JULAI 6-12, 2026
WIMBO 98 Maandiko—Yaliongozwa na Roho ya Mungu
Kwa Nini Kanuni za Biblia Ni Muhimu?
“Mtoe miili yenu iwe . . . utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.”—ROM. 12:1.
JAMBO KUU
Kufafanua maana ya kanuni na jinsi tunavyoweza kuzitambua tunaposoma Biblia.
1-2. (a) Kwa nini Biblia inaweza kuitwa kitabu cha kale? (b) Kwa nini Biblia bado ni yenye manufaa leo?
BIBLIA ni kitabu cha kale. Kilianza kuandikwa miaka 3,500 hivi iliyopita, na kilikamilishwa karibu miaka 2,000 iliyopita. Hata hivyo, “neno la Mungu” linalopatikana katika kurasa zake liko hai na lina nguvu hata leo. (Ebr. 4:12; 2 Tim. 3:16, 17) Mamilioni ya watu wanakiri kwamba Biblia imewasaidia kukabiliana na maisha katika ulimwengu huu wa leo.
2 Lakini kitabu hicho cha kale kinawezaje bado kuwa na manufaa leo? Kuna sababu mbili za msingi. Kwanza, ujumbe wa Biblia unatoka kwa “Mungu aliye hai,” Muumba mwenye hekima yote. (1 Tim. 4:10; Rom. 16:26, 27) Pili, Biblia imeandikwa katika njia inayofunua kanuni zisizopitwa na wakati. Kanuni hizo zinaendelea kuwa zenye manufaa haidhuru kipindi cha wakati ambacho mtu anaishi au changamoto anazokabili.
3. Tutajibu maswali gani katika makala hii?
3 Kanuni za Biblia ni nini? Kwa nini ni za muhimu sana kwetu leo? Tunawezaje kutambua kanuni hizo tunaposoma Biblia? Makala hii itajibu maswali hayo. Tutaona pia jinsi mafundisho ya Yesu yanavyokazia thamani ya kanuni hizo.
KANUNI ZA BIBLIA NI NINI?
4. Kanuni za Biblia ni nini?
4 Kanuni za Biblia ni kweli za msingi zinazotegemeza sheria za Mungu. Pindi fulani, kanuni ya Biblia inaweza kutajwa waziwazi katika sheria. (Mt. 22:37) Hata hivyo, kanuni ni bora kuliko sheria hususa. Sheria hususa zinaweza kuwa na matumizi machache. Zinaweza kutolewa kwa ajili ya wakati au hali hususa. Lakini kanuni za Biblia zinaonyesha kwa mapana zaidi njia ya Yehova ya kufikiri. Kanuni zinaweza kufafanuliwa kuwa sababu ya kutungwa kwa sheria fulani. Kuna sababu nzuri inayotegemeza kila sheria ya Yehova. Lakini kanuni zinazotegemeza sheria hizo zinaweza kutumiwa katika hali kadhaa tofauti na hazipitwi na wakati. (Zab. 119:111) Huenda sheria zikahitaji kubadilishwa, lakini kanuni hazipitwi na wakati.—Isa. 40:8.
5. Tunaweza kutumia mfano gani ili kuonyesha tofauti kati ya sheria na kanuni? (Tazama pia picha.)
5 Ili kutusaidia kuelewa vizuri zaidi tofauti kati ya sheria na kanuni, fikiria mfano ufuatao. Huenda mama akamwambia mtoto wake mdogo, ‘Usiguse jiko.’ Hiyo ni amri au sheria. Lakini kanuni, au wazo, linalotegemeza sheria hiyo ni: Usiguse kitu cha moto; la sivyo, utaumia. Kanuni hiyo haihusu tu jiko la moto. Inaweza kutumiwa inapohusu pasi, au kifaa kingine chochote cha moto kinachoweza kusababisha madhara. Kanuni hiyo haitumiki tu kuhusiana na vitu vilivyo katika nyumba ya familia hiyo, bali pia katika maeneo mengine. Bila shaka, kadiri mtoto anavyokua, huenda atatumia jiko. Hata hivyo, bado atahitaji kuwa makini ili asiguse sehemu ambazo zinaweza kumsababishia madhara. Hivyo, huenda sheria ikabadilika, lakini kanuni ya msingi inayotegemeza sheria hiyo haibadiliki.
Sheria inaweza kubadilika, lakini kanuni za msingi zinazoitegemeza hazibadiliki (Tazama fungu la 5)
KWA NINI KANUNI ZA BIBLIA NI MUHIMU?
6. (a) Yehova anatupatia nini katika Neno lake? (b) Yehova anaonyeshaje kwamba anatuheshimu?
6 Kwa sababu anatupenda, Yehova anatupatia mwongozo hususa kupitia sheria ili tuweze kuepuka hatari. (Yak. 2:11) Pia, anatusaidia kuelewa kanuni, au mawazo, yanayotegemeza sheria hizo. Kupitia Neno lake, anatupatia mwongozo kwa ajili ya hali nyingi maishani ambazo huenda hakuna sheria hususa. Kanuni za Biblia zinatusaidia kufanya maamuzi mazuri maishani na kutenda yaliyo sawa. Kwa kutupatia kanuni hizo, Yehova anaonyesha kwamba anatuheshimu na anaturuhusu tuwe na uhuru wa kufanya maamuzi yanayothibitisha upendo wetu kwake na kwa viwango vyake.—Gal. 5:13.
7. Tunaweza kutumia mfano gani kuonyesha thamani ya kanuni za Biblia? (Tazama pia picha.)
7 Ili kuonyesha jinsi kanuni za Biblia zinavyoweza kutusaidia, fikiria kuhusu alama za barabarani ambazo madereva huona kwenye barabara kuu katika baadhi ya nchi. Kwa ujumla, kuna aina mbili za alama za barabarani. Baadhi ya alama hizo hutujulisha sheria ambazo ikiwa watu hawatazifuata wataadhibiwa. Huenda alama hizo zikaonyesha kiwango cha juu cha mwendo unaoruhusiwa au zikaonyesha sehemu ambazo ni lazima dereva asimamishe gari. Hata hivyo, alama nyingine nyingi huwaonya madereva kuhusu hali za hatari ambazo huenda wakakabili. Kwa mfano, huenda alama hizo zikamwonya dereva kwamba barabara ina utelezi au kuna wanyama wanaovuka. Dereva mwenye uzoefu atatumia utambuzi na kuendesha gari kwa uangalifu hata ingawa hakuna sheria hususa. Pia, ikiwa kuna mvua au theluji, dereva ataendesha gari kulingana na hali hizo hatari. Vivyo hivyo, ingawa Wakristo wanaepuka kabisa mwenendo wowote unaoshutumiwa kihususa katika Neno la Mungu, wanaepuka pia mawazo au matendo yoyote yanayoweza kusababisha wavunje sheria za Mungu. Ili waweze kufanya hivyo, wanahitaji kuwa na utambuzi.
Alama nyingi za barabarani zinawaonya madereva kuhusu hatari ambazo wanaweza kukabili. Kanuni za Biblia zinaweza kutusaidia kwa njia hiyohiyo (Tazama fungu la 7)
8. Kama inavyotajwa katika Waroma 12:1, 2, kutafuta kanuni za Biblia kunaweza kutuzoeza kufanya nini?
8 Hata hivyo, kuna faida nyingi muhimu zinazotokana na kutafuta kanuni za Biblia na kuishi kulingana nazo. Kwa mfano, tunazoezwa kuelewa njia ya Yehova ya kufikiri kuhusu mambo mbalimbali. Tunaposoma masimulizi katika Maandiko, tunajitahidi kutafuta masomo tunayoweza kujifunza. Tunajiuliza kwa nini Yehova ameweka masomo hayo katika Neno lake na jinsi yanavyoweza kutunufaisha. Kwa njia hiyo, tunajifunza jinsi ya kutumia ‘nguvu zetu za kufikiri’ tunapomtumikia Yehova. Tunajihakikishia wenyewe “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Soma Waroma 12:1, 2.a
9. Tunapata faida gani nyingine tunapoishi kulingana na kanuni za Biblia? (Waebrania 5:13, 14)
9 Kujifunza kuishi kulingana na kanuni za Biblia kunatusaidia kuwa Wakristo wakomavu. Tunapoishi kulingana na kanuni za Biblia, uhusiano wetu na Yehova unaimarika. (Soma Waebrania 5:13, 14.) Huenda watoto wadogo wakahitaji orodha ndefu ya sheria, au amri, ili waweze kujua jinsi ya kutenda katika hali mbalimbali. Huenda wakatii sheria hizo kwa sababu tu wanaogopa kupewa adhabu. Lakini Yehova anatutendea kama watu wazima waliokomaa, na si kama watoto wadogo. Anatumaini kwamba tutafanya maamuzi yanayopatana na mapenzi yake, na tunapofanya hivyo, tunaufanya moyo wake ushangilie sana.—Zab. 147:11; Met. 23:15, 26; 27:11.
TUNAWEZAJE KUTAMBUA KANUNI ZA BIBLIA?
10. Tunawezaje kutambua kanuni za Biblia?
10 Tunapotafuta mambo tunayoweza kujifunza katika Biblia, tunapata kanuni zinazotusaidia kuelewa njia ya Yehova ya kufikiri na jinsi anavyohisi kuelekea mambo. Tunaweza pia kutambua kanuni tunapochunguza kwa nini sheria fulani zilitungwa na Yehova. Kadiri tunavyoelewa zaidi sababu hizo, ndivyo tutakavyoelewa vizuri zaidi njia ya Yehova ya kufikiri. Lakini ili tuelewe njia ya Mungu ya kufikiri, ni lazima tusali kwake ili atusaidie na ni lazima tusitawishe uwezo wetu wenyewe wa kufikiri. (Met. 2:10-12) Tunaweza kujiuliza maswali yafuatayo: ‘Kwa nini Mungu alitupatia sheria hii? Ikiwa Yehova hapendezwi na mwenendo huu, atahisije kuhusu mwenendo unaofanana na huo? Ninajifunza masomo gani kutokana na simulizi hili la Biblia, na ninawezaje kuyatumia katika maisha yangu?’ Tunapotambua sababu za kutungwa kwa sheria na masomo tunayojifunza kutokana na sheria hizo na masimulizi katika Biblia, tutaweza kufanya maamuzi mazuri maishani—maamuzi ambayo yanapatana na mapenzi ya Yehova.
11. Ni kwa njia gani Yesu alituonyesha jinsi ya kutambua kanuni za Biblia katika Mahubiri yake ya Mlimani? (Tazama pia picha.)
11 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alituonyesha jinsi tunavyoweza kutambua kanuni za Biblia. Acheni tuchunguze mifano mitatu. Katika kila kisa, kwanza Yesu alitaja sheria. Kisha alifunua wazo au kanuni inayotegemeza sheria hiyo. Tunapotafakari kuhusu mambo ambayo Yesu alifunua, tutaona jinsi kanuni hizo zinavyoweza kutumiwa katika ulimwengu wetu wa leo. Wakati huohuo, tutatambua jinsi masomo hayo yanavyoweza kutunufaisha kihususa maishani.
Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alituonyesha jinsi ya kutambua kanuni za Biblia zinazotegemeza sheria za Mungu (Tazama fungu la 11)
12. Ni kanuni gani moja inayotegemeza sheria inayotajwa kwenye Mathayo 5:21, 22? (Tazama pia picha.)
12 Soma Mathayo 5:21, 22. “Usiue.” Ni kanuni gani moja inayotegemeza sheria hiyo? Yehova hataki tuwachukie wengine—kupitia matendo, maneno, au hata katika mawazo yetu. Yesu alionyesha kwamba ingawa huenda mtu asiue, bado anaweza kutenda kinyume na sababu au msingi wa sheria hiyo ikiwa atamchukia ndugu yake. Ikiwa mtu ‘ataendelea kumkasirikia ndugu yake’ au kumtukana, bado mtu huyo aliyekasirika “atawajibika.” Isitoshe mitazamo na matendo hayo ndiyo hasa yanayoongoza kwenye kuua.—1 Yoh. 3:15.
13. Tunawezaje kutumia maishani kanuni inayopatikana kwenye Mathayo 5:21, 22? (Tazama pia picha.)
13 Kanuni inayopatikana kwenye Mathayo 5:21, 22 inawezaje kutumiwa leo? Tunapaswa kuepuka kuweka kinyongo. (Law. 19:18; Ayu. 36:13) Kwa nini? Kwa sababu hisia hizo zinaweza kuchochea chuki moyoni mwetu, ambayo huenda ikaongoza kwenye maneno au matendo yanayoumiza. (Met. 10:12) Mambo hayo yanatia ndani porojo na uchongezi ambao unaweza kudhuru au kuharibu sifa ya wengine. (Met. 20:19; 25:23) Hivyo, hata kabla ya kuwepo kwa mambo kama vile mitandao ya kijamii, blogu, intaneti, au programu za kutuma jumbe, Yesu alitoa kanuni ambayo ingewaonya Wakristo wakomavu kuhusu hatari zinazoweza kutokana na kutumia vifaa hivyo katika siku zetu. Hivyo, katika hali zozote, tunapaswa kuepuka kutumia maneno yenye chuki ambayo mara nyingi yanaharibu sifa ya mtu.
(Tazama fungu la 12-13)
14. Ni kanuni gani inayotegemeza sheria inayopatikana kwenye Mathayo 5:27, 28? (Tazama pia picha.)
14 Soma Mathayo 5:27, 28. “Usifanye uzinzi.” Ni kanuni gani inayotegemeza sheria hiyo? Yehova hachukii tu uasherati, bali pia mawazo yanayoongoza kwenye matendo ya uasherati. Yesu alieleza kwamba ikiwa mwanamume aliyefunga ndoa ataendelea kumtazama mwanamke (ambaye si mke wake) na kumtamani, ametenda dhambi. Hivyo, tunapaswa kuepuka kabisa mawazo yaliyopotoka kimaadili, hata ikiwa hilo litahusisha jitihada nyingi sana. (Mt. 5:29, 30) Kanuni hiyo inawahusu pia Wakristo waseja.
15. Kanuni inayopatikana kwenye Mathayo 5:27, 28 inawezaje kutumiwa leo? (Tazama pia picha.)
15 Kanuni inayopatikana kwenye Mathayo 5:27, 28 inawezaje kutumiwa leo? Tunapaswa kuepuka kukazia fikira tamaa zilizopotoka kimaadili. (2 Sam. 11:2-4; Ayu. 31:1-3) Hivyo, ni wazi kwamba Mkristo mkomavu ataepuka aina zote za ponografia. Hatajitetea kwamba anatazama tu uasherati, hivyo hafanyi jambo lolote baya. Hatajaribu kutetea vitendo hivyo kuwa ni kutazama tu “picha za ngono zisizo wazi,” ambazo watu wengine huona si zenye kuchukiza sana ikilinganishwa na aina nyingine za ponografia zinazoonyesha mambo waziwazi zaidi. Katika siku za Yesu, hakukuwa na vifaa vya kielektroni, sinema, au picha. Hata hivyo, Yesu alitupatia kanuni inayotufundisha jinsi Yehova anavyohisi kuhusu mambo ambayo huenda yakapatikana kwenye vifaa hivyo vya kisasa. Hilo linatusaidia kuelewa kwamba Yehova anachukizwa sana na mazoea ya siku hizi ya kutumiana jumbe, picha, au video za ngono kwa simu au kujihusisha katika matendo yanayoigiza uasherati kupitia intaneti. Kutii kanuni hiyo kunamsaidia mtu aliyefunga ndoa aepuke kumtendea kwa hila mwenzi wake. (Mal. 2:15) Kunawasaidia pia Wakristo wote—wenzi wa ndoa au waseja—waepuke jambo lolote linaloweza kuwaongoza kwenye uasherati.—Met. 5:3-14.
(Tazama fungu la 14-15)
16. Ni kanuni gani inayotegemeza sheria inayopatikana kwenye Mathayo 5:43, 44? (Tazama pia picha.)
16 Soma Mathayo 5:43, 44. “Lazima umpende jirani yako.” Ni kanuni gani inayotegemeza sheria hiyo? Yehova anataka tuwaone watu wote kuwa majirani wetu na tuwaonyeshe upendo. Kwa kusikitisha, Wayahudi katika siku za Yesu walitumia vibaya mwongozo huo na walifikiri kwamba sheria hiyo ilimaanisha wangeweza kuwachukia adui zao. Lakini Yesu alijua kwamba hilo halikuwa kusudi la sheria hiyo. Alijua kwamba Baba yake wa mbinguni mwenye upendo anatarajia tumwone kila mtu kuwa jirani yetu, haidhuru jamii au taifa lake.—Mt. 5:45-48.
17. Tunanufaikaje tunapotumia maishani kanuni inayopatikana kwenye Mathayo 5:43, 44? (Tazama pia picha.)
17 Tunawezaje kutumia kanuni inayopatikana kwenye Mathayo 5:43, 44 leo? Upendo wetu kwa jirani utatuchochea kukataa kujihusisha katika vita na migogoro ya ulimwengu huu. (Isa. 2:4; Mika 4:3) Utatusaidia kushughulika kwa fadhili na watu kutoka katika jamii, taifa, na dini tofauti. (Mdo. 10:34, 35) Pia, utatusaidia kuwasamehe wale waliotuumiza sisi au watu tunaowapenda.—Mt. 18:21, 22; Marko 11:25; Luka 17:3, 4.
(Tazama fungu la 16-17)
AZIMIA KUISHI KULINGANA NA KANUNI ZA BIBLIA
18. (a) Tunapaswa kuazimia kufanya nini? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?
18 Tunathamini sana kwamba Yehova yuko tayari kututendea kama watu wazima na si kama watoto! Anataka tutumie kanuni za Biblia ambazo zitatusaidia kufanya maamuzi ya hekima. (1 Kor. 14:20) Tunapofanya maamuzi hayo, acheni tuazimie “[kuendelea] kuyafahamu mapenzi ya Yehova.” (Efe. 5:17) Upendo wetu kwa Yehova, na si woga wa kuadhibiwa, utatusaidia kufanya maamuzi yanayopatana na mapenzi yake. Lakini kuna zawadi nyingine itakayotusaidia katika jambo hilo. Zawadi hiyo ni dhamiri yetu. Tutazungumzia jambo hilo katika makala inayofuata.
WIMBO 95 Nuru Inazidi Kuongezeka
a Mara nyingi Wakristo wanahitaji kuchunguza kanuni za Biblia kwa makini. Tunahitaji kuelewa jinsi kanuni za Biblia zinavyohusiana, na jinsi zinavyohusiana na maamuzi ambayo huenda tunahitaji kufanya. Tunaweza kutumia uwezo wetu wa kufikiri tuliopewa na Mungu ili kufanya maamuzi yenye usawaziko yatakayopata kibali na baraka za Yehova. Katika karne ya kwanza, njia hii ya ibada ilikuwa badiliko ambalo Wayahudi wengi waliokuwa Wakristo walihitaji kufanya. Awali waliishi kulingana na sheria nyingi zilizotokana na desturi.