Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Desemba kur. 2-7
  • Kitabu cha Ayubu Kinaweza Kukusaidia Unapoteseka

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu cha Ayubu Kinaweza Kukusaidia Unapoteseka
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MUNGU ARUHUSU AYUBU ATESEKE
  • JINSI SIMULIZI LA AYUBU LINAVYOTUSAIDIA KUVUMILIA
  • TUMIA KITABU CHA AYUBU KUWASAIDIA WENGINE
  • Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • “Mtumaini Yehova”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Kitabu Cha Biblia Namba 18—Yobu
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ayubu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Desemba kur. 2-7

MAKALA YA 48

WIMBO 129 Tutaendelea Kuvumilia

Kitabu cha Ayubu Kinaweza Kukusaidia Unapoteseka

“Kwa hakika, Mungu hatendi uovu.”—AYU. 34:12.

JAMBO KUU

Mambo tunayoweza kujifunza kutoka katika kitabu cha Ayubu kuhusu kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka na jinsi tunavyoweza kuvumilia tunapoteseka.

1-2. Kwa nini ni jambo linalofaa kwetu kusoma kitabu cha Ayubu?

JE, UMESOMA kitabu cha Ayubu hivi karibuni? Ingawa kiliandikwa miaka 3,500 hivi iliyopita, kitabu hiki cha kale kinaonwa na watu wengi kuwa kati ya vitabu bora zaidi kuwahi kuandikwa. Kikizungumzia kuhusu mpangilio wake rahisi, mtindo wake maridadi, na lugha iliyotumiwa inayofafanua mambo vizuri, kitabu kimoja cha marejeo kinamwita mwandikaji wake, “mwandikaji mwenye uwezo wa pekee.” Musa ndiye aliyeandika kitabu hicho cha pekee, lakini Mtungaji wa kitabu hicho ni Yehova Mungu.—2 Tim. 3:16.

2 Kitabu cha Ayubu ni sehemu muhimu ya Biblia. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba kinafunua wazi suala kuu linalowahusu viumbe wote wenye akili—kutakaswa kwa jina la Yehova. Kinatufundisha pia kuhusu sifa nzuri sana za Yehova, kama vile upendo wake, hekima, haki, na nguvu. Kwa mfano, kitabu cha Ayubu kinamrejelea Yehova kuwa “Mweza-Yote” mara 31, idadi ambayo inazidi mara ambazo cheo hicho kinatajwa katika vitabu vingine vyote vya Biblia kwa ujumla. Pia, kitabu cha Ayubu kinajibu maswali mengi ambayo watu hujiuliza maishani, kutia ndani swali hili ambalo linawahangaisha watu wengi: Kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka?

3. Taja baadhi ya manufaa tunayoweza kupata kwa kujifunza kitabu cha Ayubu.

3 Kama tu ambavyo tunaweza kuona mazingira yetu vizuri tunapokuwa juu ya mlima, kitabu cha Ayubu kinatusaidia kuona majaribu tunayokabili maishani tukiwa na maoni ya juu zaidi—maoni ya Yehova. Acheni tuone jinsi kitabu cha Ayubu kinavyoweza kutusaidia tunapoteseka. Tutajifunza jinsi ambavyo Waisraeli wangeweza kunufaika kutokana na simulizi la Ayubu na jinsi tunavyoweza kunufaika leo. Tutajifunza pia jinsi tunavyoweza kutumia simulizi hilo la Biblia kuwasaidia wengine.

MUNGU ARUHUSU AYUBU ATESEKE

4. Kulikuwa na tofauti gani kubwa kati ya Ayubu na Waisraeli waliokuwa nchini Misri?

4 Waisraeli walipokuwa wakiteseka wakiwa watumwa nchini Misri, mtu aliyeitwa Ayubu alikuwa akiishi katika nchi ya Usi, ambayo huenda ilikuwa upande wa mashariki wa Nchi ya Ahadi na kaskazini mwa Arabia. Tofauti kabisa na Waisraeli waliokuwa wameanza kuabudu sanamu nchini Misri, Ayubu alimtumikia Yehova kwa uaminifu. (Yos. 24:14; Eze. 20:8) Yehova alisema hivi kumhusu Ayubu: “Hakuna yeyote aliye kama yeye duniani.”a (Ayu. 1:8) Ayubu alikuwa tajiri sana na aliheshimiwa sana—kuliko mtu yeyote huko Mashariki. (Ayu. 1:3) Ni lazima Shetani alikasirika sana alipomwona mwanamume huyo maarufu na aliyeheshimiwa sana akimtumikia Mungu kwa utimilifu!

5. Kwa nini Yehova aliruhusu Ayubu ateseke? (Ayubu 1:​20-22; 2:​9, 10)

5 Shetani alidai kwamba Ayubu angeacha ibada ya kweli ikiwa angeteseka. (Ayu. 1:​7-11; 2:​2-5) Ingawa Yehova alimpenda sana Ayubu, dai zito la Shetani lilitokeza masuala mengi muhimu, hivyo Yehova alimruhusu Shetani ajaribu kuthibitisha dai lake. (Ayu. 1:​12-19; 2:​6-8) Shetani alichukua mifugo ya Ayubu, alisababisha vifo vya watoto kumi wa Ayubu, na akampiga kwa majipu yenye maumivu makali kuanzia wayo wa mguu mpaka utosini. Lakini majaribu hayo mabaya sana hayakuvunja utimilifu wa Ayubu. (Soma Ayubu 1:​20-22; 2:​9, 10.) Baadaye, Yehova alimrudishia Ayubu afya nzuri, utajiri, na alimpatia watoto kumi zaidi. Na watu wakamheshimu tena Ayubu. Pia, alimwongezea kimuujiza miaka 140 ya kuishi, ambayo ilimwezesha kuona vizazi vinne vya uzao wake. (Ayu. 42:​10-13, 16) Simulizi hilo lingewezaje kuwanufaisha watumishi wa Mungu zamani, na linawezaje kutunufaisha leo?

6. Simulizi la Ayubu lingewezaje kuwasaidia Waisraeli? (Tazama pia picha.)

6 Jinsi ambavyo Waisraeli wangeweza kunufaika. Waisraeli hawakuwa na maisha mazuri nchini Misri. Kwa mfano, walipokuwa vijana, Yoshua na Kalebu walikuwa watumwa. Kisha ingawa hawakuwa na kosa, walilazimika kuishi nyikani kwa miaka 40. Ikiwa Waisraeli walijua kuhusu simulizi la majaribu ya Ayubu na matokeo yake, bila shaka hilo liliwasaidia wao pamoja na vizazi vilivyofuata, kuelewa ni nani hasa anayesababisha kuteseka. Pia, wangeweza kuelewa vizuri zaidi kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka na jinsi anavyothamini utimilifu na uaminifu wa wanadamu.

Mwanamume Mwisraeli akitafakari huku akipanga matofali nchini Misri. Karibu naye, Wamisri wanatumia fimbo kuwapiga Waisraeli wengine wanaofanya kazi kwa bidii.

Waisraeli, ambao walikuwa watumwa Misri kwa muda mrefu, mwishowe wangekuja kujifunza kuhusu kilichompata Ayubu, na kunufaika na mfano wake (Tazama fungu la 6)


7-8. Kitabu cha Ayubu kinawezaje kuwasaidia wale wanaoteseka? Toa mfano.

7 Jinsi tunavyoweza kunufaika. Kwa kusikitisha, watu wengi leo wamepoteza imani katika Mungu kwa sababu hawaelewi kwa nini mambo mabaya yanawapata watu wazuri. Fikiria mfano wa mwanamke anayeitwa Hazelb kutoka nchini Rwanda. Alipokuwa mdogo, aliamini kwamba kuna Mungu. Lakini mambo yakabadilika. Wazazi wake walitalikiana, na hivyo akalelewa na baba wa kambo ambaye alimtendea kwa njia mbaya. Alipokuwa tineja, alibakwa. Hazel hakupata faraja alipoenda mahali alipokuwa akiabudu. Baadaye, Hazel alimwandikia Mungu barua. Alisema hivi: “Mungu, nilisali kwako, nimejitahidi kutenda mema, lakini umelipa mema yangu kwa maovu. Sasa ninakuacha, na ninapanga kufanya jambo lolote linaloniletea furaha.” Tunasikitika sana tunapoona watu, kama vile Hazel, wanapofanywa waamini kwamba Mungu ndiye anayesababisha wateseke!

8 Hata hivyo, sisi tumejifunza katika simulizi la kitabu cha Ayubu kwamba Mungu hasababishi kuteseka—Shetani ndiye anayesababisha! Tumejifunza pia kwamba tusifikiri ni lazima wale wanaoteseka wanavuna kile walichopanda. Maandiko yanasema kwamba “wakati na matukio yasiyotarajiwa” yanaweza kumwathiri mtu yeyote na wakati wowote. (Mhu. 9:11; Ayu. 4:​1, 8) Na tumejifunza kwamba tunapovumilia kwa uaminifu majaribu, tunampatia Yehova jibu la kumpa Shetani anayemdhihaki. Hilo linasaidia kutetea sifa ya Yehova. (Ayu. 2:3; Met. 27:11) Hatuchukulii kivivi hivi mambo ambayo tumejifunza—mambo hayo yanatuwezesha kujua ukweli kuhusu kwa nini sisi na wapendwa wetu tunateseka. Baadaye, Hazel alijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na akaelewa kwamba Mungu hakusababisha kuteseka kwake. Alisema hivi: “Nilisali tena kwa Mungu kutoka moyoni. Nilimwambia Yehova kwamba niliposema ninamwacha, sikuwa ninamaanisha kwamba ninamwacha yeye. Isitoshe, sikuwa nimemjua vizuri. Sasa ninaelewa kwamba Yehova ananipenda. Hatimaye, sasa nina furaha na nimeridhika.” Tunashukuru sana kwamba tunajua kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka! Acheni sasa tuchunguze jinsi simulizi la Ayubu linavyoweza kutusaidia kibinafsi tunapokabili majaribu.

JINSI SIMULIZI LA AYUBU LINAVYOTUSAIDIA KUVUMILIA

9. Fafanua hali ya Ayubu alipokuwa ameketi katika majivu. (Yakobo 5:11)

9 Mwazie Ayubu akiwa ameketi peke yake kwenye majivu, mwili wake ukiwa umejaa majipu na akiwa amelemewa na maumivu makali. Ngozi yake ni nyeusi kwa sababu ya ugonjwa na imebambuka kutoka katika mwili wake uliokonda. Akiwa amechoka kabisa, huenda ilionekana kwamba Ayubu hafanyi lolote lingine zaidi ya kujikuna kwa kutumia vigae huku akilalamika kuhusu hali yake. Lakini Ayubu hakuwa tu akiendelea kuishi licha ya kuteseka, bali alikuwa akivumilia. (Soma Yakobo 5:11.) Ni nini kilichomsaidia Ayubu kuvumilia?

10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Ayubu alikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova? Eleza.

10 Ayubu alimweleza Yehova jinsi alivyohisi. (Ayu. 10:​1, 2; 16:20) Kwa mfano, sura ya 3 inaeleza kwamba Ayubu alilalamika kwa uchungu kuhusu misiba iliyompata, ambayo alifikiri kimakosa kuwa Yehova ndiye aliyeisababisha. Kisha, katika mfululizo wa majadiliano pamoja na wale marafiki wake watatu, Ayubu alitetea kwa uthabiti utimilifu wake, akielekeza mara nyingi majibu yake kwa Yehova. Maneno ya Ayubu yalionyesha kwamba kwa muda fulani alijiona kuwa mwadilifu kuliko Mungu. (Ayu. 10:​1-3; 32:​1, 2; 35:​1, 2) Hata hivyo, alikiri kwamba jitihada zake za kutetea utimilifu wake, pindi fulani zilikuwa sawa na “mazungumzo ya ovyoovyo.” (Ayu. 6:​3, 26) Katika sura ya 31, tunasoma kwamba Ayubu alitaka Mungu amjibu na kumwambia kuwa hakustahili kuadhibiwa. (Ayu. 31:35) Bila shaka, haikuwa sawa kwa Ayubu kudai kwa uthabiti jibu la moja kwa moja kutoka kwa Mungu kuhusu sababu ya kuteseka kwake.

11. Yehova aliitikiaje baada ya Ayubu kutetea utimilifu wake?

11 Tunaposoma simulizi la Ayubu leo, tunatambua kwamba ombi lake lilionyesha alijitoa kikamili kwa Yehova na alikuwa na tumaini imara kwamba kwa njia fulani Mungu angetambua utimilifu wake. Hatimaye Yehova alipomjibu Ayubu kutoka katika dhoruba ya upepo, hakumfafanulia kwa undani sababu za kuteseka kwake. Pia, hakumshutumu Ayubu kwa sababu ya kulalamika au kudai kwamba hakuwa na hatia. Badala yake, Yehova alimpatia mwongozo kama ambavyo baba angempatia mwongozo mwana wake. Na hiyo ilikuwa njia bora ya kumsaidia Ayubu. Matokeo ni kwamba kwa unyenyekevu, Ayubu alitambua kwamba alikuwa hajui mambo mengi na akatubu kwa sababu ya kuongea bila kufikiri. (Ayu. 31:6; 40:​4, 5; 42:​1-6) Simulizi hilo lingewezaje kuwanufaisha watu zamani, na linatunufaishaje leo?

12. Waisraeli wangeweza kunufaikaje kutokana na simulizi la Ayubu?

12 Jinsi ambavyo Waisraeli wangeweza kunufaika. Waisraeli wangeweza kujifunza kutokana na mambo yaliyompata Ayubu. Fikiria mfano wa Musa. Alihitaji kuvumilia matatizo na vivunja moyo vingi alipopewa jukumu la kuwa kiongozi wa taifa la Israeli. Tofauti na Waisraeli waasi, ambao mara nyingi walilalamika dhidi ya Yehova, Musa alisali kwa Yehova na kumweleza mahangaiko yake. (Kut. 16:​6-8; Hes. 11:​10-14; 14:​1-4, 11; 16:​41, 49; 17:5) Musa pia alihitaji kuvumilia aliporekebishwa. Kwa mfano, Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi Kadeshi, huenda katika mwaka wa 40 wa kutangatanga nyikani, Musa aliongea “bila kufikiri kwa midomo yake” na akashindwa kutukuza jina la Yehova. (Zab. 106:​32, 33) Matokeo ni kwamba Yehova hakumruhusu Musa aingie katika Nchi ya Ahadi. (Kum. 32:​50-52) Ni lazima nidhamu hiyo ilimuumiza Musa; hata hivyo, kwa unyenyekevu aliikubali. Simulizi la Ayubu lingeweza kuvisaidia vizazi vilivyofuata vya Waisraeli kuvumilia majaribu waliyokabili. Kwa kutafakari kuhusu simulizi hilo, Waisraeli waaminifu wangeweza kujifunza jinsi ya kumweleza Yehova hisia zao na jinsi ya kuepuka kujiona kuwa waadilifu kuliko Yehova. Wangeweza pia kujifunza jinsi ya kukubali kwa unyenyekevu nidhamu ya Yehova.

13. Simulizi la Ayubu linawezaje kutusaidia kuvumilia? (Waebrania 10:36)

13 Jinsi sisi tunavyoweza kunufaika. Tukiwa Wakristo, sisi pia tunahitaji sifa ya uvumilivu. (Soma Waebrania 10:36.) Kwa mfano, baadhi yetu tunakabiliana na tatizo la kimwili au kihisia, matatizo katika familia, kupoteza mpendwa wetu katika kifo, au tatizo lingine kubwa. Na nyakati nyingine, maneno au matendo ya watu yanaweza kufanya iwe vigumu zaidi kuvumilia hali yetu. (Met. 12:18) Hata hivyo, kitabu cha Ayubu kinatufundisha kwamba tunaweza kumweleza Yehova hisia zetu za ndani, tukiwa na uhakika kwamba atatusikia. (1 Yoh. 5:14) Hatatuhukumu ikiwa pindi fulani dua zetu za kutoka moyoni zinaanza kuwa “mazungumzo ya ovyoovyo,” kama ilivyokuwa kwa Ayubu. Badala yake, Mungu atatupatia nguvu na hekima tunayohitaji ili kuvumilia. (2 Nya. 16:9; Yak. 1:5) Pia, huenda akaturekebisha kwa kiwango kinachohitajika, kama alivyofanya kwa Ayubu. Kitabu cha Ayubu kinatufundisha pia jinsi ya kuonyesha sifa ya uvumilivu tunapopewa shauri au nidhamu kutoka katika Neno la Yehova, tengenezo Lake, au marafiki wakomavu. (Ebr. 12:​5-7) Kama tu Ayubu alivyonufaika kwa kukubali kwa unyenyekevu shauri alilopewa, sisi pia tunanufaika tunapokubali kurekebishwa upya. (2 Kor. 13:11) Kwa kweli, tunajifunza mambo muhimu sana kutoka kwa Ayubu! Acheni sasa tuchunguze jinsi tunavyoweza kutumia simulizi la Ayubu ili kuwasaidia wengine.

TUMIA KITABU CHA AYUBU KUWASAIDIA WENGINE

14. Tunawezaje kumjibu mtu katika huduma ambaye anauliza kwa nini wanadamu wanateseka?

14 Je, umewahi kukutana na mtu katika huduma aliyetaka kujua kwa nini watu wanateseka? Ulijibuje swali lake? Huenda ulimwonyesha jambo ambalo Biblia inasema lilitokea katika bustani ya Edeni. Labda ulianza kwa kutaja kwamba Shetani, roho mwovu, aliwaeleza wenzi wa kwanza uwongo uliosababisha wamwasi Mungu. (Mwa. 3:​1-6) Kisha, huenda ulitaja kwamba baada ya uasi wa Adamu na Hawa, watu wakaanza kuteseka na kufa. (Rom. 5:12) Hatimaye, huenda ulimfafanulia kwamba Mungu ameruhusu wakati wa kutosha upite ili kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo na wa kutangaza habari njema kwamba wanadamu watakuwa wakamilifu tena wakati ujao. (Ufu. 21:​3, 4) Hiyo ni njia nzuri ya kujibu swali hilo, na inaweza kuwa na matokeo mazuri.

15. Tunawezaje kutumia kitabu cha Ayubu kumsaidia mtu anayeuliza kwa nini wanadamu wanateseka? (Tazama pia picha.)

15 Fikiria njia nyingine ya kujibu swali hilo inayopatikana katika kitabu cha Ayubu—ambayo huenda ukatumia katika huduma yako. Unaweza kuanza kwa kumpongeza mtu huyo kwa kuuliza swali hilo muhimu. Kisha, unaweza kutaja kwamba Ayubu, mtu mwaminifu aliyeteseka sana, alijiuliza swali kama hilo. Huenda hata aliamini kwamba kwa njia fulani Mungu ndiye aliyesababisha maumivu yake. (Ayu. 7:​17-21) Mtu unayezungumza naye huenda akavutiwa kujua kwamba hata zamani, watu wengine walikuwa na maoni kama yake. Kisha, kwa busara unaweza kumfafanulia kwamba Ibilisi ndiye aliyesababisha Ayubu ateseke, si Mungu. Ibilisi alifanya hivyo ili kujaribu kuthibitisha kwamba wanadamu wanamtumikia Mungu kwa faida zao za kibinafsi tu. Unaweza kuongezea kwamba ingawa Mungu hakusababisha Ayubu ateseke, aliruhusu ateseke, hivyo Mungu alionyesha kwamba anatumaini kuwa wanadamu waaminifu wanaweza kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo. Mwishowe, unaweza kufafanua kwamba baadaye Mungu alimbariki Ayubu kwa kudumisha uaminifu. Hivyo, tunaweza kuwafariji wengine kwa kuwahakikishia kwamba Yehova si chanzo cha kuteseka.

Mkusanyo wa picha: 1. Mwanamke mwenye mkazo akiwa ameshika picha iliyo kwenye fremu baada ya kufukua vitu vilivyobaki baada ya moto wa mwituni. 2. Baadaye, mwanamke huyo anasimama kwenye kigari cha machapisho kilicho karibu na kituo cha kutoa misaada na anamsikiliza dada anayemsomea andiko.

Unawezaje kutumia kitabu cha Ayubu kuwahakikishia wengine kwamba “Mungu hatendi uovu”? (Tazama fungu la 15)


16. Toa mfano unaoonyesha jinsi ambavyo kitabu cha Ayubu kinaweza kumsaidia mtu anayeteseka.

16 Fikiria jinsi kitabu cha Ayubu kilivyomsaidia Mario. Siku moja mwaka wa 2021, dada fulani alikuwa akifanya mahubiri ya simu. Katika mazungumzo yake ya kwanza, alisoma mstari wa Biblia pamoja na Mario na kumweleza kwamba Mungu anatupatia wakati ujao mzuri na tumaini na pia anasikiliza sala zetu. Dada huyo alimuuliza maoni yake kuhusu jambo hilo, na Mario alimwambia kwamba alipopiga simu alikuwa akiandika barua kabla ya kujiua. Anasema hivi: “Ninamwamini Mungu, lakini asubuhi ya leo nilijiuliza ikiwa ameniacha.” Dada alipompigia simu mara ya pili, walianza kuzungumzia kuhusu kuteseka kwa Ayubu. Mario aliamua kwamba alihitaji kusoma kitabu kizima cha Ayubu. Hivyo, dada yetu alimtumia kiunganishi cha Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Matokeo yalikuwaje? Mario alikubali kujifunza Biblia na alifurahia kujifunza mengi zaidi kuhusu Mungu mwenye upendo anayependezwa naye.

17. Kwa nini unathamini kwamba Yehova aliweka kitabu cha Ayubu katika Neno Lake lililoongozwa na roho? (Ayubu 34:12)

17 Ni wazi kwamba Neno la Mungu lina nguvu nyingi za kuwasaidia watu, kutia ndani wale wanaoteseka. (Ebr. 4:12) Tunathamini sana kwamba Yehova ameweka simulizi la Ayubu katika Neno Lake lililoongozwa na roho! (Ayu. 19:​23, 24) Kitabu cha Ayubu kinatuhakikishia kwamba “kwa hakika, Mungu hatendi uovu.” (Soma Ayubu 34:12.) Pia, kinatufundisha kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka na jinsi tunavyoweza kuvumilia. Na kinatusaidia kuwafariji wale wanaoteseka. Makala inayofuata itazungumzia jinsi kitabu cha Ayubu kinavyoweza kutusaidia kutoa shauri kwa njia yenye matokeo.

UNGEJIBUJE?

  • Tunanufaikaje kwa kuelewa kwa nini Mungu aliruhusu Ayubu ateseke?

  • Simulizi la Ayubu linawezaje kutusaidia kuvumilia majaribu?

  • Tunawezaje kutumia kitabu cha Ayubu kuwasaidia wengine?

WIMBO 156 Kwa Imani

a Inaelekea kwamba Ayubu aliishi katika kipindi cha wakati kati ya kifo cha mtumishi mwaminifu Yosefu (1657 K.W.K.) na kuwekwa rasmi kwa Musa akiwa kiongozi wa Israeli (m. 1514 K.W.K.). Inawezekana kwamba mazungumzo kati ya Yehova na Shetani na majaribu aliyokabili Ayubu, yalitokea katika kipindi hicho.

b Baadhi ya majina yamebadilishwa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2026 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki