MEI 18-24, 2026
WIMBO 35 “Mhakikishe Mambo Muhimu Zaidi”
Unawezaje Kushinda Mambo Yanayokukengeusha?
“Endeleeni kuyafahamu mapenzi ya Yehova.”—EFE. 5:17.
JAMBO KUU
Jinsi ya kukazia fikira utendaji wa kiroho licha ya hali ambazo zinaweza kutukengeusha fikira.
1-2. Jambo muhimu linawezaje kuwa kikengeusha fikira?
NI LINI mara ya mwisho ulipokabiliana na kikengeusha fikira? Huenda jambo fulani lilikukengeusha kutoka kwenye kitu ulichokuwa ukifanya na ulihitaji kuamua ni jambo gani lilikuwa muhimu zaidi. Kwa mfano, wazia kwamba simu yako ya mkononi inaita unapoendesha gari. Huenda simu hiyo ikawa ya muhimu, lakini unatambua kwamba kwa wakati huo itakukengeusha. Pindi hiyo, jambo la muhimu zaidi ni kukazia fikira kuendesha gari.
2 Maisha yetu yamejaa mambo muhimu tunayohitaji kufanya. Tunajua kwamba ni muhimu zaidi kukazia fikira utendaji wetu wa kirohoa na kuwa na ratiba nzuri ya kiroho. (Mt. 6:33) Kama madereva walio makini, watu wa Yehova wanajitahidi kutambua mambo yanayoweza kuwakengeusha wasikazie fikira barabara iliyo mbele yao.—Met. 4:25; Mt. 6:22.
3. Makala hii itatusaidiaje?
3 Hakuna yeyote kati yetu anayetaka kukengeushwa kutoka kwenye utendaji wa kiroho. Hata hivyo, sisi sote tunakabili hali zinazoweza kutukengeusha kwa urahisi. (Luka 21:34-36) Hivyo, ili kutusaidia kukazia fikira utumishi wetu kwa Yehova, acheni tuzungumzie (1) vikengeusha fikira tunavyokabili, (2) jinsi Yesu alivyoshinda mambo ambayo yangeweza kumkengeusha fikira, na (3) jinsi tunavyoweza kushinda vikengeusha fikira leo.
TUNAKABILI VIKENGEUSHA FIKIRA GANI?
4-6. Ni mambo gani yanayoweza kutukengeusha kwa urahisi?
4 Huenda sisi sote tuna mambo mengi maishani yanayohitaji kukaziwa fikira. Kwa mfano, huenda tuna matatizo ya afya au tuna mambo muhimu ya kushughulikia kwa ajili ya familia yetu au kibinafsi. Bila shaka, mambo hayo ni muhimu, na yanahitaji kukaziwa uangalifu. Lakini je, yanaweza kutukengeusha? Yanaweza, ikiwa tutayafikiria kupita kiasi na kutumia wakati na nguvu zetu nyingi kuyashughulikia.
5 Kwa kuongezea, wengi wetu tunaathiriwa kibinafsi na misukosuko ya kisiasa, hali mbaya za kiuchumi, milipuko ya magonjwa, na migogoro isiyoisha ya mfumo huu. (2 Tim. 3:1) Tunapokabili mambo hayo, huenda yakatuhangaisha sana hivi kwamba tukaanza kuyafikiria mambo hayo kila wakati.
6 Huenda tunawafahamu watu ambao maisha yao yameathiriwa sana na mambo kama hayo. Inaeleweka kwamba wanahangaishwa kihisia na yale waliyokabili. Wanadamu hawakuumbwa waishi chini ya mkazo kwa muda mrefu. Haishangazi kwamba baadhi yao wanahisi wamenyimwa fursa ya kuishi maisha ya kawaida kwa sababu ya kuvumilia changamoto hizo ngumu! Matokeo ni kwamba baadhi yao wanajaribu kupunguza mkazo walio nao kwa kutumia muda mwingi katika burudani au tafrija. Tunaweza kufanya nini tukijikuta katika hali kama hizo? Acheni tuchunguze mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwa Yesu ambayo yatatusaidia tusikengeuke kutoka katika ibada yetu.
YESU ALISHINDAJE MAMBO AMBAYO YANGEWEZA KUMKENGEUSHA?
7. Ni mambo gani ambayo yangeweza kumkengeusha Yesu?
7 Yesu angeweza kukengeushwa na mambo mengi, kama vile masuala ya kijamii na kisiasa. Katika siku zake, watu wengi walikuwa maskini na wagonjwa. (Mt. 14:14; Marko 14:7) Walitendewa isivyo haki na Waroma na Wayahudi wenzao. Watu walipoona kwamba Yesu alikuwa na nguvu na uwezo wa kufanya miujiza, walitaka kumfanya awe mfalme wao. (Yoh. 6:14, 15) Kwa kuongezea, Shetani alijaribu kumshawishi Yesu kwa kumwonyesha njia rahisi ya kuwa mtawala wa ulimwengu. (Mt. 4:8, 9) Na mtume Petro, mmoja wa marafiki wa karibu zaidi wa Yesu, pindi moja alimtia moyo afanye maisha yake yawe rahisi zaidi, kwa kusema: “Bwana jihurumie.”—Mt. 16:21, 22.
8. Yesu alishindaje mambo ambayo yangeweza kumkengeusha?
8 Yesu alishindaje mambo ambayo yangeweza kumkengeusha? Kwa njia tatu. Kwanza, aliiga njia ya Yehova ya kufikiri. (Yoh. 8:28; 14:9) Pili, aliendelea kuwa na mengi ya kufanya katika utendaji wa kiroho. (Mt. 9:35) Na tatu, aliendelea kukumbuka jambo lililokuwa muhimu zaidi. (Yoh. 4:34) Kwa uthabiti, alipinga majaribu ya Shetani na hakuyumbishwa na maneno ya Petro yaliyotolewa kwa nia nzuri, lakini hayakupatana na mapenzi ya Yehova. (Mt. 4:10; 16:23) Yesu alikataa kuruhusu mawazo, maneno, au matendo ya watu yamkengeushe ashindwe kutimiza kusudi la Mungu. Ni kweli kwamba huenda tukakabili vikengeusha fikira tofauti na alivyokabili Yesu, lakini kwa kujifunza zaidi, tunaweza kushinda vikengeusha fikira vyetu kama Yesu alivyofanya.
TUNAWEZAJE KUSHINDA MAMBO YANAYOTUKENGEUSHA FIKIRA?
9. ‘Kuendelea kuyafahamu mapenzi ya Yehova’ kunamaanisha nini? (Waefeso 5:17)
9 Jifunze njia ya Yehova ya kufikiri. Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia “[kuendelea] kuyafahamu mapenzi ya Yehova.” (Soma Waefeso 5:17.) Tunaweza kujifunza mambo yanayomfurahisha Yehova kwa kusoma na kutafakari Neno lake. Tunaweza kufanya hivyo hata wakati ambapo Biblia haizungumzii hali zetu kihususa. Jinsi gani? Kwa kufahamu vizuri njia ya Yehova ya kufikiri na kuwa tayari kuongozwa nayo.
10. Tunawezaje kujifunza njia ya Yehova ya kufikiri?
10 Tunaweza kujifunza kuhusu njia ya Yehova ya kufikiri kwa kujifunza Biblia na kuchunguza jinsi alivyoshughulika na wanadamu. (Yer. 45:5) Tunaposoma masimulizi hayo, tunaweza kujiuliza maswali yafuatayo: ‘Jambo hili linanifundisha nini kumhusu Yehova? Ninawezaje kulitumia ili kubadili njia yangu ya kufikiri?’ Bila shaka, njia yake ya kufikiri iko juu kuliko yetu. (Isa. 55:9) Hivyo, kwa kufaa tunamwomba yeye atufundishe jinsi ya kufanya mapenzi yake. (Zab. 143:10) Na tunasali tukiwa na uhakika kwamba atatusaidia kuelewa njia yake ya kufikiri na kuitumia maishani.—1 Yoh. 5:14.
11. Yehova anataka nini kutoka kwetu?
11 Tunapojifunza njia ya Yehova ya kufikiri, tunaelewa kwamba anataka tuepuke kukengeushwa ili tujithibitishe kuwa tayari kwa ajili ya mwisho wa mfumo huu. (Mt. 24:44) Hataki tulemewe na mahangaiko. (Mt. 6:31, 32) Hivyo, tunapolemewa na mahangaiko kuhusu hali yetu ya afya, kazi, nyumba, au mambo mengine ya kibinafsi na ya kifamilia, Yehova anatupatia msaada hususa. Anatualika tumtegemee yeye ili kupata hekima na nguvu za kukabiliana na matatizo yetu.—Zab. 55:22; Met. 3:5-7.
12. Taja njia moja tunayoweza kutumia ili kukabiliana na mahangaiko yanayosababishwa na matukio ya ulimwengu. (Mathayo 5:3)
12 Endelea kuwa na mengi ya kufanya katika utendaji wa kiroho. Sisi sote tunahangaishwa kwa kiwango fulani na matukio ya ulimwengu ambayo hatuwezi kudhibiti. Hivyo, ili kuepuka kukengeushwa na mambo ambayo hatuwezi kudhibiti, tunakazia fikira utendaji wetu wa kiroho. Tunaweza kuwa na furaha tunapojitahidi kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho—uhitaji ambao tumeumbwa nao. (Soma Mathayo 5:3.) Tunaweza kutosheleza uhitaji huo kwa kuendelea kumjua Yehova kupitia kujifunza Neno lake, Biblia, na kwa kufanya yote tuwezayo katika utumishi wake mtakatifu. Kwa kufanya hivyo, tutamfurahisha Yehova kwa sababu tunatumia wakati wetu kwa hekima.—Met. 23:15.
13. Tunawezaje ‘kutumia vizuri kabisa wakati wetu’?
13 Tukiwa Wakristo, tumeazimia ‘kutumia vizuri kabisa wakati wetu.’ (Efe. 5:15, 16; tazama habari za utafiti, “making the best use of your time,” nwtsty.) Tunatambua kwamba Biblia haipendekezi tutumie tu wakati wetu vizuri zaidi inapohusu shughuli za kila siku. Badala yake, inatuhimiza kufikiria kwa makini jinsi tunavyotumia wakati wetu kabla ya Yehova kuleta mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo. Tunawezaje kutumia vizuri kabisa wakati wetu? Ikiwa tutatumia wakati wetu mwingi kufuatilia taarifa za habari za karibuni kuhusu mambo mabaya yanayotokea, tunaweza kukengeuka, kuvunjika moyo, na kupunguza bidii katika ibada yetu kwa Mungu. Ni bora zaidi tujiwekee mipaka ya kiasi cha habari tutakazotazama au kusoma! Hivyo, tutaepuka kulemewa na tutaweza kuendelea kuwa na mengi ya kufanya katika utendaji wetu wa kiroho wenye kujenga. Itafaa pia ikiwa tutafikiria kupanua zaidi huduma yetu ikiwezekana, kwa mfano, kwa kufanya ziara nyingi zaidi za kurudia. Tunaelewa umuhimu wa kutumia vizuri kila fursa kuwasaidia watu “waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Tim. 2:4.
14. Kuendelea kuwa na mengi ya kufanya katika utendaji wa kiroho kunatusaidiaje? (Tazama pia picha.)
14 Tunapoendelea kuwa na mengi ya kufanya katika utendaji wa kiroho, tunadumisha mtazamo unaofaa kuhusu siku zetu. Tunapojionea misukosuko ya kisiasa, hali mbaya za kiuchumi, na milipuko ya magonjwa, hatutikiswi. Tunaona mambo hayo kuwa uthibitisho wa kwamba unabii wa Biblia unatimia. Badala ya kukengeushwa fikira isivyo lazima kwa sababu ya hofu, tuna uhakika katika kusudi la Yehova kuhusu wakati wetu ujao. Tunaweza kudumisha utulivu tunapoendelea kumtumaini Yehova atusaidie kukabiliana na hali hizo.—Zab. 16:8; 112:1, 6-8.
Licha ya matukio mabaya ya ulimwengu huu, endelea kuwa na mengi ya kufanya katika utendaji wa kiroho (Tazama fungu la 14)b
15. Kuwa “na utimamu wa akili” kunatuwezesha kufanya nini? (1 Petro 4:7)
15 Endelea kukumbuka jambo lililo muhimu zaidi. Watu wengi leo ulimwenguni wanakazia fikira kufurahia pindi za tafrija, badala ya kukazia fikira mwisho wa mfumo huu ulio karibu. Ingawa si vibaya kufurahia pindi za tafrija, tunahitaji kuwa “na utimamu wa akili” ili kuepuka kuathiriwa na maoni ya ulimwengu. (Soma 1 Petro 4:7.) Hilo linamaanisha nini kwetu? Linamaanisha kwamba tusitawishe uwezo mzuri wa kufanya maamuzi ili tuendelee kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu tafrija na tufanye maamuzi yenye hekima. Maamuzi hayo yataonyesha kwamba tunaiga njia ya Yehova ya kufikiri na yataonyesha kwamba tumeelewa vizuri jambo lililo muhimu zaidi.—2 Tim. 1:7.
16. Yesu alikazia fikira nini kifo chake kilipokaribia?
16 Yesu aliendelea kukumbuka jambo lililo muhimu zaidi. Katika saa za mwisho za maisha yake duniani kabla ya kifo chake, alikazia fikira kabisa kuendelea kuwa mshikamanifu na kutimiza mapenzi ya Mungu. Kwa sababu hiyo, alisali kwa bidii. Tofauti na Yesu ambaye aliendelea kuwa macho, wanafunzi wake walilala usingizi. Walikuwa “wamechoka kwa sababu ya huzuni.”—Luka 22:39-46; Yoh. 19:30.
17. Kwa nini watu wengi wanatumia mitandao ya kijamii, lakini inawezaje kuwa kikengeusha fikira? (Tazama pia picha.)
17 Kama wanafunzi wa Yesu, pindi fulani sisi pia tunaweza kuwa na mkazo wa kihisia. Matukio ambayo ni ishara za siku hizi za mwisho yanaweza kutusababishia mahangaiko. Watu wengi hutafuta faraja kwa kutumia mitandao ya kijamii. Wanaitumia kuwasiliana na marafiki na familia duniani kote na kushiriki habari, picha, na mambo mengine. Na wanaitumia kufurahia burudani zisizoisha. Hata hivyo, watu hao wanaweza kuzama kabisa katika burudani hizo, wakitumia wakati na nguvu zao nyingi kuzifuatilia. Ili kutusaidia tuwe na mtazamo uliosawazika kuhusu mitandao ya kijamii, tunaweza kujiuliza hivi, ‘Je, mimi huburudishwa ninapotumia mitandao ya kijamii, au inanikengeusha nisitambue jambo lililo muhimu zaidi?’
Uwezo mzuri wa kufanya maamuzi unatusaidia kuepuka kukengeushwa na mitandao ya kijamii, burudani, na tafrija (Tazama fungu la 17)
18. Kwa nini tunahitaji kuwa na uwezo mzuri wa kufanya maamuzi tunapochagua burudani?
18 Uwezo mzuri wa kufanya maamuzi unahitajika pia ikiwa tutatazama sinema au vipindi vya televisheni kwenye tovuti za sinema, tutatazama video fupi kwenye vituo vya intaneti, au tutacheza michezo ya video. Mambo hayo yanaweza kutufurahisha na kutuburudisha. Lakini tunahitaji uwezo mzuri wa kufanya maamuzi inapohusu aina na kiasi cha burudani tunayochagua. Mara nyingi tovuti za sinema huendelea kuwapendekezea watumiaji wake video mpya za kutazama ambazo huenda ni zenye ukatili au ukosefu wa maadili. Jambo hilo lilimpata ndugu yetu mmoja barani Asia. Alianza kutazama vionjo vya sinema kwenye tovuti fulani. Alipoendelea kutazama video hizo fupi zilizopendekezwa, alijipata akitazama video zilizo na ukosefu wa maadili. Hatimaye, alianza kutazama ponografia. Kwa kufaa, kupitia msaada wa wazee na utegemezo wa marafiki wa karibu, alichukua hatua thabiti—alifuta programu za tovuti za sinema na akajiwekea mipaka ya muda wa kutumia simu yake. Kisa hicho kinaonyesha kwa nini tunahitaji kuwa na uwezo mzuri wa kufanya maamuzi tunapochagua burudani.
19. Ni nini kinachoweza kutupata ikiwa tutatanguliza tafrija maishani?
19 Huenda tukahitaji pia kutumia uwezo mzuri wa kufanya maamuzi inapohusu tafrija na likizo. Sisi sote tunahitaji kupumzika pindi fulani—hilo linafaa na linatusaidia kuendelea kuwa na afya nzuri. Lakini tukikazia fikira sana mambo hayo tunaweza kukosa usawaziko, na wakati wa kutimiza mambo muhimu zaidi. (Flp. 1:10) Ni lazima sisi sote tuamue wenyewe tutafanya nini na tutatumia kiasi gani cha wakati kufanya jambo hilo. Unapofanya maamuzi hayo, jiulize hivi: ‘Je, wakati ninaotumia katika tafrija na likizo unaonyesha kwamba nina uwezo mzuri wa kufanya maamuzi? Je, nitakuwa nikihakikisha mambo yaliyo muhimu zaidi na kujitayarisha kwa ajili ya “mwisho wa mambo yote”?’
20. Tunanufaikaje tunaposhinda mambo yanayotukengeusha?
20 Tunanufaika tunaposhinda mambo yanayotukengeusha kutoka katika ratiba na utendaji wetu wa kiroho. (Isa. 48:17) Kwa msaada wa Yehova, tutakuwa na uwezo mzuri zaidi wa kupambana na changamoto maishani. Hatutatikiswa na matukio ya ulimwengu huu. Na tutaepuka kutumia wakati mwingi kupita kiasi kufurahia pindi za tafrija. Basi, acheni tuendelee kuazimia kusitawisha njia ya Yehova ya kufikiri, kuwa na mengi ya kufanya katika utendaji wa kiroho, na kuendelea kukumbuka jambo lililo muhimu zaidi. Kwa kufanya hivyo, hatutakuwa tukishinda tu vikengeusha fikira, bali pia tutaushika “imara uzima ulio wa kweli.”—1 Tim. 6:19.
WIMBO 129 Tutaendelea Kuvumilia
a UFAFANUZI WA MANENO: Utendaji wa kiroho unarejelea jambo lolote linalohusiana moja kwa moja na ibada yetu kwa Yehova—kama vile kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano, kushiriki katika ibada ya familia, na kushiriki katika huduma. Tunamwabudu pia Yehova tunapodumisha na kujenga sehemu za mikutano, tunapounga mkono kazi ya kutoa misaada, tunapojitolea katika makusanyiko, au tunapotumikia Betheli.
b MAELEZO YA PICHA: Wenzi wa ndoa wanaendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya kuhubiri badala ya kukengeushwa na matukio mabaya ya ulimwengu huu.