je! amepata kufika kwenye Jumba la Ufalme zamani? Alikuja leo namna gani ili ahudhurie? Halafu, tukimwacha mpya aseme, upesi atajiona kukaribishwa na kwamba tunapendezwa na yeye. Chukua matembezi ya kutazama Jumba la Ufalme. Kuna mambo mengi sana ya kumwonyesha mgeni na kumweleza. Kumbuka sisi tulivyojiona mara ya kwanza tulipofika kwenye Jumba la Ufalme na tuliyoona yanapendeza. Halafu mwonyeshe mpya machache ya haya. Tunaweza kueleza kusudi la mikutano mbalimbali na namna inavyoongozwa, kumwonyesha maktaba ya Jumba la Ufalme, meza ya vitabu; eleza namna vitabu vya Biblia vinavyotungwa, na namna huduma yetu mmoja mmoja inavyofanywa. Tukiona kwamba tunasema na Shahidi, tunayo mambo mengi sana ya kushiriki sote. Tunaweza kumwuliza juu ya kundi lake, wahubiri wangapi waliomo, anahubiri katika sehemu ya namna gani; mtie moyo asimulie machache ya mambo aliyoona, na sisi vile vile tunaweza kumfahamisha na kundi letu. Ndiyo, sisi sote na tufanye sehemu yetu katika kumkaribisha kila mtu kwa uchangamfu kwenye mikutano, kutia na Wakristo wenzetu ambao tumetumikia pamoja nao kwa miaka mingi. Hii ndiyo njia nyingine ya kutoa katika makusanyiko.

KUSIKILIZA SANA

16. Tunaweza kufanya nini ili kukaza fikira sana ili tupate faida kutokana na hotuba ya msemaji?

16 Njia ya tatu ni kusikiliza sana programu wakati inapotolewa. Msemaji wa kawaida anasema polepole zaidi kuliko anavyofikiri msikilizaji wa kawaida. Tutafanya nini na wakati wote huo wa ziada wa kufikiri? Tusipokuwa waangalifu tutajikuta wenyewe tunafikiria mengine kuliko yale ambayo msemaji anasema. Tunaweza kutumia wakati huu wa ziada wa kufikiri ambao sisi sote tunao katika njia hii kwa faida kamili zaidi sana: Wakati msemaji anapoendelea katika hotuba yake, tunataka si kuendelea pamoja na yeye tu, bali vile vile kuzunguka juu ya mawazo yake wakati tunapoendelea pamoja na yeye. Tusikiapo kila wazo mpya, tunaweza kujiuliza wenyewe hivi: Kwa sababu gani alisema vile? Hili linakamatanaje na mambo ambayo amekwisha kusema? Linalinganaje na yale ambayo nimekwisha kujua? Katika njia hii tunasikiliza kwa moyo wote na kufanya akili zetu kuwa na shughuli na kukazwa juu ya mawazo ya msemaji nyakati zote.

17. (a) Inatupasa tuwe na nini kwa chakula cha kiroho kinachotolewa? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Shahidi Mjapani aliyejifunza kweli alipokuwa kifungoni?

17 Ili kusikiliza katika njia hii ni lazima tupendezwe kweli kweli na kukiona chakula cha kiroho kinachotolewa kuwa bora sana. Lazima maoni yetu juu ya mkutano yawe kama yalivyokuwa maoni ya Shahidi Mjapani. Yeye alijifunza kweli wakati alipokuwa katika kifungo cha Kijapani akingojea kunyongwa. Alikuwa ameua watu wawili alipokuwa mwenye umri wa miaka kumi na minane, akahukumiwa kufa, na alikuwa amengojea kunyongwa kwake kutukia wakati wo wote kwa miaka minane. Katika mwaka wake wa tisa, alijifunza kweli na akawa mwenye bidii sana katika kuwahubiria wafungwa wenzake na wote walio nje ya kifungo ambao aliweza kuhubiria kwa barua. Alikuwa kutia moyo kukubwa kwa Mashahidi Wajapani kwa sababu ya kuona kwake kwa furaha ubora wa kweli. Shahidi huyu alisema kwamba angetoa cho chote katika ulimwengu ili ahudhurie mkutano mmoja tu pamoja na kundi, lakini hakuruhusiwa kufanya hivi. Alikufa bila kuhudhuria mkutano wakati wo wote. Mara tano kwa juma, sisi kama Wakristo tunalo jambo lenyewe ambalo mtu huyu alitamani sana. Ikiwa sisi tunaona ni jambo bora kuwapo penye kila mkutano, tutakuwa tukisikiliza kwa moyo wote, kutii amri ya Yehova “nisikilizeni kwa bidii, mle kilicho chema, na kujifurahisha nafsi zenu kwa unono.”​—Isa. 55:2.

18. Tunapata nini kutokana na maelezo penye mikutano, na jambo gani limepaswa lituongoze kutoa maelezo hayo?

18 Njia ya nne tuwezayo kutoa katika makusanyiko ni kwa kutoa maelezo na kushiriki katika mikutano. Je! si kweli kwamba hata tunaposhiriki kidogo katika mkutano, labda kutoa maelezo mafupi tu, tunapata uradhi mkubwa na furaha kutokana na mkutano? Ndiyo, furaha ya kweli inakuja wakati mtu anapoonyesha imani yake mwenyewe katika Yehova kati ya ndugu zake za Kikristo. Si shauri la kujiona kulazimishwa kutoa maelezo kisha kuacha na sehemu inayobaki ya mkutano kuwaachia wengine. Sivyo, ni upendo wetu kwa Yehova unaojaa ndani yetu na kufurika hata tunataka kumhimidi Yehova na kuonyesha upendo wetu kwake. Katika njia hii tunamtolea Yehova tunda la midomo yetu tunapokusanyika pamoja na watu wake katika ibada ya umoja.​—Ebr. 13:15.

KWA KUIMBA

19. Ijapokuwa tusiimbe vizuri zaidi, imetupasa tuoneje nyimbo zetu za sifa kwa Yehova?

19 Kuimba nyimbo za Ufalme kwa moyo na akili zetu, vile vile kwa midomo yetu, ndiyo njia ya tano ambayo tunaweza kutoa kwa moyo wote. Yatupasa tufikirie maana ya maneno wakati tunapoimba pamoja na kundi. Imetupasa tuangalie tusiruhusu akili zetu kutangatanga wakati tunapoimba maneno yanayojulikana. Tena, inatupasa tuimbe kwa kuvutwa sana, kuacha sauti tamu ya wimbo iamshe maono yetu ya ndani na moyo tumhimidi Yehova. Kweli, labda wengine watakuwa na sauti bora za kuimba, lakini kuimba kwetu kungawa hafifu ni kuzuri zaidi na kwa kupendeza kwa Yehova na kwa ndugu zetu kuliko mwimbaji bora zaidi au jamii ya waimbaji katika makanisa yote ya Babeli Mkuu. Kuimba kwetu peke yake pamoja na Wakristo wengine waliokusanyika, kunatupa nafasi nyingi kila juma kumhimidi Yehova.

KWA SALA YA UMOJA

20. (a) Kwa sababu gani ni lazima kwa kila mmoja wetu kukaza fIkira juu ya sala zinazotolewa katika kundi? (b) Tunawezaje kila mtu kutoa katika sala ya kundi lote?

20 Mwisho, moyo wetu juu ya sala ya kundi umepaswa uonyeshe roho ya kutoa hata ingawa tusiwe mtu aliyeombwa kuwakilisha kundi katika sala. Wakati sala inapotolewa mwanzoni na mwishoni mwa mkutano, je! tunasikiliza kwa makini sana, tukikaza mawazo juu ya sala ili tuweze kusema kweli “Amina” kwa maneno ambayo yamesemwa? Au tunaruhusu akili zetu kutangatanga kutoka kwa sala kwenda kwa mambo mengine ambayo tutafanya wakati au mkutano ukiisha kumalizika kama kuweka vitabu vyetu, au kumwona ndugu fulani, au magumu nyumbani? Yehova, ambaye ni mtu mkubwa na mwenye kuheshimiwa kuliko wote katika ulimwengu mzima, anasikiliza sala. Yehova anasikiliza yote yanayosemwa ingawa ana mambo makubwa yanayompasa kushughulika nayo. Ikiwa yeye anapendezwa sana na sala inayotolewa kwa ajili yetu, je! sisi tusisikilize kwa makini hata tuweze kukubali na kusema “Amina”? Yehova atakubali sala hiyo kana kwamba ilitoka kwa kila mmoja wa sisi ikiwa moyo na akili zetu viko pamoja na sala. Hivi ndivyo sisi mmoja mmoja tunavyotoa katika sala ya kundi lote hata inakuwa sala ya umoja ya kumhimidi Yehova.

21. (a) Simulia njia mbalimbali ambazo tunaweza kumhimidi Yehova katikati ya makusanyiko. (b) Tamaa yetu imepaswa iwe nini kama alivyosema Daudi katika Zaburi 27:4?

21 Hivyo basi, tumekwisha kuona kuna sababu ngapi za maana sana kwa kumhimidi Yehova kati ya makusanyiko, na tumezungumza namna tunavyoweza kutoa kwa nafsi yote kwa kusudi la kumhimidi Yehova kwa umoja kama kundi. Tunafanya hivyo kwa kujitayarisha kabisa, kwa kuwakaribisha wote kwenye mikutano, kwa kusikiliza sana kwa moyo wetu wote, kwa kushiriki katika kutoa maelezo, na kwa kujiunga katika kuimba na sala kwa moyo na akili zetu. Kwa kutoa katika njia hizi zote tutaona uzuri wa Yehova kati ya makusanyiko. Ndipo tutakapojiona sikuzote kama Daudi wakati aliposema: “Neno moja nimelitaka kwa [Yehova], nalo ndilo nitakalolitafuta, nikae nyumbani mwa [Yehova] siku zote za maisha yangu. Niutazame uzuri wa [Yehova] na kutafakari hekaluni mwake.” (Zab. 27:4) Ndiyo, sikuzote na iwe tamaa yetu ya moyo kumhimidi na kumsifu Yehova kati ya makusanyiko!

​—Kutoka The Watchtower, July 1, 1972.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Ili kumhimidi Yehova katika makusanyiko, yatupasa tutangulie kujifunza habari iliyopangwa

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kukaribisha wageni, na ndugu kwa uchangamfu, kwenye Jumba la Ufalme kwaweza kuwatia moyo katika jitihada zao kumkaribia Mungu

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuimba nyimbo za Ufalme kwa moyo na akili zetu ni njia moja ya kumhimidi Yehova

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wakati sala inapotolewa penye mkutano, je! wewe unasikiliza sana, hivyo kushiriki katika onyesho hili la ibada?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki