MHUSIKA KATIKA BIBLIA
Obadia—Sitawisha Sifa ya Kumwogopa Mungu
Obadia alikuwa msimamizi wa nyumba ya Mfalme Ahabu aliyekuwa mwovu, mtawala aliyeruhusu uovu wa ibada ya Baali ujae nchini. Hata hivyo, ‘tangu alipokuwa kijana,’ Obadia alimwogopa sana Yehova. (1 Fal. 18:1-13) Hivyo, Malkia Yezebeli alipoamuru kwamba manabii wote wa Yehova wauawe, Obadia alijua kwamba alihitaji kutenda kwa ujasiri ili kuzuia uovu huo. Kumficha nabii mmoja tu kulikuwa jambo la hatari sana; hata hivyo, Obadia aliwaficha manabii 100 na aliwapatia chakula wakati wa njaa kali! Wazia jinsi ilivyokuwa vigumu sana kuepuka kugunduliwa na mamia ya manabii wa uwongo waliomtumikia mfalme na malkia.—1 Fal. 18:19.
Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa mwanamume huyo aliyemwogopa Mungu? Ingawa Obadia alimwogopa Ahabu, alimwogopa Mungu zaidi. Hilo lilimpa ujasiri wa kuhatarisha uhai wake ili kuwalinda ndugu zake. Ikiwa ibada ya kweli imepigwa marufuku katika eneo unaloishi, wewe pia unaweza kusitawisha sifa ya kumwogopa Mungu. Woga wa aina hiyo utatuimarisha ili tuwategemeze ndugu na dada zetu wanaokabili majaribu.