Kitulizo cha Huzuni
Je! unajisikia mwenye huzuni? Ikiwa hivyo, una mengi ya kufanya juu yake.
KASIMIRI alikuwa mtu mwenye furaha sana. Kwa miaka mingi alitumikia kama mmisionari wa Kikristo katika nchi geni. Ndipo siku moja, kutokana na sumu ya DDT, akapooza sehemu moja. Jambo hili lilimwachisha utumishi wa umisionari lakini halikumwacha katika maisha ya uvivu.
Ingawa hakutumia kwa uzuri kabisa viungo vyake, aliendelea alivyoweza na utumishi wa wakati wote mpaka siku moja alipopatwa na ugonjwa wa moyo akiwa mwenye umri wa miaka sitini na sita. Angeweza kuhuzunika sana kutokana na shida kubwa alizoziona, lakini je! alijisikia vile? Hapana; aliendeleza furaha yake, na nia yake ya kirafiki, kwa baraka yake na wengine. Aliweka mfano mzuri kwa wengine ambao nyakati nyingine wanaweza kupatwa na shida na kuwa na huzuni.
GUMU LILILOKO KOTE
Kuhuzunika kuna maana ya kusikitika, kuwa na majonzi. Kuna maana ya kuvunjika moyo, kuwa dhaifu kwa kiroho. Kuna maana ya kutazamia hali ya sasa na ya wakati ujao kuwa mbaya.
Watu wengi leo wamehuzunika kwa sababu ya hali za ufukara katika ulimwengu. Wengine wanahuzunika kwa sababu ya hali mbaya ya afya, uzee au shida za kimwili kama vile kushindwa kuona vizuri. Si wachache wanaohuzunishwa na upweke, kama vile wanaume na wanawake ambao ni wazee na ambao wamepoteza wapenzi wao kwa kifo.
Wengine wanaruhusu mabaya, shida na udhalimu waliovumilia kuwadhoofisha kwa kiroho. Nyakati nyingine wapenda haki wanavunjwa moyo na udhaifu na makosa yao. Tena, mhubiri wa Kikristo anaweza kuona huzuni kwa sababu ya upinzani au ubaridi anaokuta akihubiri habari njema za ufalme wa Mungu.
JE! UNASUMBULIWA NA HALI ZA ULIMWENGU?
Je! zinakusumbua? Kama ni hivyo, hiyo ni afadhali kuliko wewe kukasirishwa na kufanya jeuri mara kwa mara kama wengi wanavyofanya leo. Watu kama hao wanafanya mambo kuwa mabaya zaidi kwao wenyewe na kwa wengine. Jambo la kupendeza, ni kwamba kuna njia nyingine. Hakuna sababu ya kuhuzunika au kulipuka kwa hasira. Unaweza kupata faraja kutoka kwa Neno la Mungu. Yeye anaona yanayotendeka.—Ebr. 4:13.
Ndiyo, msikilize Mfalme Sulemani mwenye hekima aliyeshauri: “Ujapokuwa unaona maskini kuonewa, na hukumu na haki kuondolewa kwa jeuri . . . usilistaajabie jambo hilo; kwa sababu, aliye juu kuliko walio juu huangalia; tena wako walio juu kupita hao.”—Mhu. 5:8.
Si kwamba tu Yehova anaona yote yakitendeka, bali tena atayanyosha mambo wakati wake, kama vile Sulemani anavyotuhakikishia: “Kwa sababu hukumu juu ya tendo baya haitekelezwi upesi, mioyo ya wanadamu huthibitishwa ndani yao ili kutenda mabaya. Ajapokuwa mwenye dhambi amefanya maovu mara mia, akazidisha siku zake; lakini hata hivyo najua hakika ya kwamba itakuwa heri kwao wamchao Mungu, wenye kicho mbele zake; walakini haitakuwa heri kwa mwovu, wala hatazidisha siku zake, zilizo kama kivuli; kwa sababu hana kicho mbele za Mungu.”—Mhu. 8:11-13.
Kweli, maneno hayo yaliandikwa zamani, lakini utimizo wa unabii wa Biblia unatupa sababu za kuamini kwamba kizazi hiki kitaona Yehova akiondoka ili kuumeza uovu wote. (Mt. 24:3-34; Sef. 3:8) Kwa kuwa hili liko hivyo, una sababu ya kufanya kama Yesu alivyosema, ‘inua kichwa chako juu, kwa kuwa ukombozi wako umekaribia.’—Luka 21:28.
JE! SABABU YAKE NI MWILI?
Au sababu ya kuhuzunika kwako ni kushindwa kwa hali fulani ya kimwili? Mara kwa mara afya mbaya inafanya hali kuwa za kuhuzunisha; mbaya zaidi kuliko kawaida. Kama ni hivyo, jaribu kutengeneza mambo kwa kutumia utaratibu kwa mambo yote, kazini, rahani, na chakulani. Jifunze kuburudika, na uhakikishe kwamba unapumzika na kulala kwa kutosha. Kama kazi yako au njia ya maisha ni ya kukaa unaweza kupata mazoezi ya kila siku ya namna fulani yenye msaada.
Kuhuzunika vile vile kunaweza kusababishwa na kizuizi katika mwili. Kama hilo ndilo gumu lako basi mkumbuke mtume Paulo. Anasema aliteswa na “mwiba katika mwili,” ambao alimwomba Mungu mara kwa mara auondoe. Lakini kuliko kumwondolea Paulo mzigo huu, Mungu alimwambia: “Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu.” Kuliko kuhuzunika kwa vile gumu hilo halikuondolewa, Paulo alisema: “Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu [kama hema].” Ndiyo, fanya shida yako kama kitu cha kujivunia kwa Bwana kuliko kuhuzunika na fanya hivyo kwa kuendelea ijapokuwa shida hii! Kwa mfano wa siku hizi mfikirie mhubiri Kasimiri, aliyetajwa mwanzoni.—2 Kor. 12:7-9.
Kwa upande mwingine, inaweza kuwa huzuni yako ina sababu kubwa zaidi. Inajulikana kwamba hypoglycemia, ugonjwa wa kukosa sukari katika damu, unasababisha kuhuzunika kwa mtu. Ndipo tena, mageuzi ya mwanamke au ‘mabadiliko ya maisha’ yanaweza kumfanya ajione hivyo. Nyakati kama hizo kitulizo kinaweza kuwa ni namna nzuri ya kuponya au utabibu.
JE! YAWEZA KUWA NI UPWEKE?
Upweke unaweza kuumiza sana. Na vile vile na tamaa ya vijana ya kutaka kuwa nyumbani. Kama mojawapo ya hizo ndiyo sababu ya huzuni yako, basi jaribu kuirekebisha. Chini ya hali za sasa unaweza kukubali kuwa si kila mmoja atafurahia maisha ya jamaa yenye furaha. Kama wewe huna mwenzi wa ndoa, kumbuka kwamba si watu wote waliooa wana furaha na kwamba waliooa wanaweza kujiona upweke ingawa hawako peke yao. Namna gani hivyo? Kwa sababu ya kutoshirikiana iwapasavyo.—1 Kor. 7:28.
Ndilo jambo kubwa wale walio peke yao watajaribu kufanya, kujifunza kushirikiana na wengine. Kuwa tayari kuanza mazungumzo. Sababu gani usijaribu kuonyesha moyo wa kupenda usio wa kichoyo kwa wengine? Tafuta wale ambao vile vile wanaonekana kuwa peke yao. Itakuwa ni faida kwako na kwa wengine. Kama mtume ashaurivyo: “Semeni kwa kuzifariji nafsi zilizo na huzuni.”—1 The. 5:14, NW.
Kuza kukamatana kwa karibu na Muumba wako, Yehova Mungu, kwa kuliendea Neno lake Biblia. Zaidi Zaburi, Injili na nyaraka za Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki yaliyoongozwa na roho ya Mungu yamejaa misaada kwa huzuni. Lakini usiyasome kwa haraka; huwezi kupata faraja ya kutosha kwa kusoma haraka. Soma kwa sauti kama hali zikiruhusu; hata usomapo kwa utulivu, soma kwa njia ambayo unaona maana ya usemi iliyo sawa. Sikiliza maneno ya Yesu: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, [na kuwa wanafunzi wangu]; . . . nanyi mtapata raha nafsini mwenu.”—Mt. 11:28-30.
Msaada mwingine wa kushinda huzuni inayosababishwa na upweke ni kumgeukia Yehova Mungu mara kwa mara katika sala, si nyakati fulani tu katika siku. Sikiliza shauri la ‘kudumu katika sala,’ na “ombeni bila kukoma.” Kwa sababu ya kuwa na nafasi hii ya ajabu ya sala haikupasi ujione upweke wakati wo wote, kwa vile wakati wote unaye wa kuzungumza naye, Yehova Mungu. Hakuna shaka juu yake, sala ni njia mojawapo ya kuweza kufuata shauri: “Umtwike [Yehova] mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.”—Rum. 12:12; 1 The. 5:17; Zab. 55:22.
Lisilo la kusahauliwa vile vile ni kwamba unaweza kufarijika na kupata raha kutokana na kuimba nyimbo za Ufalme zilizotolewa na Watch Tower Society. Si kwamba nyimbo za kupendeza ni dawa tu kwa huzuni bali vile vile maneno yaliyounganishwa na nyimbo hizi, kwa mfano, Namba 97, “Zeri Katika Gileadi,” yanaleta faraja.
JE! UMEHUZUNIKA KWA SABABU YA UDHALIMU?
Je! umehuzunika kwa sababu ya mabaya, au kuumia kwa sababu ya kuvumilia udhalimu? Je! wewe ni mmoja wa wanaoumizwa na ubaguzi wa rangi? Au umehuzunika kwa sababu ya kutendewa mabaya na jamaa au rafiki?
Maelekeo ya leo ni kulipiza kisasi kwa wanaokuletea taabu, lakini Neno la Mungu linashauri mara kwa mara kwa kupinga mwendo huu: “Msimlipe mtu ye yote ovu kwa ovu . . . msijilipize kisasi, wapenzi, bali ipisheni ghadhabu; maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu mimi; mimi nitalipiza, anena Yehova.’”—Rum. 12:17, 19, NW.
Kuliko kurudisha baya kwa baya, mwambie Yehova juu yake katika sala, na ujaribu kuwatendea mema wale waliokutenda mabaya. Pata faraja kutokana na ahadi ya Mungu kwamba yeye anakaa “pamoja na yeye aliye na roho iliyotubu na kunyenyekea, ili kuzifufua roho za wanyenyekevu, na kuifufua mioyo yao waliotubu.” Fikiria hilo! “Aliye juu, aliyetukuka,” Mkuu wa ulimwengu wote na Mwenye Enzi Yote, Yehova Mungu, anafurahia wanaotubu na kunyenyekea!—Isa. 57:15.
Kumbuka kwamba Yehova si mwenye haki tu bali pia ni Mungu mwenye hekima na upendo. Anangoja mpaka wakati ufaao kabisa na kuukomesha udhalimu. Kama alivyoona Mfalme Sulemani, kwa kila jambo Mungu ana majira yake, wakati wa kuvumilia hali mbaya, na wakati wa kuzikomesha na kuleta haki, furaha na amani. Hivyo uwe na imani na kufanya kama nabii wa Mungu Mika alivyosema alifanya: “Nitamngojea Mungu wa wokovu wangu.” Ni kwa faida yako kujifunza kungojea na kuvumilia mambo haya.—Mhu. 3:1, 8; Mika 7:7.
UDHAIFU NA MAKOSA
Huzuni inaweza kuwa sehemu yako kwa kuwa kama mpenda haki unasikitikia udhaifu na makosa yako. Unaweza kuwa na shida ya kuzuia ulimi wako au hasira yako. Au unaweza kuwa na kosa la siri linalokusumbua. Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba “tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.” Na kama Wakristo watasameheana mara sabini na Saba, bila shaka Mungu pia atawasamehe.—1 Yohana 1:9; Mt. 18:22.
Uwe na faraja vile vile kutokana na kweli kwamba hata mtume Mkristo Paulo alipambana na uovu katika mwili wake. Aliandika: “Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda, ndilo nilitendalo.” Hata alijisema mwenyewe kama “maskini mimi!” Hata hivyo alikuwa mwenye shukrani kwa Mungu kwa sababu kwa moyo wake aliweza kuendelea kumtumikia Mungu.—Rum. 7:19-25.
JE! NI UBARIDI, KUPINGA AU MATESO?
Je! wewe ni mtumishi wa Yehova unayehuzunishwa na ubaridi au mienendo ya uadui unayokuta katika utumishi wako? Je! umetumikia sana na bado ukapata matokeo kidogo kutokana na utumishi wako?
Lakini Maandiko yanasemaje? Je! hayatufahamishi kwamba hii inaweza kuwa ni sehemu ya Wakristo? Kweli! Mwanafunzi Yakobo (5:10) anatuambia tufanyeje basi? “Ndugu, watwaeni manabii walionena kwa jina la [Yehova], wawe mfano wa kustahimili mabaya, na wa uvumilivu.” Nabii mmojawapo alikuwa Yeremia. Ingawa nyakati fulani alihuzunika hakukata tamaa au kuacha. Hata Yerusalemu ulipokwisha kuharibiwa aliweza kusema: “[Yehova] ni mwema kwa hao wamngojeao, kwa hiyo nafsi imtafutayo.”—Omb. 3:25; Yer. 20:8, 9.
Au fikiria aliyoyavumilia mtume Paulo kama anavyosema katika 2 Kor. 11:22-33. Hata hivyo aliweza kuandika: “Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi.”—2 Kor. 4:8-10.
Yaache maneno ya Yesu vile vile yakufariji: “Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Kwa kadiri unavyoendelea mbele kwa bidii katika utumishi wa Kikristo ijapokuwa kupinga au mateso ndivyo unavyoushinda ulimwengu. Kwa kufanya hivyo, unaonyesha wazi kwamba Mungu ni wa kweli na Shetani Ibilisi kuwa mwongo, na kwa hiyo uzima utapata na kuufurahisha moyo wa Yehova Mungu. Ungependa nini zaidi kuliko hicho?—Mit. 27:11; Mt. 10:22.
“KWA KADIRI YA IMANI YENU”
Wakati mmoja vipofu wawili walimwomba Yesu awarehemu. Yesu kwa kuwajibu aliwauliza: “Mnaamini kwamba naweza kufanya hili?” Walipojibu wanaamini, alirudisha uweza wao wa kuona akisema: “Kwa kadiri ya imani yenu mpate.”—Mt. 9:27-30.
Cho chote ambacho ndicho chanzo cha huzuni yako—hali za ulimwengu, udhaifu wa mwili, upweke, magumu, dhambi na makosa, ubaridi wa kupinga au mateso—kuna msaada wa kutegemewa, usioweza kushindwa wa kumaliza gumu lako. Neno la Mungu limejawa na ahadi za hakika. Lakini unapaswa uwe na imani, kama Yesu alivyowaambia wale vipofu: ‘Kwa kadiri ya imani yako utapata.’ Na yapaswa iwe imani ya kweli, imani itakayoonyeshwa wazi kuwa hai kwa kazi, imani inayoonyesha bidii ya kweli. Ni kama vile mwanafunzi Yakobo alisisitiza: “Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa.”—Yak. 2:26.
Kusoma tu makala hii hakutoshi. Fanya jambo fulani juu yake! Tumia wakati zaidi kusoma Neno la Mungu, fikiria kuzungumza na Mungu, uwe mwenye urafiki, jaribu kuwafariji wengine, shirikiana na Wakristo wa kweli. Kwa kufanya hivyo, unaweza kutazamia maneno ya mtunga Zaburi kuwa ya kweli kwa upande wako: “Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha.”—Zab. 126:5.