Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w26 Februari kur. 2-7
  • Jinsi ya Kuwasaidia Watu Wetu wa Ukoo Wasioamini

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kuwasaidia Watu Wetu wa Ukoo Wasioamini
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2026
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINSI SIFA YA HURUMA INAVYOWEZA KUKUCHOCHEA KUWASAIDIA
  • JINSI YA KUTENDA WATU WETU WA UKOO WANAPOZUNGUMZA AU KUTENDA KWA NJIA ISIYO YA FADHILI
  • ENDELEA KUWA NA SUBIRA NA TUMAINI
  • WAONYESHE KWAMBA UNAWAPENDA
  • USIKATE TAMAA KUELEKEA WATU WAKO WA UKOO
  • Kweli Huleta, “Si Amani, Bali Upanga”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • Tafuta Majibu ya Maswali Haya
    Programu ya Kusanyiko la Mzunguko la 2025-2026 Lililo na Mwangalizi wa Mzunguko
  • Maamuzi Yanayoonyesha Unamtegemea Yehova
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
  • Je, Bado Unaweza Kujifunza Kutokana na Mafundisho ya Msingi ya Biblia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2026
w26 Februari kur. 2-7

APRILI 6-12, 2026

WIMBO 82 “Acheni Nuru Yenu Iangaze”

Jinsi ya Kuwasaidia Watu Wetu wa Ukoo Wasioamini

“Tusife moyo katika kufanya mema.”—GAL. 6:9.

JAMBO KUU

Jinsi ya kudumisha uhusiano mzuri na watu wa ukoo wasioamini na jinsi ya kuwasaidia kiroho, ikiwa inawezekana.

1-2. Ni mambo gani ambayo huenda yaliathiri uhusiano wetu pamoja na watu wetu wa ukoo tulipoanza kujifunza kweli?

YESU alimwambia hivi mwanamume aliyetaka kuwa mfuasi wake: “Nenda nyumbani kwa watu wako wa ukoo, ukawaambie mambo yote ambayo Yehova amekufanyia.” (Marko 5:19) Kwa kusema hivyo, Yesu alionyesha alitambua kwamba kiasili wanadamu wanatamani kuwaeleza habari njema wapendwa wao.

2 Je, unakumbuka jinsi ulivyohisi ulipojifunza Biblia kwa mara ya kwanza? Huenda ulitamani sana kuwaeleza wapendwa wako! Hata hivyo, huenda hawakupendezwa na mambo uliyowaeleza. Au huenda njia uliyotumia kuwaeleza kweli ilisababisha hali ya kutoelewana kati yenu. Ikiwa ndivyo, unawezaje kudumisha au kurudisha uhusiano mzuri na watu wako wa ukoo bila kulegeza msimamo wako inapohusu viwango vya Kikristo?

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Katika makala hii, tutazungumzia: (1) Jinsi sifa ya huruma inavyoweza kutuchochea kuwaonyesha upendezi wa kibinafsi watu wetu wa ukoo wasioamini,a hata ikiwa hawakubali kweli; (2) jinsi ya kutenda watu wetu wa ukoo wanapozungumza au kutenda kwa njia isiyo ya fadhili; (3) jinsi ambavyo kuwa na mtazamo wa subira na tumaini kunavyoweza kuwasaidia watu wetu wa ukoo waitambue kweli; na (4) jinsi tunavyoweza kuwaonyesha kwamba tunawapenda.

JINSI SIFA YA HURUMA INAVYOWEZA KUKUCHOCHEA KUWASAIDIA

4. Yesu aliwatendeaje watu ambao hawakupendezwa na ujumbe wake?

4 Yesu hakuacha mara moja kuwasaidia watu ambao hawakupendezwa na ujumbe wake. Alijilinganisha na mfanyakazi wa shamba la mizabibu aliyejitahidi sana ili kuuwezesha mtini usiozaa matunda uweze kuzaa tena. (Luka 13:​6-9) Yesu alipotoa mfano huo, tayari alikuwa amejaribu kwa zaidi ya miaka mitatu kuwasaidia Wayahudi wawe na imani kumwelekea. Kwa nini aliendelea kuwasaidia? Yesu aliwahurumia watu na hilo lilimsaidia kuwaonyesha subira.

5. Ni nini kilichomchochea Yesu kuwahurumia Wayahudi wenzake?

5 Yesu aliwahurumia Wayahudi wenzake kwa sababu viongozi wa kidini walishindwa kuwasaidia kusitawisha imani ya kweli katika Mungu. Yesu aliona kwamba watu hao walikuwa kama “kondoo wasio na mchungaji.” (Marko 6:34) Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alilililia jiji la Yerusalemu kwa sababu alijua kwamba wakaaji wake wengi wangeuawa kwa sababu ya kukosa imani. (Luka 19:​41-44) Tunapokuwa na upendo wa namna hiyo kuelekea watu wetu wa ukoo, tutachochewa kuwasaidia.

6. Kwa nini tunapaswa kuwaonyesha subira watu wetu wa ukoo wasioamini? (Wagalatia 6:9)

6 Soma Wagalatia 6:9. Hata ikiwa watu wetu wa ukoo hawapendezwi na mambo tunayoamini, tunapaswa kuwaonyesha subira na kutokufa moyo katika “kufanya mema.” Tunajua kwamba inachukua muda kwa mtu kushinda ubaguzi uliokita mizizi na kusitawisha imani katika Yehova. Je, pindi moja, wewe pia ulikuwa kama wale ambao ‘hawakuwa na tumaini na walikuwa bila Mungu katika ulimwengu’? (Efe. 2:12) Ikiwa ndivyo, bila shaka mtu fulani alikusaidia. Je, huchochewi pia kuwasaidia watu wako wa ukoo kutosheleza mahitaji yao ya kiroho ikiwa inawezekana?

JINSI YA KUTENDA WATU WETU WA UKOO WANAPOZUNGUMZA AU KUTENDA KWA NJIA ISIYO YA FADHILI

7. Ni mambo gani ambayo huenda yaliwazuia ndugu nusu wa Yesu kumwamini?

7 Huenda ndugu nusu wa Yesu walisikia kuhusu miujiza aliyofanya Yesu katika eneo la Galilaya. (Luka 4:​14, 22-24) Hata hivyo, mwanzoni hawakumwamini. (Yoh. 7:5) Kwa nini? Biblia haisemi. Lakini inataja mambo mawili yaliyowazuia baadhi ya Wayahudi kuwa wanafunzi wa Yesu. Baadhi yao waliogopa kukataliwa na majirani wao. (Yoh. 9:​18-22) Wengine walikuwa wamemjua Yesu tangu akiwa mdogo na ilikuwa vigumu kwao kuamini kwamba alikuwa mwakilishi wa Mungu. (Marko 6:​1-4) Huenda ndugu nusu wa Yesu waliathiriwa pia na mtazamo huo. Je, inawezekana kwamba wapendwa wetu wameathiriwa na maoni kama hayo?

8. Ni jambo gani linaloweza kuwafanya watu wetu wa ukoo waseme au kutenda kwa njia isiyo na fadhili?

8 Fikiria sababu inayofanya waseme na kutenda kwa njia hiyo. Huenda ndugu za Yesu walikuwa miongoni mwa watu wa ukoo ambao pindi moja walisema alikuwa “amerukwa na akili.” (Marko 3:21) Kwa nini huenda walifikia mkataa huo? Muktadha unaonyesha Yesu alikuwa na mengi ya kufanya hivi kwamba hata hakupata muda wa kula chakula. (Marko 3:20) Je, watu wake wa ukoo walifikiri kuwa alikuwa na msimamo mkali? Inawezekana. Watu wetu wa ukoo wanaweza kufikiria kuwa tuna msimamo mkali inapohusu dini yetu. Ikiwa wanahisi hivyo, tunapaswa kuonyesha kupitia matendo yetu kwamba kwa kweli sisi ni wenye usawaziko.

9. Ni nini kinachoweza kuwasaidia watu wetu wa ukoo wabadili maoni yao kutuhusu? (1 Petro 3:​1, 2) (Tazama pia picha.)

9 Endelea kuwa mwenye fadhili na usawaziko. Maneno na matendo yetu yenye fadhili yanaweza kuwachochea watu wetu wa ukoo wabadili maoni yao kutuhusu. (Soma 1 Petro 3:​1, 2.) Mume asiyeamini anaweza kujihisi amepuuzwa au akakasirika mke wake anapohudhuria mikutano ya kutaniko au anaposhiriki katika huduma. Kwa kuwa hataki mume wake ahisi hivyo, huenda dada huyo akabadili ratiba yake ya utendaji wa kiroho ili atumie muda mwingi zaidi pamoja naye. Kwa mfano, anaweza kushiriki katika huduma wakati ambapo mume wake ana shughuli nyingi au hayuko nyumbani. Kwa kuwa mwenye kunyumbulika na mwenye usawaziko, mke Mkristo anaweza kumsaidia mume wake abadili maoni yake kuelekea Mashahidi.

Mkusanyo wa picha: 1. Dada anamwandalia mume wake asiye Shahidi mlo wa mchana na kahawa kabla ya kwenda kazini. 2. Baadaye, anashiriki katika huduma pamoja na dada mwingine na anamwonyesha mwanamke aliye mlangoni kweli ya Biblia kwenye simu yake.

Maneno na matendo yetu yenye fadhili yanaweza kubadili maoni ya mwenzi asiyeamini kuelekea Mashahidi (Tazama fungu la 9)g


10. Tunawezaje kumwiga Yesu tunaposhutumiwa?

10 Usihisi kwamba ni lazima ujibu kila mara unaposhutumiwa. Yesu hakujitetea aliposhtakiwa kwa uwongo kwamba alikuwa akila na kunywa kupita kiasi. Badala yake, aliwatia moyo watu wajithibitishie wenyewe madai hayo. (Mt. 11:19) Pia, alionyesha kupitia mfano wake kwamba alikuwa na mtazamo wenye usawaziko kuhusu maisha. (Linganisha Yohana 2:​2, 6-10.) Vivyo hivyo, usihisi kwamba ni lazima ujibu kila mara unaposhutumiwa. Badala yake, kupitia matendo yako waonyeshe watu wako wa ukoo kwamba wewe ni mwenye usawaziko na furaha, na waache wao wenyewe wajithibitishie hilo. Huenda wakachochewa kukataa habari za uwongo ambazo wamesikia kutuhusu.

ENDELEA KUWA NA SUBIRA NA TUMAINI

11. Yesu aliwatendeaje ndugu zake wasioamini?

11 Masimulizi ya Injili yanaonyesha kwamba Yesu aliwaonyesha subira ndugu zake. Kwa mfano, inaelekea wao pia walikuwa katika jiji la Kana Yesu alipofanya muujiza wake wa kwanza. (Yoh. 2:​11, 12) Kama ilivyotajwa awali, ndugu za Yesu hawakumwamini. Hata hivyo, Yesu aliendelea kushirikiana nao. Biblia inafunua kwamba miaka mitatu hivi baada ya kufanya muujiza wake wa kwanza huko Kana, Yesu alikuwa akizungumza na ndugu zake kwa fadhili.—Yoh. 7:​5-8.

12. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kutumaini kwamba baadhi ya watu wetu wa ukoo watasikiliza ujumbe wetu?

12 Uelewaji wetu mzuri kuhusu rehema za Yehova unaweza kutusaidia kuendelea kuwa wenye tumaini. Dini za uwongo zitakapoharibiwa, huenda watu wetu wa ukoo wakakumbuka kwamba tuliwaambia kuhusu tukio hilo.b (Ufu. 17:16) Huenda hata wakajiunga nasi katika ibada safi baada ya dhiki kuu kuanza. Na ikiwa watu wetu wa ukoo wanakabili hali ngumu sasa, bila shaka tutajitahidi kadiri tuwezavyo kuwasaidia. Huenda ikawa rahisi zaidi kwao kukubali kweli za Biblia wanapoona kwamba tunawaonyesha fadhili na upendo wa kweli.

WAONYESHE KWAMBA UNAWAPENDA

13. Ingawa tuna mambo mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu nini?

13 Hata ingawa tuna mambo mengi ya kufanya katika utumishi wetu kwa Yehova, hatutaki watu wetu wa ukoo wahisi kwamba hatuna wakati wa kuwa pamoja nao au hatuwapendi. (Mt. 7:12) Tunawezaje kuwaonyesha kwamba tunawajali? Fikiria mambo haya machache.

14-15. Ni kwa njia gani moja tunaweza kuonyesha kwamba tunawapenda watu wetu wa ukoo wasioamini? Toa mfano.

14 Wasiliana nao kwa ukawaida na waonyeshe kwamba unawapenda. Tunaonyesha kwamba tunawapenda watu wetu wa ukoo kwa kuwasiliana nao kwa ukawaida kuhusu jinsi tunavyoendelea. Kwa mfano, tunaweza kuwatumia ujumbe mfupi pamoja na picha kadhaa tulizopiga tulipokuwa likizo, tuliposafiri, au tulipokuwa katika tafrija pamoja na marafiki wetu. Huenda zawadi ndogo au barua yenye maneno yenye fadhili ikatosha kuboresha uhusiano wetu pamoja nao. Tunapofanya mambo kama hayo, tunawaonyesha kwamba tunawapenda.

15 Fikiria mfano wa Anna, dada anayeishi Armenia. Familia yake hutumia wakati mwingi pamoja hasa katika sherehe za siku za kuzaliwa na sikukuu. Anna alipokubali kweli, watu wake wa ukoo walianza kuwa na wasiwasi kuhusu jinsi ambavyo imani yake mpya ingeathiri uhusiano wao. Walikuwa na wasiwasi pia kuhusu jinsi ambavyo uamuzi wake wa kuwa Shahidi ungeathiri wakati wake ujao. Anna anawasaidiaje kupunguza wasiwasi wao? Anasema hivi: “Ninapowatembelea watu wangu wa ukoo, mimi huwaeleza kuhusu maisha yangu na mambo ambayo ninafanya. Pia, mimi huwaalika nyumbani kwangu na kuwatambulisha kwa marafiki wangu. Matokeo ni kwamba watu wangu wengi wa ukoo wanawafahamu vizuri watu nilio karibu nao na hawana wasiwasi kuwahusu.” Anaongezea hivi: “Watu wangu wengi wa ukoo wameniambia kuhusu ambavyo nina furaha, na hawana wasiwasi tena kunihusu.”

16. Yesu alionyeshaje kwamba alipendezwa kibinafsi na Yakobo, ndugu yake nusu? (Tazama pia maelezo ya chini.)

16 Waonyeshe kwamba unawajali. Baada ya kufufuliwa, Yesu alionyesha kwamba anamjali Yakobo, ndugu yake, kwa kumtokea kibinafsi. (1 Kor. 15:7) Je, unaweza kuwazia jinsi Yakobo alivyohisi baada ya kutambua kwamba Yesu hakuwa amekata tamaa kumwelekea? Inaelekea Yakobo alisadiki kwamba Yesu ni Masihi wakati huo walipokutana. Baada ya kukutana na Yesu, huenda Yakobo aliwasaidia watu wengine katika familia yao wafikie mkataa sahihi kuhusu utambulisho wa Yesu.c—Mdo. 1:14.

17. Tunawezaje kutumia kanuni inayopatikana katika Waroma 12:15? (Tazama pia picha.)

17 Soma Waroma 12:15. Tukionyesha kwamba tunawajali wapendwa wetu pindi wanapohitaji zaidi msaada wetu—iwe ni nyakati nzuri au nyakati mbaya—huenda tukawasaidia wabadili mtazamo wao kutuelekea.d Kwa mfano, tunaweza kuwapongeza wanapopata mtoto na kuwapa zawadi ili kuwaonyesha kwamba tunafurahi pamoja nao. Watu wa familia wanapopoteza mpendwa wao katika kifo, tunaweza kuwafariji tunapozungumza nao, kuwasaidia kwa njia hususa, au kuwaandikia kadi yenye maneno yanayofariji. Na bila shaka, tunaweza kuwatembelea kwa ukawaida, hasa wanapokabili hali ngumu.

Dada katika picha zilizotangulia, akipiga picha pamoja na mume wake asiyeamini na mama mkwe wake aliye kwenye kiti cha magurudumu.

Ukionyesha kwamba unawajali wapendwa wako pindi wanapohitaji zaidi msaada wako, huenda wakabadili mtazamo wao kukuelekea na kuelekea mambo unayoamini (Tazama fungu la 17)h


Je, Utahudhuria Harusi au Mazishi?

Harusi na mazishi ni pindi ambazo kwa kawaida hukutanisha pamoja watu wa familia. Kabla ya kuamua kuhudhuria matukio hayo, unaweza kufikiria kanuni zifuatazo za Biblia.

  • Je, tukio hilo litahusisha ibada ya kidini au la? (2 Kor. 6:​14, 15)

  • Ikiwa utahudhuria, je, utaweza kuepuka kushinikizwa kushiriki katika desturi za kidini au zisizo za Kimaandiko? (Met. 22:3)

  • Je, watu wako wa ukoo wasioamini wanajua kwamba hutashiriki katika mazoea yasiyopatana na Maandiko?

  • Ikiwa utahudhuria tukio katika jengo la ibada, uamuzi wako unaweza kuwaathirije waabudu wenzako? (Flp. 1:10)

Vyovyote vile utakavyoamua, sikuzote jitahidi kuwaeleza wapendwa wako msimamo wako kwa njia iliyo wazi na kwa busara. Zaidi ya yote, fanya yote uwezayo kudumisha dhamiri njema mbele za Mungu.f

18. Tunawezaje kumwiga mwanafunzi Andrea?

18 Watambulishe kwa waabudu wenzako. Mwanafunzi Andrea alipomtambua Yesu kuwa Masihi, kwa furaha alimtambulisha Petro, ndugu yake, kwa Yesu. (Yoh. 1:​40-42) Je, tunaweza kufanya hivyo pia? Kwa mfano, je, tunaweza kumwalika pindi fulani mtu wetu wa ukoo kwenye mkutano au kushiriki naye mlo pamoja na rafiki zetu? Tunapomtambulisha kwa waabudu wenzetu, ataona kwamba Mashahidi ni watu wa kawaida, walio wema na wenye fadhili.

19. Hata ikiwa watu wetu wa ukoo hawaelewi kikamili baadhi ya mambo tunayoamini, tunapaswa kuwatendeaje? (1 Petro 3:15)

19 Soma 1 Petro 3:15. Huenda watu wetu wa familia wasielewe kikamili kwa nini tunakataa kufanya mambo fulani, lakini sikuzote watakumbuka fadhili na heshima tunayowaonyesha. Huenda pia wakathamini jitihada zetu za kutumia wakati pamoja nao, kwa kuwa pindi fulani hatuwezi kuwa pamoja nao. Kwa mfano, hatuwezi kushiriki nao katika sherehe na desturi zisizopatana na Maandiko, lakini pindi nyingine tofauti tunaweza kuwatembelea, kushiriki nao mlo, na kuwapatia zawadi.

USIKATE TAMAA KUELEKEA WATU WAKO WA UKOO

20. Kwa nini mfano wa Yakobo unatutia moyo?

20 Yakobo alikosa fursa ya kuandamana pamoja na Yesu katika huduma yake, lakini hatimaye akaja kuwa mwanafunzi. (Gal. 1:​18, 19; 2:9) Ingawa hakuwa mwanafunzi wa mapema wa Yesu, ni wazi kwamba Yakobo alitumia mafundisho ya Yesu. Kwa mfano, akiongozwa na roho aliandika barua iliyorejelea yale Mahubiri ya Mlimani.e

21. Kwa nini hatupaswi kukata tamaa inapohusu watu wetu wa ukoo?

21 Licha ya jitihada zetu nyingi, huenda watu wetu wa ukoo wasioamini wasipendezwe na kweli au wasiitikie vizuri tunapowaonyesha upendezi wa kibinafsi. Kwa nini hatupaswi kukata tamaa? Kwa sababu tutakuwa tunamwiga Mungu wetu mwenye rehema, Yehova, na Yesu, Mwana wake, kila mara tunapowaonyesha fadhili watu wetu wa ukoo. (Luka 6:​33, 36) Baada ya muda, mwenendo wetu wenye upendo unaweza kuwachochea wabadili maoni yao kutuhusu. Huenda hata wakakumbuka mambo tunayoamini ambayo tulishiriki nao wakati uliopita. Ikiwa hatutakata tamaa kuwaelekea, huenda tukapata shangwe inayotokana na kuwaona wapendwa wetu wakijiunga nasi katika ibada ya kweli!

UNGEJIBUJE?

  • Sifa ya huruma inawezaje kutuchochea kuwasaidia watu wetu wa ukoo wasioamini?

  • Kwa nini tunahitaji kuendelea kuwa wenye subira tunaposhughulika na watu wetu wa ukoo wasioamini?

  • Tunawezaje kuwaonyesha watu wetu wa ukoo kwamba tunawapenda?

WIMBO 60 Ni Uzima Kwao

a UFAFANUZI WA MANENO: Katika Biblia, si sikuzote maneno “asiye mwamini” au “asiyeamini” yanarejelea mtu asiye na imani ya kidini au asiyeamini kwamba kuna Mungu. (1 Kor. 7:12; tazama habari za utafiti, “an unbelieving wife,” nwtsty.) Katika makala hii, maneno hayo yanarejelea mtu ambaye hamwabudu Yehova Mungu kwa njia ambayo Mashahidi wa Yehova wanafanya.

b Tazama makala, “Tunajua Nini Kuhusu Hukumu za Yehova za Wakati Ujao?” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 2024, uku. 11, fu. 11-13.

c Angalau Yakobo na Yuda, ndugu wawili wa kimwili wa Yesu, walikubali kweli baada ya Yesu kufa na kufufuliwa.

d Tazama sanduku “Je, Utahudhuria Harusi au Mazishi?”

e Linganisha Yakobo 1:2 na Mathayo 5:​11, 12; Yakobo 1:19 na Mathayo 5:22; Yakobo 1:22; 2:24 na Mathayo 7:21; Yakobo 2:13 na Mathayo 5:7; 6:​14, 15.

f Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kushughulikia hali kama hizo, tazama makala, “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2002, na Novemba 15, 2007.

g MAELEZO YA PICHA: Kabla ya kwenda katika huduma, kwa fadhili dada anamwandalia mume wake mlo.

h MAELEZO YA PICHA: Dada huyohuyo, anatenga wakati ili kumtembelea mama mkwe wake ambaye si Shahidi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki